Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mtu Anahisije Anaposhuka Moyo?
    Amkeni!—2009 | Julai
    • Mtu Anahisije Anaposhuka Moyo?

      “NILIPOKUWA na umri wa miaka 12,” anakumbuka James,a “niliamka na kuketi kitandani, na nikajiuliza hivi, ‘Je, leo ndiyo siku yangu ya kufa?’” James alikuwa ameshuka moyo sana. James anasema hivi miaka 30 baadaye: “Kila siku maishani mwangu nimepambana na ugonjwa huu wa kihisia na kiakili.” Alipokuwa mtoto, James alihisi kwamba yeye hakuwa mtu wa maana kabisa hata akararua picha zake za utotoni. “Sikudhani nilikuwa mtu wa maana hivi kwamba nikumbukwe,” anasema.

      Kwa sababu sisi sote huhisi tumehuzunika mara kwa mara, tunaweza kukata kauli kwamba tunaelewa jinsi mtu aliyeshuka moyo anavyohisi. Lakini mtu aliye na ugonjwa wa kushuka moyo sana anahisije?

      Mgeni Asiyetakikana

      Tofauti na huzuni ya muda, mara nyingi ugonjwa wa kushuka moyo sana unamzuia mtu asifanye shughuli zake za kila siku.

      Kwa mfano, kwa zaidi ya miaka 40, Álvaro amekumbwa na “woga, kuchanganyikiwa kiakili, kuhangaika, na huzuni nyingi.” Anasema hivi: “Kwa sababu ya kushuka moyo, niliathiriwa sana na maoni ya wengine. Kila mara nilijihisi mwenye hatia mambo yalipoenda mrama.” Anaeleza kwamba kushuka moyo ni kama “kuwa na maumivu makali bila kujua maumivu hayo yanatoka wapi, kuwa na hofu bila kujua ni kwa nini na, jambo baya hata zaidi, kutotaka hata kidogo kuzungumzia hali yako.” Hata hivyo, sasa amepata kitulizo. Amejua chanzo cha tatizo lake. Anasema, “Kujua kwamba wengine pia wanakabili tatizo kama langu kumenifanya nijihisi vizuri.”

      Nchini Brazili, Maria mwenye umri wa miaka 49 anasema kwamba kushuka moyo kulimfanya akose usingizi, apatwe na maumivu, audhike, na awe na “huzuni isiyoisha.” Maria alipata kitulizo ugonjwa wake ulipogunduliwa. “Lakini nikaanza kuwa na wasiwasi,” anasema, “kwa sababu ni watu wachache sana wanaoelewa ugonjwa huo, na unaonwa kuwa wenye kuaibisha.”

      Je, Kuna Sababu ya Kuhuzunika?

      Ingawa nyakati nyingine inakuwa rahisi kujua ni nini kinachokufanya ushuke moyo, mara nyingi ugonjwa huo huja bila kutarajiwa. “Ghafula maisha yako yanafunikwa na wingu la huzuni bila sababu yoyote,” anaeleza Richard kutoka Afrika Kusini. “Hakuna mtu unayemjua ambaye amekufa, na hakuna jambo lolote lenye kuhuzunisha limetukia. Hata hivyo, unajihisi ukiwa mchovu na umehuzunika. Na hakuna chochote kinachoweza kuondoa wingu hilo. Unakata tamaa kabisa na hujui ni kwa nini.”

      Kushuka moyo si ugonjwa wa kuaibikia. Hata hivyo, Ana anayeishi Brazili aliaibika ilipogunduliwa anaugua ugonjwa wa kushuka moyo. “Hata sasa, miaka minane baadaye bado ninaaibika,” anasema. Anashindwa hasa kukabiliana na hisia za kuhuzunika sana. Anaeleza hivi: “Nyakati nyingine ninateseka sana hivi kwamba ninahisi maumivu. Misuli yangu yote huuma.” Nyakati hizo inakuwa vigumu kutoka kitandani. Kisha kuna pindi Ana hulia mfululizo. Anasema, “Mimi hulia mpaka ninahisi uchovu, ni kana kwamba damu imeacha kuzunguka mwilini.”

      Biblia inakubali kwamba mtu anaweza kushuka moyo sana. Kwa mfano, mtume Paulo alihangaika kwamba mtu mmoja ‘angemezwa na huzuni yake ya kupita kiasi [‘angezama katika uchungu mwingi mno,’ Verbum Bible].’ (2 Wakorintho 2:7) Watu fulani hufadhaika sana hivi kwamba wanaona ni afadhali wafe. Wengi huhisi kama nabii Yona aliyesema: “Ni afadhali mimi nife kuliko niwe hai.”—Yona 4:3.

      Watu walioshuka moyo wanaweza kufanya nini ili kukabiliana na ugonjwa huo wenye kufadhaisha?

      [Maelezo ya Chini]

      a Majina katika makala hizi yamebadilishwa.

      [Blabu katika ukurasa wa 3]

      “Ghafula maisha yako yanafunikwa na wingu la huzuni bila sababu yoyote”

  • Jinsi ya Kutibu Ugonjwa wa Kushuka Moyo
    Amkeni!—2009 | Julai
    • Jinsi ya Kutibu Ugonjwa wa Kushuka Moyo

      “MIMI na mume wangu tumetafuta matibabu, tukabadili mtindo wetu wa maisha, na kujitahidi kuwa na ratiba inayonifaa,” anasema Ruth, ambaye ameugua ugonjwa wa kushuka moyo kwa miaka mingi. “Sasa inaonekana tumepata dawa inayonifaa na ninahisi nafuu. Lakini wakati nilipohisi hakuna chochote kinachoweza kunisaidia, mume wangu na marafiki walinionyesha upendo nyakati zote na hivyo kunisaidia nisikate tamaa.”

      Kama vile kisa cha Ruth kinavyoonyesha, watu wanaougua ugonjwa wa kushuka moyo sana wanahitaji msaada kutia ndani matibabu yoyote yanayofaa. Ni hatari kupuuza ugonjwa huo kwa sababu mara nyingine ukikosa kutibiwa mtu anaweza kufa. Miaka elfu mbili hivi iliyopita, Yesu Kristo alisema kwamba watu wenye ujuzi wa kitiba wanaweza kumsaidia mtu aliposema “wale walio wagonjwa wanamhitaji [tabibu].” (Marko 2:17) Ukweli ni kwamba matabibu wanaweza kuwasaidia sana wagonjwa walioshuka moyo.a

      Mapendekezo Yanayoweza Kusaidia

      Kuna matibabu mbalimbali kwa ajili ya ugonjwa wa kushuka moyo ikitegemea dalili na kiwango cha ugonjwa. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 5, “Aina Mbalimbali za Ugonjwa wa Kushuka Moyo.”) Watu fulani wanaweza kutibiwa na daktari wa kawaida, lakini wengine wanahitaji usaidizi wa wataalamu. Huenda daktari akampa mgonjwa dawa za kutuliza akili au akapendekeza matibabu mengine. Wengine wamepata matokeo mazuri kwa kutumia mitishamba, kubadili vyakula, au kufanya mazoezi.

      Mambo Yanayosababisha Matatizo

      1. Marafiki wenye nia nzuri ambao hawana ujuzi mwingi au hawana ujuzi wowote wa mambo ya kitiba wanaweza kujaribu kukufanya ukubali matibabu fulani na ukatae mengine. Huenda pia wakakuamulia ikiwa utatumia mitishamba, dawa ulizoandikiwa na daktari, au kukukataza usitumie chochote.

      Fikiria hili: Hakikisha kwamba mashauri yoyote unayokubali yanatoka kwa chanzo kinachotegemeka. Mwishowe wewe ndiye utakayejiamulia baada ya kupata habari kamili.

      2. Kuvunjika moyo kunaweza kufanya wagonjwa waache matibabu waliyochagua kwa sababu hawapati nafuu au matibabu hayo yanawadhuru kwa njia fulani.

      Fikiria hili: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” (Methali 15:22) Huenda matibabu yoyote yakawa na matokeo mazuri kukiwa na mawasiliano mazuri kati ya daktari na mgonjwa. Mweleze waziwazi daktari mahangaiko na dalili zako, na umuulize ikiwa unahitaji kubadili matibabu au uvumilie kwa muda kabla ya kuanza kupata matokeo mazuri.

      3. Kujitumaini kupita kiasi kunaweza kuwafanya wagonjwa waache matibabu yao ghafula baada ya majuma machache tu kwa sababu wanahisi nafuu. Wanaweza kusahau jinsi ugonjwa huo ulivyowadhoofisha kabla ya wao kuanza kupata matibabu hayo.

      Fikiria hili: Kuacha matibabu ghafula bila kuambiwa na daktari kunaweza kuwa na matokeo mabaya na hata kuhatarisha uhai wako.

      Ingawa Biblia si kitabu kinachozungumzia mambo ya kitiba, Yehova Mungu, Mtungaji wa Biblia ndiye Muumba wetu. Makala inayofuata itachunguza faraja na mwongozo ambao Neno la Mungu linawapa wale walioshuka moyo na pia wale wanaowatunza.

      [Maelezo ya Chini]

      a Amkeni! halipendekezi matibabu yoyote hususa. Kila mtu anapaswa kuchunguza matibabu mbalimbali kabla ya kufanya uamuzi wake.

      [Sanduku katika ukurasa wa 5]

      AINA MBALIMBALI ZA UGONJWA WA KUSHUKA MOYO

      Matibabu yanayofaa yanategemea mtu anaugua aina gani ya ugonjwa wa kushuka moyo.

      ◼ Ugonjwa wa kushuka moyo sana una dalili ambazo zinaweza kudumu kwa miezi sita au zaidi usipotibiwa na zinaathiri sana maisha ya mgonjwa.

      ◼ Ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia. Wagonjwa wanaweza kusisimka sana kwa muda mrefu na ghafula washuke moyo sana.—Ona makala “Kuishi na Ugonjwa wa Kihisia,” katika Amkeni! la Januari 8, 2004 (8/1/2004).

      ◼ Ugonjwa wa kushuka moyo kidogo haudhoofishi kama ugonjwa wa kushuka moyo sana lakini dalili zake humzuia mgonjwa asiweze kuendelea na shughuli zake za kawaida. Pia watu wanaougua ugonjwa huo wanaweza kushuka moyo sana kwa vipindi vifupi.

      ◼ Ugonjwa wa kushuka moyo baada ya kujifungua huwapata wanawake wengi na huathiri sana hisia.—Ona makala “Kuelewa Mshuko wa Moyo Baada ya Kujifungua” katika Amkeni! la Juni 8, 2003, (8/6/2003).

      ◼ Ugonjwa wa kushuka moyo katika majira fulani hasa unatokea katika majira ya kupukutika kwa majani na majira ya baridi kali kwa sababu ya ukosefu wa mwangaza wa jua. Kwa kawaida ugonjwa huo huisha katika majira ya kuchipua na majira ya kiangazi.

  • Msaada Kutoka kwa “Mungu wa Faraja”
    Amkeni!—2009 | Julai
    • Msaada Kutoka kwa “Mungu wa Faraja”

      MFALME DAUDI alipatwa na maumivu makali ya kihisia na ‘fikira nyingi zinazofadhaisha.’ Hata hivyo, hakuwahi kutilia shaka kwamba Muumba anatuelewa sana. Aliandika hivi: “Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua. Wewe mwenyewe umepata kujua kuketi kwangu na kusimama kwangu. Umeichunguza fikira yangu tokea mbali. Kwa maana hamna neno hata moja katika ulimi wangu, lakini, tazama! Ee Yehova, tayari unajua yote.”—Zaburi 139:1, 2, 4, 23.

      Sisi pia tunaweza kuwa na hakika kwamba Muumba wetu anatuelewa na anaelewa jinsi kushuka moyo kunavyoathiri akili na mioyo yetu isiyo mikamilifu. Anajua kinachofanya tushuke moyo na jinsi tunavyoweza kukabiliana na hali za sasa. Isitoshe, ametuonyesha jinsi atakavyoondoa kushuka moyo kabisa. Hakuna mtu mwingine yeyote anayeweza kutusaidia hivyo isipokuwa Mungu wetu aliye na huruma “mwenye kufariji wenye huzuni.”—2 Wakorintho 7:6, Zaire Swahili Bible.

      Lakini huenda watu walioshuka moyo wakajiuliza Mungu anaweza kuwasaidia jinsi gani wanapokuwa na hisia zenye kufadhaisha.

      Je, Mungu anaweza kufikiwa na walioshuka moyo?

      Mungu yuko karibu sana na watumishi wake walioshuka moyo ni kana kwamba anakaa pamoja na “mtu aliyepondwa na mwenye roho ya unyenyekevu, ili kuipa uhai roho ya watu wa hali ya chini na kuupa uhai moyo wa wale wanaopondwa.” (Isaya 57:15) Inafariji sana kujua kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho”!—Zaburi 34:18.

      Walioshuka moyo wanaweza kufarijiwa na Mungu jinsi gani?

      Wakati wowote ule, waabudu wa Mungu wanaweza kumfikia “msikiaji wa sala,” ambaye anaweza kuwasaidia kukabiliana na hali na hisia zenye kufadhaisha. (Zaburi 65:2) Biblia inatuhimiza tummiminie yaliyo mioyoni mwetu: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.

      Vipi ikiwa tunafikiri kwamba sala zetu hazisikiwi kwa sababu tunajiona hatufai?

      Kushuka moyo kunaweza kufanya tukate kauli kwamba hatujitahidi vya kutosha kumpendeza Mungu. Hata hivyo, Baba yetu wa mbinguni anaelewa hisia zetu dhaifu, “akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zaburi 103:14) Ingawa “huenda mioyo yetu ikatuhukumu kuwa na hatia,” tunaweza ‘kuihakikishia mioyo yetu’ kwamba “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yohana 3:19, 20) Kwa hiyo, unaposali unaweza kutumia maneno kutoka katika mistari ya Biblia kama vile Zaburi 9:9, 10; 10:12, 14, 17; na 25:17.

      ◼ Namna gani ikiwa tumefadhaika sana hata hatuwezi kueleza tunavyohisi?

      Unapolemewa na hisia zenye kuumiza hivi kwamba inakuwa vigumu kuzungumza kwa njia inayoeleweka, usikate tamaa! Endelea kusali kwa “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote,” ukijua kwamba anaelewa hisia na mahitaji yako. (2 Wakorintho 1:3) Maria, aliyetajwa awali katika makala hizi, anasema: “Nyakati nyingine ninapochanganyikiwa sana, huwa sijui nisali kuhusu nini. Lakini ninajua kwamba Mungu anaelewa, naye hunisaidia.”

      ◼ Mungu anajibu sala zetu jinsi gani?

      Biblia haisemi kwamba Mungu anaondoa matatizo yetu yote sasa. Hata hivyo, Mungu anatupa nguvu za kukabiliana na “mambo yote” kutia ndani kushuka moyo. (Wafilipi 4:13) “Ilipogunduliwa kwamba nina ugonjwa wa kushuka moyo,” anasema Martina, “nilimwomba Yehova aniponye mara moja kwa sababu sikudhani ningeweza kukabiliana na hali hiyo. Sasa ninaridhika tu kusali anipe nguvu za kila siku.”

      Maandiko ni chanzo muhimu cha nguvu kutoka kwa Mungu ambazo zinawasaidia watu wakabiliane na kushuka moyo. Sarah, ambaye ameugua ugonjwa wa kushuka moyo kwa miaka 35, amejionea faida za kusoma Biblia kila siku. Anasema hivi: “Ninathamini sana matibabu ambayo nimepata. Hata hivyo, ninatambua jinsi kusoma Neno la Mungu kumenisaidia kiroho na kimwili. Nina zoea la kulisoma.”

      Watu Hawatashuka Moyo Tena!

      Yesu Kristo alipokuwa duniani alitumia nguvu alizopewa na Mungu kuponya magonjwa yenye kuumiza. Yesu alitaka sana kuwapa kitulizo watu waliougua magonjwa yenye kuhuzunisha. Isitoshe, yeye mwenyewe anajua maumivu makali ya kuwa na hisia zenye kufadhaisha. Usiku uliotangulia kifo chake chenye maumivu, “Kristo alitoa dua na pia maombi kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo, pamoja na vilio vyenye nguvu na machozi.” (Waebrania 5:7) Ingawa Yesu alifadhaika sana wakati huo, tunafaidika sasa kwa sababu “anaweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.”—Waebrania 2:18; 1 Yohana 2:1, 2.

      Biblia inafunua kwamba Mungu anakusudia kuondoa hali zote zenye kufadhaisha ambazo husababisha kushuka moyo. Anaahidi: “Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya; na mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, na muwe na shangwe milele katika hivi ninavyoumba.” (Isaya 65:17, 18) “Mbingu mpya,” yaani, Ufalme wa Mungu, utawezesha kuwe na “dunia mpya,” yaani, jamii ya watu waadilifu duniani walio na afya kamilifu kimwili, kihisia, na kiroho. Magonjwa yote yatafutiliwa mbali kabisa.

      “Nimeita jina lako, Ee Yehova, kutoka katika shimo la chini kabisa. Uisikilize sauti yangu. Usifiche sikio lako kwa ombi langu la kitulizo, kwa kilio changu cha kuomba msaada. Umekaribia katika siku ile ambayo niliendelea kukuita. Ukasema: ‘Usiogope.’”—Maombolezo 3:55-57

      ‘SEMENI KWA KUWAFARIJI WALIOHUZUNIKA’

      Barbara anaposhuka moyo sana na kuhisi hafai kabisa, yeye na mume wake humpigia simu Gerard, rafiki yao ambaye ni mwangalizi Mkristo. Kila mara yeye husikiliza kwa subira Barbara anapolia sana na kumweleza mawazo yaleyale yenye kufadhaisha ambayo amemwambia tena na tena.

      Gerard amejifunza kusikiliza bila kuhukumu, kubishana, au kushutumu. (Yakobo 1:19) Kama vile Biblia inavyoshauri, amejifunza ‘kusema kwa kuwafariji waliohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14) Kwa subira, yeye humhakikishia Barbara kwamba Yehova Mungu, familia yake, na rafiki zake, wanamwona kuwa mtu mwenye thamani sana. Kwa kawaida yeye humsomea andiko moja au mawili, hata ingawa amemsomea baadhi ya maandiko hayo wakati uliopita. Kisha, kila mara yeye husali pamoja na Barbara na mume wake kupitia simu, na hilo huwafariji sana.—Yakobo 5:14, 15.

      Gerard anatambua kwamba yeye si daktari na hachukui kamwe daraka la madaktari wa Barbara. Hata hivyo, kwa kuongezea matibabu anayopata, yeye humpa maandiko yenye kuliwaza na sala zenye kufariji, jambo ambalo ni madaktari wachache sana wanaweza kufanya.

      Ili ‘useme kwa kuwafariji waliohuzunika’

      Unaweza kusema: “Nilitaka tu kukuambia kwamba nimekuwa nikikufikiria sana. Ninajua unakuwa mgonjwa mara kwa mara. Unaendeleaje?”

      Kumbuka: Zungumza kwa unyoofu na usikilize ukijiweka katika hali yake, hata kama mtu aliyeshuka moyo atasema mambo yaleyale aliyowahi kusema.

      Unaweza kusema: “Ninapendezwa sana na mambo ambayo unaweza kufanya (au “ninavutiwa na sifa zako za Kikristo”) licha ya ugonjwa wako. Hata kama huwezi kufanya mambo yote ambayo ungependa, Yehova anakupenda na kukuthamini, na sisi pia.”

      Kumbuka: Uwe mwenye huruma na fadhili.

      Unaweza kusema: “Nilisoma andiko hili lenye kutia moyo.” Au unaweza kusema, “Nilikukumbuka niliposoma andiko hili ninalopenda sana.” Kisha soma au unukuu andiko hilo.

      Kumbuka: Usizungumze kana kwamba unamshauri.

      Faraja Kutoka kwa Maandiko

      Lorraine anatiwa nguvu na ahadi ya Yehova katika Isaya 41:10: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.”

      Álvaro anasema kwamba maneno ya Zaburi 34:4, 6 humfariji mara nyingi: “Nilimuuliza Yehova, naye akanijibu, naye akanikomboa kutoka katika mambo yote yenye kuniogopesha. Huyu mwenye kuteseka aliita, na Yehova mwenyewe akasikia. Na Yeye akamwokoa kutoka katika taabu zake zote.”

      Naoya anasema kwamba kusoma Zaburi 40:1, 2 humfariji: “Nilimtumainia Yehova kwa bidii, kwa hiyo akanitegea sikio lake na kusikia kilio changu cha kuomba msaada. . . . Akazifanya imara hatua zangu.”

      Zaburi 147:3 inamhakikishia Naoko kwamba Yehova “anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”

      Maneno ya Yesu katika Luka 12:6, 7 humsaidia Eliz ategemee ulinzi wa Yehova: “Shore watano huuzwa kwa sarafu mbili za thamani ndogo, sivyo? Na bado hakuna hata mmoja wao husahaulika mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.”

      Maandiko Mengine:

      • Zaburi 39:12: “Uisikie sala yangu, Ee Yehova, na usikilize kilio changu cha kutaka msaada. Usikae kimya machozi yangu yanapotoka.”

      • 2 Wakorintho 7:6: Mungu ‘hufariji wenye huzuni.’—“Zaire Swahili Bible.”

      • 1 Petro 5:7: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu ya Mungu, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki