Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuishi na Ugonjwa wa Kihisia
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Kwa mfano, inakadiriwa kwamba zaidi ya watu milioni 330 ulimwenguni pote wameshuka moyo sana, hali inayowafanya wahuzunike sana na wasipendezwe na shughuli za kila siku. Inakadiriwa kwamba miaka 20 ijayo, idadi ya watu walioshuka moyo itazidi ile ya wagonjwa wengine isipokuwa tu wagonjwa wa moyo. Basi si ajabu kwamba watu wanasema ugonjwa huo umewakumba watu wengi kama mafua.

  • Kuishi na Ugonjwa wa Kihisia
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Mtu Hulemewa na Huzuni Anaposhuka Moyo

      Wengi wetu tunajua jinsi mtu huhisi anapohuzunika. Baada ya muda mfupi, labda saa au siku kadhaa, huzuni hiyo huisha. Hata hivyo, ugonjwa wa kushuka moyo ni tofauti. Kwa njia gani? Dakt. Mitch Golant anasema kwamba ‘sisi ambao hatuna ugonjwa wa kushuka moyo tunajua kwamba hatimaye huzuni hutoweka, lakini kwa watu wenye ugonjwa huo huzuni hufuatwa na msisimuko, kisha hisia hizo hubadilika-badilika daima.’

      Ugonjwa wa kushuka moyo huathiri watu kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wengine huugua katika majira fulani, hasa majira ya baridi kali. Kitabu kilichochapishwa na Chama cha Kitiba cha Umma kinasema: “Watu wanaoshuka moyo katika majira fulani huathiriwa zaidi wakiwa katika maeneo ya kaskazini ya dunia na kukiwa na mawingu mengi. Ingawa inasemekana kwamba watu hao huathiriwa zaidi wakati wa baridi kali, wakati mwingine wao huathiriwa pia wanapofanya kazi mahali penye giza, wakati wowote ambapo kuna mawingu, na wasipoona vizuri.”

      Ni nini kinachosababisha ugonjwa wa kushuka moyo? Haijulikani waziwazi. Ijapokuwa huenda mtu akarithi ugonjwa huo, mara nyingi watu huathiriwa na mambo yanayotukia maishani. Imeonekana kwamba wanawake huathiriwa mara mbili zaidi ya wanaume.a Lakini haimaanishi kwamba wanaume hawawezi kuugua. Inakadiriwa kwamba kati ya asilimia 5 na 12 ya wanaume wataugua ugonjwa wa kushuka moyo wakati fulani maishani mwao.

      Mtu anapougua ugonjwa huo, karibu maisha yake yote huathiriwa. Sheila, anayeugua ugonjwa huo, anasema mgonjwa “huvurugika kabisa, hukosa kujiamini na kujiheshimu, hushindwa kufikiri vizuri na kufanya maamuzi vizuri, na huumia sana anapozidiwa.”

      Wakati mwingine mgonjwa anaweza kufarijika kwa kumweleza mtu mwingine anayejali hisia zake. (Ayubu 10:1) Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba kushuka moyo hakuwezi kumalizwa kwa kuwa na maoni yanayofaa tu wakati hali hiyo inaposababishwa na kemikali za mwili. Wakati huo, mgonjwa hawezi kudhibiti huzuni yake. Isitoshe, tayari huwa amefadhaishwa na hali hiyo kama tu watu wa familia na marafiki.

      Mfikirie Paula,b Mkristo aliyehuzunika vibaya kabla ugonjwa wake haujatambuliwa. Anasema: “Wakati mwingine nilipokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, nilirudi kwenye gari na kulia bila sababu yoyote. Nilijihisi mpweke sana na nilifadhaika sana. Ijapokuwa nilikuwa na marafiki wengi walionijali, bado nilihuzunika.”

      Ellen pia alipatwa na jambo kama hilo, na alihitaji kulazwa hospitalini. Anasema: “Nina mume, wana wawili, na mabinti-wakwe wawili, na wote wananipenda sana.” Basi, Ellen anapaswa kuwa na furaha na kuhisi anathaminiwa na familia yake. Lakini mtu anaposhuka moyo, huwa na mawazo mabaya, hata ya kipumbavu, na anaweza kulemewa.

      Pia ugonjwa huo unaweza kuathiri sana familia nzima. Dakt. Golant anaandika hivi: “Mtu unayempenda anaposhuka moyo, unaishi na wasiwasi kwa kuwa hujui kama atapata nafuu au atashuka moyo zaidi. Unaweza kuhisi mpweke na hata kuhuzunika na kukasirika kwa kuwa unaona maisha yamebadilika kabisa.”

      Mara nyingi, watoto wanaweza kutambua kwamba mzazi ameshuka moyo. Dakt. Golant anaandika hivi: “Mtoto wa mama aliyeshuka moyo hutambua haraka hisia za mama yake, na huona mabadiliko yoyote yanayotokea.” Dakt. Carol Watkins anasema kwamba watoto wa mzazi aliyeshuka moyo “wanaweza kuwa na tabia zisizofaa, kushindwa kujifunza, na kutopatana na marafiki. Wanaweza kushuka moyo pia.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki