Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tumaini kwa Wanaougua
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Tumaini kwa Wanaougua

      ZAMANI, watu waliwaepuka watu wenye magonjwa ya kihisia. Hivyo, wengi waliougua walitengwa na jamii. Baadhi yao walifutwa kazi au hawangeweza kuajiriwa. Wengine walikataliwa na watu wa familia. Mara nyingi, jambo hilo lilizidisha matatizo na kuwazuia wasipate msaada.

      Hata hivyo, katika miaka ya majuzi ugonjwa wa kushuka moyo na wa hisia zinazobadilika-badilika umeeleweka zaidi. Sasa inajulikana kwamba magonjwa hayo yanaweza kutibiwa. Lakini si rahisi sikuzote kupata msaada. Kwa nini?

      Kutambua Dalili

      Ugonjwa wa kihisia hauwezi kutambuliwa kwa kupima damu au kwa picha ya eksirei. Badala yake, tabia ya mtu, jinsi anavyofikiri, na kufanya maamuzi huchunguzwa kwa muda fulani. Dalili fulani lazima zionekane ili ugonjwa huo utambuliwe. Nyakati nyingine watu wa familia na marafiki huwa hawajui kwamba mtu anaugua ugonjwa huo wanapoona dalili. Dakt. David J. Miklowitz anaandika hivi: “Hata watu wanapoona tabia ya mtu imebadilika, wao huwa na maoni tofauti kuhusu kisababishi chake.”

      Isitoshe, hata watu wa familia wanapoona kwamba mtu ni mgonjwa sana, huenda wakashindwa kumsadikisha kwamba anahitaji matibabu. Au ikiwa wewe ndiwe mgonjwa, huenda usitake kutafuta msaada. Dakt. Mark S. Gold anaandika hivi: “Labda unaamini yale unayofikiri unaposhuka moyo—kwamba hufai, hivyo hakuna haja ya kuomba msaada ikiwa huna tumaini. Huenda ukataka kutafuta ushauri lakini unafikiri kwamba kushuka moyo ni jambo la aibu, kwamba wewe ndiwe mwenye lawama. . . . Labda hujui kwamba umeshuka moyo.” Hata hivyo, watu walioshuka moyo sana wanahitaji kumwona daktari.

      Bila shaka, sote hushuka moyo wakati fulani na hiyo haimaanishi kwamba tuna ugonjwa wa kihisia. Lakini vipi hisia hizo zikiendelea? Ama vipi zikidumu kwa muda mrefu isivyo kawaida, labda majuma mawili au zaidi? Zaidi ya hayo, tuseme huzuni hiyo haikuruhusu kufanya shughuli za kila siku, iwe ni kazini, shuleni, au shughuli za kirafiki. Wakati huo, huenda ikafaa kumwona daktari anayeweza kuchunguza na kutibu magonjwa ya kihisia.

      Iwapo ugonjwa huo umesababishwa na kasoro ya kemikali mwilini, huenda ukaandikiwa dawa. Katika visa fulani, huenda mgonjwa akapewa mashauri ya kumsaidia akabiliane na hali hiyo. Nyakati nyingine, njia zote mbili zimetumiwa kwa matokeo.a Jambo la maana ni kutafuta na kupata msaada. Lenore, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika aliyetajwa katika makala iliyotangulia, anasema: “Mara nyingi wagonjwa huogopa na kuaibika kwa sababu ya hali yao. Hata hivyo, mtu huaibika zaidi anapojua ana tatizo na hatafuti msaada anaohitaji sana.”

  • Tumaini kwa Wanaougua
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Hali yake ni kama ya Brandon ambaye ameshuka moyo. Anasema: “Nilipokuwa kijana, mara nyingi nilitaka kujiua kwa sababu nilijihisi sifai hata kidogo. Nilienda kumwona daktari nikiwa na miaka 30 na kitu.” Kama Lenore, Brandon anatumia dawa kukabiliana na ugonjwa huo, lakini mengi zaidi yanahusika. Anasema: “Ili niwe na afya bora, mimi hutunza akili na mwili wangu. Mimi hupumzika na kula vizuri. Mimi pia hujaza akili na moyo wangu kwa mawazo yajengayo kutoka katika Biblia.”

      Hata hivyo, Brandon anasema ugonjwa wa kushuka moyo ni tatizo la kitiba si la kiroho. Kutambua jambo hilo ni muhimu ili kupona. Brandon asimulia: “Wakati mmoja Mkristo mwenzangu mwenye nia nzuri aliniambia kwa kuwa andiko la Wagalatia 5:22, 23 linasema kwamba shangwe ni tunda la roho takatifu ya Mungu, nimeshuka moyo kwa sababu nimeihuzunisha roho hiyo. Jambo hilo lilinifanya nihisi hatia na kushuka moyo hata zaidi. Lakini nilipoanza kupata msaada, huzuni ilianza kwisha. Nilihisi vizuri zaidi! Laiti ningetafuta msaada mapema.”

      Kushinda Hisia Mbaya

      Hata baada ya ugonjwa kugunduliwa na kuanza kutibiwa, yaelekea mgonjwa ataendelea kuathiriwa. Kelly, ambaye anapambana na ugonjwa mbaya wa kushuka moyo amefaidika sana kutokana na msaada wa daktari. Pia, ametambua kwamba msaada wa wengine ni muhimu sana. Mwanzoni, Kelly hakutaka kuomba msaada kwa sababu hakutaka kuwa mzigo kwa wengine. Anasema: “Nilihitaji kujifunza kuomba msaada na kuukubali. Nilipowaeleza wengine jinsi nilivyohisi ndipo nilipoanza kupata nafuu.”

      Akiwa Shahidi wa Yehova, Kelly huhudhuria mikutano pamoja na waamini wenzake kwenye Jumba la Ufalme. Hata hivyo, wakati mwingine hata pindi hizo zenye furaha huleta magumu. Anasema: “Mara nyingi mwangaza, kuchangamana na watu, na kelele hunisumbua sana. Kisha mimi huhisi hatia na kushuka moyo zaidi kwa sababu nahisi kwamba naugua kwa kuwa mimi si mtu wa kiroho.” Kelly hushughulikiaje hali hiyo? Anasema: “Nimejifunza kwamba ugonjwa wa kushuka moyo unahitaji kutibiwa. Ninapougua, haimaanishi kwamba upendo wangu kwa Mungu na kwa Wakristo wenzangu umepungua. Ugonjwa wangu si kipimo cha hali yangu ya kiroho.”

  • Tumaini kwa Wanaougua
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

      Mgonjwa Anapopewa Dawa

      Wengine hufikiri kwamba kutumia dawa ni udhaifu. Lakini wazia jambo hili: Mtu mwenye ugonjwa wa kisukari anahitaji kutumia dawa, kutia ndani kujichoma sindano za insulini. Je, inamaanisha kwamba mtu huyo ni dhaifu? La, hasha! Hiyo ni njia ya kusawazisha kemikali mwilini mwa mgonjwa ili aendelee kuwa na afya.

      Ndivyo ilivyo pia na matibabu ya ugonjwa wa kushuka moyo au wa hisia zinazobadilika-badilika. Ingawa watu wengi wamefaidika kutokana na ushauri ambao umewasaidia kuelewa ugonjwa wao, inafaa kutahadhari. Ikiwa kemikali za mwili zinahusika, ugonjwa huo hauwezi kumalizwa kwa mashauri. Steven, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika anasimulia: “Daktari aliyenitibu alitumia mfano huu: Unaweza kumfundisha sana mtu fulani kuendesha gari, lakini ukimpa gari ambalo halina usukani au breki, basi mafunzo hayo hayatamsaidia. Vivyo hivyo, huenda mashauri pekee yasimsaidie mtu aliyeshuka moyo. Hatua ya kwanza ni kusawazisha kemikali za ubongo.”

  • Wengine Wanaweza Kusaidiaje?
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Wengine Wanaweza Kusaidiaje?

      LABDA unamjua mtu anayeugua ugonjwa wa kushuka moyo au wa hisia zinazobadilika-badilika. Ikiwa ndivyo, unawezaje kumtegemeza? D. J. Jaffe wa Shirika la Kitaifa la Wagonjwa wa Akili anashauri hivi: “Tofautisha ugonjwa na mgonjwa; chukia ugonjwa lakini umpende mgonjwa.”

      Kwa sababu ya kuwa na subira na upendo, mwanamke anayeitwa Susanna alifaulu kufanya hivyo. Rafiki yake aliugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Susanna anasema: “Nyakati nyingine hata hakutaka kuniona.” Badala ya kukata tamaa, Susanna alifanya utafiti ili aufahamu ugonjwa huo. Anasema: “Sasa natambua jinsi rafiki yangu alivyoathiriwa na ugonjwa wake.” Susanna anasema kwamba kuna faida kubwa kumwelewa mgonjwa. Anasema: “Jambo hilo linaweza kukusaidia kupenda na kuthamini zaidi sifa nzuri za mgonjwa.”

      Ikiwa anayeugua ni mshiriki wa familia, anahitaji kutiwa moyo sana. Mario, aliyetajwa katika makala zilizotangulia, alijifunza jambo hilo mapema. Mke wake, Lucia, ambaye pia alitajwa mapema, anaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Mario anasema: “Mwanzoni, nilifaidika kwa kuandamana na mke wangu alipoenda kumwona daktari na kujifunza kuhusu ugonjwa huo wa ajabu ili nifahamu jambo ambalo tunakabili. Mimi na Lucia tulizungumza sana na tukashughulikia hali yoyote iliyotokea.”

      Utegemezo wa Kutaniko la Kikristo

      Biblia huwashauri Wakristo wote ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika’ na ‘kuwa wenye ustahimilivu kuelekea wote.’ (1 Wathesalonike 5:14) Unawezaje kufanya hivyo? Kwanza, ni muhimu kuelewa tofauti kati ya ugonjwa wa akili na wa kiroho. Kwa mfano, mwandikaji wa Biblia Yakobo alisema kwamba sala inaweza kumsaidia mtu mwenye ugonjwa wa kiroho apone. (Yakobo 5:14, 15) Hata hivyo, Yesu alisema kwamba wale wenye matatizo ya kimwili wanahitaji daktari. (Mathayo 9:12) Bila shaka, inafaa sikuzote kusali kwa Yehova kuhusu matatizo yoyote, kutia ndani ya afya. (Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7) Lakini, Biblia haisemi kwamba matatizo ya kiafya yanaweza kusuluhishwa tu kwa kuongeza utendaji wa kiroho.

      Hivyo, Wakristo wenye utambuzi huepuka kudokeza kwamba watu walioshuka moyo wamejiletea matatizo. Matamshi kama hayo ni kama yale ya watu waliodai kumfariji Ayubu lakini hawakumsaidia. (Ayubu 8:1-6) Ukweli ni kwamba mara nyingi ugonjwa wa kushuka moyo hauwezi kupona bila matibabu, hasa ikiwa mgonjwa ameshuka moyo sana na hata anataka kujiua. Katika hali kama hizo, daktari anahitajika.

      Isitoshe, kuna mambo ambayo Wakristo wenzetu wanaweza kufanya ili kusaidia. Bila shaka, subira inahitajiwa. Kwa mfano, shughuli fulani za Kikristo zinaweza kuwashinda watu wenye magonjwa ya kihisia. Diane, mwenye hisia zinazobadilika-badilika, anasema: “Ni vigumu kwangu kuhubiri. Ni vigumu kuwapelekea wengine habari njema zenye furaha kutoka kwa Biblia nikiwa sijisikii vizuri na sina furaha.”

      Ili uwasaidie wagonjwa hao, jitahidi kuwa mwenye huruma. (1 Wakorintho 10:24; Wafilipi 2:4) Jaribu kuona mambo kama mgonjwa anavyoyaona. Usimlemee mgonjwa kwa kumtarajia afanye mengi. Carl, ambaye ameshuka moyo, anasema: “Watu wasipotarajia mengi kutoka kwangu, pole kwa pole mimi huanza kujiheshimu. Kwa msaada wa marafiki wenye umri mkubwa nimeweza kujenga uhusiano wa karibu na Mungu na nimepata furaha nyingi sana kwa kuwasaidia wengine wafanye hivyo.”

      Wagonjwa wanaweza kupata kitulizo kikubwa wakisaidiwa. Fikiria mfano wa mwanamke Mkristo anayeitwa Brenda ambaye pia ana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Anasema: “Marafiki wangu kutanikoni wamenisaidia na kunijali ninaposhuka moyo badala ya kunishutumu kuwa dhaifu kiroho. Mara nyingi wameniruhusu tuandamane kwenye utumishi na kuacha nisikilize tu au kunihifadhia kiti kwenye Jumba la Ufalme ili niingie wakati ambapo watu wote wameketi.”

      Cherie, ambaye ameshuka moyo na alitajwa katika makala iliyotangulia, pia amesaidiwa sana na wazee wa kutaniko wenye upendo na wanaojali. Anasema: “Wazee hunihakikishia kwamba Yehova ananipenda na hunisomea Neno la Mungu, Biblia, na kunieleza juu ya kusudi la Yehova la kuleta paradiso yenye amani na afya bora. Wanaposali nami hata kwenye simu, mimi hujihisi vizuri. Ninajua kwamba Yehova na ndugu zangu hawajanitupa na hilo huniimarisha.”

      Hakuna shaka kwamba watu wa familia na marafiki wanaweza kumsaidia sana mgonjwa ajihisi vizuri. Lucia anasema: “Sasa naona ninaweza kudhibiti maisha yangu. Mimi na mume wangu tumejitahidi kukabiliana na hali hiyo, na sasa hali ni afadhali sana.”

      Wengi ambao wamepambana na magonjwa ya akili wametambua kwamba hilo ni pambano la muda mrefu. Hata hivyo, Biblia inaahidi kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Hakutakuwa na magonjwa yenye kutaabisha ambayo yanawakumba watu wengi leo. Inachangamsha moyo sana kufikiria ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya ambapo magonjwa yote, kutia ndani ya kihisia, yatatokomea kabisa. Biblia inasema kwamba wakati huo hakutakuwa maombolezo wala kilio wala maumivu.—Ufunuo 21:4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki