-
Kuishi na Ugonjwa wa KihisiaAmkeni!—2004 | Januari 8
-
-
Hisia Zinazobadilika-Badilika
Ugonjwa wa kushuka moyo hutatiza sana. Lakini iwapo pia mtu aliyeshuka moyo anasisimuka kupita kiasi, huwa anaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika.c Lucia anayeugua ugonjwa huo anasema: “Hisia za mtu anayeugua ugonjwa huo hubadilika-badilika daima.” Jarida The Harvard Mental Health Letter linasema kwamba katika kipindi cha kusisimuka kupita kiasi, mgonjwa “anaweza kuingilia mambo ya wengine na kuwatawala, na ghafula anaweza kushikwa na hasira.”
Lenore anakumbuka wakati aliposisimuka kupita kiasi. Anasema: “Nilikuwa na nguvu nyingi sana. Wengine waliniona kuwa mwanamke shujaa. Watu wengine waliniambia, ‘Laiti ningekuwa kama wewe.’ Mara nyingi nilijihisi nikiwa na nguvu nyingi sana, kana kwamba ningeweza kufanya jambo lolote. Nilifanya mazoezi kupita kiasi. Nilifanya kazi kila siku ijapokuwa nililala kwa muda mfupi sana—kwa saa mbili au tatu tu. Lakini, bado niliamka nikiwa na nguvu nyingi.”
Hata hivyo, baada ya muda Lenore akaanza kushuka moyo. Anasema: “Kipindi cha msisimuko kilipofikia upeo, nilihisi hasira kutoka ndani kama mashine iliyokuwa ikiendeshwa bila kuzimwa. Kwa ghafula, hisia zangu nzuri zikabadilika, nikawa mkali na mjeuri. Niliwafokea washiriki wa familia bila sababu. Nilikuwa mwenye hasira, mwenye chuki, na singejizuia hata kidogo. Baada ya hisia hizo zenye kutisha, nilichoka ghafula, nikalia, na kushuka moyo sana. Nilihisi kuwa mwovu na asiyefaa kitu. Wakati mwingine, ningebadilika na kuwa mchangamfu kama zamani kana kwamba hakuna kitu kilichokuwa kimetukia.”
Hisia zinazobadilika-badilika za mgonjwa huwavuruga washiriki wa familia. Mary, ambaye mume wake ana ugonjwa huo anasema hivi: “Mimi huvurugika ninapomwona mume wangu akiwa mwenye furaha na akiongea sana halafu ghafula anabadilika na kushuka moyo na kunyamaza. Ni vigumu sana kwetu kuamini kwamba hawezi kujizuia.”
Ni kweli kwamba mgonjwa hutaabishwa zaidi na ugonjwa huo. Mgonjwa mmoja anayeitwa Gloria anasema hivi: “Mimi hutamani niwe kama watu wanaoweza kudhibiti maisha yao. Ni mara chache tu ambapo wagonjwa wenye hisia zinazobadilika-badilika huishi maisha ya kawaida.”
Ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika husababishwa na nini? Ni rahisi zaidi mtu arithi ugonjwa huo kuliko ule wa kushuka moyo. Chama cha Kitiba cha Marekani kinasema: “Kulingana na uchunguzi wa kisayansi, watu wa karibu zaidi wa familia, yaani wazazi, ndugu, dada, au watoto wa watu wenye ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika wako katika hatari ya kupatwa na ugonjwa huo mara 8 mpaka 18 zaidi ya watu wanaotoka katika familia zisizo na ugonjwa huo. Isitoshe, kuna uwezekano mkubwa wa kushuka moyo sana ikiwa mtu wa familia ana ugonjwa huo.”
Tofauti na kushuka moyo, inaonekana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika huwapata wanaume na wanawake kwa kiwango kilekile. Ijapokuwa mara nyingi ugonjwa huo huanza mtu anapokuwa mtu mzima, vijana na watoto wamepatikana na ugonjwa huo. Hata hivyo, kuchunguza dalili na kuutambua ugonjwa huo ni jambo gumu sana hata kwa wataalamu wa tiba. Dakt. Francis Mark Mondimore wa Chuo cha Tiba katika Chuo Kikuu cha Johns Hopkins, anaandika hivi: “Ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika ni ugonjwa wa akili unaobadilika kama kinyonga kwani dalili za wagonjwa hutofautiana na hata kipindi kimoja cha ugonjwa hutofautiana na kingine kwa mgonjwa yuleyule. Ugonjwa huo ni kama zimwi linalosababisha hofu nyingi na kutoweka, kisha hutokea tena kwa kishindo baada ya miaka mingi na kumfanya mgonjwa asisimuke kupita kiasi.”
-
-
Kuishi na Ugonjwa wa KihisiaAmkeni!—2004 | Januari 8
-
-
c Madaktari wanasema kwamba mara nyingi kila hisia huendelea kwa miezi mingi. Hata hivyo, wanasema kwamba hisia za wagonjwa fulani hubadilika haraka-haraka mara kadhaa kwa mwaka. Hisia za wagonjwa wachache hubadilika-badilika katika kipindi cha saa 24.
-