Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tumaini kwa Wanaougua
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Iwapo ugonjwa huo umesababishwa na kasoro ya kemikali mwilini, huenda ukaandikiwa dawa. Katika visa fulani, huenda mgonjwa akapewa mashauri ya kumsaidia akabiliane na hali hiyo. Nyakati nyingine, njia zote mbili zimetumiwa kwa matokeo.a Jambo la maana ni kutafuta na kupata msaada. Lenore, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika aliyetajwa katika makala iliyotangulia, anasema: “Mara nyingi wagonjwa huogopa na kuaibika kwa sababu ya hali yao. Hata hivyo, mtu huaibika zaidi anapojua ana tatizo na hatafuti msaada anaohitaji sana.”

      Lenore anaelezea hali yake hivi: “Nililala kwa mwaka mmoja hivi. Kisha, siku moja nilipojihisi nina nguvu kidogo, niliamua kumwona daktari.” Lenore alipimwa na kupatikana na ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika, na kupewa matibabu. Hilo lilibadilisha maisha yake. Lenore anasema: “Mimi hujihisi vizuri ninapotumia dawa, ingawa ninahitaji kujikumbusha kwamba nikiacha kuzitumia ugonjwa utarudi.”

  • Tumaini kwa Wanaougua
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Lucia, aliyetajwa mapema katika mfululizo huu wa makala, anathamini sana matibabu mazuri ambayo amepata. Anasema: “Daktari amenisaidia sana kujua jinsi ya kushughulikia hisia zangu zinazobadilika-badilika.” Lucia pia anakazia umuhimu wa kupumzika. Anasema hivi: “Usingizi ni wa maana sana katika kushughulika na msisimuko wa kupita kiasi. Ninapokosa kulala vizuri, msisimuko unaongezeka. Nimejizoeza kupumzika kitandani hata kama sipati usingizi.”

      Sheila, aliyetajwa mapema pia, amefaidika kwa kuandika jinsi anavyohisi kila siku katika kitabu. Mtazamo wake umebadilika sana. Lakini bado anapata magumu fulani. Sheila anasema: “Kwa sababu fulani, uchovu hunifanya niathiriwe na mawazo mabaya. Lakini nimejua kuyakomesha au angalau kuyapunguza.”

      Kufarijiwa na Neno la Mungu

      Biblia huwaimarisha wengi walio na ‘fikira zinazofadhaisha.’ (Zaburi 94:17-19, 22) Kwa mfano, Cherie alisema kwamba andiko la Zaburi 72:12, 13 lilimsaidia sana. Hapo mtunga-zaburi anasema hivi kuhusu Mfalme aliyewekwa na Mungu, Yesu Kristo: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini.” Cherie pia ametiwa moyo na maneno ya mtume Paulo kwenye Waroma 8:38, 39: “Nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu.”

      Elaine, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika, ameimarishwa kwa sababu ana uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Yeye hufarijiwa sana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Moyo uliovunjika na kupondwa, Ee Mungu, hutaudharau.” (Zaburi 51:17) Anasema: “Nimefarijiwa kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova, ananielewa. Nimeimarishwa kwa kumkaribia katika sala, hasa ninapofadhaika na kusononeka sana.”

      Kama tulivyoona, ni vigumu kuishi na ugonjwa wa kihisia. Hata hivyo, Cherie na Elaine wamegundua kwamba kumtegemea Mungu katika sala na kupata matibabu yanayofaa kumewawezesha waboreshe maisha yao. Watu wa familia na marafiki wanaweza kuwasaidiaje watu wanaougua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika au wa kushuka moyo?

  • Tumaini kwa Wanaougua
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      Maoni ya Mwenzi wa Ndoa

      “Kabla Lucia hajawa mgonjwa, wengine walivutiwa na hekima yake. Hata sasa watu wanapomtembelea mke wangu wakati ambapo ametulia, wao huvutiwa na uchangamfu wake. Lakini wengi hawajui kwamba nyakati nyingine Lucia hushuka moyo halafu anasisimuka kupita kiasi. Hiyo ni dalili ya ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika ambao ameugua kwa miaka minne iliyopita.

      “Anaposisimuka, mara nyingi yeye hukaa macho hadi saa saba, saa nane, au hata saa tisa usiku akiwaza na kuwazua. Yeye huwa na nguvu nyingi sana. Yeye huhangaishwa na mambo madogo sana na kutumia pesa vibaya. Yeye hujiingiza kwenye hatari kubwa sana, akifikiri kwamba hawezi kuathiriwa kiadili, kimwili, au vinginevyo. Hali hiyo ya kusisimuka kupita kiasi inaweza kumfanya atake kujiua. Baadaye msisimuko huo hufuatwa na kushuka moyo kwa kiwango kilekile cha msisimuko.

      “Maisha yangu yamebadilika sana. Hata ingawa Lucia anapata matibabu, yale tunayoweza kutimiza leo ni tofauti na yale tuliyotimiza zamani au tutakayotimiza wakati ujao. Mambo hayo hubadilika kulingana na hali zetu. Imenibidi nibadilike sana.”—Mario.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

      Mgonjwa Anapopewa Dawa

      Wengine hufikiri kwamba kutumia dawa ni udhaifu. Lakini wazia jambo hili: Mtu mwenye ugonjwa wa kisukari anahitaji kutumia dawa, kutia ndani kujichoma sindano za insulini. Je, inamaanisha kwamba mtu huyo ni dhaifu? La, hasha! Hiyo ni njia ya kusawazisha kemikali mwilini mwa mgonjwa ili aendelee kuwa na afya.

      Ndivyo ilivyo pia na matibabu ya ugonjwa wa kushuka moyo au wa hisia zinazobadilika-badilika. Ingawa watu wengi wamefaidika kutokana na ushauri ambao umewasaidia kuelewa ugonjwa wao, inafaa kutahadhari. Ikiwa kemikali za mwili zinahusika, ugonjwa huo hauwezi kumalizwa kwa mashauri. Steven, anayeugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika anasimulia: “Daktari aliyenitibu alitumia mfano huu: Unaweza kumfundisha sana mtu fulani kuendesha gari, lakini ukimpa gari ambalo halina usukani au breki, basi mafunzo hayo hayatamsaidia. Vivyo hivyo, huenda mashauri pekee yasimsaidie mtu aliyeshuka moyo. Hatua ya kwanza ni kusawazisha kemikali za ubongo.”

  • Wengine Wanaweza Kusaidiaje?
    Amkeni!—2004 | Januari 8
    • Wengine Wanaweza Kusaidiaje?

      LABDA unamjua mtu anayeugua ugonjwa wa kushuka moyo au wa hisia zinazobadilika-badilika. Ikiwa ndivyo, unawezaje kumtegemeza? D. J. Jaffe wa Shirika la Kitaifa la Wagonjwa wa Akili anashauri hivi: “Tofautisha ugonjwa na mgonjwa; chukia ugonjwa lakini umpende mgonjwa.”

      Kwa sababu ya kuwa na subira na upendo, mwanamke anayeitwa Susanna alifaulu kufanya hivyo. Rafiki yake aliugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Susanna anasema: “Nyakati nyingine hata hakutaka kuniona.” Badala ya kukata tamaa, Susanna alifanya utafiti ili aufahamu ugonjwa huo. Anasema: “Sasa natambua jinsi rafiki yangu alivyoathiriwa na ugonjwa wake.” Susanna anasema kwamba kuna faida kubwa kumwelewa mgonjwa. Anasema: “Jambo hilo linaweza kukusaidia kupenda na kuthamini zaidi sifa nzuri za mgonjwa.”

      Ikiwa anayeugua ni mshiriki wa familia, anahitaji kutiwa moyo sana. Mario, aliyetajwa katika makala zilizotangulia, alijifunza jambo hilo mapema. Mke wake, Lucia, ambaye pia alitajwa mapema, anaugua ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Mario anasema: “Mwanzoni, nilifaidika kwa kuandamana na mke wangu alipoenda kumwona daktari na kujifunza kuhusu ugonjwa huo wa ajabu ili nifahamu jambo ambalo tunakabili. Mimi na Lucia tulizungumza sana na tukashughulikia hali yoyote iliyotokea.”

      Utegemezo wa Kutaniko la Kikristo

      Biblia huwashauri Wakristo wote ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika’ na ‘kuwa wenye ustahimilivu kuelekea wote.’ (1 Wathesalonike 5:14) Unawezaje kufanya hivyo? Kwanza, ni muhimu kuelewa tofauti kati ya ugonjwa wa akili na wa kiroho. Kwa mfano, mwandikaji wa Biblia Yakobo alisema kwamba sala inaweza kumsaidia mtu mwenye ugonjwa wa kiroho apone. (Yakobo 5:14, 15) Hata hivyo, Yesu alisema kwamba wale wenye matatizo ya kimwili wanahitaji daktari. (Mathayo 9:12) Bila shaka, inafaa sikuzote kusali kwa Yehova kuhusu matatizo yoyote, kutia ndani ya afya. (Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7) Lakini, Biblia haisemi kwamba matatizo ya kiafya yanaweza kusuluhishwa tu kwa kuongeza utendaji wa kiroho.

      Hivyo, Wakristo wenye utambuzi huepuka kudokeza kwamba watu walioshuka moyo wamejiletea matatizo. Matamshi kama hayo ni kama yale ya watu waliodai kumfariji Ayubu lakini hawakumsaidia. (Ayubu 8:1-6) Ukweli ni kwamba mara nyingi ugonjwa wa kushuka moyo hauwezi kupona bila matibabu, hasa ikiwa mgonjwa ameshuka moyo sana na hata anataka kujiua. Katika hali kama hizo, daktari anahitajika.

      Isitoshe, kuna mambo ambayo Wakristo wenzetu wanaweza kufanya ili kusaidia. Bila shaka, subira inahitajiwa. Kwa mfano, shughuli fulani za Kikristo zinaweza kuwashinda watu wenye magonjwa ya kihisia. Diane, mwenye hisia zinazobadilika-badilika, anasema: “Ni vigumu kwangu kuhubiri. Ni vigumu kuwapelekea wengine habari njema zenye furaha kutoka kwa Biblia nikiwa sijisikii vizuri na sina furaha.”

      Ili uwasaidie wagonjwa hao, jitahidi kuwa mwenye huruma. (1 Wakorintho 10:24; Wafilipi 2:4) Jaribu kuona mambo kama mgonjwa anavyoyaona. Usimlemee mgonjwa kwa kumtarajia afanye mengi. Carl, ambaye ameshuka moyo, anasema: “Watu wasipotarajia mengi kutoka kwangu, pole kwa pole mimi huanza kujiheshimu. Kwa msaada wa marafiki wenye umri mkubwa nimeweza kujenga uhusiano wa karibu na Mungu na nimepata furaha nyingi sana kwa kuwasaidia wengine wafanye hivyo.”

      Wagonjwa wanaweza kupata kitulizo kikubwa wakisaidiwa. Fikiria mfano wa mwanamke Mkristo anayeitwa Brenda ambaye pia ana ugonjwa wa hisia zinazobadilika-badilika. Anasema: “Marafiki wangu kutanikoni wamenisaidia na kunijali ninaposhuka moyo badala ya kunishutumu kuwa dhaifu kiroho. Mara nyingi wameniruhusu tuandamane kwenye utumishi na kuacha nisikilize tu au kunihifadhia kiti kwenye Jumba la Ufalme ili niingie wakati ambapo watu wote wameketi.”

      Cherie, ambaye ameshuka moyo na alitajwa katika makala iliyotangulia, pia amesaidiwa sana na wazee wa kutaniko wenye upendo na wanaojali. Anasema: “Wazee hunihakikishia kwamba Yehova ananipenda na hunisomea Neno la Mungu, Biblia, na kunieleza juu ya kusudi la Yehova la kuleta paradiso yenye amani na afya bora. Wanaposali nami hata kwenye simu, mimi hujihisi vizuri. Ninajua kwamba Yehova na ndugu zangu hawajanitupa na hilo huniimarisha.”

      Hakuna shaka kwamba watu wa familia na marafiki wanaweza kumsaidia sana mgonjwa ajihisi vizuri. Lucia anasema: “Sasa naona ninaweza kudhibiti maisha yangu. Mimi na mume wangu tumejitahidi kukabiliana na hali hiyo, na sasa hali ni afadhali sana.”

      Wengi ambao wamepambana na magonjwa ya akili wametambua kwamba hilo ni pambano la muda mrefu. Hata hivyo, Biblia inaahidi kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Hakutakuwa na magonjwa yenye kutaabisha ambayo yanawakumba watu wengi leo. Inachangamsha moyo sana kufikiria ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya ambapo magonjwa yote, kutia ndani ya kihisia, yatatokomea kabisa. Biblia inasema kwamba wakati huo hakutakuwa maombolezo wala kilio wala maumivu.—Ufunuo 21:4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki