Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Mungu Anatuadhibu?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 1
    • Je, Mungu Anatuadhibu?

      “Nafikiri hii ni tembatsu (adhabu kutoka kwa Mungu), ingawa ninawasikitikia watu walioathiriwa na msiba huo,” akasema kiongozi mmoja wa kisiasa nchini Japani baada ya nchi hiyo kukumbwa na tsunami na tetemeko la ardhi la kipimo cha 9.0 mwezi wa Machi 2011.

      Baada ya watu zaidi ya 220,000 kufa katika tetemeko la ardhi nchini Haiti mwezi wa Januari 2010, kasisi fulani maarufu, anayehubiri kwenye televisheni, alidai kwamba watu hao walikufa kwa sababu “walikuwa wamefanya mkataba na ibilisi” na walihitaji “kumrudia mungu.”

      “Mungu anataka kuamsha dhamiri zetu zilizokufa ganzi,” akatangaza kasisi mmoja Mkatoliki wakati watu 79 walipokufa katika msongamano wa watu huko Manila, Ufilipino. Gazeti moja nchini humo lilisema kwamba “asilimia 21 ya watu wazima wanaamini kwamba Mungu anaonyesha hasira yake kupitia maporomoko ya ardhi, vimbunga na misiba mingine” inayotokea mara kwa mara katika nchi hiyo.

      WAZO la kwamba Mungu anatumia misiba kuwaadhibu watu wabaya si jipya. Mwaka wa 1755, baada ya watu 60,000 hivi kuangamizwa na tetemeko la ardhi, moto, na tsunami iliyokumba jiji la Lisbon, Ureno, mwanafalsafa maarufu Voltaire aliuliza: “Je, uovu ulikuwa umejaa Lisbon, kuliko Paris, ambako watu wanajifurahisha sana kwa anasa zilizopotoka?” Kwa kweli, mamilioni ya watu wamejiuliza kama Mungu anatumia misiba ya asili kuwaadhibu watu. Katika nchi nyingi, misiba hiyo inaitwa kazi ya Mungu.

      Kwa kuzingatia hali hizo, tunahitaji kujiuliza: Je, kweli Mungu amekuwa akitumia misiba ya asili kuwaadhibu watu? Je, kuongezeka kwa misiba katika nyakati za hivi karibuni ni adhabu kutoka kwa Mungu?

      Wanapokimbilia kumlaumu Mungu, wengine wanataja masimulizi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Mungu alivyoleta uharibifu akitumia nguvu za asili. (Mwanzo 7:17-22; 18:20; 19:24, 25; Hesabu 16:31-35) Hata hivyo, tunapochunguza kila tukio katika masimulizi hayo ya Biblia, tunaona mambo matatu ya pekee. Kwanza, onyo lilitolewa mapema. Pili, tofauti na misiba ya asili inayotokea leo, ambayo inasababisha vifo vya watu wazuri kwa wabaya, uharibifu uliosababishwa na Mungu ulitenganisha wazuri na wabaya. Watu waovu kabisa au wale waliokataa kusikiliza maonyo ndio tu walioangamizwa. Tatu, Mungu aliandaa njia ili watu wasio na hatia waponyoke.—Mwanzo 7:1, 23; 19:15-17; Hesabu 16:23-27.

      Katika misiba mingi sana ambayo imesababisha vifo vya mamilioni ya watu leo, hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba Mungu ndiye anayeisababisha. Basi, kwa nini misiba hiyo imeongezeka sana? Tunawezaje kukabiliana nayo? Na je, kuna wakati ambapo misiba haitakuwapo tena? Utapata majibu katika makala zinazofuata.

  • Kukabiliana na Misiba ya Asili
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 1
    • Kukabiliana na Misiba ya Asili

      Kwa kuwa misiba ya asili inatokea mara nyingi na kusababisha uharibifu mkubwa, mtu anaweza kufanya nini ili kukabiliana nayo? Acheni tuzungumzie hatua fulani ambazo mtu anaweza kuchukua.

      Epuka maeneo hatari.

      Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Methali 22:3) Shauri hilo la hekima linaweza kutumiwa kuhusiana na misiba. Onyo linapotolewa kuhusu mlima wa volkano unaokaribia kulipuka, mafuriko, au kimbunga kinachokuja, wale wanaoishi katika eneo linalokabili hatari wanapaswa kutenda kwa hekima kwa kuhamia maeneo yaliyo salama. Uhai ni wenye thamani kuliko nyumba au vitu vya kimwili.

      Huenda inawezekana kwa watu fulani kuamua kwamba hawataishi katika eneo hatari. Ripoti fulani ya utafiti inasema: “Maeneo fulani yanakabili hatari kubwa zaidi ya kukumbwa na misiba. Ni sehemu ndogo sana ya Dunia ambayo ina maeneo hayo hatari na misiba mingi mikubwa ya wakati ujao itatokea katika maeneo hayo.” Kwa mfano, inaweza kuwa hivyo katika maeneo tambarare ya pwani au maeneo yanayokabili hatari ya matetemeko ya ardhi. Ikiwa unaweza kuepuka kuishi katika maeneo hayo au kuhamia eneo lililo salama zaidi, huenda ukapunguza sana hatari ya kupatwa na misiba.

      Jitayarishe kwa ajili ya msiba.

      Hata ingawa unaweza kuchukua hatua zote zinazohitajiwa, huenda bado ukapatwa na msiba usiotazamia. Unaweza kukabiliana kwa urahisi na msiba huo ikiwa umejitayarisha mapema. Hatua hiyo inapatana pia na shauri ambalo limetajwa kwenye Methali 22:3. Je, una mfuko wa dharura ulio na vitu vya kutumia wakati wa msiba? Kitabu kimoja (1-2-3 of Disaster Education) kinapendekeza kwamba mfuko huo uwe na vitu vifuatavyo: Vifaa vya huduma ya kwanza, chupa zilizo na maji, vyakula visivyoharibika upesi, na hati muhimu. Huenda pia ikawa jambo la hekima kuzungumzia pamoja na familia yako aina ya misiba ambayo inaweza kutokea na hatua mnazoweza kuchukua msiba ukitokea.

      Dumisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.

      Hilo linaweza kukusaidia katika hali yoyote ile. Biblia inamwita Mungu “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” Andiko lingine linamfafanua kuwa Mungu “ambaye huwafariji wale walioshushwa chini.”—2 Wakorintho 1:3, 4; 7:6.

      Ndiyo, Mungu anaelewa vizuri hali zinazowapata wote wanaomwamini. Ni Mungu mwenye upendo na anatutia moyo kwa njia mbalimbali. (1 Yohana 4:8) Tunaposali kwa Mungu ili tupate roho takatifu, bali si miujiza, roho hiyo inaweza kutusaidia katika hali yoyote ile. Roho takatifu inaweza kutukumbusha masimulizi ya Biblia ambayo yanaweza kutufariji na kututuliza tunapopatwa na misiba. Kwa kweli, watumishi waaminifu wa Mungu wanaweza kuhisi kama Daudi, mfalme wa Israeli la kale, aliyesema: “Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya, kwa maana wewe uko pamoja nami; fimbo yako na gongo lako ndivyo vitu vinavyonifariji.”—Zaburi 23:4.

      Tunaposali kwa Mungu ili tupate roho takatifu, bali si miujiza, roho hiyo inaweza kutusaidia katika hali yoyote ile

      Wakristo husaidiana.

      Katika karne ya kwanza nabii Mkristo aliyeitwa Agabo alisema kwamba “njaa kali ilikuwa karibu kuja juu ya dunia nzima inayokaliwa; ambayo, kama ilivyo, ilitukia wakati wa Klaudio.” Njaa hiyo iliwaathiri sana wanafunzi wengi wa Yesu huko Yudea. Wanafunzi waliokuwa katika maeneo mengine walifanya nini waliposikia kuhusu hali ngumu iliyowapata Wakristo wenzao? Simulizi linasema: “Wanafunzi wakaamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, wafanye huduma ya kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea.” (Matendo 11:28, 29) Kwa upendo, walitoa misaada ili kushughulikia hali hiyo.

      Leo, misiba mibaya inapotokea, watumishi wa Mungu wanatenda kwa njia hiyohiyo. Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa kuwasaidia waamini wenzao. Kwa mfano, tetemeko kubwa la ardhi lilipotokea huko Chile, mnamo Februari 27, 2010, Mashahidi wa Yehova walichukua hatua haraka ili kuwasaidia wale walioathiriwa. Karla, ambaye nyumba yake ilisombwa na tsunami, anaeleza: “Nilifarijiwa na kutiwa moyo kuona kwamba asubuhi iliyofuata [Mashahidi wenzetu] waliwasili kutoka maeneo mengine ili kutusaidia. Bila shaka, Yehova alitufariji kupitia wema tulioonyeshwa na wajitoleaji hao. Nilihisi kwamba ninapendwa na kulindwa.” Babu yake, ambaye si Shahidi, aliona msaada uliotolewa. Alisema: “Wametenda kwa njia tofauti kabisa na jinsi ambavyo nimeona kwa miaka mingi katika kanisa langu.” Jambo hilo lilimchochea kuwaomba Mashahidi wa Yehova wajifunze Biblia pamoja naye.

      Wakristo husaidiana ili wakabiliane na madhara yanayosababishwa na misiba

      Kushirikiana na watu wanaompenda Mungu kunaweza kutusaidia sana wakati wa taabu. Hata hivyo, je, kuna wakati ambapo watu hawatateseka tena duniani kwa sababu ya misiba? Acheni tuone Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo.

  • Misiba Itakwisha Hivi Karibuni!
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 1
    • Misiba Itakwisha Hivi Karibuni!

      IKIWA mtu fulani angekuambia, “Misiba itakwisha hivi karibuni,” ungetendaje? Huenda ukamjibu, “Wewe unaota. Misiba ni sehemu ya maisha.” Au huenda ukawaza, ‘Anafikiri anaweza kunidanganya?’

      Ingawa inaonekana kuwa misiba itaendelea kuwepo, kuna msingi wa kuwa na tumaini hakika kwamba mambo yatabadilika. Hata hivyo, mabadiliko hayo hayataletwa na wanadamu. Wanadamu hawawezi kuelewa kikamili jinsi mambo yanavyotokea au kwa nini yanatokea kiasili, na pia hawawezi kuyazuia au kuyabadili. Mfalme Sulemani wa Israeli la kale, ambaye alijulikana kwa sababu ya hekima yake na kuchunguza mambo kwa makini aliandika: “Wanadamu hawawezi kuvumbua kazi ambayo imefanywa chini ya jua; lakini hata wanadamu waendelee namna gani kufanya kazi kwa bidii kutafuta, bado hawagundui. Na hata wakisema kwamba wana hekima ya kutosha kuweza kujua, hawawezi kuvumbua.”—Mhubiri 8:17.

      Ikiwa wanadamu hawawezi kuzuia misiba ya asili, ni nani anayeweza? Biblia inasema kwamba Muumba wetu ndiye anayeweza kuleta mabadiliko hayo. Yeye ndiye aliyeumba mifumo ya kimazingira duniani, kama vile mzunguko wa maji. (Mhubiri 1:7) Na kinyume na wanadamu, Mungu ana nguvu nyingi zisizo na mipaka. Akithibitisha jambo hilo, nabii Yeremia alisema: “Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama, wewe mwenyewe umeziumba mbingu na dunia kwa nguvu zako kuu na kwa mkono wako ulionyooshwa. Jambo hilo lote si la ajabu mno kwako.” (Yeremia 32:17) Kwa kuwa Mungu aliumba dunia na vitu vyake vya asili, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba anajua jinsi ya kuongoza mambo ili watu waishi duniani kwa amani na usalama.—Zaburi 37:11; 115:16.

      Basi, Mungu ataletaje mabadiliko yanayohitajiwa? Kumbuka kuwa makala ya pili katika mfululizo huu ilitaja kwamba mambo mengi yenye kutisha ambayo yanatukia duniani leo yanafanyiza “ishara” inayoonyesha “umalizio wa mfumo wa mambo.” Yesu alisema: “Mnapoona mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.” (Mathayo 24:3; Luka 21:31) Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali ya mbinguni iliyofanyizwa na Mungu, utaleta mabadiliko makubwa duniani, hata utadhibiti nguvu za asili. Ingawa Yehova Mungu ana uwezo wa kufanya jambo hilo, ameamua kumpa Mwana wake kazi hiyo. Nabii Danieli alisema hivi kumhusu: “Naye akapewa utawala na heshima na ufalme, ili vikundi vyote vya watu, vya mataifa na lugha vimtumikie yeye.”—Danieli 7:14.

      Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, amepewa nguvu za kutosha kuleta mabadiliko yote yanayohitajiwa ili kufanya dunia iwe mahali penye kupendeza. Yesu alipokuwa duniani miaka elfu mbili hivi iliyopita, alionyesha kwa kiwango kidogo uwezo wake wa kudhibiti nguvu za asili. Pindi moja, yeye na wanafunzi wake walipokuwa ndani ya mashua kwenye Bahari ya Galilaya, ‘kulitokea dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi, na mawimbi yakawa yakiipiga mashua kwa nguvu, hivi kwamba karibu mashua ifunikwe na maji.’ Wanafunzi wake waliingiwa na hofu na wakaanza kumlilia Yesu kwa sababu waliogopa kufa. Yesu alifanya nini? ‘Aliukemea upepo na kuiambia bahari: “Nyamaza, utulie!” Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.’ Wanafunzi wake walishangaa na kuuliza: “Kwa kweli huyu ni nani, kwa sababu hata upepo na bahari zinamtii?”—Marko 4:37-41.

      Tangu wakati huo, Yesu ameinuliwa na kwenda mbinguni na amepewa mamlaka na nguvu nyingi zaidi. Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, ana jukumu na pia uwezo wa kuhakikisha kwamba watu wanaishi kwa amani na usalama duniani.

      Hata hivyo, kama tulivyoona, matatizo na misiba mingi inatokana na wanadamu, yaani, inasababishwa au kufanywa iwe mibaya zaidi na shughuli za watu wenye ubinafsi na pupa. Ufalme huo utawachukulia hatua gani wale wanaoendelea na shughuli hizo na kukataa kubadilika? Biblia inasema kwamba Bwana Yesu atakuja “kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” Ndiyo, ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’—2 Wathesalonike 1:7, 8; Ufunuo 11:18.

      Baadaye, ‘Mfalme huyo wa wafalme,’ Yesu Kristo, atadhibiti kabisa nguvu za asili za dunia. (Ufunuo 19:16) Atahakikisha kwamba raia wa Ufalme hawatateseka tena kwa sababu ya msiba wowote. Atatumia uwezo wake kuongoza nguvu za asili ili hali ya hewa na majira mbalimbali yawafaidi wanadamu. Matokeo ni kwamba jambo ambalo Yehova Mungu aliwaahidi watu wake zamani za kale litatimia: “Hakika mimi pia nitawapa ninyi manyunyu yenu ya mvua wakati wake unaofaa, nayo nchi itatoa mazao yake, nao mti wa shambani utatoa matunda yake.” (Mambo ya Walawi 26:4) Watu watajenga nyumba bila kuogopa kwamba watazipoteza katika msiba fulani: “Na hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.”—Isaya 65:21.

      Unapaswa Kufanya Nini?

      Bila shaka, kama watu wengine wengi, wewe pia unavutiwa na ahadi ya kuishi katika ulimwengu usio na misiba inayosababisha uharibifu. Hata hivyo, unapaswa kufanya nini ili uishi katika ulimwengu huo? Kwa kuwa “wale wasiomjua Mungu” na “wale wasiotii habari njema” hawatastahili kuishi katika ulimwengu huo usio na misiba ambao utakuja, ni wazi kwamba ni lazima mtu ajifunze sasa kumhusu Mungu na kuunga mkono mpango wake wa kuitawala dunia. Mungu anataka tumjue na kutii habari njema za Ufalme ambao amesimamisha kupitia Mwana wake.

      Kujifunza Biblia kwa makini ndiyo njia bora ya kufanya hivyo. Biblia ina miongozo inayoweza kumsaidia mtu astahili kuishi katika mazingira salama ambayo yatakuwapo chini ya utawala wa Ufalme. Tunakutia moyo uwaombe Mashahidi wa Yehova wakusaidie kujifunza mambo ambayo Biblia inafundisha. Wako tayari kufanya hivyo. Jambo moja ni hakika—ukijitahidi kumjua Mungu na kutii habari njema, basi maneno ya Methali 1:33 yatathibitika kuwa ya kweli kwako: “Kwa habari yake mtu anayenisikiliza, yeye atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki