-
Sitawisha Sifa Zinazoweza Kukusaidia Kufanya WanafunziMnara wa Mlinzi—2007 | Novemba 15
-
-
Sitawisha Sifa Zinazoweza Kukusaidia Kufanya Wanafunzi
“Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—MATHAYO 28:19.
1. Watumishi fulani wa Mungu nyakati za kale walihitaji kusitawisha ustadi na mitazamo gani?
NYAKATI nyingine, ni lazima watumishi wa Yehova wasitawishe ustadi na mitazamo ambayo itawasaidia kufanya mapenzi yake. Kwa mfano, kwa kutii amri ya Mungu, Abrahamu na Sara walitoka jiji la Uru lenye ufanisi na baadaye wakahitaji kusitawisha sifa na uwezo mbalimbali ambao watu walioishi ndani ya mahema walistahili kuwa nao. (Waebrania 11:8, 9, 15) Ili kuwaongoza Waisraeli katika Nchi ya Ahadi, Yoshua alihitaji ujasiri, kumtegemea Yehova, na kujua Sheria yake. (Yoshua 1:7-9) Na ustadi wowote ambao huenda tayari Bezaleli na Oholiabu walikuwa nao, uliboreshwa au kuongezwa na roho ya Mungu ili wanaume hao washiriki na kusimamia kwa mafanikio ujenzi wa maskani na kazi iliyohusiana nayo.—Kutoka 31:1-11.
2. Tutazungumzia maswali gani yanayohusiana na kazi ya kufanya wanafunzi?
2 Karne nyingi baadaye, Yesu Kristo aliwaagiza hivi wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kabla ya hapo, watu hawakuwa wamepewa pendeleo la kufanya kazi kubwa kama hiyo. Ni sifa gani zinazohitajiwa katika kazi ya kufanya wanafunzi? Tunaweza jinsi gani kusitawisha sifa hizo?
Onyesha Unampenda Sana Mungu
3. Amri ya kufanya wanafunzi inatupa nafasi gani?
3 Ili kuzungumza na watu na kujitahidi kuwasadikisha wamwabudu Mungu wa kweli, tunahitaji kumpenda sana Yehova. Waisraeli wangeweza kuthibitisha kwamba walimpenda Mungu kwa kutii kwa moyo wote amri zake, kwa kutoa dhabihu zilizokubalika, na kwa kumsifu kwa nyimbo. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13; 30:19, 20; Zaburi 21:13; 96:1, 2; 138:5) Tukiwa wafanya-wanafunzi, sisi pia tunatii amri za Mungu, lakini tunaonyesha pia upendo wetu kwa Yehova kwa kuzungumza na wengine kumhusu yeye na makusudi yake. Tunahitaji kusema kwa usadikisho na kuchagua maneno yanayofaa ili kuonyesha jinsi tunavyohisi kikweli kuhusu tumaini letu tulilopewa na Mungu.—1 Wathesalonike 1:5; 1 Petro 3:15.
4. Kwa nini Yesu alifurahia kuwafundisha watu kumhusu Yehova?
4 Kwa kuwa alimpenda sana Yehova, Yesu alifurahia sana kuzungumza kuhusu makusudi ya Mungu, Ufalme, na ibada ya kweli. (Luka 8:1; Yohana 4:23, 24, 31) Kwa kweli, Yesu alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Maneno haya ya mtunga-zaburi yanamhusu Yesu: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu. Nimetangaza habari njema ya uadilifu katika kutaniko kubwa. Tazama! Siizuii midomo yangu. Ee Yehova, wewe mwenyewe unajua hivyo vema.”—Zaburi 40:8, 9; Waebrania 10:7-10.
5, 6. Wafanya-wanafunzi wanahitaji kuwa na sifa gani kuu?
5 Wakichochewa na upendo kwa Mungu, nyakati nyingine wapya ambao wamejifunza kweli za Biblia hivi karibuni wanasema kwa usadikisho mwingi kumhusu Yehova na Ufalme wake hivi kwamba wanakuwa na matokeo sana katika kuwasadikisha wengine wayachunguze Maandiko. (Yohana 1:41) Kumpenda Mungu ni sifa kuu ambayo inatuchochea katika kazi ya kufanya wanafunzi. Hivyo basi, tuendelee kudumisha upendo huo kwa kusoma na kutafakari Neno lake kwa ukawaida.—1 Timotheo 4:6, 15; Ufunuo 2:4.
6 Bila shaka, kumpenda Yehova kulimsaidia Yesu Kristo kuwa mwalimu mwenye bidii. Lakini hiyo haikuwa sababu pekee iliyomfanya awe mhubiri wa Ufalme mwenye matokeo. Hivyo basi, ni sifa gani nyingine iliyomfanya Yesu apate mafanikio katika kazi ya kufanya wanafunzi?
Wahangaikie Watu kwa Upendo
7, 8. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu watu?
7 Yesu aliwahangaikia watu na alipendezwa sana nao. Hata kabla ya kuwa mwanadamu na akiwa “stadi wa kazi” wa Mungu, Yesu alipendezwa na vitu vilivyohusiana na wanadamu. (Methali 8:30, 31) Akiwa mwanadamu duniani, Yesu aliwahurumia watu, na akawaburudisha wale waliokuja kwake. (Mathayo 11:28-30) Yesu alionyesha upendo na huruma ya Yehova, na jambo hilo liliwavuta watu kwenye ibada ya Mungu wa pekee wa kweli. Watu wa namna zote walimsikiliza Yesu kwa sababu aliwahangaikia kwa upendo na kufikiria hali zao.—Luka 7:36-50; 18:15-17; 19:1-10.
8 Mwanamume fulani alipomuuliza Yesu kile ambacho alihitaji kufanya ili aurithi uzima wa milele, ‘Yesu alimtazama na kumpenda.’ (Marko 10:17-21) Kuhusu watu fulani ambao walifundishwa na Yesu huko Bethania, tunasoma hivi: “Yesu alimpenda Martha na dada yake na Lazaro.” (Yohana 11:1, 5) Yesu aliwajali sana watu hivi kwamba badala ya kupumzika, aliamua kuwafundisha. (Marko 6:30-34) Kuwahangaikia sana wanadamu wenzake kwa upendo kulimfanya Yesu awe na matokeo zaidi kuliko mtu mwingine yeyote yule katika kuwavuta watu kwenye ibada ya kweli.
9. Paulo alikuwa na mtazamo gani akiwa mfanya-wanafunzi?
9 Pia, mtume Paulo alipendezwa sana na watu aliowahubiria. Kwa mfano, aliwaambia hivi wale ambao waligeuka na kuwa Wakristo huko Thesalonike: “Tukiwa na upendo mwororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa ninyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu ninyi mlikuwa wapendwa kwetu.” Kwa sababu ya jitihada zenye upendo za Paulo, watu fulani huko Thesalonike ‘walitoka kwenye ibada ya sanamu ili kumtumikia Mungu aliye hai.’ (1 Wathesalonike 1:9; 2:8) Tukiwahangaikia watu kikweli kama walivyofanya Yesu na Paulo, huenda sisi pia tukafurahia kuona habari njema ikifikia mioyo ya wale ambao ‘wana mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’—Matendo 13:48.
Onyesha Roho ya Kujidhabihu
10, 11. Kwa nini roho ya kujidhabihu inahitajiwa tunapojaribu kufanya wanafunzi?
10 Wale wanaopata matokeo katika kazi ya kufanya wanafunzi wana roho ya kujidhabihu. Bila shaka, hawaoni kupata mali kuwa jambo la maana zaidi. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Jinsi itakavyokuwa vigumu kwa wale wenye pesa kuingia katika ufalme wa Mungu!” Wanafunzi walishangaa waliposikia maneno hayo, lakini Yesu aliongeza hivi: “Wanangu, jinsi ilivyo vigumu kuingia katika ufalme wa Mungu! Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Marko 10:23-25) Yesu aliwapendekezea wafuasi wake waishi maisha rahisi ili wakazie fikira kazi ya kufanya wanafunzi. (Mathayo 6:22-24, 33) Kwa nini roho ya kujidhabihu inatusaidia katika kazi ya kufanya wanafunzi?
11 Jitihada nyingi zinahitajiwa ili kufundisha mambo yote ambayo Yesu aliamuru. Kwa kawaida, Mkristo anayetaka kufanya wanafunzi anajitahidi kujifunza Biblia kila juma na mtu anayependezwa. Ili kupata nafasi zaidi za kuwatafuta watu wanyoofu, wahubiri fulani wa Ufalme wameacha kazi ya wakati wote na kutafuta kazi ya muda. Maelfu ya Wakristo wamejifunza lugha nyingine ili kuwahubiria watu wa makabila fulani katika eneo lao. Wakristo wengine wanaoshiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi wamehama makwao na kwenda katika eneo au nchi nyingine ili kushiriki kwa ukamili zaidi katika mavuno. (Mathayo 9:37, 38) Yote hayo yanahitaji roho ya kujidhabihu. Lakini mengi zaidi yanahitajiwa ili kuwa na matokeo katika kazi ya kufanya wanafunzi.
Uwe Mwenye Subira Lakini Usipoteze Wakati
12, 13. Kwa nini subira ni ya maana sana katika kufanya wanafunzi?
12 Subira ni sifa nyingine ambayo inatusaidia kufanya wanafunzi. Watu wanahitaji kuchukua hatua ya haraka wanaposikia ujumbe wetu wa Kikristo, lakini mara nyingi kufanya wanafunzi kunachukua wakati mrefu na kunahitaji subira. (1 Wakorintho 7:29) Yesu alikuwa mwenye subira kumwelekea ndugu yake wa kambo, Yakobo. Ingawa inaelekea Yakobo alijua vizuri kazi ya Yesu ya kuhubiri, kwa muda fulani alisitasita kuwa mwanafunzi wake. (Yohana 7:5) Hata hivyo, katika kipindi kifupi kati ya kifo cha Kristo na Pentekoste 33 W.K., inaonekana kwamba Yakobo alikuja kuwa mwanafunzi, kwa kuwa Maandiko yanadokeza kwamba alikusanyika kwa ajili ya sala pamoja na mama yake, ndugu zake, na mitume. (Matendo 1:13, 14) Yakobo alifanya maendeleo mazuri ya kiroho, na baadaye akawa na madaraka mazito katika kutaniko la Kikristo.—Matendo 15:13; 1 Wakorintho 15:7.
13 Kama wakulima, Wakristo wanakuza sifa ambazo mara nyingi zinakua polepole, yaani, uelewaji wa Neno la Mungu, upendo kwa Yehova, na roho kama ya Kristo. Subira inahitajiwa ili kukuza sifa hizo. Yakobo aliandika hivi: “Onyesheni subira, akina ndugu, mpaka kuwapo kwa Bwana. Tazama! Mkulima huendelea kungojea matunda yenye thamani ya nchi, anayasubiri mpaka apate mvua ya mapema na mvua ya baadaye. Ninyi pia onyesheni subira; fanyeni mioyo yenu kuwa imara, kwa sababu kuwapo kwa Bwana kumekaribia.” (Yakobo 5:7, 8) Yakobo alikuwa akiwahimiza waamini wenzake ‘waonyeshe subira mpaka kuwapo kwa Bwana.’ Ikiwa wanafunzi hawakuelewa jambo fulani, kwa subira Yesu alieleza au kutoa mfano ili kuwasaidia. (Mathayo 13:10-23; Luka 19:11; 21:7; Matendo 1:6-8) Kwa kuwa sasa Bwana yupo, sisi pia tunahitaji kuwa wenye subira tunapojitahidi kufanya wanafunzi. Wale ambao wanakuwa wafuasi wa Yesu katika siku zetu wanahitaji kufundishwa kwa subira.—Yohana 14:9.
14. Ingawa sisi ni wenye subira, tunaweza jinsi gani kutumia kwa hekima wakati wetu tukiwa wafanya-wanafunzi?
14 Hata ingawa sisi ni wenye subira, neno halizai matunda ndani ya mioyo ya watu wengi ambao tumeanza kujifunza nao Biblia. (Mathayo 13:18-23) Kwa hiyo, baada ya kufanya jitihada za kutosha ili kuwasaidia, kwa hekima tunapaswa kuacha kutumia wakati wetu pamoja na watu kama hao na kujaribu kutafuta wale ambao huenda watathamini zaidi kweli ya Biblia. (Mhubiri 3:1, 6) Bila shaka, huenda hata watu ambao wanaithamini kweli ya Biblia wakahitaji kusaidiwa zaidi ili wabadili maoni yao, mitazamo yao, na mambo wanayotanguliza maishani. Hivyo, tunakuwa wenye subira kama Yesu alivyokuwa mwenye subira kuelekea wanafunzi wake ambao walikuwa na tatizo la kusitawisha mtazamo unaofaa.—Marko 9:33-37; 10:35-45.
Sitawisha Ufundi wa Kufundisha
15, 16. Kwa nini kueleza mambo kwa njia rahisi na kujitayarisha vizuri ni muhimu tunapofanya wanafunzi?
15 Kumpenda Mungu, kuwahangaikia watu, roho ya kujidhabihu, na subira ni mambo ya maana ili kufanikiwa katika kazi ya kufanya wanafunzi. Pia, ustadi wa kufundisha unahitaji kusitawishwa, kwa kuwa unatuwezesha kueleza mambo waziwazi na kwa njia rahisi. Kwa mfano, maneno mengi ya Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, yalikuwa yenye matokeo hasa kwa sababu yalikuwa rahisi. Inaelekea unakumbuka maneno kama haya ya Yesu: “Jiwekeeni hazina mbinguni.” “Msiwape mbwa kitu kitakatifu.” “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 6:20; 7:6; 11:19; 22:21) Bila shaka, Yesu hakutumia tu semi fupifupi. Alifundisha kwa njia iliyokuwa wazi na akaeleza mambo kwa wakati uliofaa. Unaweza kuiga jinsi gani njia ya Yesu ya kufundisha?
16 Kujitayarisha kwa uangalifu ni jambo la maana ili kufundisha kwa njia rahisi na iliyo wazi. Mhudumu ambaye hakujitayarisha ana mwelekeo wa kuzungumza kupita kiasi. Huenda asiweke wazi mambo makuu kwa sababu anazungumza sana, akisema kila jambo ambalo anajua kuhusu habari hiyo. Tofauti na hilo, mhudumu ambaye amejitayarisha vizuri anamfikiria mwanafunzi, anatafakari kuhusu habari, na anaeleza waziwazi mambo yanayohitajiwa tu. (Methali 15:28; 1 Wakorintho 2:1, 2) Anafikiria habari ambazo tayari mwanafunzi anajua na mambo yanayopaswa kukaziwa wakati wa funzo. Huenda mhudumu akajua mambo mengi yenye kupendeza kuhusu habari hiyo, lakini ili habari iwe wazi ni lazima aepuke habari ambazo si za lazima.
17. Tunaweza kuwasaidia jinsi gani watu wafikiri kwa kutumia Maandiko?
17 Pia, Yesu aliwasaidia watu kufikiri, badala ya kuwapa habari tu. Kwa mfano, katika pindi moja, aliuliza hivi: “Unaonaje, Simoni? Wafalme wa dunia hupokea ushuru au kodi ya kichwa kutoka kwa nani? Kutoka kwa wana wao au kutoka kwa wageni?” (Mathayo 17:25) Huenda tukafurahia sana kuifafanua Biblia hivi kwamba tunahitaji kujizuia ili kumruhusu mwanafunzi ajieleze au aeleze jambo mnalozungumzia katika funzo la Biblia la nyumbani. Kwa kawaida, hatupaswi kuwauliza watu maswali mengi. Badala yake, tukitoa mifano mizuri kwa busara na tukiuliza maswali yaliyofikiriwa vizuri, tunaweza kuwasaidia waelewe mawazo ya Biblia yaliyo katika vichapo vyetu vya Biblia.
18. Ni nini kinachohusika katika kusitawisha “ufundi wa kufundisha”?
18 Maandiko yanasema kuhusu “ufundi wa kufundisha.” (2 Timotheo 4:2; Tito 1:9) Uwezo huo wa kufundisha unatia ndani mengi zaidi ya kumsaidia mtu aweke akilini mambo hakika. Tunapaswa kujaribu kumsaidia mwanafunzi wa Biblia aelewe tofauti kati ya kweli na uwongo, lililo zuri na lililo baya, hekima na upumbavu. Tunapofanya hivyo na kujitahidi kumsaidia mtu ampende Yehova kutoka moyoni, huenda akaona kwa nini anapaswa kumtii Yehova.
Shiriki kwa Bidii Katika Kazi ya Kufanya Wanafunzi
19. Wakristo wote wanaweza kusaidia jinsi gani katika kufanya wanafunzi?
19 Kutaniko la Kikristo ni tengenezo la kufanya wanafunzi. Mtu mpya anapokuwa mwanafunzi, wengine wanashangilia kutia ndani Shahidi wa Yehova aliyempata na kumsaidia kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha. Kikundi cha watu kinapokuwa katika shughuli za kumtafuta mtoto aliyepotea, huenda mtu mmoja tu katika kikundi hicho ndiye atakayempata mtoto huyo. Lakini mtoto huyo anapoungana tena na wazazi wake, kila mtu aliyehusika katika shughuli hiyo ya kumtafuta anashangilia. (Luka 15:6, 7) Vivyo hivyo, kutaniko lote linahusika katika kazi ya kufanya wanafunzi. Wakristo wote wanashiriki katika kuwatafuta wale ambao huenda wakawa wanafunzi wa Yesu. Na mtu mpya anapoanza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme, kila Mkristo katika Jumba la Ufalme anamsaidia mtu huyo kuithamini zaidi ibada ya kweli. (1 Wakorintho 14:24, 25) Hivyo, Wakristo wote wanaweza kushangilia kwamba mamia ya maelfu ya wanafunzi wapya wanafanywa kila mwaka.
20. Unapaswa kufanya nini ikiwa unataka kuwafundisha wengine kweli ya Biblia?
20 Wakristo wengi waaminifu wangefurahi kumfundisha mtu fulani kumhusu Yehova na ibada ya kweli. Hata hivyo, huenda wasiweze kufanya hivyo hata wakijitahidi kadiri gani. Ikiwa hiyo ndiyo hali yako, endelea kuimarisha upendo wako kwa Yehova, wahangaikie watu, jidhabihu, uwe mwenye subira, na ujitahidi kuboresha ustadi wako wa kufundisha. Zaidi ya yote, sali kuhusu tamaa yako ya kufundisha kweli. (Mhubiri 11:1) Pata faraja kwa kujua kwamba kila jambo unalofanya katika utumishi wa Yehova linasaidia katika kazi ya kufanya wanafunzi ambayo inamtukuza Mungu.
-
-
Mwige Mfanya-wanafunzi MkuuMnara wa Mlinzi—2007 | Novemba 15
-
-
Mwige Mfanya-wanafunzi Mkuu
“Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.”—LUKA 8:18.
1, 2. Kwa nini unapaswa kufikiria sana jinsi Yesu alivyoshughulika na watu katika huduma yake?
YESU KRISTO alikuwa akitimiza daraka lake akiwa Mwalimu Mkuu na Mfanya-Wanafunzi Mkuu alipowaambia wafuasi wake hivi: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.” (Luka 8:16-18) Kanuni hiyo inatumika katika huduma yako ukiwa Mkristo. Ukisikiliza maagizo ya kiroho, utayatumia na kuwa mtangazaji wa Ufalme mwenye matokeo. Bila shaka, leo huwezi kuisikia sauti ya Yesu, lakini unaweza kusoma yale aliyosema na kufanya, kama yanavyofunuliwa katika Maandiko. Yanafunua nini kuhusu jinsi Yesu alivyowashughulikia watu katika huduma yake?
2 Yesu alikuwa mhubiri bora wa habari njema na mwalimu stadi sana wa kweli za Kimaandiko. (Luka 8:1; Yohana 8:28) Kazi ya kufanya wanafunzi inatia ndani kuhubiri na kufundisha. Hata hivyo, Wakristo fulani ambao ni wahubiri wenye kusifika wanaona ni vigumu kuwafundisha watu vizuri. Ingawa kuhubiri kunatia ndani kutangaza ujumbe, kwa kawaida ili kuwafundisha watu kumhusu Yehova na makusudi yake, ni lazima mwalimu ajenge uhusiano pamoja na mwanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Anaweza kufanya hivyo kwa kumwiga Yesu Kristo, yule Mwalimu Mkuu na Mfanya-Wanafunzi Mkuu.—Yohana 13:13.
3. Jitihada zako za kufanya wanafunzi zitakuwa na matokeo gani ukimwiga Yesu?
3 Ukiiga njia za Yesu za kufundisha, utakuwa ukifuata himizo hili la mtume Paulo: “Endeleeni kutembea kwa hekima kuelekea wale walio nje, mkijinunulia wakati unaofaa. Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:5, 6) Kumwiga Yesu katika kazi ya kufanya wanafunzi kunahitaji jitihada, lakini kufanya hivyo kutakuwezesha kufundisha vizuri kwa sababu kutakusaidia ‘umjibu kila mtu’ kulingana na uhitaji wake.
Yesu Aliwatia Wengine Moyo Wazungumze
4. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa msikilizaji mzuri?
4 Tangu akiwa mtoto, Yesu alikuwa na desturi ya kuwasikiliza watu na kuwatia moyo watoe maoni yao. Kwa mfano, alipokuwa na umri wa miaka 12, wazazi wake walimkuta katikati ya walimu hekaluni, “akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” (Luka 2:46) Yesu hakwenda hekaluni ili kuwaaibisha walimu kwa ujuzi wake. Alienda huko ili kusikiliza, ingawa pia aliuliza maswali. Mwelekeo wake wa kusikiliza vizuri huenda ni moja ya sifa zilizomfanya apate kibali cha Mungu na wanadamu.—Luka 2:52.
5, 6. Tunajua jinsi gani kwamba Yesu aliwasikiliza wale ambao aliwafundisha?
5 Baada ya kubatizwa na kutiwa mafuta awe Masihi, Yesu aliendelea kuwasikiliza watu. Hakuwa mwenye shughuli nyingi sana za kuwafundisha watu hivi kwamba akawasahau wale waliokuja kumsikiliza. Mara nyingi, alitua kidogo, aliwauliza maoni yao, na kusikiliza majibu yao. (Mathayo 16:13-15) Kwa mfano, baada ya kifo cha Lazaro, ndugu ya Martha, Yesu alimwambia Martha hivi: “Kila mtu aliye hai na ananiamini hatakufa kamwe.” Kisha akamuuliza Martha: “Je, unaamini hilo?” Na bila shaka Yesu alisikiliza Martha alipomjibu hivi: “Ndiyo, Bwana; nimeamini kwamba wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu.” (Yohana 11:26, 27) Ilipendeza kama nini kumsikia Martha akieleza imani yake kwa njia hiyo!
6 Wanafunzi wengi walipomwacha Yesu, yeye alitaka kujua maoni ya mitume wake. Hivyo aliuliza hivi: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Simoni Petro akamjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele; na sisi tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.” (Yohana 6:66-69) Maneno hayo yalimfurahisha Yesu kama nini! Bila shaka, maneno kama hayo ya imani kutoka kwa mwanafunzi wa Biblia yatakufurahisha wewe pia.
Yesu Alisikiliza kwa Heshima
7. Kwa nini Wasamaria wengi walimwamini Yesu?
7 Sababu nyingine iliyomfanya Yesu awe na matokeo mazuri katika kazi ya kufanya wanafunzi ni kwamba aliwajali watu na kuwasikiliza kwa heshima. Kwa mfano, pindi moja Yesu alimhubiria mwanamke Msamaria karibu na chemchemi ya Yakobo huko Sikari. Wakati wa mazungumzo hayo, Yesu hakuzungumza tu; alimsikiliza mwanamke huyo. Alipokuwa akimsikiliza, Yesu alitambua kwamba alipendezwa na ibada na akamwambia kwamba Mungu alikuwa akitafuta watu ambao wangemwabudu kwa roho na kweli. Yesu alimheshimu na kumhangaikia mwanamke huyo, na hivyo mwanamke huyo akawaambia wengine kumhusu Yesu, na “wengi wa Wasamaria kutoka jiji hilo walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke.”—Yohana 4:5-29, 39-42.
8. Mwelekeo wa watu wa kutaka kutoa maoni yao unaweza kukusaidia jinsi gani kuanzisha mazungumzo katika huduma?
8 Kwa kawaida, watu wanafurahia kutoa maoni yao. Kwa mfano, wakaaji wa kale wa Athene walifurahia kutoa maoni yao na kusikiliza mambo mapya. Hilo lilimwongoza mtume Paulo kutoa hotuba iliyokuwa na matokeo mazuri kwenye Areopago katika jiji hilo. (Matendo 17:18-34) Unapoanza mazungumzo pamoja na mwenye nyumba katika huduma yako leo, unaweza kusema, “Ninakutembelea kwa sababu ningependa kujua maoni yako kuhusu [habari fulani].” Sikiliza maoni ya mtu huyo, na useme jambo fulani kuhusu maoni yake, au uliza swali kuhusu maoni hayo. Kisha, kwa fadhili mwonyeshe yale ambayo Biblia inasema juu ya habari hiyo.
Yesu Alijua Jinsi ya Kuanzisha Mazungumzo
9. Yesu alifanya nini kabla ya ‘kuwafungulia Maandiko’ Kleopa na msafiri mwenzake?
9 Yesu hakukosa kamwe jambo la kusema. Zaidi ya kuwa msikilizaji mzuri, mara nyingi Yesu alijua yale ambayo watu walikuwa wakifikiri, na alijua ni nini hasa alipaswa kusema. (Mathayo 9:4; 12:22-30; Luka 9:46, 47) Kwa mfano: Muda mfupi baada ya ufufuo wa Yesu, wanafunzi wawili walikuwa wakisafiri kwa miguu kutoka Yerusalemu kwenda Emau. Simulizi la Injili linasema hivi: “Walipokuwa wakiongea na kujadiliana, Yesu akakaribia, akaanza kutembea pamoja nao; lakini macho yao yalizuiwa wasiweze kumtambua. Akawaambia: ‘Ni mambo gani haya ambayo mnajadiliana kati yenu wenyewe mnapotembea?’ Nao wakasimama tuli wakiwa na nyuso zenye huzuni. Yule aliyeitwa Kleopa akajibu, akamwambia: ‘Je, wewe unakaa peke yako kama mgeni katika Yerusalemu na kwa hiyo huyajui mambo ambayo yametukia humo siku hizi?’ Naye akawaambia: ‘Mambo gani?’” Mwalimu Mkuu aliwasikiliza walipokuwa wakieleza kwamba Yesu Mnazareti aliwafundisha watu, alifanya miujiza, na aliuawa. Sasa watu wengine walikuwa wakisema kwamba alifufuliwa kutoka kwa wafu. Yesu alimwacha Kleopa na msafiri mwenzake wajieleze. Kisha, akawaeleza mambo waliyohitaji kujua, ‘akawafungulia Maandiko.’—Luka 24:13-27, 32.
10. Unaweza kujua jinsi gani maoni ya kidini ya mtu unayekutana naye katika huduma yako?
10 Huenda usijue jambo lolote kuhusu maoni ya kidini ya mwenye nyumba fulani. Ili kujua maoni yake, labda unaweza kusema kwamba ungependa kusikia yale ambayo watu wanafikiri kuhusu sala. Kisha unaweza kuuliza, “Je, unafikiri kweli kuna yeyote anayesikiliza sala?” Huenda jibu utakalopewa litafunua mengi kuhusu maoni ya mtu huyo na malezi yake ya kidini. Ikiwa anapendezwa na mambo ya kidini, huenda ukajua mengi zaidi kuhusu maoni yake kwa kuuliza, “Je, unafikiri Mungu anasikiliza sala zote, au huenda kuna sala nyingine ambazo hasikilizi?” Maswali kama hayo yanaweza kuongoza kwenye mazungumzo mazuri. Ikiwa inafaa kumwonyesha yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hilo, utahitaji kufanya hivyo kwa busara, lakini hupaswi kushambulia imani ya mtu huyo. Ikiwa anafurahia kukusikiliza, huenda akataka umrudie. Lakini namna gani akiuliza swali ambalo huwezi kujibu? Unaweza kufanya utafiti fulani na kurudi ukiwa tayari kumtolea ‘sababu ya tumaini lililo ndani yako, lakini ukifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.’—1 Petro 3:15.
Yesu Alifundisha Wale Waliostahili
11. Ni nini kitakachokusaidia kuwapata watu wanaostahili kufundishwa?
11 Yesu, yule mtu mkamilifu, alikuwa na utambuzi ambao ulimwezesha kujua watu waliostahili kufundishwa. Si jambo rahisi kwetu kuwapata wale ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Matendo 13:48) Ilikuwa hivyo pia kwa mitume ambao Yesu aliwaambia hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mtakapoingia, tafuteni ni nani humo anayestahili.” (Mathayo 10:11) Kama mitume wa Yesu, unapaswa pia kuwatafuta watu walio tayari kusikiliza na kufundishwa kweli za Kimaandiko. Unaweza kuwapata watu wanaostahili kwa kusikiliza kwa makini mtu mmoja baada ya mwingine, na kufikiria mtazamo wa kila mtu.
12. Unaweza kuendelea kumsaidia jinsi gani mtu anayependezwa?
12 Baada ya kuachana na mtu aliyependezwa kwa kadiri fulani na ujumbe wa Ufalme, ingefaa uendelee kufikiria mahitaji yake ya kiroho. Ukiandika mambo ambayo umejifunza baada ya kuzungumza na mtu fulani kuhusu habari njema, hilo litakusaidia kuendelea kumsaidia kiroho. Unapofanya ziara ya kurudia, unahitaji kusikiliza kwa makini ikiwa unataka kujifunza mengi zaidi kuhusu imani ya kidini, mtazamo, au hali za mtu huyo.
13. Ni nini kinachoweza kukusaidia kutambua maoni ya mtu kuhusu Biblia?
13 Unaweza jinsi gani kuwatia watu moyo wakueleze maoni yao kuhusu Neno la Mungu? Katika maeneo fulani, swali hili linafaa, “Je, unaona ni vigumu kuielewa Biblia?” Mara nyingi, jibu la swali hilo linafunua mtazamo wa mtu kuelekea mambo ya kiroho. Njia nyingine ni kusoma andiko na kuuliza, “Una maoni gani kuhusu hilo?” Kama Yesu, unaweza kutimiza mengi katika huduma yako kwa kutumia maswali vizuri. Hata hivyo, ni vizuri kuwa mwangalifu.
Yesu Alitumia Maswali Vizuri
14. Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unapendezwa na maoni ya watu bila kuwahoji?
14 Pendezwa na maoni ya wengine bila kuwaaibisha. Iga njia za Yesu. Hakuuliza maswali bila busara, lakini aliuliza maswali ambayo yalichochea fikira. Pia, Yesu alikuwa msikilizaji mwenye fadhili ambaye aliwaburudisha watu wanyoofu na kuwafanya wastarehe. (Mathayo 11:28) Watu wa aina zote walijihisi huru kuzungumza naye kuhusu matatizo yao. (Marko 1:40; 5:35, 36; 10:13, 17, 46, 47) Ukitaka watu wajisikie huru kukueleza maoni yao kuhusu Biblia na mafundisho yake, unapaswa kuepuka kuwahoji.
15, 16. Unaweza kuanzisha jinsi gani mazungumzo na watu kuhusu mambo ya kidini?
15 Zaidi ya kutumia maswali vizuri, unaweza kumtia mtu moyo azungumze kwa kusema jambo fulani lenye kupendeza na kisha kusikiliza itikio lake. Kwa mfano, Yesu alimwambia Nikodemo hivi: “Mtu asipozaliwa tena, hawezi kuuona ufalme wa Mungu.” (Yohana 3:3) Maneno hayo yalikuwa yenye kuvutia sana hivi kwamba Nikodemo hangejizuia kuitikia na kumsikiliza Yesu. (Yohana 3:4-20) Wewe pia unaweza kuanzisha mazungumzo na watu kwa njia kama hiyo.
16 Leo, kutokea kwa dini nyingi mpya ni habari inayowavutia watu wengi barani Afrika, Ulaya Mashariki, na Amerika ya Latini. Katika maeneo kama hayo, mara nyingi unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema hivi: “Sielewi kwa nini kuna dini nyingi mno. Lakini ninatumaini kuona hivi karibuni watu kutoka katika mataifa yote wakiunganishwa katika ibada ya kweli. Je, ungependa kuona jambo hilo likitukia?” Kwa kusema jambo fulani lenye kushangaza kuhusu tumaini lako, unaweza kuwachochea watu watoe maoni yao. Ni rahisi watu kujibu maswali wanapopewa nafasi ya kuchagua kati ya majibu mawili. (Mathayo 17:25) Baada ya mwenye nyumba kujibu swali lako, jibu swali hilo kwa kutumia andiko moja au mawili. (Isaya 11:9; Sefania 3:9) Ukimsikiliza kwa makini na kufikiria jibu lake, unaweza kujua yale mtakayozungumzia utakaporudi.
Yesu Aliwasikiliza Watoto
17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alipendezwa na watoto?
17 Yesu hakupendezwa tu na watu wazima, bali pia na watoto. Alijua michezo ya watoto na mambo waliyozungumzia. Nyakati nyingine aliwaita watoto waje kwake. (Luka 7:31, 32; 18:15-17) Watoto wengi walikuwa kati ya umati wa watu waliomsikiliza Yesu. Wavulana walipopiga kelele wakimsifu Masihi, Yesu alitambua jambo hilo na kuonyesha kwamba Maandiko yalikuwa yamelitabiri. (Mathayo 14:21; 15:38; 21:15, 16) Leo, watoto wengi wanakuwa wanafunzi wa Yesu. Unaweza kuwasaidia jinsi gani?
18, 19. Unaweza jinsi gani kumsaidia kiroho mtoto wako?
18 Ili kumsaidia kiroho mtoto wako, unapaswa kumsikiliza. Unahitaji kuelewa mawazo yake ambayo huenda hayapatani na maoni ya Yehova. Hata mtoto wako akisema nini, ni jambo la hekima kumpongeza kwanza. Kisha unaweza kutumia maandiko kumsaidia mtoto wako kuelewa maoni ya Yehova kuhusu mambo.
19 Maswali yanaweza kukusaidia kutambua maoni ya watoto. Lakini watoto hawapendi hata kidogo kuulizwa-ulizwa maswali. Badala ya kumuuliza mtoto wako maswali magumu, kwa nini usiseme mambo machache yanayokuhusu wewe mwenyewe? Ikitegemea jambo mnalozungumzia, unaweza kumweleza jinsi ulivyokuwa ukihisi na kwa nini ulihisi hivyo. Kisha unaweza kumuuliza, “Je, wewe pia unahisi hivyo?” Jibu la mtoto wako linaweza kuongoza kwenye mazungumzo mazuri ya Kimaandiko yenye kujenga.
Endelea Kumwiga Mfanya-Wanafunzi Mkuu
20, 21. Kwa nini unapaswa kuwa msikilizaji mzuri katika kazi yako ya kufanya wanafunzi?
20 Iwe unazungumzia jambo fulani na mtoto wako au na mtu mwingine yeyote, ni lazima usikilize kwa makini. Kwa kweli, kufanya hivyo ni uthibitisho wa upendo. Kwa kusikiliza, unatenda kwa njia ya unyenyekevu, na hivyo unamheshimu na kumhangaikia kwa upendo msikilizaji wako. Bila shaka, kusikiliza kunamaanisha kukazia uangalifu yale ambayo mtu huyo anasema.
21 Unaposhiriki katika huduma ya Kikristo, endelea kuwasikiliza wenye nyumba kwa makini. Ikiwa unasikiliza kwa makini sana yale wanayosema, inaelekea utatambua ni kweli gani za Biblia zitakazowavutia. Kisha, jitahidi kuwasaidia kwa kutumia njia mbalimbali za kufundisha ambazo Yesu alitumia. Ukifanya hivyo, utathawabishwa kwa kuwa mwenye shangwe na uradhi kwa sababu unamwiga Mfanya-Wanafunzi Mkuu.
-