-
Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga SanaSiri ya Furaha ya Familia
-
-
UHITAJI MUHIMU WA NIDHAMU
20. Nidhamu ni nini, nayo itiweje?
20 Nidhamu ni kuzoeza kunakosahihisha akili na moyo. Watoto wanaihitaji daima. Paulo awashauri akina baba ‘waendelee kuwalea watoto wao katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’ (Waefeso 6:4) Wazazi wanapaswa watie nidhamu kwa upendo, kama vile Yehova hufanya. (Waebrania 12:4-11) Nidhamu inayotegemea upendo inaweza kutiwa kupitia njia ya kusababu. Kwa sababu hiyo, tunaambiwa “kusikiliza nidhamu.” (Mithali 8:33, NW) Nidhamu yapaswa itiweje?
21. Wazazi wakumbuke kanuni zipi wanapowatia watoto wao nidhamu?
21 Wazazi fulani hufikiri kwamba kuwatia watoto wao nidhamu kunahusisha kusema nao tu kwa sauti ya kutisha, kuwakemea, au hata kuwatukana. Hata hivyo, juu ya habari iyo hiyo, Paulo huonya hivi: “Nanyi, akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu.” (Waefeso 6:4) Wakristo wote wanahimizwa wawe ‘waanana kuelekea wote wakiagiza kwa upole wale wasio na mwelekeo ufaao.’ (2 Timotheo 2:24, 25) Ingawa wazazi Wakristo hutambua uhitaji wa uthabiti, wao hujaribu kukumbuka maneno haya wanapowatia watoto wao nidhamu. Lakini nyakati nyingine, kusababu hakutoshi, na aina fulani ya adhabu huenda ikahitajiwa.—Mithali 22:15.
22. Ikiwa mtoto anahitaji kuadhibiwa, anapasa asaidiwe kuelewa nini?
22 Watoto tofauti hutaka aina tofauti-tofauti za nidhamu. Watoto fulani ‘hawasahihishwi kwa maneno tu.’ Kwao, adhabu ya pindi kwa pindi inayotolewa kwa ajili ya kutotii huenda ikawa yenye kuokoa uhai. (Mithali 17:10; 23:13, 14; 29:19, NW) Lakini, ni lazima mtoto aelewe ni kwa nini anaadhibiwa. “Fimbo na maonyo hutia hekima.” (Mithali 29:15; Ayubu 6:24, italiki ni zetu.) Zaidi ya hayo, adhabu ina mipaka. “Nitakurudi kwa hukumu [“kwa kadiri inayofaa,” “NW”],” Yehova akawaambia watu wake. (Yeremia 46:28b) Biblia haiungi mkono hata kidogo kule kupiga mjeledi kwa hasira au mapigo makali, yanayochubua na hata kumjeruhi mtoto.—Mithali 16:32.
23. Mtoto anapaswa aweze kufahamu nini anapoadhibiwa na wazazi wake?
23 Yehova alipowaonya watu wake kwamba yeye angewatia nidhamu, alisema hivi kwanza: “Usiogope wewe . . . kwa maana mimi ni pamoja nawe.” (Yeremia 46:28a) Vivyo hivyo, nidhamu ya wazazi, iwe ni katika namna gani inayofaa, haipaswi kamwe imwache mtoto akihisi amekataliwa. (Wakolosai 3:21) Badala ya hivyo, mtoto apaswa ahisi kwamba nidhamu inatiwa kwa sababu mzazi yu ‘pamoja naye,’ kwenye upande wake.
-