Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kazi ya Madaktari Inabadilika
    Amkeni!—2005 | Januari 22
    • Kazi ya Madaktari Inabadilika

      Mwaka wa 1174, Maimonides aliteuliwa kuwa daktari wa familia ya watawala wa Misri, naye alifanya kazi kwa siku nyingi katika makao ya mfalme. Aliandika hivi kuhusu maisha yake ya kila siku: “Mimi hula chakula kidogo mara moja tu kwa siku. Kisha mimi huanza kuwashughulikia wagonjwa, kuwaandikia dawa, na kuwapa maagizo. Wagonjwa huja kutibiwa hata usiku, na nyakati nyingine . . . mimi huchoka sana na kushindwa kuongea.”

      SIKUZOTE madaktari wamelazimika kujitoa mhanga. Lakini hali ambazo madaktari wanakabili sasa katika jamii zinabadilika haraka sana. Kazi yao huchosha kama vile ilivyomchosha Maimonides. Lakini je, wao huheshimiwa kama zamani? Hali za leo zimeathirije maisha ya madaktari na uhusiano wao na wagonjwa?

      Uhusiano Umebadilika

      Katika sehemu fulani, huenda wengine wakakumbuka jinsi daktari alivyobeba dawa zake zote ndani ya mkoba mweusi. Sawa na leo, watu walikuwa na maoni mbalimbali kuhusu madaktari. Madaktari wengi waliheshimiwa kwa sababu ya uwezo wao na cheo chao, na walipendwa kwa sababu ya maadili yao. Kwa upande mwingine, walishutumiwa kwa ada walizotoza, kulaumiwa kwa makosa yao, na watu waliwachambua kwa sababu walidhania hawana huruma.

      Licha ya hayo, madaktari wengi walifurahia sana kutibu familia ileile kwa vizazi kadhaa. Waliwatembelea wagonjwa mara nyingi nyumbani kwao, na nyakati nyingine katika maeneo ya mashambani, walikula chakula pamoja na familia waliyoitembelea au hata kukaa usiku wote wakimsaidia mama kujifungua. Mara nyingi, madaktari ndio waliowapendekezea wagonjwa dawa za kutumia. Madaktari waliojitoa mhanga waliwatibu maskini bila malipo, na waliwahudumia watu wakati wowote ule.

      Bila shaka, madaktari fulani bado wanafanya hivyo, lakini katika maeneo mengi uhusiano kati ya madaktari na wagonjwa umebadilika sana katika miaka ya karibuni kuliko ilivyokuwa zamani. Mabadiliko hayo yamesababishwa na nini? Hebu kwanza tuzungumzie lile zoea la madaktari kuwatembelea wagonjwa nyumbani.

      Kuwatembelea Wagonjwa Nyumbani

      Zamani ilikuwa kawaida kwa madaktari kuwatembelea wagonjwa nyumbani, na zoea hilo bado linaendelea katika maeneo fulani. Lakini madaktari wanaacha kufanya hivyo ulimwenguni pote. Gazeti The Times of India linasema: “Madaktari waliowatia moyo wagonjwa vitandani, waliofahamiana sana na familia na kuwa tayari kuwatembelea wagonjwa nyumbani wakati wowote walipohitajiwa, wanazidi kupungua kwa sababu siku hizi madaktari wengi wamekuwa wataalamu wa ugonjwa hususa.”

      Kwa sababu ujuzi wa tiba umeongezeka sana, madaktari wengi wanasomea tiba ya ugonjwa hususa na wanafanya kazi wakiwa kikundi. Hivyo, wagonjwa wanaweza kutibiwa na daktari tofauti kila mara wanapoenda kutibiwa. Basi, madaktari wengi hawawezi kuwa na uhusiano wa muda mrefu pamoja na familia moja kama ilivyokuwa zamani.

      Madaktari waliacha kuwatembelea wagonjwa nyumbani miaka mia moja hivi iliyopita wakati ambapo walianza kuchunguza magonjwa katika maabara na kutumia vifaa vya kuwapima wagonjwa. Katika maeneo mengi, mashirika ya afya yaliona kwamba madaktari wanapoteza wakati kwa kuwatembelea wagonjwa nyumbani. Sasa wagonjwa wengi wanaweza kusafiri kwa urahisi ili kumwona daktari. Isitoshe, sasa wafanyakazi wa afya na wale wanaotoa huduma za dharura wanafanya kazi zilizofanywa tu na madaktari.

      Hali Zimebadilika

      Leo ni madaktari wachache wanaofanya kazi kwa kujitegemea. Mara nyingi, huduma za tiba hutolewa na mashirika ya serikali au mashirika mengine ya afya yanayowaajiri madaktari. Hata hivyo, madaktari wengi hawapendi kuajiriwa. Mara nyingi, mashirika hayo huwataka madaktari wawahudumie wagonjwa wengi kwa muda mfupi. Dakt. Sheila Perkins wa Uingereza anasema hivi: “Ninatazamiwa kutumia dakika saba hadi kumi kumhudumia mgonjwa mmoja. Na ninahitaji kutumia sehemu kubwa ya wakati huo kurekodi habari kwenye kompyuta. Hakuna wakati wa kutosha kufahamiana na mgonjwa. Inafadhaisha sana.”

      Hali zinazobadilika zimewafanya wagonjwa wawe na mamlaka zaidi. Kuna wakati ambapo maagizo ya madaktari hayangepingwa. Lakini, leo katika nchi nyingi ni lazima daktari amfahamishe mgonjwa kuhusu matibabu mbalimbali na matokeo yake ili mgonjwa akubali kutibiwa akiwa anafahamu vizuri matibabu hayo. Uhusiano kati ya daktari na mgonjwa umebadilika. Watu fulani huona daktari kuwa mtaalamu tu.

      Katika ulimwengu huu unaozidi kubadilika, kuna madaktari wengi wanawake. Watu wengi huwapenda madaktari wanawake kwani wao huonekana kuwa wasikivu. Hivyo, inaonekana wanawafanya watu wawaone madaktari kuwa wenye huruma.

      Watu wengi wanawapenda madaktari wanaoelewa hisia na mfadhaiko wa wagonjwa. Hata hivyo, ni wagonjwa wangapi wanaoelewa hisia za madaktari na mfadhaiko wanaokabili? Hapana shaka kwamba kufanya hivyo kutaboresha uhusiano kati ya daktari na mgonjwa. Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Maimonides

      [Hisani]

      Brown Brothers

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Zamani, madaktari walikuwa wakiwatembelea wagonjwa nyumbani

  • Matatizo ya Madaktari
    Amkeni!—2005 | Januari 22
    • Matatizo ya Madaktari

      “Mtu mmoja na mke wake walikuja kuniona wakitumaini kwamba ningemtibu mtoto wao aliyezaliwa majuzi. Nilipomchunguza nilifadhaika. Ugonjwa wake haungeweza kuponywa. Je, unaweza kuwazia jinsi nilivyohisi nilipowajulisha wazazi hao kwamba mwana wao atakuwa kipofu? Nilihuzunika sana walipokuwa wakiondoka ofisini mwangu. Lakini, punde baadaye mgonjwa mwingine akaingia huku akitazamia nimkaribishe kwa uchangamfu! Hilo ndilo hunifadhaisha.”—Mtaalamu wa macho huko Amerika Kusini.

      KWA kawaida wagonjwa hawaendi kumwona daktari ili kuyashughulikia matatizo ya daktari. Wagonjwa huhangaikia tu matatizo yao. Kwa hiyo, ni watu wachache sana wanaoelewa matatizo ambayo madaktari wanakabili kila siku.

      Ni wazi kwamba kila mtu hukabili mfadhaiko, na si wanatiba tu wanaokabili mfadhaiko. Hata hivyo, kwa sababu watu wengi hushughulika na madaktari kwa njia mbalimbali, ni muhimu kuelewa matatizo ya madaktari na jinsi yanavyowaathiri.

      Madaktari huanza kukabili mfadhaiko mapema maishani wanapotafuta nafasi ya kuingia chuo kikuu. Kisha, wanapoanza mafunzo ya tiba, hisia zao huathiriwa sana. Hapo ndipo hisia na utu wa mwanafunzi wa tiba huanza kubadilika.

      Mafunzo ya Tiba Huathiri Hisia

      Wanafunzi wa tiba wanaweza kwenda kwenye chumba cha upasuaji hata katika juma la kwanza la masomo. Huenda wanafunzi wengi wasiwe wameona maiti. Wanafunzi wengi huchukizwa wanapoona maiti zilizo uchi na zilizokauka zinapopasuliwa ili kuchunguza viungo vya mwili. Inawabidi wanafunzi watafute njia za kukabiliana na hisia zao. Mara nyingi wao hutumia ucheshi kwa kuzipatia maiti majina ya utani. Ijapokuwa watu wengine wanaweza kuudhiwa na jambo hilo, ni lazima wanafunzi wa tiba wafanye hivyo ili wasiifikirie maiti kuwa mtu.

      Kisha, wao hupata mafunzo ya tiba katika hospitali. Kabla ya kufikia umri wa makamo, watu wengi huwa hawafikirii kuhusu ufupi wa maisha. Lakini wanafunzi wa tiba hukabili uhakika huo mapema maishani wakati wanapowaona watu walio na magonjwa yasiyoweza kupona na wanapowaona watu wakifa. Mwanafunzi mmoja alisema kwamba alichukizwa sana alipoona mambo hayo kwa mara ya kwanza. Wanafunzi wa nchi tajiri na hata wa nchi maskini wanaweza kushangaa sana kuona wagonjwa wakinyimwa matibabu kwa sababu ya ukosefu wa pesa za kuyagharimia.

      Madaktari wapya hushughulikiaje mfadhaiko? Mara nyingi inawabidi wafanyakazi wa afya waepuke kujihusisha kihisia na wagonjwa kwa kutowaona kuwa watu. Badala ya kumrejelea mgonjwa kuwa mtu, huenda wakasema, “Daktari, kuna mguu uliovunjika katika chumba cha pili.” Hilo linaweza kuchekesha ikiwa huelewi sababu yao ya kusema hivyo.

      Kuwahurumia Watu Kunaweza Kuchosha

      Ijapokuwa madaktari wamezoezwa kuwa wanasayansi, wengi wao hutumia muda mwingi sana kuzungumza na wagonjwa. Madaktari fulani huona ni vigumu kuwa na uhusiano wa karibu na wagonjwa. Kama ilivyotajwa mwanzoni, mojawapo ya mambo magumu zaidi anayokabili daktari ni kumpasha mtu habari mbaya. Wengine hufanya hivyo kila siku. Watu wenye matatizo huhitaji kueleza jinsi wanavyohisi, na madaktari hawana budi kuwasikiliza. Kuwashughulikia watu walio na wasiwasi kunaweza kuwachosha sana madaktari.

      Daktari mmoja huko Kanada aliandika hivi kuhusu miaka yake ya kwanza-kwanza ya udaktari: “Nilikuwa na kazi nyingi sana: nilitumia wakati mwingi kuwasaidia watu wenye uhitaji; watu waliofadhaika walitaka niwasikilize; watu walitaka niwatibu; watu walitumia hila ili wajifaidi; watu walikuja kuniona; watu walinisihi niwatembelee; watu walinipigia simu nyumbani hata nikiwa kitandani. Kila mahali ni watu, watu, watu. Nilitaka kuwasaidia, lakini nililemewa.”—A Doctor’s Dilemma, cha John W. Holland.

      Je, madaktari huacha kufadhaika kadiri wakati unavyopita? Madaktari ambao wamefanya kazi kwa miaka mingi huwa na madaraka zaidi. Mara nyingi, maamuzi mazito yanayohusu uhai wa mgonjwa huhitaji kufanywa papo hapo, na nyakati nyingine yanafanywa bila kuwa na habari kamili. Daktari mmoja wa Uingereza anasema hivi: “Nilipokuwa kijana, sikujali maamuzi niliyofanya, kama vile vijana wasivyojali wanapoendesha gari ovyoovyo. Lakini mtu huthamini uhai zaidi kadiri anavyozidi kuzeeka. Siku hizi, mimi huwa mwangalifu sana ninapofanya maamuzi ya kitiba.”

      Mfadhaiko huwaathirije madaktari? Tabia ya madaktari ya kutojihusisha kihisia na wagonjwa inaweza kuathiri uhusiano wao na familia zao. Ni vigumu kuepuka tabia hiyo. Madaktari fulani huonyesha huruma nyingi wanapowasaidia wagonjwa kukabiliana na hisia zao. Lakini wanaweza kufanya hivyo kwa kadiri gani bila kuchoka? Hilo ni tatizo kubwa linalowakabili madaktari.

      Wagonjwa Wenye Vichwa Vigumu

      Mara nyingi madaktari wanapoulizwa jambo linalowafadhaisha zaidi wanaposhughulika na wagonjwa, wao husema kwamba wanahangaishwa hasa na wagonjwa wenye vichwa vigumu. Labda unafahamu wagonjwa wenye sifa zifuatazo.

      Kwanza, kuna wagonjwa ambao humpotezea daktari wakati kwa kusema mambo mengi yasiyo na maana bila kueleza matatizo yao. Kisha, kuna wagonjwa ambao humpigia daktari simu usiku au mwishoni mwa juma ijapokuwa hakuna jambo la dharura, au husisitiza wapewe matibabu ambayo daktari hataki kuyapendekeza. Pia, kuna wagonjwa ambao hawamwamini daktari. Wagonjwa fulani hutafuta habari muhimu kuhusu ugonjwa wao katika Intaneti na vyombo vingine, na hilo linaweza kuwasaidia. Hata hivyo, utafiti wao unaweza kuwafanya wamtilie shaka daktari. Huenda daktari asiwe na wakati wa kutosha kueleza faida zote na madhara yote ya matibabu yanayopendekezwa katika utafiti huo. Madaktari hufadhaika sana wagonjwa wanapokataa kufuata maagizo yao kwa sababu ya kutowaamini. Hatimaye, kuna wagonjwa wasio na subira. Wagonjwa hao huacha kutumia dawa kabla hawajapona, kisha wanatafuta matibabu kwingineko.

      Katika maeneo mengine, tatizo kubwa ambalo madaktari wanakabili ni kushughulika na mawakili.

      Madaktari Wenye Tahadhari

      Katika nchi nyingi, kesi zinazowasilishwa mahakamani dhidi ya madaktari zinaongezeka. Mawakili fulani huwasilisha mashtaka madogo-madogo ili wajitajirishe. Msimamizi wa Chama cha Kitiba cha Marekani alisema kwamba kesi hizo “zinafanya bima za madaktari zigharimu pesa nyingi sana.” Anaongeza hivi: “Kesi hizo husababisha mahangaiko mengine. Shtaka la uwongo linaweza kumwathiri sana daktari kwa kumwaibisha, kumpotezea wakati, . . . kumfadhaisha, na kumtia wasiwasi.” Madaktari fulani wamejiua kwa sababu hiyo.

      Hivyo, madaktari fulani hufanya maamuzi kwa kufikiria jinsi watakavyojitetea mahakamani badala ya kujali masilahi ya mgonjwa. Gazeti Physician’s News Digest linasema: “Leo madaktari wengi huwatibu wagonjwa kwa uangalifu sana ili wasishtakiwe.”

      Madaktari wanapozidi kukabili hali ngumu, wengi wao hujiuliza jinsi siku za usoni zitakavyokuwa. Wagonjwa wengi pia hujiuliza swali hilo wanapoona magonjwa fulani yakizidi licha ya maendeleo ya kitiba. Makala inayofuata inawapa madaktari na wagonjwa tumaini zuri la wakati ujao.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

      KUSHIRIKIANA NA DAKTARI

      1. Ili usipoteze wakati, panga mapema jinsi utakavyomweleza daktari tatizo lako kwa ukamili na uanze na mambo muhimu

      2. Ikiwa hakuna jambo la dharura, usimpigie simu daktari wakati ambapo hayuko kazini

      3. Uwe na subira. Uchunguzi kamili na matibabu yanayofaa huchukua muda mrefu

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      ‘KUTIBU MAGONJWA YA KAWAIDA HURIDHISHA’

      “Kazi ya udaktari huku hutofautiana sana na ile ya madaktari katika maeneo yaliyoendelea. Huku, watu huona kwamba wakijifunza kazi fulani wataepuka umaskini, hivyo wengi husomea udaktari. Lakini, madaktari ni wengi na nafasi za kazi ni chache. Hivyo, madaktari hupata mshahara mdogo sana. Ni wagonjwa wachache tu wanaoweza kugharimia matibabu katika hospitali za kibinafsi. Ninafanya kazi katika hospitali iliyojengwa zamani. Paa yake inavuja na ina vifaa duni. Kuna madaktari wawili na wauguzi watano. Tunawahudumia watu 14,000.

      “Nyakati nyingine wagonjwa hufikiri kwamba siwachunguzi vya kutosha, lakini huwezi kumchunguza mgonjwa mmoja kwa muda mrefu ikiwa wagonjwa wengine 25 wanataka kuhudumiwa. Hata hivyo, mimi huridhika ninapowatibu wagonjwa, hata wale wenye magonjwa ya kawaida tu. Kwa mfano, akina mama huwaleta watoto wao ambao wamekuwa wagonjwa kwa sababu ya kukosa chakula cha kutosha, kukosa maji mwilini, na kuendesha. Watoto hao huwa na macho makavu na sura isiyopendeza. Mimi huwaeleza akina mama jinsi ya kutumia maji yenye chumvi, dawa za minyoo, na dawa za kuua viini. Matibabu hayo yakifanikiwa, mtoto huanza kula tena. Juma moja baadaye, mtoto huonekana tofauti—akiwa na macho maangavu, akitabasamu, na kuchezacheza. Nilitaka kuwa daktari ili nifurahie kuwasaidia watu kwa njia kama hizo.

      “Nilitamani kuwatibu wagonjwa tangu nilipokuwa mdogo. Hata hivyo, masomo ya tiba yalibadili kabisa maoni yangu. Niliwaona watu wakifa kwa kukosa kiasi kidogo sana cha pesa walizohitaji ili watibiwe na kuendelea kuishi. Ilinibidi kuwa sugu ili nisihuzunishwe na hali hiyo. Nilianza kuwa na huruma tena nilipoonyeshwa katika Biblia sababu inayofanya watu wateseke na kufahamu kwamba Mungu ana huruma. Siku hizi, ninaweza kulia.”

      [Picha]

      Dakt. Marco Villegas anafanya kazi katika mji fulani wa Amazonia huko Bolivia

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki