-
Je, Sayari Dunia Itaangamizwa Kabisa?Mnara wa Mlinzi—1998 | Juni 15
-
-
Je, Sayari Dunia Itaangamizwa Kabisa?
MWISHO wa karne ya 20 unakaribia, na karne ya 21 iko karibu kuanza. Katika hali hiyo, idadi inayoongezeka ya watu ambao kwa kawaida wangekazia uangalifu mdogo au kutokazia uangalifu wowote unabii mbalimbali wa maangamizo wanajiuliza kama tukio fulani lenye umaana wa kutikisa ulimwengu laweza kutokea karibuni.
Huenda ukawa umeona makala za magazeti juu ya jambo hilo—hata vitabu vizima ambavyo vimezungumzia habari hiyo. Kuhusu ujuzi wa yale yatakayotokea mwanzoni mwa karne ya 21, ni lazima tungoje tuone. Watu fulani husema kwamba kuufikia mwisho wa mwaka wa 2000 hutokeza tofauti ya mwaka mmoja tu (au dakika moja, kutoka mwaka wa 2000 hadi mwaka wa 2001) na yaelekea hautakuwa na matokeo makubwa. Jambo linalohangaisha zaidi watu wengi ni wakati ujao wa sayari yetu ulio mbali.
Unabii mmoja ambao siku hizi hukaziwa mara nyingi wasema kwamba kwenye pindi fulani—iwe ni katika wakati ujao wa karibu au wakati ujao ulio mbali—Dunia sayari yenyewe inakusudiwa kuangamizwa kabisa. Fikiria matabiri machache kama hayo yenye kuhuzunisha.
Katika kitabu chake The End of the World—The Science and Ethics of Human Extinction, kilichochapishwa mara ya kwanza mwaka wa 1996, mwandishi na mwana-falsafa, John Leslie, atoa njia tatu ambazo huenda uhai wa mwanadamu duniani ukaisha. Kwanza, yeye auliza hivi: “Je, vita ya nyuklia yenye kuenea pote ingeweza kumaanisha mwisho wa jamii ya kibinadamu?” Kisha aongeza kusema hivi: “Hali ambayo yawezekana zaidi kuwako . . . ingekuwa kutoweka kabisa kwa uhai kwa sababu ya matokeo ya mnururisho: kansa, kudhoofika kwa mfumo wa kinga hivi kwamba maradhi yenye kuambukiza yaenea pote, au kasoro nyingi za wakati wa kuzaliwa. Kungeweza pia kuwa na vifo vya vijiumbe muhimu kwa hali nzuri ya mazingira.” Uwezekano wa tatu ambao Bw. Leslie atokeza ni kwamba dunia yaweza kugongwa na nyotamkia au sayari ndogo: “Kwa habari ya hizo nyotamkia na sayari ndogo ambazo mizingo yake ni ya kiasi cha kwamba siku moja huenda zikagonga Dunia, yaonekana kunazo zipatazo elfu mbili, zikiwa na kipenyo cha kati ya kilometa moja hadi kilometa kumi. Pia bado kuna idadi ndogo zaidi (kukadiria kungekuwa jambo la kukisia tu) ya nyokamkia kubwa zaidi, na idadi kubwa zaidi ya nyingine ndogo zaidi.”
Ufafanuzi Ulio Wazi wa “Siku ya Maangamizi”
Au fikiria mwanasayansi mwingine, Paul Davies, profesa katika Chuo Kikuu cha Adelaide, Australia. Alifafanuliwa na gazeti la Washington Times kuwa “mwandikaji wa sayansi wa kimataifa aliye bora zaidi.” Katika mwaka wa 1994 aliandika kitabu The Last Three Minutes, ambacho kimeitwa “kielelezo asili cha vitabu vyote vya siku ya maangamizi.” Sura ya kwanza ya kitabu hicho inaitwa “Siku ya Maangamizi,” nayo yafafanua mpangilio wa kuwaziwa wa yale yawezayo kutukia kama nyotamkia ingegonga sayari Dunia. Soma sehemu ya ufafanuzi wake wenye kutia hofu sana:
“Sayari yatetemeka kwa nguvu sawa na mitetemeko ya dunia elfu kumi. Wimbi lenye kishindo la hewa iliyoondolewa mahali pake lapita kwa kasi juu ya uso wa tufe, likiharibu majengo yote, likiponda tikitiki kila kitu njiani mwake. Eneo lililo tambarare kuzunguka sehemu iliyogongwa lainuka kufanyiza milima ya mawe yaliyoyeyuka, yenye urefu wa kilometa kadhaa, kufanyizwa kwa hiyo kukitokeza kreta yenye upana wa kilometa 150 ambayo yaacha wazi sehemu za ndani za Dunia. . . . Safu kubwa mno ya mabaki ya mawe yatandaza katika angahewa, ikifunika jua kabisa lisionekane katika sayari yote. Sasa mahali pa nuru ya jua panachukuliwa na ule mng’ao mkali wenye kumetameta na wenye kuleta maafa ya mabilioni ya nyota zipitazo kwa kasi angani, ukichoma ardhi iliyo chini kwa joto lake lenye kuunguza, huku vitu vilivyoondolewa mahali pake vikianguka tena kwenye angahewa.”
Profesa Davies aendelea kuhusianisha mpangilio huo wa kuwaziwa na ule utabiri kwamba nyotamkia iitwayo Swift-Tuttle ingegonga dunia. Yeye aongeza kuonya kwamba, ingawa tukio kama hilo huenda lisitukie katika wakati ujao ulio karibu, katika maoni yake “karibuni au baadaye, Swift-Tuttle, au kitu kingine chenye kufanana nayo, kitaigonga Dunia.” Mkataa wake wategemea makadirio yadokezayo kwamba, vitu 10,000 vyenye kipenyo cha nusu kilometa au zaidi huzunguka Dunia katika mizingo yenye kupitana.
Je, unaamini kwamba matazamio kama hayo yenye kuogofya ni halisi? Idadi yenye kushangaza ya watu yaamini hivyo. Lakini wao hupuuza hangaiko lolote kwa kujipa moyo kwamba jambo hilo halitatukia katika wakati wao. Ingawa hivyo, kwa nini sayari Dunia iharibiwe—ama karibuni ama mileani nyingi kutoka sasa? Bila shaka, dunia yenyewe siyo chanzo kikuu cha taabu ipatayo wakazi wake, wawe binadamu au wanyama. Kinyume cha hilo, je, mwanadamu siye wa kulaumiwa kwa mengi ya matatizo ya karne hii ya 20 kutia na uwezekano wa ‘kuiangamiza dunia’ kabisa?—Ufunuo 11:18.
Usimamizi Mbaya wa Mwanadamu Warekebishwa
Vipi ule uwezekano zaidi kwamba mwanadamu mwenyewe huenda akaiangamiza au kuiharibu dunia kwa usimamizi wake mbaya na pupa? Ni wazi kwamba uharibifu mkubwa wa sehemu za dunia tayari umetokea kupitia ukataji-misitu kupita kiasi, uchafuzi wa angahewa usiozuiwa, na kuharibiwa kwa mito. Hali hiyo ilitolewa muhtasari kwa kufaa miaka ipatayo 25 iliyopita na waandishi Barbara Ward na René Dubos katika kitabu chao Only One Earth: “Maeneo matatu makubwa ya uchafuzi ambayo ni lazima tuyachunguze—hewa, maji, na udongo—bila shaka yafanyiza sehemu tatu muhimu kwa uhai katika sayari yetu.” Na hiyo hali haijabadilika kimsingi kuwa bora tangu wakati huo, je, imefanya hivyo?
Tunapofikiria uwezekano wa mwanadamu wa kuiangamiza au kuiharibu dunia kwa upumbavu wake mwenyewe, twaweza kutiwa moyo kwa kufikiria uwezo wa kustaajabisha wa sayari Dunia wa kujirudisha na kujirekebisha upya. Akifafanua uwezo huo wa kushangaza wa kujirudisha katika hali yake ya kawaida, René Dubos atoa maoni haya yenye kutia moyo katika kitabu kingine, The Resilience of Ecosystems:
“Watu wengi huhofu kwamba ufahamu kuhusu kudhoofika kwa mazingira umechelewa sana kuja kwa sababu madhara ambayo tayari yamefanyiwa mifumikolojia hayawezi kurekebishwa. Kwa maoni yangu, kutazamia mabaya huko hakuna msingi mzuri kwa sababu, mifumikolojia ina uwezo mkubwa mno wa kujirudisha katika hali yake ya kawaida kutoka katika madhara yenye kuipata.
“Mifumikolojia ina taratibu kadhaa za kujirekebisha. . . . Taratibu hizo huwezesha mifumikolojia kushinda matokeo ya mivurugo kwa kuanzisha tena tu usawaziko wa ikolojia hatua kwa hatua.”
Inawezekana
Kielelezo chenye kutokeza cha jambo hilo katika miaka ya majuzi ni kusafishwa hatua kwa hatua kwa Thames, mto wa London wenye kujulikana sana. Kitabu The Thames Transformed, kilichoandikwa na Jeffery Harrison na Peter Grant, hutoa habari za mafanikio hayo yenye kutokeza ambayo hudhihirisha yale yawezayo kutimizwa watu wafanyapo kazi pamoja kwa manufaa ya umma kwa ujumla. Dyuki wa jiji la Edinburg la Uingereza aliandika katika utangulizi wake kwenye kitabu hicho hivi: “Hatimaye hapa pana simulizi la mafanikio la kiwango kikubwa sana hivi kwamba lastahili kuchapishwa ijapokuwa huenda likawatia moyo watu fulani wadhani kwamba matatizo ya kuhifadhi mazingira kwa kweli si mabaya kama walivyosadikishwa. . . . Wote waweza kuwa na uhakika kutokana na mafanikio ambayo yamepatikana katika Thames. Habari njema ni kwamba inawezekana na mipango yao pia inaweza kufanikiwa.”
Katika sura “Usafishaji Mkubwa,” Harrison na Grant waandika kwa shauku kuhusu yale ambayo yamefanywa kwa mafanikio katika miaka 50 iliyopita: “Kwa mara ya kwanza ulimwenguni, mto uliokuwa umechafuliwa vibaya na wenye viwanda vingi umerekebishwa kwa kiwango kikubwa hivi kwamba ndege wa majini, na samaki wamerudi kwa wingi. Uhakika wa kwamba badiliko kama hilo limetokea kwa haraka hivyo, katika hali ambayo mwanzoni ilionekana isiyo na tumaini, watoa kitia-moyo hata kwa mhifadhi wanyama mwenye kutarajia mabaya zaidi.”
Kisha Harrison na Grant wafafanua hilo badiliko hivi: “Hali ya huo mto ilizidi kuharibika kadiri miaka ilivyopita, labda, pigo la mwisho likija wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili wakati ambapo karakana za kusafisha maji machafu na mabomba ya maji machafu yalipoharibika. Wakati wa miaka ya 1940 na 1950, hali ya Thames ilikuwa katika kiwango cha chini zaidi. Huo mto ulikuwa sawa na mtaro wa takataka ulio wazi; maji yalikuwa meusi, bila oksijeni, na wakati wa miezi ya kiangazi uvundo kutoka Thames ulisikika katika eneo kubwa. . . . Hatimaye samaki waliokuwako kwa wingi walikuwa wamefukuzwa, isipokuwa mikunga wachache walioweza kubaki hai kwa sababu ya uwezo wao wa kupumua moja kwa moja kutoka sehemu ya juu ya maji. Ndege wa maeneo ya ndani yaliyo mapana na wazi, yenye kujaa majengo kati ya London na Woolwich, walipungua wakabaki bata-mwitu na bata weupe wachache, nao walikuwa hai kwa sababu ya nafaka iliyomwagika kutoka katika gati za nafaka wala si kwa sababu ya ugavi wa chakula cha asili. . . . Basi ni nani angeliamini urekebishaji wenye kutazamisha ambao ulikuwa karibu kutokea? Katika muda wa miaka kumi maeneo hayohayo ya mto yasiyo na chochote yangebadilishwa na kuwa kimbilio la spishi nyingi za ndege wa majini, kutia na ndege wanaokuja kupisha majira ya baridi kali, ambao idadi yao hufika bata-mwitu 10,000 na vitwitwi 12,000.”
Bila shaka, hayo yafafanua badiliko moja tu katika sehemu ndogo moja ya tufe. Hata hivyo, twaweza kujifunza mengi kutokana na kielelezo hicho. Chaonyesha kwamba sayari Dunia haipasi kufikiriwa kwamba itaangamizwa kwa sababu ya usimamizi mbaya, pupa na kutojali kwa mwanadamu. Elimu ifaayo na jitihada yenye muungano kwa manufaa ya wanadamu kwa ujumla yaweza kusaidia dunia kurekebisha uharibifu wa ikolojia yake, mazingira, na uso wa nchi. Lakini vipi maangamizi yawezayo kutokana na kani zitokazo nje, kama vile nyotamkia au sayari ndogo zenye kuzunguka huku na kule?
Makala inayofuata ina jibu lenye kuridhisha kwa swali hilo lenye kutatanisha.
-
-
Dunia—Kwa Nini Iko Hapa?Mnara wa Mlinzi—1998 | Juni 15
-
-
Dunia—Kwa Nini Iko Hapa?
Kuna swali upaswalo kufikiria: Je, sayari yetu nzuri ilitokezwa na Muumba mwenye akili ambaye ana kusudi fulani kwa dunia na kwa wanadamu wanaoishi juu yake? Kutatua suala hilo kwa kukuridhisha kwaweza kukusaidia uelewe wakati ujao una nini kwa ajili ya sayari yetu.
WANASAYANSI wengi ambao wamechunguza ulimwengu na dunia yetu kwa undani, wameona uthibitisho mbalimbali wenye kuonyesha kuwako kwa Muumba, kwamba Mungu ndiye aliyeiumba. Fikiria maelezo kutoka kwa mwanasayansi mmoja tu:
Profesa Paul Davies aandika katika kitabu The Mind of God: “Kuwako kwa ulimwengu wenye utaratibu, na upatano, wenye miundo imara iliyo na utaratibu na utata, kwahitaji sheria na hali za aina ya pekee sana.”
Baada ya kuzungumzia “sadfa” kadhaa ambazo waastrofizikia na wengineo wamezifahamu, Profesa Davies aongeza kusema hivi: “Mtu afikiriapo sadfa hizi kwa pamoja, hizo huandaa uthibitisho wenye kuvutia kwamba, uhai kama tuujuavyo hutegemea kwa njia nyetivu sheria muhimu za fizikia, na pia aksidenti ambazo huonekana kutokea bila kutarajiwa katika takwimu halisi ambazo ulimwengu umeteua ili kutokeza uzito mbalimbali wa mata zilizo ndogo zaidi, kani ya uwezo, na kadhalika. . . . Yatosha kusema kwamba, kama tungejifanya kuwa Mungu na kuteua takwimu za uzito huo mbalimbali vile tupendavyo kwa kugeuza seti ya vifundo, tungepata kwamba namna ambavyo tumegeuza vifundo hivyo vyote, ingefanya ulimwengu uwe usioweza kukalika. Katika visa fulani yaonekana kana kwamba vifundo tofauti-tofauti lazima viwekwe katika hali nzuri kabisa ikiwa ulimwengu utakuwa katika hali itakayofanya uhai usitawi. . . . Uhakika wa kwamba hata mabadiliko madogo ya namna mambo yalivyo, yaweza kufanya ulimwengu usiweze kufanyiwa uchunguzi, bila shaka ni jambo la hakika, lenye umaana mkubwa.”
Kwa watu wengi matokeo ya uchunguzi ulio hapo juu yamaanisha kwamba, dunia yetu pamoja na ulimwengu wote, ulitokezwa na Muumba mwenye kusudi. Ikiwa ndivyo ilivyo, twahitaji kwanza kabisa kujua ni kwa nini aliiumba dunia. Twahitaji pia kuhakikisha, tukiweza, kusudi lake kwa dunia ni nini. Kwa habari hii, jambo lisilo la kawaida hutokea. Licha ya kupendwa kwa uatheisti kulikoenea pote, idadi ya watu yenye kushangaza bado huamini katika Muumba mwenye akili. Makanisa yaliyo mengi ya Jumuiya ya Wakristo husema tu juu ya Mungu mweza yote na Muumba wa ulimwengu wetu. Hata hivyo, ni mara chache dini hizi husema kwa uhakika na usadikisho juu ya wakati ujao wa dunia katika kusudi la Mungu.
Biblia Husema Nini?
Ni jambo la akili kutegemea chanzo cha habari ambacho kimekubaliwa na wengi kuwa kimetoka kwa Muumba. Chanzo hicho ni Biblia. Mojawapo ya taarifa zake iliyo rahisi na wazi zaidi kuhusiana na wakati ujao wa dunia yetu, yapatikana kwenye Mhubiri 1:4. Twasoma hivi: “Kizazi huenda, kizazi huja; nayo dunia hudumu daima.” Biblia hueleza waziwazi ni kwa nini Yehova Mungu aliiumba dunia. Yaonyesha pia kwamba aliiweka katika mahali paifaapo kabisa katika ulimwengu na kuhusiana na jua letu, ili kutegemeza uhai juu yake. Mungu Mweza Yote alimpulizia nabii wa kale, Isaya, aandike hivi: “Maana BWANA, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine.”—Isaya 45:18.
Lakini vipi njia anazositawisha mwanadamu za kuharibu uhai wote duniani? Katika hekima yake isiyolinganika, Mungu atangaza kwamba ataingilia kabla ya wanadamu kuweza kuharibu uhai wote kwenye sayari yetu. Ona ahadi hii yenye kutumainisha katika Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia: “Mataifa wakawa na hasira ya kisasi, na hasira ya kisasi yako mwenyewe ikaja, na wakati uliowekwa rasmi kwa ajili ya wafu kuhukumiwa, na kuwapa thawabu yao watumwa wako hao manabii na watakatifu na wale wanaohofu jina lako, wadogo na wakubwa, na kuwaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.”—Ufunuo 11:18.
Yehova hutufunulia lile lililokuwa kusudi lake la awali la kuiumba dunia, kito hiki katika anga, kama vile mwanaanga mwenye kuzunguka dunia alivyoifafanua. Mungu aliikusudia iwe paradiso ya tufeni pote, ikiwa imekaliwa na wanadamu kwa furaha—wanaume kwa wanawake—wote wakiishi kwa amani na upatano. Alipanga kujaza watu kwenye sayari hatua kwa hatua kwa kuwaruhusu wanadamu wawili wa kwanza wazae watoto. Ili awafurahishe wenzi wawili wa kwanza wa kibinadamu, Yehova alikuwa ameifanya sehemu ndogo ya dunia iwe paradiso. Kwa vile uzazi wa familia za kibinadamu ungeendelea kwa miaka na karne nyingi, bustani ya Edeni ingepanuka hatua kwa hatua hadi wakati ambapo andiko la Mwanzo 1:28 lingetimizwa: “Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.”
Tuonapo sasa hali yenye kusikitisha ya dunia na ya wakazi wake, je, hilo humaanisha kwamba kusudi la Mungu la awali kwa dunia limeshindwa? Au je, amebadili kusudi lake na kuamua kwamba kwa sababu ya upotovu wa wanadamu, ataruhusu sayari iangamizwe kabisa na kuanza mambo upya? La, twaweza kuwa na uhakika kwamba hakuna yoyote ya hali hizo za mambo itakuwa hivyo. Biblia hutuambia kwamba chochote ambacho Yehova hukusudia ni lazima hatimaye kitukie, kwamba chochote aamuacho hakiwezi kuzuiwa na mtu yeyote au hata jambo lisilotarajiwa. Yeye atuhakikishia hivi: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:11.
Kusudi la Mungu Lilikatizwa, Si Kubadilishwa
Kwa sababu ya uasi wa Adamu na Hawa na kufukuzwa kwao kutoka katika bustani ya Edeni, ilikuwa wazi kwamba kusudi la Mungu la kuwa na dunia iliyo paradiso lingetimizwa bila wao kuwako. Hata hivyo, Yehova alionyesha papo hapo kwamba baadhi ya watoto wao wangetekeleza amri yake ya awali. Ni kweli, hilo lingechukua wakati, hata karne nyingi, lakini hakuna jambo lionyeshalo ni wakati mwingi kadiri gani ambao ungalihusika katika kutekeleza amri hiyo ya awali, hata kama wote wawili, Adamu na Hawa wangaliendelea kuishi wakiwa wakamilifu. Jambo la hakika ni kwamba, kufikia mwisho wa Utawala wa Milenia wa Kristo Yesu—miaka zaidi ya elfu moja kuanzia sasa—hali za Kiparadiso za Edeni zitaenea duniani pote na sayari Dunia itakaliwa na wazao wenye amani na furaha wa wanadamu wawili wa kwanza. Kwa kweli, uwezo wa Yehova akiwa Mkusudiaji asiyeweza kukosea utatetewa kwa umilele!
Kisha kutakuwa na utimizo wa unabii mbalimbali wenye kusisimua ambao Mungu alipulizia muda mrefu uliopita. Maandiko kama vile Isaya 11:6-9 yatatimizwa kwa utukufu: “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. Ng’ombe na dubu watalisha pamoja; watoto wao watalala pamoja; na simba atakula majani kama ng’ombe. Na mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia mkono wake katika pango la fira. Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”
Afya mbaya na ugonjwa wenye kuleta kifo yatakuwa mambo ya wakati uliopita kama vile kifo chenyewe kitakavyokuwa. Je, kuna jambo lolote liwezalo kuwa dhahiri zaidi ya maneno hayo sahili yapatikanayo katika kitabu cha mwisho cha Biblia? “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.
Naam, twaweza kujipa moyo—sayari yetu Dunia iliyo nzuri itadumu. Na liwe pendeleo lako kuokoka mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo pamoja na mazoea yake yenye kuangamiza dunia. Ulimwengu mpya ulio safi wenye kutokezwa na Mungu uko karibu. Na wapendwa wengi wataamka kutoka katika kifo kupitia muujiza wa ufufuo. (Yohana 5:28, 29) Kwa kweli, dunia yetu itadumu, nasi twaweza kudumu pamoja nayo na kuifurahia.
-