-
Sanamu za Kuchorwa—Zilianza Kutumiwa ZamaniMnara wa Mlinzi—2002 | Julai 1
-
-
Sanamu za Kuchorwa—Zilianza Kutumiwa Zamani
“Sanamu za kuchorwa hutusaidia kukaribia wema na utakatifu wa Mungu na Watakatifu wake.”—ASKOFU MKUU WA KANISA LA OTHODOKSI LA UGIRIKI HUKO AUSTRALIA
NI SIKU yenye joto kali sana ya mwezi wa Agosti na jua linaangaza kwenye ngazi zinazoelekea kwenye nyumba ya watawa ya “Mama Mtakatifu Zaidi wa Mungu,” kwenye kisiwa cha Tínos, katika Bahari ya Aegea. Joto hilo kali halipunguzi bidii ya wahiji zaidi ya 25,000 wa Kanisa la Othodoksi la Ugiriki ambao wanatembea polepole wakijitahidi kuifikia sanamu ya kuchorwa iliyopambwa sana ya mama ya Yesu.
Msichana mdogo aliyelemaa na mwenye maumivu na mfadhaiko atembea kwa magoti yanayovuja damu nyingi. Karibu naye kuna mwanamke mzee aliyesafiri kutoka mbali na ingawa amechoka, yeye anaendelea tu kukokota miguu yake. Mwanamume wa makamo atoa jasho jingi anapojikakamua kwa hamu na kwa wasiwasi kupita katikati ya umati unaosukumana. Wote wanataka kuifikia sanamu hiyo ya Maria ili kuibusu na kuisujudia.
Bila shaka watu hawa wenye kushikilia dini sana wanataka kumwabudu Mungu kwa unyofu. Hata hivyo, ni wangapi kati yao wanaojua kwamba ibada ya sanamu za kuchorwa ilianzishwa na wapagani karne nyingi kabla ya Ukristo?
Kuenea kwa Sanamu za Kuchorwa
Katika maeneo ambako watu wanafuata imani ya Kiothodoksi, sanamu za kuchorwa zinapatikana kila mahali. Sanamu za Yesu, Maria, na “watakatifu” wengine wengi huonwa kuwa muhimu sana katika makanisa. Mara nyingi watu wa dini hutukuza sanamu hizo kwa kuzibusu, kuchoma uvumba, na kuwasha mishumaa. Zaidi ya hayo, karibu wafuasi wote wa Kanisa la Othodoksi wametenga mahali fulani pa kuweka sanamu na kutolea sala katika nyumba zao. Ni jambo la kawaida kwa wafuasi wa Kanisa la Othodoksi kusema kwamba kuabudu sanamu huwafanya wawe karibu na Mungu. Wengi huamini kwamba Mungu amezipa sanamu hizo utakatifu na uwezo wa kufanya miujiza.
Yaelekea waumini hao wangeshangaa kujua kwamba Wakristo wa karne ya kwanza hawakutumia sanamu za kuchorwa katika ibada yao. Kitabu Byzantium kinasema: ‘Wakristo wa mapema walichukia kabisa kuabudu picha za watakatifu. Waliwaiga wafuasi wa dini ya Kiyahudi ambao walichukia sana ibada ya sanamu.’ Kitabu hicho kinasema: ‘Kuanzia Karne ya Tano na kuendelea sanamu za kuchorwa ziliabudiwa sana hadharani na faraghani.’ Ikiwa Wakristo wa karne ya kwanza hawakuabudu sanamu hizo, basi zoea hilo lilianzia wapi?
Chanzo cha Sanamu za Kuchorwa
Mtafiti aitwaye Vitalij Ivanovich Petrenko aliandika: “Ibada ya sanamu na pia desturi zinazoambatana na zoea hilo zilianza kabla ya Ukristo na ‘zilianzishwa na wapagani.’” Wanahistoria wengi hukubaliana naye na kusema kwamba ibada ya sanamu za kuchorwa ilianza katika dini za kale za Babiloni, Misri, na Ugiriki. Kwa mfano, katika Ugiriki ya kale watu waliamini kwamba sanamu zilikuwa na uwezo kama wa Mungu. Wengine walifikiri kwamba baadhi ya sanamu hizo hazikutengenezwa na wanadamu bali zilishuka kutoka mbinguni. Wakati wa misherehekeo ya kipekee watu waliandamana jijini wakiwa wamebeba sanamu hizo na kuzitolea dhabihu. ‘Watu wa kidini waliziona sanamu hizo kuwa miungu ingawa jitihada zilikuwa zimefanywa kuwaeleza tofauti kati ya mungu na sanamu,’ akasema Petrenko.
Imani na mazoea hayo yalipenyaje katika Ukristo? Mtafiti huyo alisema kwamba, karne kadhaa baada ya kifo cha mitume wa Kristo, “imani ya Kikristo, hasa huko Misri, ilikabiliwa na ‘imani mbalimbali za kipagani’ ambazo zilitokana na desturi na imani za Wamisri, Wagiriki, Wayahudi, na watu wa Mashariki na Waroma. Imani hizo zilichanganywa na mafundisho na desturi za Kikristo.’” Kwa sababu hiyo, ‘watengenezaji stadi wa sanamu za Kikristo walianza kuchanganya mafundisho ya dini mbalimbali kwa kutengeneza sanamu ambazo walizifanya zionekane kama za Kikristo ingawa bado zilikuwa za kipagani.’
Muda si muda watu walianza kuabudu sanamu hizo faraghani na hadharani. Katika kitabu The Age of Faith mwanahistoria Will Durant anaeleza jinsi jambo hilo lilivyotukia kwa kusema: ‘Idadi ya watakatifu wenye kuabudiwa ilipoongezeka, ilihitajika kuwatambulisha na kuwakumbuka. Kwa hiyo picha zilichorwa kwa wingi kuwakilisha watakatifu hao kutia ndani na Maria. Sanamu za Kristo zenye sura ya kuwaziwa tu pamoja na msalaba wake zilianza kuabudiwa. Watu wa kawaida walitumia sanamu hizo kama hirizi. Watu walianza kufikiri kwamba sanamu na picha za watakatifu wa zamani zingepasa kutukuzwa. Hata walianza kuziabudu kwa kuzisujudu, kuzibusu, kuwasha mishumaa, na kuchoma uvumba. Walizipamba kwa maua na kuzitazamia zifanye miujiza. Mara nyingi Mababa na vilevile washiriki wa mabaraza ya Kanisa waliwaeleza watu kwamba sanamu hizo hazikuwa miungu bali ziliwakumbusha tu miungu yao, lakini watu hawakujali.’
Leo, huenda watu wengi wanaotumia sanamu hizo za kuchorwa wakasema kwamba wanaziheshimu tu, hawaziabudu. Huenda wakasema kwamba sanamu hizo zinafaa na huwasaidia sana kumwabudu Mungu. Labda hata wewe una maoni kama hayo. Lakini swali ni, Mungu ana maoni gani kuhusu sanamu za kuchorwa? Je, huenda ikawa kutukuza sanamu hizo ni sawa na kuziabudu? Je, mazoea hayo yanaweza kukuathiri bila kujua?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]
Sanamu za Kuchorwa Ni Nini?
Tofauti na sanamu za kuchongwa ambazo Wakatoliki hutumia sana katika ibada yao, kuna picha au sanamu za kuchorwa za Kristo, Maria, “watakatifu,” malaika, watu, na matukio fulani katika Biblia au katika historia ya Kanisa la Othodoksi. Kwa kawaida picha hizo huchorwa kwenye ubao unaoweza kubebeka.
Kulingana na Kanisa la Othodoksi “michoro hiyo ya Watakatifu ni tofauti na picha za wanadamu wa kawaida.” Pia, picha hizo zilichorwa bila kuonyesha kama vitu fulani vilikuwa mbali na vingine vilikuwa karibu. Kwa kawaida ‘michoro hiyo haina vivuli wala haionyeshi kama ni mchana au ni usiku.’ Pia inaaminiwa kwamba Mungu ‘anaweza kuwa ndani’ ya mbao na rangi ya picha hizo.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Matumizi ya sanamu yalitokana na wapagani
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
© AFP/CORBIS
-
-
Mwabudu Mungu “Katika Roho”Mnara wa Mlinzi—2002 | Julai 1
-
-
Mwabudu Mungu “Katika Roho”
“Basi, mtamlinganisha Mungu na nani? Au mtamfananisha na mfano [“sanamu,” NW] wa aina gani?” ISAYA 40:18
LABDA unaamini kabisa kwamba kutumia sanamu za kuchorwa kunakubalika katika kumwabudu Mungu. Huenda ukaona kwamba sanamu hizo zinaweza kuboresha uhusiano wako na Msikiaji wa sala, ambaye anaweza kufikiriwa kwamba hana utu kwa kuwa haonekani.
Lakini je, sisi tu huru kabisa kuamua jinsi tutakavyomwabudu Mungu? Je, si Mungu ndiye mwenye mamlaka ya kuamua njia inayokubalika na isiyokubalika? Yesu alieleza maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo aliposema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6)a Maneno hayo yanaonyesha kwamba hatupaswi kutumia sanamu za kuchorwa au vitu vingine vitakatifu katika ibada.
Naam, kuna ibada fulani hususa ambayo Yehova Mungu hukubali. Ibada ipi? Katika pindi nyingine, Yesu alisema hivi: “Saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”—Yohana 4:23, 24.
Je, Mungu ambaye “ni roho” anaweza kuwakilishwa na sanamu? La. Hata sanamu ya kuchorwa iwe nzuri namna gani, haiwezi kuufikia utukufu wa Mungu. Kwa hiyo sanamu inayosemekana inamwakilisha Mungu haiwezi kuonyesha kikweli jinsi alivyo. (Waroma 1:22, 23) Je, mtu anaweza kuwa ‘anaabudu katika kweli’ ikiwa anamwabudu Mungu kupitia picha fulani iliyochorwa na binadamu?
Fundisho la Biblia Lililo Wazi
Sheria ya Mungu ilikataza kutengeneza sanamu kwa ajili ya ibada. Amri ya pili katika zile Amri Kumi inasema: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu chochote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia.” (Kutoka 20:4, 5) Pia Maandiko ya Kikristo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yanaamuru hivi: “Ikimbieni ibada ya sanamu.”—1 Wakorintho 10:14.
Kwa kweli, wengi husisitiza kwamba hawaabudu sanamu wanapozitumia katika ibada. Kwa mfano, mara nyingi Wakristo wa Kanisa la Othodoksi husema kwamba hawaabudu sanamu za kuchorwa ambazo wao huzisujudia, kuzipigia magoti, na kusali mbele yake. Kasisi mmoja wa Kanisa la Othodoksi aliandika: “Sisi hutukuza sanamu hizo kwa sababu ni takatifu, na kwa sababu tunaheshimu yule zinayemwakilisha.”
Hata hivyo, swali linabaki: Je, Mungu hukubali sanamu za kuchorwa zitumiwe kwa kusudi la kumtukuza? Biblia haisemi tunapaswa kufanya hivyo. Waisraeli walipotengeneza sanamu ya ndama, wakidai eti walikusudia kumwabudu Yehova, yeye alikataa kabisa ibada hiyo na kusema kwamba walikuwa wameasi imani.—Kutoka 32:4-7.
Hatari Iliyofichika
Ni hatari kutumia sanamu katika ibada. Huenda kufanya hivyo kukawashawishi watu waanze kuabudu sanamu inayosemekana inamwakilisha Mungu badala ya kumwabudu Mungu mwenyewe. Yaani, wanaifanya sanamu hiyo kuwa kitu cha kuabudiwa.
Vitu kadhaa vilianza kuabudiwa katika siku za Waisraeli. Kwa mfano, Musa alitengeneza nyoka ya shaba wakati Waisraeli walipokuwa wakisafiri nyikani. Mwanzoni, mfano huo wa nyoka ulikuwa wa kuponya. Wale walioadhibiwa kwa kuumwa na nyoka wangetazama nyoka hiyo ya shaba na Mungu angewasaidia. Lakini inaonekana kwamba baada ya Waisraeli kuingia katika Bara Lililoahidiwa, waligeuza nyoka hiyo ya shaba kuwa sanamu ya kuabudiwa kana kwamba nyoka yenyewe ilikuwa na uwezo wa kuponya. Waliichomea uvumba na hata kuipa jina, Nehushtani.—Hesabu 21:8, 9; 2 Wafalme 18:4.
Waisraeli pia walijaribu kutumia sanduku la agano kama kifaa cha uchawi dhidi ya maadui wao, lakini wakashindwa vibaya. (1 Samweli 4:3, 4; 5:11) Katika siku za Yeremia, raia wa Yerusalemu walijali zaidi hekalu kuliko walivyojali ibada ya Mungu iliyofanywa humo hekaluni.—Yeremia 7:12-15.
Leo watu wengi bado wana maelekeo ya kuabudu vitu badala ya kumwabudu Mungu. Mtafiti aitwaye Vitalij Ivanovich Petrenko alisema: ‘Mtu anapoanza kuabudu sanamu ya kuchorwa, anakabiliwa na hatari ya kuwa mwabudu sanamu. Ni wazi kwamba kuabudu vitu ni zoea la kipagani ambalo limegeuzwa kuwa ibada ya sanamu za kuchorwa kupitia mafundisho yanayopendwa na wengi.’ Vivyo hivyo, kasisi wa Kanisa la Othodoksi la Ugiriki Demetrios Constantelos anasema hivi katika kitabu chake Understanding the Greek Orthodox Church: ‘Inawezekana kwa Mkristo kuanza kuabudu sanamu ya kuchora.’
Yale madai kwamba sanamu za kuchorwa husaidia tu watu katika ibada yanatiliwa shaka sana. Kwa nini? Je, si kweli kwamba sanamu fulani za Maria au za “watakatifu” zinaonwa kuwa zinastahili ujitoaji zaidi na zina uwezo mkubwa zaidi ya sanamu nyingine za watu haohao waliokufa zamani? Kwa mfano, huko Tínos, Ugiriki, kuna wafuasi fulani wa Kanisa la Othodoksi ambao wamejitoa kwa sanamu moja ya kuchorwa ya Maria, na kuna wengine ambao wamejitoa kwa sanamu nyingine ya Maria huko Soumela, kaskazini mwa Ugiriki. Vikundi hivyo viwili vinaamini kwamba sanamu yao ndiyo ina uwezo zaidi wa kufanya miujiza, ingawa sanamu zote mbili zinawakilisha mtu yuleyule aliyekufa zamani. Hivyo, kihalisi watu huona kwamba sanamu fulani za kuchorwa zina nguvu nao huziabudu.
Kusali kwa “Watakatifu” au Maria?
Namna gani kuabudu watu fulani kama Maria au “watakatifu”? Yesu alipojaribiwa na Shetani, alimjibu hivi akitumia andiko la Kumbukumbu la Torati 6:13: “Uabudu Bwana Mungu wako, umutumikie yeye peke yake.” (Mathayo 4:10, Zaire Swahili Bible) Baadaye alisema kwamba waabudu wa kweli watamwabudu “Baba,” peke yake. (Yohana 4:23) Kwa kujua hayo, malaika mmoja alimkemea mtume Yohana aliyejaribu kumwabudu, akisema: “Usifanye hivi, . . . abudu Mungu.”—Ufunuo 22:9, ZSB.
Je, inafaa kusali kwa Maria, mama ya Yesu, au kusali kwa “watakatifu” fulani, ukiwataka wakuombee kwa Mungu? Biblia inatoa jibu lililo wazi kabisa: “Mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, mwanadamu Kristo Yesu.”—1 Timotheo 2:5.
Linda Uhusiano Wako Pamoja na Mungu
Kutumia sanamu za kuchorwa katika ibada, ni kinyume cha mafundisho ya Biblia na hakuwezi kuwasaidia watu kupata kibali cha Mungu au kupata wokovu. Kinyume cha hilo, Yesu alisema kwamba tunaweza kupata uhai wa milele kwa kumjua Mungu wa pekee wa kweli, kufahamu utu wake usio na kifani, na pia makusudi yake na jinsi anavyoshughulika na wanadamu. (Yohana 17:3) Sanamu za kuchorwa ambazo hazina uwezo wa kuona, kuhisi, au hata kuongea haziwezi kumsaidia mtu amjue Mungu ili kumwabudu kwa njia inayokubalika. (Zaburi 115:4-8) Tunaweza kujifunza mambo muhimu sana kumhusu Mungu wa pekee wa kweli kupitia Neno lake, Biblia.
Kuabudu sanamu za kuchorwa hakutunufaishi, bali kunaweza kuleta hatari ya kiroho. Namna gani? Kwanza kabisa jambo hilo linaweza kuharibu uhusiano wetu na Yehova. Kuhusu Waisraeli ‘waliomkasirisha kwa sanamu zenye kuchukiza,’ Mungu alitabiri hivi: “Nitaficha uso wangu.” (Kumbukumbu la Torati 32:16, 20, The New American Bible) Ili kurudisha uhusiano wao pamoja na Mungu walihitaji ‘kutupa sanamu zao.’—Isaya 31:6, 7.
Kwa hiyo, ushauri huu wa Kimaandiko unafaa: “Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu.”—1 Yohana 5:21.
[Maelezo ya Chini]
a Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, Maandiko yote yamenukuliwa katika Biblia ya Union Version.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Watu Waliosaidiwa Kuabudu “Katika Roho”
Olivera alikuwa mfuasi mwenye bidii wa Kanisa la Othodoksi la Albania. Wakati nchi hiyo ilipopiga dini marufuku mwaka wa 1967, Olivera aliendelea kuabudu kisiri. Alitumia malipo yake kidogo ya uzeeni kununua uvumba, mishumaa, na sanamu za kuchorwa za dhahabu na fedha. Alificha vitu hivyo kitandani mwake na mara nyingi alilala kwenye kiti fulani kilichokuwa karibu na kitanda chake kwa kuwa hakutaka vitu hivyo vionekane au viibwe. Alipotembelewa na Mashahidi wa Yehova mapema miaka ya 1990, Olivera alitambua kwamba ujumbe wao ulikuwa wa kweli na ulitoka katika Biblia. Alielewa maana ya kuabudu “katika roho” kulingana na Biblia, na akajifunza maoni ya Mungu kuhusu kutumia sanamu za kuchorwa. (Yohana 4:24) Shahidi aliyejifunza Biblia pamoja naye aligundua kwamba idadi ya sanamu zilizokuwa nyumbani kwa Olivera ilizidi kupungua kila mara alipomtembelea. Mwishowe Olivera hakuwa na sanamu yoyote. Baada ya kubatizwa, Olivera alisema: “Leo, badala ya kuwa na sanamu za kuchorwa zisizoweza kunisaidia, nina roho takatifu ya Yehova. Ninashukuru sana kwa kuwa ninaweza kupata roho yake bila kutumia sanamu.”
Athena, kutoka kisiwa cha Lesbos, huko Ugiriki, alikuwa mfuasi mwenye bidii sana wa Kanisa la Othodoksi. Alikuwa mmoja wa wanakwaya na alifuata mapokeo ya kanisa kwa makini sana kutia ndani kuabudu sanamu za kuchorwa. Mashahidi wa Yehova walimsaidia Athena kufahamu kwamba kuna mambo fulani aliyofunzwa ambayo yalikuwa kinyume cha Biblia. Mambo hayo yalitia ndani kuabudu sanamu za kuchorwa na misalaba. Athena aliamua kufanya uchunguzi wake mwenyewe kuhusu chanzo cha sanamu hizo. Baada ya kuchunguza kwa kina katika vitabu fulani vinavyozungumzia sanamu, alipata uthibitisho wa kwamba chanzo cha sanamu hizo si cha Kikristo. Kwa kuchochewa na tamaa ya kumwabudu Mungu “katika roho,” Athena aliharibu sanamu zake, ingawa zilikuwa za pesa nyingi. Hata hivyo, Athena hakujali hasara aliyopata mradi tu angeweza kumwabudu Mungu katika njia inayokubalika na safi kiroho.—Matendo 19:19.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]
Je, Sanamu za Kuchorwa Ni Kazi ya Sanaa Tu?
Katika miaka ya hivi majuzi, sanamu za kuchorwa za Kanisa la Othodoksi zimekusanywa kote ulimwenguni. Wanaokusanya sanamu hizo huziona kuwa vitu vya sanaa tu vinavyoonyesha utamaduni wa Byzantium wala hawavioni kuwa vitu vitakatifu vya kidini. Ni kawaida kuona mtu asiyeamini kuwa kuna Mungu amepamba nyumba au ofisi yake kwa sanamu hizo.
Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawasahau kusudi kuu la sanamu ambalo ni ibada. Ingawa Wakristo hawawakatazi wengine kuweka sanamu, wao hawaziweki hata kama ni kwa kusudi la kuzikusanya tu. Jambo hilo linapatana na kanuni inayopatikana kwenye andiko la Kumbukumbu la Torati 7:26: “Machukizo [sanamu zinazotumiwa katika ibada] usitie ndani ya nyumba yako, usije wewe kuwa kitu cha haramu mfano wake; ukichukie kabisa, na kukikataa kabisa.”
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mungu hakukubali sanamu zitumiwe katika ibada
[Picha katika ukurasa wa 8]
Ujuzi wa Biblia hutusaidia kumwabudu Mungu katika roho
-