-
Kujinyima Chakula na Kuwa na Hamu ya Chakula Isiyo ya Kawaida—Mambo Hakika, HatariAmkeni!—1999 | Januari 22
-
-
Kujinyima Chakula—Njaa ya Kujiletea
Watu wanaoteseka kwa kujinyima chakula, ama hukataa kula au hula kiasi kidogo sana hivi kwamba wanakosa lishe ya kutosha. Mfikirie Antoinette mwenye umri wa miaka 17, anayesema kwamba wakati fulani huenda uzito wake ulipungua kufikia kilogramu 37—uzito kidogo sana kwa kijana mwenye urefu wa futi tano na inchi saba. “Sikula zaidi ya kalori 250 kwa siku na niliandika kwenye kitabu chakula nilichokula,” yeye asema.
Watu wanaojinyima chakula wana hofu ya chakula, na watafanya yote wawezayo ili kujizuia kuongeza uzito. “Nilianza kutema chakula changu kwenye karatasi ya kupangusia mdomo nikijifanya kwamba nilikuwa nikipangusa mdomo wangu,” asema Heather. Susan alifanya mazoezi kwa bidii ili kupunguza uzito wake. “Karibu kila siku,” asema, “nilikimbia kilometa 12, au kuogelea kwa muda wa saa moja, au sivyo nilihisi wasiwasi na hatia iwapo sikufanya mazoezi. Na kila asubuhi nilifurahia sana, kwa kawaida furaha yangu pekee, kupanda juu ya mizani ili kuthibitisha kwamba uzito wangu ulipungua kilogramu 45.”
Jambo la kinyume, watu fulani wanaojinyima chakula huwa wapishi bora na wataandaa chakula kitamu sana ambacho wao wenyewe hukataa kukionja. “Hali yangu ilipokuwa mbaya sana,” asema Antoinette, “nilitayarisha chakula chote cha mchana nyumbani na kuwatayarishia ndugu na dada yangu mdogo chakula cha kubeba. Singewaruhusu wakaribie friji. Nilihisi kana kwamba jiko lilikuwa langu peke yangu.”
Kulingana na kitabu A Parent’s Guide to Anorexia and Bulimia, watu fulani wanaojinyima chakula “huwa safi kupita kiasi na waweza kuwadai wengine katika familia nzima wafikie viwango vyao visivyo halisi na visivyofikika. Hakuna gazeti au viatu au kikombe cha kahawa kiwezacho kuachwa mahali pasipopafaa hata kwa dakika chache. Huenda wakahangaikia sana afya ya kibinafsi na sura, wakitumia muda mwingi kuvalia, mlango ukiwa umefungwa na kuwakataza wengine wasiingie ili kujitayarisha kwenda shuleni au kazini.”
Tatizo hili la kujinyima chakula husitawi namna gani? Hasa, tineja au mtu mzima mchanga—mara nyingi mwanamke—huanza harakati za kupunguza ratili kadhaa. Hata hivyo, anapofikia mradi wake, hukosa kuridhika. Anapojitazama kwenye kioo, bado hujiona kuwa mnene, na kwa hiyo anaamua kwamba litakuwa jambo bora kupunguza ratili nyingine chache. Jambo hili huendelea mpaka mwenye kupunguza uzito anapofikia asilimia 15 au zaidi chini ya kiwango cha kawaida kwa urefu wake.
Kufikia kiwango hiki marafiki na washiriki wa familia huanza kuonyesha wasiwasi kwamba mwenye kupunguza uzito anaonekana mwembamba sana, hata kuwa amedhoofika. Lakini mtu anayejinyima chakula huona mambo kwa njia tofauti. “Sikudhani nilionekana nimekonda,” asema Alan, mwanamume mwenye urefu wa futi tano na inchi tisa anayejinyima chakula ambaye wakati mmoja uzito wake ulipungua na kufikia kilogramu 33. “Kadiri upunguzavyo uzito,” asema, “ndivyo akili yako hupotoka na kukosa kujiona waziwazi.”a
Baada ya muda, kujinyima chakula kwaweza kuongoza kwenye matatizo makubwa ya afya, kutia ndani kupoteza ugumu wa mifupa na kuharibika kwa figo. Hata kwaweza kuua. “Daktari wangu aliniambia kwamba nilikuwa nimeunyima mwili wangu virutubishi vingi sana hivi kwamba ningaliendelea na mazoea yangu ya kula kwa miezi miwili, ningalikufa kutokana na utapiamlo,” asema Heather. Jarida The Harvard Mental Health Letter laripoti kwamba kwa pindi inayozidi miaka kumi, karibu asilimia 5 ya wanawake wanaobainishwa kuwa wanajinyima chakula hufa.
-
-
Kujinyima Chakula na Kuwa na Hamu ya Chakula Isiyo ya Kawaida—Mambo Hakika, HatariAmkeni!—1999 | Januari 22
-
-
a Wataalamu fulani wanadai kwamba upungufu wa asilimia 20 hadi 25 wa uzito wa mtu kwa ujumla waweza kuchochea mabadiliko ya kemikali katika akili yanayoweza kubadili mtazamo wake, yakimfanya aone mafuta mahali hayapo.
-