-
‘Nina Kazi Nyingi Sana!’Amkeni!—2009 | Aprili
-
-
Kufuatia Utajiri
Hata hivyo, kwa vijana fulani, badala ya kuwasaidia kufikia malengo yao, ni kana kwamba kuwa na usawaziko huwa ni kikwazo. Wanafunzi kama hao huamini kwamba siri ya kufanikiwa ni kuwa na kazi yenye mshahara mnono na utajiri unaotokana na kazi kama hiyo. Pope aliona kwamba baadhi ya vijana aliokutana nao walikuwa na maoni kama hayo. Alisema hivi: “Wanafunzi hao walitamani kulala kwa muda mrefu zaidi na kuboresha afya yao, lakini ratiba yao yenye utendaji mwingi unaotia ndani shule, familia, na kufanya kazi hakukuwaruhusu kufanya mabadiliko waliyotaka. Vivyo hivyo, walitamani kutumia muda mwingi zaidi pamoja na marafiki, kufanya mambo mengine, au kupumzika kwa siku kadhaa lakini wengi waliamini kwamba hawawezi kufanya mambo hayo na bado waendelee kupata maksi za juu. Walitambua kwamba walihitaji kufanya uamuzi na kwa maoni yao, kufanikiwa maishani kulikuwa muhimu zaidi kuliko kupata furaha sasa.”
Ni vizuri kwa wanafunzi kama hao wenye bidii kufikiria maneno haya ya mtu mmoja mwenye hekima: “Je, mtu atafaidi nini akiupata utajiri wote wa ulimwengu na hali amepoteza maisha yake? Au, mtu atatoa kitu gani kiwe badala ya maisha yake?” (Mathayo 16:26, Biblia Habari Njema) Kwa maneno hayo Yesu Kristo alionya kwamba miradi yoyote tunayojitahidi kufikia katika ulimwengu huu haina faida kwa sababu inaweza kutudhuru kimwili, kihisia, na kiroho.
Katika kitabu chake The Price of Privilege, mwanasaikolojia Madeline Levine aliandika kwamba “kuwa na pesa, elimu, mamlaka, umashuhuri, na vitu vya kimwili hakumsaidii mtu asikose furaha au asipatwe na matatizo ya kihisia.” Pope, aliyetajwa awali, alisema hivi: “Mimi huwaona watoto na wazazi wengi wakijaribu kufikia viwango vya juu sana walivyojiwekea kwa sababu wanaamini wakifikia viwango hivyo watafanikiwa.” Aliongeza hivi: “Tunapaswa kujitahidi kuwa na afya kiakili, kimwili, na kutambua mambo yaliyo muhimu maishani.”
Kuna mambo muhimu zaidi kuliko pesa. Mambo hayo yanatia ndani kuwa na afya nzuri ya kihisia, kimwili, dhamiri nzuri, na urafiki pamoja na Muumba wetu. Hizo ni zawadi zenye thamani sana kutoka kwa Mungu. Ukizipoteza kwa sababu ya kufuatilia umashuhuri au utajiri, huenda usizipate tena. Ukiwa na hilo akilini, ona kile ambacho Yesu alifundisha: “Heri wanaojiona kuwa maskini mbele ya Mungu, maana Utawala wa mbinguni ni wao.”—Mathayo 5:3, The New Testament in Kiswahili with Catholic Notes.
Vijana wengi wamekubali kweli hiyo. Ingawa wanajitahidi sana shuleni, wao wanatambua kwamba kufaulu katika masomo na kupata utajiri hakuwezi kuwapa furaha ya kudumu. Wanatambua kwamba kufuatia miradi kama hiyo kunawaletea mfadhaiko usiohitajika. Wanafunzi hao wamejifunza kwamba kumaliza ‘umaskini wao mbele za Mungu’ ndio msingi wa kuwa na furaha wakati ujao. Wachapishaji wa gazeti hili au Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukuonyesha jinsi unavyoweza kuwa na furaha unapomaliza umaskini wako mbele za Mungu.
-
-
‘Nina Kazi Nyingi Sana!’Amkeni!—2009 | Aprili
-
-
[Picha katika ukurasa wa 6]
UKUTA WA ULINZI WA KUWAZIA
“Vitu vyenye thamani vya tajiri ni mji wake wenye nguvu, navyo ni kama ukuta wa ulinzi katika mawazo yake.” (Methali 18:11) Zamani, watu walitegemea kuta ndefu ili kujilinda dhidi ya mashambulizi. Lakini hebu wazia unaishi katika jiji lililozungukwa na ukuta wa kuwaziwa tu. Hata ujaribu kujisadikisha kadiri gani, ukuta huo hauwezi kukulinda dhidi ya maadui wako.
Kama watu wanaoishi katika eneo lililo wazi hivyo, vijana wanaofuatilia utajiri watatamaushwa. Je, wewe ni mzazi? Ni vizuri kumsaidia mtoto wako kuepuka mtego wa kufuatilia vitu vya kimwili na kuishi katika jiji kama hilo lenye ukuta wa kuwaziwa.
Kweli za Biblia zifuatazo zinaweza kukusaidia kuzungumza na mwana au binti yako:
◼ Utajiri mwingi hutokeza matatizo mengi kuliko kuyatatua. “Wingi alio nao tajiri haumruhusu kulala.”—Mhubiri 5:12; 1 Timotheo 6:9, 10.
◼ Mtu akiwa na mipango mizuri hahitaji kuwa na utajiri ili awe na furaha. “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.”—Methali 21:5; Luka 14:28.
◼ Mapato ya kadiri yanayotimiza mahitaji ya mtu humfanya aridhike. “Usinipe umaskini wala utajiri.”—Methali 30:8.d
[Maelezo ya Chini]
d Habari zaidi kuhusu mtego wa kufuatilia vitu vya kimwili inaweza kupatikana katika Amkeni! la Aprili 8, 2003, ukurasa wa 20-21.
-