Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mume na Mzee—Kusawazisha Hayo Madaraka
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Oktoba 15
    • Mume na Mzee—Kusawazisha Hayo Madaraka

      ‘Mwangalizi apaswa kuwa mume wa mke mmoja.’—1 TIMOTHEO 3:2, NW.

      1, 2. Kwa nini useja wa mapadri si wa Kimaandiko?

      KATIKA karne ya kwanza, Wakristo waaminifu walihangaikia kusawazisha madaraka yao mbalimbali. Mtume Paulo aliposema kwamba Mkristo anayedumu akiwa mseja “atazidi kufanya vema,” je, alimaanisha kwamba mwanamume huyo angefaa zaidi kutumikia akiwa mwangalizi katika kutaniko la Kikristo? Je, alikuwa akifanya useja kuwa takwa la kuwa mzee? (1 Wakorintho 7:38) Useja ni takwa kwa makasisi Wakatoliki. Lakini je, useja wa mapadri ni wa Kimaandiko? Makanisa ya Othodoksi ya Mashariki huruhusu mapadri wao wa parokia wawe wanaume waliooa, lakini hawaruhusu maaskofu wao wafanye hivyo. Je, hilo lapatana na Biblia?

      2 Wengi wa mitume 12 wa Kristo, washiriki wa msingi wa kutaniko la Kikristo, walikuwa wanaume waliooa. (Mathayo 8:14, 15; Waefeso 2:20) Paulo aliandika hivi: “Je, hatuna ruhusa kumchukua mke Mkristo katika ziara zetu, kama vile wafanyavyo mitume wengine, ndugu zake Bwana, na pia Kefa [Petro]?” (1 Wakorintho 9:5, Habari Njema kwa Watu Wote) Kichapo New Catholic Encyclopedia chakubali kwamba “chanzo cha sheria ya useja ni cha kikanisa” na kwamba “wahudumu katika AJ [Agano Jipya] hawakuwa chini ya wajibu wa useja.” Mashahidi wa Yehova hufuata kigezo cha Kimaandiko badala ya sheria ya kikanisa.—1 Timotheo 4:1-3.

      Kuwa Mzee na Ndoa Ni Mambo Yanayopatana

      3. Ni mambo gani ya hakika ya Kimaandiko yaonyeshayo kwamba waangalizi Wakristo waweza kuwa wanaume waliooa?

      3 Badala ya kutaka kwamba wanaume waliowekwa rasmi wawe waangalizi wasioe, Paulo alimwandikia Tito hivi: “Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee [Kigiriki, pre·sbyʹte·ros] katika kila mji kama vile nilivyokuamuru; ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii. Maana imempasa askofu [“mwangalizi,” NW] [Kigiriki, e·piʹsko·pos, litokapo neno “askofu”] awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa kuwa ni wakili wa Mungu.”—Tito 1:5-7.

      4. (a) Twajuaje kwamba ndoa si takwa kwa waangalizi Wakristo? (b) Ndugu mseja aliye mzee ana faida gani?

      4 Kwa upande mwingine, ndoa si takwa la Kimaandiko la kuwa mzee. Yesu alidumu akiwa mseja. (Waefeso 1:22) Paulo, mwangalizi mwenye kutokeza katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, alikuwa asiyeoa wakati huo. (1 Wakorintho 7:7-9) Leo, kuna Wakristo wengi waseja wanaotumikia wakiwa wazee. Hali yao ya useja labda huwaruhusu wawe na wakati mwingi zaidi kushughulikia wajibu wao mbalimbali wakiwa waangalizi.

      ‘Mtu Aliyeoa Amegawanyika’

      5. Ndugu waliooa wakubali jambo gani la hakika la Kimaandiko?

      5 Mwanamume Mkristo anapooa, yeye apaswa kung’amua kwamba anajipatia madaraka mapya yatakayotaka wakati na uangalifu wake. Biblia hutaarifu hivi: “Yeye asiyeoa hujishughulisha na mambo ya Bwana, ampendezeje Bwana; bali yeye aliyeoa hujishughulisha na mambo ya dunia hii, jinsi atakavyompendeza mkewe [“naye amegawanyika,” NW].” (1 Wakorintho 7:32-34) Kugawanyika katika maana ipi?

      6, 7. (a) Mwanamume aliyeoa “amegawanyika” (NW) katika njia gani moja? (b) Paulo awatolea shauri gani Wakristo waliofunga ndoa? (c) Hilo lingeweza kuathirije uamuzi wa mwanamume wa kukubali mgawo wa kazi?

      6 Kwanza, mtu aliyeoa anamkabidhi mtu mwingine mamlaka juu ya mwili wake mwenyewe. Paulo alieleza jambo hilo kwa wazi sana: “Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe.” (1 Wakorintho 7:4) Watu fulani wanaofikiria ndoa huenda wakahisi kwamba onyo hilo la upole halina maana sana kwa sababu ngono haitakuwa jambo kuu katika ndoa yao. Hata hivyo, kwa kuwa usafi wa kiadili kabla ya ndoa ni takwa la Kimaandiko, kwa kweli Wakristo hawajui mahitaji ya kindani ya atakayekuwa mwenzi wao wakati ujao.

      7 Paulo aonyesha kwamba hata wenzi ‘wanaofikiri mambo ya roho’ lazima wafikirie mahitaji ya ngono ya mmoja na mwenzake. Aliwashauri Wakristo katika Korintho hivi: “Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu.” (Warumi 8:5; 1 Wakorintho 7:3, 5) Kwa kuhuzunisha, kumekuwa na visa vya uzinzi wakati ambapo shauri hilo halikufuatwa. Kwa sababu hiyo, Mkristo aliyefunga ndoa apaswa achunguze mambo kwa uangalifu kabla ya kukubali mgawo wa kazi utakaomtenganisha na mkewe kwa kipindi kirefu cha wakati. Yeye hana tena uhuru uleule wa kutenda aliokuwa nao alipokuwa mseja.

      8, 9. (a) Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba Wakristo waliofunga ndoa “hujishughulisha na mambo ya dunia hii”? (b) Wakristo waliofunga ndoa wajishughulishe kufanya nini?

      8 Yaweza kusemwa katika maana gani kwamba wanaume Wakristo waliooa, kutia na wazee, “hujishughulisha na mambo ya dunia hii [“ulimwengu,” NW] [koʹsmos]”? (1 Wakorintho 7:33) Ni dhahiri sana kwamba Paulo hakuwa akisema juu ya mambo mabaya ya ulimwengu huu, ambayo Wakristo wote wa kweli wapaswa kuepuka. (2 Petro 1:4; 2:18-20; 1 Yohana 2:15-17) Neno la Mungu hutuagiza “kukataa ubaya na tamaa za kidunia [“kilimwengu,” NW] [ko·smi·kosʹ]; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa.”—Tito 2:12.

      9 Kwa hiyo, Mkristo aliyefunga ndoa “hujishughulisha na mambo ya dunia hii” kwa habari ya kwamba yeye huhangaikia kihalali mambo ya kimwili ambayo ni sehemu ya maisha ya kawaida ya ndoa. Hayo yatia ndani nyumba, chakula, mavazi, tafrija—kuongezea mahangaiko mengine yasiyohesabika ikiwa kuna watoto. Lakini hata kwa wenzi wasio na watoto, ikiwa ndoa hiyo itafanikiwa, mume na pia mke lazima ajishughulishe ili apate ‘kumpendeza’ mwenzi wake wa ndoa. Hilo ni la upendezi mahususi kwa wazee Wakristo wasawazishapo madaraka yao.

      Waume Wema na pia Wazee Wema

      10. Ili Mkristo astahili kuwa mzee, ndugu zake na watu walio nje wapaswa kuweza kuona nini?

      10 Ingawa ndoa si takwa la kuwa mzee, ikiwa mwanamume Mkristo alioa, kabla ya kupendekezwa kwa ajili ya kuwekwa rasmi kuwa mzee, kwa hakika apaswa kutoa uthibitisho wa kujitahidi kuwa mume mwema, mwenye upendo, huku akitumia ukichwa ifaavyo. (Waefeso 5:23-25, 28-31) Paulo aliandika hivi: “Ni neno la kuaminiwa; mtu akitaka kazi ya askofu [“mwangalizi,” NW], atamani kazi njema. Basi imempasa askofu [“mwangalizi,” NW] awe mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja.” (1 Timotheo 3:1, 2) Yapaswa iwe dhahiri kwamba mzee anafanya kadiri awezavyo ili kuwa mume mwema, mke wake awe ni Mkristo mwenzake au la. Kwa kweli, hata watu walio nje ya kutaniko wapaswa kuweza kuona kwamba anamtunza mke wake vizuri na yale madaraka yake mengine. Paulo aliongeza hivi: “Imempasa kushuhudiwa mema na watu walio nje; ili asianguke katika lawama na mtego wa Ibilisi.”—1 Timotheo 3:7.

      11. Fungu la maneno “mume wa mke mmoja” ladokeza nini, kwa hiyo wazee wachukue hatua zipi za kujihadhari?

      11 Bila shaka, fungu la maneno “mume wa mke mmoja” lakataza ndoa ya wake wengi, na pia ladokeza uaminifu wa ndoa. (Waebrania 13:4) Wazee wahitaji hasa kuwa waangalifu wanaposaidia dada kutanikoni. Wapaswa kuepuka kuwa peke yao wanapomtembelea dada fulani anayehitaji shauri na faraja. Wangefanya vema kuandamana na mzee mwingine, mtumishi wa huduma, au hata mke wao ikiwa ni jambo la kufanya ziara ya kutia moyo tu.—1 Timotheo 5:1, 2.

      12. Wake wa wazee na wa watumishi wa huduma wajitahidi kufaana na ufafanuzi upi?

      12 Kama ilivyo, mtume Paulo alipokuwa akiorodhesha matakwa ya wazee na watumishi wa huduma, alikuwa na shauri pia la kuwapa wake wa wale wanaofikiriwa kwa ajili ya mapendeleo hayo. Aliandika hivi: “Vivyo hivyo wake zao na wawe wastahivu; si wasingiziaji; watu wa kiasi, waaminifu katika mambo yote.” (1 Timotheo 3:11) Mume Mkristo aweza kuchangia sana kumsaidia mkewe afaane na ufafanuzi huo.

      Wajibu Mbalimbali wa Kimaandiko kwa Mke

      13, 14. Hata ikiwa mke wa mzee si Shahidi mwenzake, kwa nini akae naye na awe mume mwema?

      13 Bila shaka, shauri hili wanalopewa wake wa wazee au wa watumishi wa huduma latarajia kwamba wake hao wenyewe ni Wakristo waliojiweka wakfu. Kwa ujumla, ndivyo ilivyo kwa sababu Wakristo wanatakwa wafunge ndoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Lakini namna gani ndugu aliyekuwa tayari ameoa mke asiyeamini alipoweka maisha yake wakfu kwa Yehova, au yule ambaye mke wake aiacha kweli kwa kosa lisilo la mume?

      14 Jambo hilo lenyewe, lisingemzuia asiwe mzee. Hata hivyo, lisingempa haki ya kutengana na mkewe kwa sababu tu yeye hashiriki itikadi zake. Paulo alishauri hivi: “Je! umefungwa kwa mke? usitake kufunguliwa.” (1 Wakorintho 7:27) Aliendelea kutaarifu hivi: “Iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye asimwache. Lakini yule asiyeamini akiondoka, na aondoke. Hapo huyo ndugu mume au ndugu mke hafungiki. Lakini Mungu ametuita katika amani. Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?” (1 Wakorintho 7:12, 15, 16) Hata ikiwa mkewe si Shahidi, mzee apaswa kuwa mume mwema.

      15. Mtume Petro hutolea shauri gani waume Wakristo, na matokeo yaweza kuwa nini mzee akithibitika kuwa mume mwenye kumpuuza mke?

      15 Mkewe awe ni mwamini mwenzake au la, mzee Mkristo apaswa kutambua kwamba mke wake ahitaji uangalifu wake wenye upendo. Mtume Petro aliandika hivi: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” (1 Petro 3:7) Mume ambaye kwa kukusudia anakosa kushughulikia mahitaji ya mkewe huhatarisha uhusiano wake mwenyewe pamoja na Yehova; hilo laweza kumzuia asimfikie Yehova kama kwamba ‘kwa wingu, maombi yasipite.’ (Maombolezo 3:44) Hilo lingeweza kuongoza kwenye kutostahili kwake tena kutumikia akiwa mwangalizi Mkristo.

      16. Paulo atoa jambo gani kuu, na wazee wahisije juu ya hilo?

      16 Kama ilivyoonyeshwa, jambo kuu la hoja ya Paulo ni kwamba mwanamume anapooa, anaacha kiasi fulani cha uhuru aliokuwa nao akiwa mwanamume mseja uliomruhusu ‘amhudumie Bwana pasipo [“kukengeushwa fikira,” NW].’ (1 Wakorintho 7:35) Ripoti zaonyesha kwamba wazee fulani waliooa hawajakuwa na usawaziko siku zote katika kusababu juu ya maneno ya Paulo yaliyopuliziwa. Katika tamaa yao ya kutimiza yale wanayohisi kwamba wazee wema wanapaswa kufanya, huenda wakapuuza baadhi ya wajibu wao mbalimbali wa kimume. Huenda wengine wakapata ugumu wa kukataa pendeleo la kutaniko, hata ikiwa kulikubali kungekuwa na madhara ya kiroho kwa wake zao. Wanafurahia mapendeleo yanayoambatana na ndoa, lakini je, wako tayari kutimiza madaraka yanayoambatana nayo?

      17. Ni jambo gani ambalo limewapata wake fulani, na hilo lingaliwezaje kuepukwa?

      17 Bila shaka, kuwa na bidii akiwa mzee ni jambo linalostahili pongezi. Hata hivyo, je, Mkristo amesawazika ikiwa, katika kutimiza wajibu wake mbalimbali kutanikoni, anapuuza madaraka yake ya Kimaandiko kwa mke wake? Huku akitamani kuwategemeza walio kutanikoni, mzee mwenye usawaziko atahangaikia pia hali ya kiroho ya mke wake. Baadhi ya wake wa wazee wamekuwa dhaifu kiroho, na wengine ‘wameangamia’ kiroho. (1 Timotheo 1:19) Ingawa mke ana daraka la kufanyia kazi wokovu wake mwenyewe, katika visa vingi hilo lingaliweza kuepukwa ikiwa mzee ‘angalimlisha na kumtunza’ mkewe, “kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa.” (Waefeso 5:28, 29) Kwa hakika, ni lazima wazee ‘watunze nafsi zao, na lile kundi lote nalo.’ (Matendo 20:28) Ikiwa wameoa, hilo latia ndani wake zao.

      “Dhiki Katika Mwili”

      18. Ni zipi baadhi ya sehemu za “dhiki” ambazo Wakristo waliofunga ndoa hupatwa nazo, na hilo lingeweza kuathirije utendaji mbalimbali wa wazee?

      18 Mtume aliandika hivi pia: “Mwanamwali akiolewa, hana hatia; lakini watu kama hao watakuwa na dhiki katika mwili nami nataka kuwazuilia hayo.” (1 Wakorintho 7:28) Paulo alitamani kuwazuilia wale walioweza kufuata kielelezo chake cha useja wasiwe na mahangaiko yasiyoepukika yanayoambatana na ndoa. Hata kwa wenzi wasio na watoto, huenda mahangaiko hayo yakatia ndani matatizo ya afya au ya kifedha na pia madaraka ya Kimaandiko kwa wazazi waliozeeka wa mwenzi. (1 Timotheo 5:4, 8) Lazima mzee akabiliane na madaraka hayo kwa njia ya kuweka kielelezo chema, na nyakati nyingine hilo laweza kuathiri utendaji wake mbalimbali akiwa mwangalizi Mkristo. Kwa kufurahisha, wazee wanafanya kazi bora katika kutimiza madaraka yao ya familia na ya kutaniko.

      19. Paulo alimaanisha nini aliposema: “Wale walio na wake na wawe kama hawana”?

      19 Paulo aliongeza hivi: “Muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana.” (1 Wakorintho 7:29) Bila shaka, kwa sababu ya yale aliyokuwa ameandika tayari katika sura hii ya Wakorintho, ni dhahiri kwamba hakumaanisha kwamba Wakristo waliofunga ndoa kwa njia fulani wawapuuze wake zao. (1 Wakorintho 7:2, 3, 33) Alionyesha alichomaanisha, alipoandika hivi: “[Acha] wale wautumiao ulimwengu huu, [wawe] kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.” (1 Wakorintho 7:31) Sasa, hata zaidi kuliko katika siku ya Paulo au katika siku ya mtume Yohana, ‘ulimwengu unapita.’ (1 Yohana 2:15-17, HNWW) Kwa hiyo, Wakristo waliofunga ndoa wanaoona uhitaji wa kutoa dhabihu katika kumfuata Kristo hawawezi kujishughulisha kabisa katika shangwe na mapendeleo ya ndoa.—1 Wakorintho 7:5.

      Wake Wenye Kujidhabihu

      20, 21. (a) Ni dhabihu zipi ambazo wake Wakristo wengi wako tayari kutoa? (b) Mke aweza kutazamia nini kihalali kutoka kwa mumewe, hata ikiwa mume ni mzee?

      20 Kama vile wazee watoavyo dhabihu ili kuwafaidi wengine, wake wengi wa wazee wamejitahidi kusawazisha madaraka yao katika ndoa pamoja na masilahi ya maana ya Ufalme. Maelfu ya wanawake Wakristo wanafurahi kushirikiana na waume wao ili kuwawezesha watimize wajibu wao mbalimbali wakiwa waangalizi. Yehova awapenda kwa sababu hiyo, naye hubariki ile roho bora waonyeshayo. (Filemoni 25) Hata hivyo, shauri la Paulo lenye usawaziko laonyesha kwamba wake wa waangalizi wanaweza kutazamia kihalali kwa kiasi wakati na uangalifu kutoka kwa waume wao. Ni wajibu wa Kimaandiko wa wazee waliooa kuwatolea wake zao wakati wa kutosha ili asawazishe madaraka yake akiwa mume na mwangalizi.

      21 Lakini namna gani ikiwa, mzee Mkristo ni baba pia, zaidi ya kuwa mume? Hilo laongezea madaraka yake na kumfungulia uwanja mwingine wa uangalizi, kama tutakavyoona katika makala ifuatayo.

  • Baba na Mzee—Kutimiza Mafungu Yote Mawili
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Oktoba 15
    • Baba na Mzee—Kutimiza Mafungu Yote Mawili

      “Mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje Kanisa la Mungu?” —1 TIMOTHEO 3:5.

      1, 2. (a) Katika karne ya kwanza, waangalizi waseja na waangalizi waliooa wasiokuwa na watoto waliweza kuwatumikiaje ndugu zao? (b) Akila na Prisila ni kielelezo jinsi gani kwa wenzi wengi wa ndoa leo?

      WAANGALIZI katika kutaniko la Kikristo la mapema waliweza kuwa wanaume waseja au wanaume waliooa, wasio na watoto au wanaume waliooa, waliokuwa na watoto. Bila shaka baadhi ya Wakristo hao waliweza kufuata shauri la Paulo lililotolewa katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, sura ya 7, wakidumu wakiwa waseja. Yesu alikuwa ametaarifu hivi: “Wako matowashi waliojifanya kuwa matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 19:12) Wanaume hao waseja, kama vile Paulo na labda baadhi ya waandamani wake wa kusafiri, wangekuwa huru kusafiri ili kusaidia ndugu zao.

      2 Biblia haisemi kama Barnaba, Marko, Sila, Luka, Timotheo, na Tito walikuwa wanaume waseja. Ikiwa walikuwa wameoa, ni dhahiri kwamba walikuwa na uhuru vya kutosha kutoka madaraka ya familia ili waweze kusafiri sana kwenda kwenye migawo mbalimbali. (Matendo 13:2; 15:39-41; 2 Wakorintho 8:16, 17; 2 Timotheo 4:9-11; Tito 1:5) Huenda ikawa waliandamana na wake zao, kama vile Petro na “mitume wengine,” ambao yaonekana walienda na wake zao walipokuwa wakienda mahali-mahali. (1 Wakorintho 9:5) Akila na Prisila ni kielelezo cha wenzi wa ndoa waliokuwa tayari kuhama-hama, wakimfuata Paulo kutoka Korintho hadi Efeso, kisha kuhamia Roma, na kurudi Efeso tena. Biblia haisemi ikiwa walikuwa na watoto wowote. Utumishi wao wa kujitoa kwa ajili ya ndugu zao uliwapatia shukrani za “makanisa ya Mataifa yote.” (Warumi 16:3-5; Matendo 18:2, 18; 2 Timotheo 4:19) Leo, bila shaka kuna wenzi wengi wa ndoa ambao, kama vile Akila na Prisila, wangeweza kutumikia makutaniko mengine, labda kwa kuhama palipo na uhitaji mkubwa zaidi.

      Baba na Mzee

      3. Ni jambo gani lidokezalo kwamba wazee wengi wa karne ya kwanza walikuwa wanaume waliooa, waliokuwa na familia?

      3 Inaonekana kwamba katika karne ya kwanza W.K., wazee Wakristo walio wengi walikuwa wanaume waliooa, waliokuwa na watoto. Paulo alipoorodhesha sifa za ustahili zilizotakwa kwa mwanamume ‘anayefikia cheo cha mwangalizi,’ alitaarifu kwamba Mkristo huyo apaswa kuwa “mwenye kuisimamia nyumba yake vema, ajuaye kutiisha watoto katika ustahivu.”—1 Timotheo 3:1, 4, linganisha NW.

      4. Ni jambo gani lililotakwa kwa wazee waliooa, walio na watoto?

      4 Kama vile tumeona, mwangalizi hakuwa na wajibu wa kuwa na watoto, au hata wa kuoa. Lakini ikiwa alikuwa ameoa, ili aweze kustahili kuwa mzee au mtumishi wa huduma, Mkristo alipaswa atumie ukichwa ifaavyo na kwa upendo juu ya mke wake na kujionyesha kuwa mwenye uwezo wa kudumisha watoto wake wakiwa chini ya unyenyekeo ufaao. (1 Wakorintho 11:3; 1 Timotheo 3:12, 13) Udhaifu wowote mzito katika kuisimamia nyumba yake ungemfanya ndugu asistahili mapendeleo ya pekee kutanikoni. Kwa nini? Paulo aeleza hivi: “Mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe atalitunzaje Kanisa la Mungu?” (1 Timotheo 3:5) Ikiwa wale wa mwili wake mwenyewe hawakuwa tayari kunyenyekea uangalizi wake, wengine wangeitikiaje?

      ‘Kuwa na Watoto Waaminio’

      5, 6. (a) Paulo alimtajia Tito takwa jipi kwa habari ya watoto? (b) Ni nini kinachotazamiwa kwa wazee walio na watoto?

      5 Alipokuwa akimwagiza Tito aweke rasmi waangalizi katika makutaniko ya Krete, Paulo aliweka masharti haya: “Ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii. Maana imempasa askofu [“mwangalizi,” NW] awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa kuwa ni wakili wa Mungu.” Ni nini kinachomaanishwa hasa na takwa la ‘kuwa na watoto waaminio?’—Tito 1:6, 7.

      6 Maneno “watoto waaminio” yarejezea vijana ambao tayari wameweka wakfu maisha zao kwa Yehova na wamebatizwa, au watoto wachanga wanaofanya maendeleo kuelekea wakfu na ubatizo. Washiriki wa kutaniko hutazamia watoto wa wazee kwa ujumla kuwa wenye tabia nzuri na watiifu. Yapaswa ionekane wazi kwamba mzee anafanya yote awezavyo ili kuijenga imani ya watoto wake. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Lakini namna gani ikiwa kijana ambaye amepokea mazoezi akataa kumtumikia Yehova au hata afanya dhambi nzito?

      7. (a) Kwa nini ni dhahiri kwamba Mithali 22:6 halionyeshi kanuni isiyonyumbuka? (b) Mtoto wa mzee asipoamua kumtumikia Yehova, kwa nini huyo mzee hatapoteza mapendeleo yake mara moja?

      7 Ni dhahiri kwamba mithali iliyonukuliwa juu haitoi kanuni imara. Haibatilishi kanuni ya hiari ya kuchagua. (Kumbukumbu la Torati 30:15, 16, 19) Mwana au binti afikapo umri wa kuchukua madaraka, lazima afanye uamuzi wa kibinafsi kuhusu wakfu na ubatizo. Ikiwa ni wazi kwamba mzee ametoa msaada, mwongozo, na nidhamu ya kiroho inayohitajiwa, na bado kijana haamui kumtumikia Yehova, baba haonwi mara moja kutostahili kutumikia akiwa mwangalizi. Kwa upande mwingine, ikiwa mzee ana watoto wadogo kadhaa wanaoishi nyumbani, wanaokuwa wagonjwa kiroho na kuingia matatani mfululizo, huenda asionwe tena kuwa “mwenye kuisimamia nyumba yake vema.” (1 Timotheo 3:4) Jambo ni kwamba, yapaswa iwe dhahiri kwamba mwangalizi anafanya vizuri kadiri awezavyo kuwa na “watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii.”a

      Aliyeoa “Mke Asiyeamini”

      8. Mzee atendeje kuelekea mke wake asiyeamini?

      8 Kuhusu wanaume Wakristo waliooa wake wasioamini, Paulo aliandika hivi: “Iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye asimwache . . . Kwa maana . . . mke asiyeamini hutakaswa katika mumewe; kama isingekuwa hivyo, watoto wenu wangekuwa si safi; bali sasa ni watakatifu. Kwa maana . . . wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?” (1 Wakorintho 7:12-14, 16) Neno “asiyeamini” hapa halirejezei mke asiye na itikadi za kidini bali larejezea mwanamke ambaye hajajiweka wakfu kwa Yehova. Huenda alikuwa Myahudi, au mwamini katika miungu ya kipagani. Leo, huenda mzee akawa ameoa mwanamke aliye wa dini tofauti, aliye mwagnosti, au hata Mwatheisti. Ikiwa anakubali kukaa na mume huyo, mume hapaswi kumwacha kwa sababu tu ya itikadi zinazotofautiana. Apaswa bado ‘kukaa naye kwa akili; na kumpa heshima, kama chombo kisicho na nguvu,’ akiishi na matumaini ya kumwokoa.—1 Petro 3:7; Wakolosai 3:19.

      9. Katika nchi ambamo sheria yampa mume na pia mke haki ya kuwafunulia watoto wao itikadi za kidini za kila mmoja wao, mzee atendeje, na hilo litaathirije mapendeleo yake?

      9 Ikiwa mwangalizi ana watoto, atatumia ukichwa wake kama mume au baba ifaavyo katika kuwalea “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Katika nchi nyingi sheria huwapa wenzi wote wawili wa ndoa haki ya kuwatolea watoto wao maagizo ya kidini. Katika hali hiyo huenda mke akadai kutumia haki yake ya kuwafunulia watoto wake itikadi na mazoea yake ya kidini, ambayo huenda yakatia ndani kuwapeleka kwenye kanisa lake.b Bila shaka, watoto wapaswa kufuata dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia kwa habari ya kutoshiriki katika sherehe zisizo za kweli za kidini. Akiwa kichwa cha familia, baba atatumia haki yake mwenyewe ya kujifunza pamoja na watoto wake na kuwapeleka mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme iwezekanapo. Wafikapo umri ambao katika huo wanaweza kufanya maamuzi yao wenyewe, watajiamulia ni njia ipi watakayoenda. (Yoshua 24:15) Ikiwa wazee wenzake na washiriki wa kutaniko waweza kuona kwamba anafanya yote ambayo sheria yamruhusu afanye ili kuwaagiza watoto wake ifaavyo katika njia ya kweli, hataonwa kutostahili kuwa mwangalizi.

      “Kuisimamia Nyumba Yake Vema”

      10. Ikiwa mtu aliye na familia ni mzee, wajibu wake wa msingi ni nini?

      10 Hata kwa mzee aliye baba na mke wake ni Mkristo mwenzake, si kazi rahisi kugawa ifaavyo wakati na uangalifu wake kati ya mke wake, watoto wake, na madaraka ya kutaniko. Maandiko huonyesha wazi sana kwamba baba Mkristo ana wajibu wa kutunza mke na watoto wake. Paulo aliandika hivi: “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Timotheo 5:8) Katika barua iyo hiyo, Paulo alitaarifu kwamba wanaume wale tu ambao wameoa na tayari wamejionyesha kuwa waume na baba wema ndio wapaswao kupendekezwa kutumikia wakiwa waangalizi.—1 Timotheo 3:1-5.

      11. (a) Mzee ‘awatunze walio wake’ katika njia zipi? (b) Hilo laweza kumsaidiaje mzee atimize madaraka yake ya kutaniko?

      11 Mzee apaswa ‘kuwatunza’ walio wake si kimwili tu bali pia kiroho na kihisiamoyo. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Tengeneza kazi yako huko nje, jifanyizie kazi yako tayari shambani, ukiisha, jenga nyumba yako.” (Mithali 24:27) Kwa hiyo huku akiandaa mahitaji ya kimwili, ya kihisiamoyo, na ya kitafrija ya mke na watoto wake, mwangalizi apaswa pia kuwajenga kiroho. Hilo lataka wakati—wakati ambao hataweza kutolea mambo ya kutaniko. Lakini ni wakati uwezao kuwa na faida nyingi kwa habari ya furaha na hali ya kiroho ya familia. Hatimaye, familia yake ikiwa imara kiroho, huenda mzee akahitaji kutumia wakati mchache zaidi katika kushughulikia matatizo ya familia. Hilo litaiacha akili yake ikiwa huru zaidi ili kushughulikia mambo ya kutaniko. Kielelezo chake akiwa mume mwema na baba mwema kitakuwa chenye manufaa ya kiroho kwa kutaniko.—1 Petro 5:1-3.

      12. Baba walio wazee waweke kielelezo chema katika jambo jipi la familia?

      12 Kuisimamia nyumba vema hutia ndani kuratibu wakati ili kusimamia funzo la familia. Ni jambo la maana hasa kwamba wazee waweke kielelezo chema katika habari hii, kwa maana familia imara hufanyiza makutaniko imara. Wakati wa mwangalizi haupaswi kwa ukawaida kutumiwa sana katika kushughulikia mapendeleo mengine ya utumishi hivi kwamba anakosa wakati wa kujifunza pamoja na mke na watoto wake. Ikiwa hali imekuwa hivyo, apaswa kuchunguza tena ratiba yake. Huenda akahitaji kuratibu upya au kupunguza wakati anaotolea mambo mengine, hata akikataa mapendeleo fulani pindi kwa pindi.

      Uangalizi Wenye Usawaziko

      13, 14. “Mtumwa mwaminifu mwenye akili” amewatolea wazee walio na familia shauri jipi?

      13 Shauri la kusawazisha madaraka ya familia na ya kutaniko si jipya. Kwa miaka kadhaa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” amekuwa akiwatolea wazee shauri kuhusu jambo hili. (Mathayo 24:45) Miaka 37 iliyopita, Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Septemba 15, 1959, kurasa 553 na 554, lilishauri hivi: “Je, kwa kweli si jambo hasa la kusawazisha madai yote hayo ya wakati wetu? Katika usawaziko huo acha masilahi ya familia yako mwenyewe yakaziwe. Bila shaka Yehova Mungu asingemtazamia mtu atumie wakati wake wote katika utendaji wa kutaniko, katika kusaidia ndugu zake na majirani wake wapate wokovu, walakini asishughulikie wokovu wa nyumba yake mwenyewe. Mke na watoto wa mwanamume ni daraka la kwanza.”

      14 Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 1986, ukurasa 22, lilishauri hivi: “Kushiriki katika huduma ya shambani mkiwa jamaa kutafanya mkaribiane zaidi, hata hivyo mahitaji ya namna ya pekee ya watoto yanahitaji ujitie katika wajibu wa kutumia pamoja nao wakati wako wa faragha na nishati ya maoni yako ya moyoni. Basi, usawaziko unahitajiwa ili kuamua ni kiasi gani cha wakati unachoweza kutumia kwa wajibu mbalimbali wa . . . kutaniko, na bado uwatunze kiroho, katika maoni ya moyoni, na kimwili ‘wale walio wako mwenyewe.’ [Mkristo] lazima ‘ajifunze kwanza kuzoea utawa katika jamaa [yake] mwenyewe.’ (1 Timotheo 5:4, 8, NW)”

      15. Kwa nini mzee aliye na mke na watoto ahitaji hekima na ufahamu?

      15 Mithali ya Kimaandiko yataarifu hivi: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa ufahamu huthibitika.” (Mithali 24:3) Ndiyo, ili mwangalizi aweze kutimiza wajibu wake mbalimbali wa kitheokrasi na wakati uleule aijenge nyumba yake, kwa hakika kabisa ahitaji hekima na ufahamu. Kimaandiko, yeye ana nyanja zaidi ya moja za uangalizi—madaraka yake ya familia na madaraka yake ya kutaniko yanahusika. Ahitaji ufahamu ili kudumisha usawazisho kati yazo. (Wafilipi 1:9, 10) Ahitaji hekima ili kuweka mambo ya kutangulizwa. (Mithali 2:10, 11) Hata ahisi kadiri gani kwamba ana wajibu wa kushughulikia kutaniko lake, apaswa kung’amua kwamba akiwa mume na baba, daraka lake la kwanza alilopewa na Mungu ni utunzaji na wokovu wa familia yake.

      Baba Wema na pia Wazee Wema

      16. Mzee ana faida gani ikiwa yeye ni baba pia?

      16 Mzee mwenye watoto wenye adabu nzuri aweza kuwa faida kwelikweli. Ikiwa amejifunza kuitunza familia yake vizuri, anaweza kusaidia familia nyinginezo kutanikoni. Aelewa matatizo yazo vizuri zaidi na aweza kutoa shauri lionyeshalo uzoefu wake mwenyewe. Kwa furaha, maelfu ya wazee kotekote ulimwenguni wanafanya kazi bora wakiwa waume, baba, na waangalizi.

      17. (a) Mwanamume aliye baba na pia mzee asisahau nini kamwe? (b) Washiriki wengine wa kutaniko waonyesheje hisia-mwenzi?

      17 Ili mtu aliye na familia awe mzee, lazima awe Mkristo mkomavu ambaye, atunzapo mke na watoto wake, aweza kupanga mambo yake ili aweze kutolea wengine kutanikoni wakati na uangalifu. Hapaswi kusahau kamwe kwamba kazi yake ya uchungaji huanzia nyumbani. Wakijua kwamba wazee walio na wake na watoto wana madaraka ya familia yao na ya wajibu wao mbalimbali wa kutaniko, washiriki wa kutaniko watajaribu kutodai wakati wao isivyofaa. Mathalani, mzee aliye na watoto wapaswao kwenda shuleni asubuhi ijayo huenda asiweze sikuzote kukaa muda fulani baada ya mikutano ya jioni. Washiriki wengine wa kutaniko wapaswa kuelewa jambo hilo na kuonyesha hisia-mwenzi.—Wafilipi 4:5.

      Wazee Wetu Wapaswa Kuwa Wenye Thamani Kubwa Kwetu

      18, 19. (a) Uchunguzi wetu wa 1 Wakorintho sura ya 7 umetuwezesha kung’amua nini? (b) Tuwaoneje wanaume hao Wakristo?

      18 Uchunguzi wetu wa sura ya 7 ya barua ya kwanza ya Paulo kwa Wakorintho umetuwezesha kuona kwamba, wakifuata shauri la Paulo, kuna wanaume wengi waseja wanaotumia uhuru wao ili kutumikia masilahi ya Ufalme. Pia kuna maelfu ya ndugu waliooa, wasio na watoto, ambao, huku wakiwapa wake zao uangalifu unaostahili, hutumikia wakiwa waangalizi wema katika wilaya, mizunguko, makutaniko, na matawi ya Watch Tower, wake zao wakishirikiana nao kwa njia inayostahili pongezi. Mwishowe, katika yale makutaniko karibu 80,000 ya watu wa Yehova, kuna baba wengi ambao hawatunzi tu wake zao na watoto wao kwa upendo bali pia huchukua wakati ili kutumikia ndugu zao wakiwa wachungaji wanaojali.—Matendo 20:28.

      19 Mtume Paulo aliandika hivi: “Wazee watawalao vema na wahesabiwe kustahili heshima maradufu; hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha.” (1 Timotheo 5:17) Ndiyo, wazee wasimamiao nyumba zao na kutaniko vema wastahili upendo na staha yetu. Twapaswa kwa kweli “kuwachukua watu wa namna hiyo kuwa wenye thamani kubwa.”—Wafilipi 2:29, NW.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki