-
“Zawadi Zikiwa Wanadamu” Ili Kutunza Kondoo za YehovaMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 1
-
-
Uhitaji wa ‘Kurekebisha Upya’ Unapozuka
8. Nyakati nyingine sisi sote huhitaji kurekebishwa upya katika njia zipi?
8 Kwanza, “zawadi zikiwa wanadamu” huandaliwa “kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu,” Paulo asema. (Waefeso 4:12) Nomino ya Kigiriki inayotafsiriwa ‘kurekebisha upya’ hurejezea “kunyosha” kitu. Tukiwa wanadamu wasiokamilika, sote tunahitaji kurekebishwa upya mara kwa mara—ili kufikiri kwetu, mitazamo yetu, au mwenendo wetu “zinyoshwe” kwa kupatana na kufikiri kwa Mungu na mapenzi yake. Yehova ametuandalia kwa upendo “zawadi zikiwa wanadamu” ili watusaidie kufanya marekebisho yanayohitajika. Wao hufanyaje hivyo?
9. Mzee anaweza kusaidiaje kumrekebisha upya kondoo aliyekosea?
9 Nyakati fulani, huenda mzee akahitaji kumsaidia kondoo aliyekosea, ambaye labda ‘amechukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya kuijua.’ Mzee anaweza kusaidiaje? Andiko la Wagalatia 6:1 lasema kwamba “jaribuni kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole.” Kwa hiyo mzee atoapo shauri, hamkemei mkosaji kwa maneno makali. Shauri lapasa kumtia moyo, wala si ‘kumwogofya,’ yule anayelipokea. (2 Wakorintho 10:9; linganisha Ayubu 33:7.) Huenda mtu huyo tayari ameaibika, kwa hiyo mchungaji mwenye upendo huepuka kuiponda roho yake. Wakati shauri, hata karipio zito, linapotolewa kwa upendo, yaelekea litanyosha kufikiri au mwenendo wa mkosaji, na kwa njia hiyo limrekebishe.—2 Timotheo 4:2.
10. Kuwarekebisha upya wengine kunatia ndani nini?
10 Yehova alipoandaa “zawadi zikiwa wanadamu” ili kuturekebisha upya, alitazamia wazee wawe wenye kuburudisha kiroho na wenye kustahili kuigwa na watu wake. (1 Wakorintho 16:17, 18; Wafilipi 3:17) Kurekebisha upya wengine kunatia ndani kuwasaidia waaminifu wadumu kufuata mwendo unaofaa, na kuwasahihisha wale wanaofuatilia mwendo wenye makosa.a Leo, kwa kuwa kuna matatizo mengi sana yanayoelekea kuvunja moyo, wengi wanahitaji kitia-moyo ili waendelee. Huenda wengine wakahitaji msaada unaotolewa kwa wororo ili kufikiri kwao kunyoshwe kupatana na kufikiri kwa Mungu. Kwa mfano, baadhi ya Wakristo waaminifu hupambana na hisia za ndani zinazowafanya wahisi kwamba hawastahili wala hawafai. “Nafsi zilizoshuka moyo” kama hao huenda wakaona kuwa Yehova hawezi kamwe kuwapenda na kwamba Mungu hawezi hata kuzikubali jitihada zao bora za kumtumikia. (1 Wathesalonike 5:14) Lakini kufikiri hivyo hakupatani na jinsi Mungu awaonavyo waabudu wake kikweli.
11. Wazee wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale wanaopambana na hisia za kuona kuwa hawafai?
11 Enyi wazee, mnaweza kufanya nini ili kuwasaidia watu kama hao? Waonyesheni kwa fadhili uthibitisho wa Kimaandiko unaoonyesha kuwa Yehova humjali kila mmoja wa watumishi wake, nanyi wahakikishieni kuwa maandiko hayo ya Biblia huwahusu wao kibinafsi. (Luka 12:6, 7, 24) Wasaidieni waelewe kuwa Yehova ‘amewavuta’ ili wamtumikie, na basi ni lazima awe anawathamini. (Yohana 6:44) Wahakikishieni kuwa si wao pekee—watumishi wengi waaminifu wa Yehova wamekuwa na hisia kama hizo. Wakati mmoja nabii Eliya alishuka moyo sana hivi kwamba akatamani kufa. (1 Wafalme 19:1-4) Baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta katika karne ya kwanza walihisi kuwa mioyo yao ‘inawalaumu.’ (1 Yohana 3:20) Tunafarijika kujua kwamba watu waaminifu katika nyakati za Biblia walikuwa na “hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Mnaweza pia kupitia makala zenye kutia moyo zilizo katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! mkiwa pamoja na watu waliovunjika moyo. Mungu ambaye amewakabidhi nyinyi mkiwa “zawadi zikiwa wanadamu” hatakosa kuona jitihada zenu zenye upendo za kumfanya awe na matumaini tena.—Waebrania 6:10.
‘Kulijenga’ Kundi
12. Ni nini kionyeshwacho na usemi “kuujenga mwili wa Kristo,” na ufunguo wa kulijenga kundi ni nini?
12 Pili, “zawadi zikiwa wanadamu” wamekabidhiwa kwa kusudi la “kuujenga mwili wa Kristo.” (Waefeso 4:12) Hapo Paulo anatumia usemi wa mfano. ‘Kujenga’ hutukumbusha ujenzi, na “mwili wa Kristo” hurejezea watu—washiriki wa kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. (1 Wakorintho 12:27; Waefeso 5:23, 29, 30) Wazee wanahitaji kuwasaidia ndugu zao waimarike kiroho. Kusudi lao ni ‘kulijenga na si kulibomoa’ kundi. (2 Wakorintho 10:8) Ufunguo wa kulijenga kundi ni upendo, kwa sababu “upendo hujenga.”—1 Wakorintho 8:1.
13. Inamaanisha nini kuwa mwenye hisia-mwenzi, na kwa nini ni muhimu wazee waonyeshe hisia-mwenzi?
13 Sehemu moja ya upendo inayowasaidia wazee kulijenga kundi ni hisia-mwenzi. Kuwa na hisia-mwenzi kwamaanisha kuwahurumia wengine—kujiweka katika hali ya fikira zao na hisia zao, mkikumbuka mapungukio yao. (1 Petro 3:8) Kwa nini ni muhimu kwa wazee kuwa na hisia-mwenzi? Sababu muhimu zaidi ni kwamba Yehova—yeye ambaye huandaa “zawadi zikiwa wanadamu”—ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Watumishi wake wanapoteseka au wakiwa katika maumivu, yeye huwahurumia. (Kutoka 3:7; Isaya 63:9) Yeye hufikiria udhaifu wao. (Zaburi 103:14) Basi, wazee wanaweza kuonyeshaje hisia-mwenzi?
14. Wazee wanaweza kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi kwa njia zipi?
14 Mtu ambaye amevunjika moyo anapowajia, wao husikiliza, wakitambua hisia zake. Wao hujaribu kuelewa malezi, utu, na hali mbalimbali za ndugu zao. Kisha wazee wanapotoa msaada wa Kimaandiko wenye kujenga, itakuwa rahisi kwa kondoo kuukubali kwa sababu unatoka kwa wachungaji wanaowaelewa na kuwajali kikweli. (Mithali 16:23) Hisia-mwenzi pia husababisha wazee kufikiria mapungukio ya wengine na hisia ambazo zinaweza kutokezwa na mapungukio hayo. Kwa mfano, huenda Wakristo fulani waaminifu wakahisi wana hatia kwa sababu hawawezi kufanya zaidi katika kumtumikia Mungu, labda kwa sababu ya uzee au ugonjwa. Kwa upande mwingine, huenda wengine wakahitaji kitia-moyo ili kuiboresha huduma yao. (Waebrania 5:12; 6:1) Hisia-mwenzi itawafanya wazee watafute “maneno yapendezayo” yanayowajenga wengine. (Mhubiri 12:10) Kondoo za Yehova wanapojengwa na kuchochewa, upendo wao kwa Mungu utawasukuma kufanya yote wawezayo katika kumtumikia!
Wanaume Wanaoendeleza Umoja
15. Usemi “umoja katika imani” humaanisha nini?
15 Tatu, “zawadi zikiwa wanadamu” wameandaliwa ili “sisi sote tuufikie umoja katika imani na katika ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu.” (Waefeso 4:13) Usemi “umoja katika imani” haumaanishi umoja wa itikadi pekee bali pia umoja wa waamini. Hiyo basi ni sababu nyingine ambayo imefanya Mungu atupe “zawadi zikiwa wanadamu”—ili kuendeleza umoja miongoni mwa watu wake. Wao hufanyaje hivyo?
16. Kwa nini ni muhimu kwa wazee kudumisha umoja miongoni mwao?
16 Kwanza kabisa, ni lazima wadumishe umoja miongoni mwao wenyewe. Ikiwa wachungaji wamegawanyika, huenda kondoo wakapuuzwa. Wakati wenye thamani ambao ungetumiwa katika kulichunga kundi huenda ukatumiwa isivyofaa katika mikutano mirefu na mijadala juu ya masuala yasiyo ya lazima. (1 Timotheo 2:8) Huenda wazee wasikubaliane tu juu ya kila suala wanalozungumzia, kwa sababu wao ni watu walio na nyutu ambazo huenda zikawa tofauti-tofauti sana. Umoja haumaanishi kwamba wasiwe na maoni yanayotofautiana au hata kwamba wasiyatoe kwa njia yenye usawaziko wakati wanapozungumzia mambo kwa wazi. Wazee hudumisha umoja wao kwa kusikiliza kila mmoja kwa heshima pasipo kuhukumu mapema. Na maadamu hakuna kanuni ya Biblia inayokiukwa, kila mmoja anapaswa kuwa tayari kukubali na kuunga mkono uamuzi wa mwisho wa baraza la wazee. Roho ya kunyenyekea huonyesha kuwa wao wanaongozwa na “hekima ya kutoka juu,” ambayo ni “yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu.”—Yakobo 3:17, 18.
17. Wazee wanaweza kusaidiaje kudumisha umoja kutanikoni?
17 Wazee pia wako macho kudumisha umoja kutanikoni. Uvutano wenye kusababisha migawanyiko—kama vile porojo yenye kudhuru, mwelekeo wa kushuku wengine, au roho yenye ugomvi—unapotisha kuvuruga amani, wao hutoa shauri lenye kusaidia mara moja. (Wafilipi 2:2, 3) Kwa mfano, huenda wazee wanawafahamu watu fulani walio wachambuzi kupita kiasi au walio na mwelekeo wa kuingilia mambo ya wengine, na hivyo kuwa wadukizi. (1 Timotheo 5:13; 1 Petro 4:15) Wazee watajaribu kuwasaidia watu kama hao watambue kuwa mwendo wa aina hiyo ni kinyume cha mambo ambayo tumefundishwa na Mungu na kwamba kila mmoja ni lazima “[achukue] mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5, 7; 1 Wathesalonike 4:9-12) Kwa kutumia Maandiko, wataeleza kuwa Yehova humwachia kila mmoja wetu aamue mambo mengi akitumia dhamiri yake mwenyewe, na basi yeyote miongoni mwetu asiwahukumu wengine kwa masuala kama hayo. (Mathayo 7:1, 2; Yakobo 4:10-12) Ili tutumikie pamoja kwa umoja, ni lazima kuwe na hali ya kutumainiana na staha kutanikoni. “Zawadi zikiwa wanadamu” hutusaidia kuhifadhi amani na umoja wetu kwa kutoa shauri la Kimaandiko inapohitajika.—Waroma 14:19.
Kulilinda Kundi
18, 19. (a) “Zawadi zikiwa wanadamu” hutulinda kutokana na watu gani? (b) Kondoo wanahitaji kulindwa kutokana na hatari gani nyingine, na wazee hutendaje ili kuwalinda kondoo?
18 Nne, Yehova huandaa “zawadi zikiwa wanadamu” ili kutulinda tusiathiriwe na “kila upepo wa fundisho kwa njia ya mbinu ya hadaa ya watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Waefeso 4:14) Neno la awali lililotafsiriwa “hadaa” linasemekana kuwa lamaanisha “kudanganya kwenye mchezo wa dadu [mchezo wa kamari]” au “mbinu ya kutumia dadu kwa udanganyifu.” Je, hilo halitukumbushi namna waasi-imani wajanja wanavyotenda? Wakitumia hoja zenye ujanja, wao hutumia Maandiko vibaya wakijaribu kuwahadaa Wakristo wa kweli waiache imani yao. Lazima wazee wawe macho kutambua hao “mbwa-mwitu wenye kuonea”!—Matendo 20:29, 30.
19 Kondoo za Yehova wanahitaji kulindwa kutokana na hatari nyingine vilevile. Daudi, mchungaji wa kale, alilinda kwa ujasiri kondoo za baba yake kutokana na wanyama-wawindaji. (1 Samweli 17:34-36) Leo vilevile, huenda kukawa nyakati ambapo wachungaji Wakristo wenye kujali wanapaswa kuonyesha ujasiri ili waweze kulilinda kundi kutokana na yeyote ambaye huenda akawatenda vibaya au kuwaonea kondoo za Yehova, hasa wale walio dhaifu. Wazee watafanya haraka kuwaondoa kutanikoni watenda-dhambi wenye kukusudia ambao hutumia ujanja, udanganyifu, na hila kimakusudi ili kuendeleza uovu.b—1 Wakorintho 5:9-13; linganisha Zaburi 101:7.
-
-
Kuthamini “Zawadi Zikiwa Wanadamu”Mnara wa Mlinzi—1999 | Juni 1
-
-
‘Sisi Ni Wafanyakazi Wenzenu’
4, 5. (a) Paulo analifananisha kutaniko na nini, na kwa nini kielezi hicho chafaa? (b) Kielezi cha Paulo kinaonyesha nini kuhusiana na jinsi tunavyopaswa kuwaona na kuwatendea wenzetu?
4 Yehova amewakabidhi “zawadi zikiwa wanadamu” kiasi fulani cha mamlaka kutanikoni. Bila shaka, wazee hawangependa kutumia vibaya mamlaka yao, ingawa wao wanajua kuwa ni rahisi sana kwa wanadamu wasiokamilika kufanya hivyo. Basi, wao wanapaswa kujionaje kuhusiana na washiriki wengine wa kundi? Fikiria kielezi ambacho mtume Paulo alitumia. Akiisha kuzungumzia sababu ya kuandaliwa kwa “zawadi zikiwa wanadamu,” Paulo aliandika hivi: “Na tukue kwa upendo katika mambo yote katika yeye aliye kichwa, Kristo. Kutoka katika yeye mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane kupitia kila kiungo ambacho hupa kile kihitajiwacho, kulingana na utendaji wa kila kiungo kimoja-kimoja katika kipimo kipasacho, hutokeza ukuzi wa mwili ili kujijenga huo wenyewe katika upendo.” (Waefeso 4:15, 16) Hivyo Paulo alilifananisha kutaniko, pamoja na wazee na washiriki wengine, na mwili wa binadamu. Kwa nini kielezi hicho chafaa?
5 Mwili wa binadamu una viungo vingi mbalimbali lakini una kichwa kimoja pekee. Hata hivyo, hakuna chochote mwilini—kiwe ni msuli, neva, au mshipa wa damu—ambacho hakifai. Kila kiungo ni muhimu, nacho huchangia jambo fulani kwa afya na uzuri wa mwili wote. Vivyo hivyo, kutaniko limefanyizwa na washiriki mbalimbali, lakini kila mmoja—wachanga kwa wazee, wenye nguvu au wenye udhaifu—anaweza kuchangia jambo fulani kwa afya ya kiroho na uzuri wa kutaniko kwa ujumla. (1 Wakorintho 12:14-26) Yeyote asione kuwa hafai chochote. Kwa upande mwingine wenye kupita kiasi, yeyote asijione kuwa bora, kwa kuwa sisi sote—wachungaji na kondoo vilevile—ni sehemu ya mwili, na kuna kichwa kimoja tu, Kristo. Hivyo Paulo atoa mfano mzuri wa upendo, kujali, na staha tunazopaswa kuonyeshana. Kutambua jambo hilo kunawasaidia wazee kuwa na maoni ya unyenyekevu na yenye usawaziko juu ya daraka lao kutanikoni.
-