Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Matatizo ya Pekee ya Familia za Kambo
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
    • Huenda wenzi wapya wa ndoa wasing’amue msukosuko wa kihisia-moyo, matatizo katika kuonyesha uaminifu-mshikamanifu, na hisia za wivu na uchungu wa moyo ambao kufika kwa mzazi wa kambo husababisha katika watoto hao wa kambo. Huenda watoto hao wakawaza kwamba mzazi wao halisi anampenda huyo mzazi wa kambo zaidi yao. Isitoshe, huenda mzazi halisi aliyeachwa na mwenzi akashindwa kuelewa upendo wenye kuendelea kati ya watoto na mwenzi wa kwanza. Mvulana mmoja alijaribu kueleza uhusiano wake mzuri pamoja na baba yake halisi, akisema, “Mama, ninajua Baba alikutesa, lakini amekuwa mwema kwangu!” Usemi kama huo, ingawa ni wa moyo mnyofu, waweza kumfanya mama aone uchungu mwingi kuelekea baba ya mtoto huyo.

      Baba mmoja wa kambo aliungama: “Kwa kweli sikuwa tayari kushughulika na matatizo yote yanayohusiana na kulea watoto wangu wa kambo. Niliingia katika hali hiyo nikifikiri kwamba kwa kuwa sasa nilikuwa nimeoa mama yao, nilikuwa baba yao. Kwangu, hilo lilionekana kuwa jambo lisilo gumu sana! Sikuelewa upendo ambao watoto hao walikuwa nao kwa baba yao halisi, nami nilifanya makosa mengi sana.”

      Mikazo inaweza kuzuka hasa kuhusiana na nidhamu. Watoto huhitaji nidhamu yenye upendo, lakini mara nyingi wao huikinza hata inapotoka kwa mzazi wao halisi. Basi, inakuwa vigumu zaidi kama nini kwao kuipokea kutoka kwa mzazi wa kambo! Kwa kawaida, anapokabiliwa na nidhamu kama hiyo, mtoto wa kambo atasema maneno kama, “Wewe si baba yangu halisi!” Maneno kama hayo yanaweza kumvunja moyo kama nini mzazi mwenye nia njema!

  • Familia za Kambo Zinaweza Kufanikiwa
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Machi 1
    • Upendo wa kweli husaidia kupunguza kutopatana na huunganisha watu wenye malezi mbalimbali na nyutu tofauti sana. Nao husaidia kushinda hali yenye kuvunja moyo inayotokana na talaka au kifo cha mzazi halisi. Mwanamume mmoja aliyepata kuwa baba wa kambo afafanua matatizo yake hasa: “Mara nyingi nilihangaikia hisia zangu mno nisiweze kuchanganua hisia-moyo za watoto wangu wa kambo au hata za mke wangu. Ilinibidi nijifunze kutokuwa na hisia nyepesi mno. Jambo muhimu zaidi ni kwamba nilijifunza kuwa mnyenyekevu.” Upendo ulimsaidia kufanya marekebisho yaliyohitajika.

      Mzazi Halisi

      Upendo waweza kusaidia katika kushughulika na uhusiano wa watoto pamoja na baba yao halisi ambaye sasa hayupo. Baba wa kambo afunua siri hii: “Nilitaka watoto wangu wa kambo wanipende zaidi ya vile walivyompenda baba yao halisi. Walipomtembelea baba yao halisi, sikuweza kukinza kishawishi cha kumchambua. Waliporudi baada ya kuwa na wakati mzuri pamoja naye, nilihisi vibaya sana. Walipokuwa na wakati mbaya, nilifurahi. Kwa kweli nilihofia kupoteza shauku yao kwangu. Jambo lililokuwa gumu zaidi ni kung’amua na kukubali umuhimu wa fungu la baba halisi katika maisha ya watoto wangu wa kambo.”

      Upendo wa kweli ulimsaidia baba huyo wa kambo kukabili uhakika wa kwamba halikuwa jambo la akili kutarajia kupendwa “mara moja.” Hakupaswa kuhisi amekataliwa wakati watoto walipokosa kumkubali mara moja. Alikuja kung’amua kwamba huenda asiweze kamwe kuchukua kabisa mahali pa baba halisi katika mioyo ya watoto wake. Hao watoto walimjua mwanamume huyo tangu walipokuwa wachanga kabisa, ilhali huyo baba wa kambo alikuwa mtu mpya ambaye ingembidi ajitahidi ili apate kupendwa na watoto hao. Mtafiti Elizabeth Einstein adhihirisha jambo linalowapata watu wengi anaposema hivi: “Mahali pa baba halisi hapawezi kamwe kuchukuliwa na mwingine—kamwe. Hata mzazi aliyekufa au aliyewaacha watoto huendelea kuwa na ushawishi muhimu katika maisha ya watoto hao.”

      Nidhamu—Suala Nyeti

      Biblia huonyesha kwamba nidhamu yenye upendo ni muhimu kwa vijana, nao hutia ndani watoto wa kambo. (Mithali 8:33) Wataalamu kadhaa wameanza kukubaliana na yale ambayo Biblia husema kuhusu jambo hilo. Profesa Ceres Alves de Araújo alisema: “Kiasili hakuna yeyote apendaye kuwekewa mipaka, lakini hiyo inahitajika. ‘La’ ni neno litoalo kinga.”

      Hata hivyo, katika familia zenye mzazi wa kambo, maoni kuhusu nidhamu yaweza kutokeza ugomvi mkubwa. Watoto wa kambo wameathiriwa kwa kadiri fulani na mtu mzima ambaye sasa hayupo. Yaelekea wana tabia au desturi ambazo huenda zikamwudhi mzazi wa kambo. Na yawezekana hawaelewi ni kwa nini mzazi wa kambo anashikilia sana mambo fulani. Utaishughulikiaje hali hiyo kwa mafanikio? Paulo ahimiza kwa bidii hivi: “Fuatia . . . upendo, uvumilivu, tabia-pole.” (1 Timotheo 6:11) Upendo wa Kikristo husaidia wazazi wa kambo na watoto wawe wapole na wenye subira wanapojifunza kuelewana. Ikiwa mzazi wa kambo anakosa subira, ‘hasira, hasira ya kisasi, usemi wenye kuudhi’ waweza kuharibu haraka uhusiano wowote ambao umepatikana.—Waefeso 4:31.

      Ufahamu wenye kina kuhusu yale yatakayosaidia katika jambo hilo ulitolewa na nabii Mika. Yeye alisema: “BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema [“fadhili,” NW], na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” (Mika 6:8) Haki ni jambo muhimu nidhamu inapotolewa. Lakini namna gani fadhili? Mzee mmoja Mkristo asimulia kwamba mara nyingi ilikuwa vigumu kuwaamsha watoto wake wa kambo Jumapili asubuhi ili washiriki katika ibada ya kutaniko. Badala ya kuwakemea vikali, alijaribu kuwa mwenye fadhili. Aliamka mapema, akatayarisha kiamsha-kinywa, kisha akapelekea kila mmoja wao kinywaji chenye joto. Tokeo likawa kwamba walielekea zaidi kusikiza ombi lake la kuwataka waamke.

      Profesa Ana Luisa Vieira de Mattos alitoa maelezo yafuatayo yenye kupendeza: “Kilicho muhimu si aina ya familia bali ni ubora wa uhusiano huo. Katika utafiti wangu nimeng’amua kwamba vijana walio na matatizo ya kitabia karibu sikuzote hutoka katika familia ambamo mna usimamizi dhaifu wa wazazi, ukosefu wa sheria na mawasiliano.” Yeye pia alisema: “Yapaswa kukaziwa sana kwamba kulea watoto kwamaanisha uhitaji wa kusema la.” Kwa kuongezea, Madakt. Emily na John Visher walisema: “Kimsingi, nidhamu huwa na matokeo wakati ambapo mtu anayeipokea anajali juu ya itikio la mwenye kuitoa na vilevile uhusiano wake pamoja naye.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki