Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mambo Manne Unayopaswa Kujua Kuhusu Talaka
    Amkeni!—2010 | Februari
    • 4 Jinsi Talaka Inavyowaathiri Watoto

      “Niliumia sana,” anasema José, baba aliyetalikiana na mke wake huko Hispania. “Niliumia hata zaidi nilipogundua kwamba mume wa dada yangu ndiye aliyekuwa mpenzi wa mke wangu. Nilitaka tu kufa.” José aligundua kwamba wavulana wake wawili, wenye umri wa miaka miwili na minne, waliathiriwa pia na mwenendo wa mama yao. “Hawangeweza kuelewa hali hiyo,” anasema. “Hawakuelewa kwa nini mama yao alikuwa akiishi na mjomba wao na kwa nini mimi, dada yangu na mama yangu tuliishi pamoja. Nilipotaka kwenda mahali popote, waliniuliza, ‘Utarudi saa ngapi?’ au walisema, ‘Baba, usituache!’”

      Sad children

      Mara nyingi watoto wanakuwa majeruhi waliosahauliwa katika uwanja wa vita vya talaka. Lakini namna gani ikiwa wazazi wote wawili wanazozana kila wakati? Katika kisa kama hicho, je, kweli talaka “itawafaidi watoto”? Katika miaka ya hivi karibuni, wazo hilo limepingwa vikali—hasa wakati ambapo matatizo ya ndoa si mabaya sana. Kitabu The Unexpected Legacy of Divorce kinasema hivi: “Watu wengi wazima ambao wamenaswa katika ndoa zisizo na furaha watashangaa kujua kwamba watoto wao wanaridhika na jinsi hali ilivyo. Hawajali ikiwa Mama na Baba wanalala katika vitanda tofauti maadamu tu familia iko pamoja.”

      Ni kweli kwamba watoto hujua wakati wazazi wanapozozana, na mkazo katika ndoa unaweza kuathiri sana akili na mioyo yao. Hata hivyo, ni makosa kukata kauli haraka kwamba talaka itawafaidi watoto. “Inaonekana kwamba ndoa inawapa wazazi msingi mzuri wa kutoa nidhamu inayofaa ambayo watoto hukubali, hata ikiwa ndoa hiyo ina matatizo,” wanasema Linda J. Waite na Maggie Gallagher katika kitabu chao, The Case for Marriage.

      Huenda hili likatokea: Talaka inaweza kuwaathiri vibaya sana watoto wako hasa ikiwa huwatii moyo wawe na uhusiano mzuri na mwenzi wako wa zamani.—Ona sanduku “Nimenaswa Katikati.”

  • Mambo Manne Unayopaswa Kujua Kuhusu Talaka
    Amkeni!—2010 | Februari
    • “NIMENASWA KATIKATI”

      “Wazazi wangu walitalikiana nilipokuwa na umri wa miaka 12. Kwa kiasi fulani nilifurahi. Kulikuwa na utulivu na amani nyumbani kwa kuwa hakukuwa na ugomvi kati yao kama ilivyokuwa hapo awali. Lakini bado nilikuwa nimechanganyikiwa.

      “Baada ya talaka, nilitaka kuwa na uhusiano mzuri na wazazi wangu, na nilijaribu sana kutojihusisha katika mambo yao. Lakini haidhuru nilifanya nini, bado nilijihisi ni kama nimenaswa katikati. Baba yangu aliniambia alikuwa na wasiwasi kwamba mama angefanya nimchukie. Hivyo, kila mara ilibidi nimhakikishie kwamba mama hakuwa akijaribu kufanya hivyo. Mama pia alikuwa na wasiwasi mwingi. Aliogopa kwamba nilikuwa nikisikiliza mambo mabaya ambayo baba alikuwa akisema kumhusu. Hali hiyo ilikuwa mbaya hivi kwamba singewaeleza wazazi wangu hisia zangu kwa kuwa sikutaka kuwaumiza. Kwa hiyo, tangu nilipokuwa na umri wa miaka 12 na kuendelea, sikumweleza yeyote jinsi nilivyohisi kuhusu talaka yao.”—Sandra.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki