-
Mambo Manne Unayopaswa Kujua Kuhusu TalakaAmkeni!—2010 | Februari
-
-
4 Jinsi Talaka Inavyowaathiri Watoto
“Niliumia sana,” anasema José, baba aliyetalikiana na mke wake huko Hispania. “Niliumia hata zaidi nilipogundua kwamba mume wa dada yangu ndiye aliyekuwa mpenzi wa mke wangu. Nilitaka tu kufa.” José aligundua kwamba wavulana wake wawili, wenye umri wa miaka miwili na minne, waliathiriwa pia na mwenendo wa mama yao. “Hawangeweza kuelewa hali hiyo,” anasema. “Hawakuelewa kwa nini mama yao alikuwa akiishi na mjomba wao na kwa nini mimi, dada yangu na mama yangu tuliishi pamoja. Nilipotaka kwenda mahali popote, waliniuliza, ‘Utarudi saa ngapi?’ au walisema, ‘Baba, usituache!’”
Mara nyingi watoto wanakuwa majeruhi waliosahauliwa katika uwanja wa vita vya talaka. Lakini namna gani ikiwa wazazi wote wawili wanazozana kila wakati? Katika kisa kama hicho, je, kweli talaka “itawafaidi watoto”? Katika miaka ya hivi karibuni, wazo hilo limepingwa vikali—hasa wakati ambapo matatizo ya ndoa si mabaya sana. Kitabu The Unexpected Legacy of Divorce kinasema hivi: “Watu wengi wazima ambao wamenaswa katika ndoa zisizo na furaha watashangaa kujua kwamba watoto wao wanaridhika na jinsi hali ilivyo. Hawajali ikiwa Mama na Baba wanalala katika vitanda tofauti maadamu tu familia iko pamoja.”
Ni kweli kwamba watoto hujua wakati wazazi wanapozozana, na mkazo katika ndoa unaweza kuathiri sana akili na mioyo yao. Hata hivyo, ni makosa kukata kauli haraka kwamba talaka itawafaidi watoto. “Inaonekana kwamba ndoa inawapa wazazi msingi mzuri wa kutoa nidhamu inayofaa ambayo watoto hukubali, hata ikiwa ndoa hiyo ina matatizo,” wanasema Linda J. Waite na Maggie Gallagher katika kitabu chao, The Case for Marriage.
Huenda hili likatokea: Talaka inaweza kuwaathiri vibaya sana watoto wako hasa ikiwa huwatii moyo wawe na uhusiano mzuri na mwenzi wako wa zamani.—Ona sanduku “Nimenaswa Katikati.”
-