Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Msiwe na Wasiwasi Juu ya Kesho”
    Amkeni!—2010 | Julai
    • “Msiwe na Wasiwasi Juu ya Kesho”

      Renée alikuwa amekata tamaa. Mume wake Matthew, hakuwa ameajiriwa kwa zaidi ya miaka mitatu. “Nilikuwa nimefadhaika sana,” anasema Renée. “Nilivunjika moyo sana kwa kuwa sikujua ni nini ambacho kingetokea!” Matthew alijaribu kumtuliza mke wake kwa kumweleza kwamba hakuna wakati ambapo wamewahi kukosa kile walichohitaji. “Lakini bado huna kazi!” Renée akajibu. “Tunahitaji pesa!”

      BILA shaka kupoteza kazi humfanya mtu ahangaike. Mtu asiye na kazi hujiuliza, ‘Nitakaa kwa muda gani bila kazi? Tunaweza kutosheleza mahitaji ya familia yetu kwa njia gani?’

      Ingawa ni kawaida kuwa na mahangaiko kama hayo, Yesu Kristo alitoa mashauri haya mazuri yanayoweza kupunguza mahangaiko. Alisema hivi: “Msiwe na wasiwasi juu ya kesho . . . Matatizo ya siku moja yanawatosheni kwa siku hiyo.”—Mathayo 6:34, Biblia Habari Njema.

      Tambua Mambo Yanayokutia Wasiwasi

      Yesu hakuwa akisema kwamba tunapaswa kutenda kana kwamba hatuna matatizo. Hata hivyo, kuhangaikia mambo yanayoweza kutokea kesho kutakuongezea tu wasiwasi leo. Kwa kweli, hatuwezi kuzuia mambo yatakayotokea kesho, yawe mazuri au mabaya. Lakini tunaweza kuchukua hatua za kukabiliana na mahangaiko ya leo.

      Bila shaka, si rahisi kufanya hivyo. Rebekah, ambaye mume wake alikuwa amepoteza kazi aliyokuwa ameifanya kwa miaka 12 anasema hivi: “Unapokabiliwa na hisia kali, ni vigumu kufikiria mambo kihalisi. Lakini tulilazimika kufanya hivyo. Kwa hiyo, nilijaribu kudhibiti hisia zangu. Mambo yaliyonitia wasiwasi yalipokosa kutokea, nilitambua kwamba kuhangaika hakuna faida yoyote. Tulipokazia fikira mambo ya sasa na matatizo yaliyokuwapo, tulipunguza mfadhaiko.”

      Jiulize: ‘Ni nini kinachonitia wasiwasi? Kuna uwezekano gani kwamba jambo linalonitia wasiwasi litatukia? Mimi hutumia nguvu nyingi kadiri gani kuhangaika kuhusu jambo ambalo huenda likatokea au lisitokee?’

      Jifunze Kuridhika

      Mtazamo wetu unaweza kuathiri hisia zetu. Kwa hiyo, Biblia inatuhimiza tuwe na mtazamo huu wa akili: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:8) Kuridhika kunamaanisha kupunguza mambo tunayotaka na kutosheka wakati mahitaji yetu ya kila siku yanapotimizwa. Kujitahidi kutosheleza tamaa zetu kutavuruga jitihada zetu za kupunguza gharama.—Marko 4:19.

      Renée alifaulu kukuza sifa ya kuridhika baada ya kuona hali yake kihalisi. Anasema hivi: “Hatujawahi kukosa umeme au gesi, wala hatujakosa makao. Tatizo kuu ni kwamba hatukuwa tumezoea kuishi kwa njia hiyo, na tamaa yangu ya kudumisha maisha tuliyokuwa nayo iliongeza tu mfadhaiko wangu.”

      Punde si punde, Renée alitambua kwamba si hali zake zilizofanya maisha yake yawe magumu bali ni mtazamo wake. Anasema hivi: “Nilihitaji kuona hali yetu kihalisi bila kukazia fikira jinsi nilivyotaka mambo yawe. Nilipoanza kuridhika na yale ambayo Mungu alituandalia kila siku, nilikuwa na furaha zaidi.”

      Jiulize: ‘Je, mahitaji yangu ya leo yameshughulikiwa? Ikiwa ndivyo, je, ninaweza kukazia fikira mambo ya leo nikiwa na uhakika kwamba ya kesho yatashughulikiwa pia?’

      Kuwa na mtazamo unaofaa ndiyo hatua ya kwanza ya kukabiliana na ugumu wa kupunguza gharama zetu.a Lakini unaweza kuchukua hatua gani zinazofaa ikiwa mapato yako yameathiriwa na kupoteza kazi?

      [Maelezo ya Chini]

      a Ili upate habari zaidi kuhusu kutafuta na kudumisha kazi, ona Amkeni! la Julai 8, 2005 (8/7/2005), ukurasa wa 3-11.

      [Sanduku katika ukurasa wa 5]

      Mvumilivu Hula Mbivu!

      Baada ya kutafuta kazi kwa majuma kadhaa bila kufaulu, Fred alihisi kwamba juhudi zake zimegonga mwamba. Alisema hivi, “Ilikuwa kama kusubiri mtu akuchukue kwenye kituo cha basi lakini hakuna anayetokea.” Fred aliamua kufanya yote ambayo angeweza. Alituma maombi ya kazi kwenye kampuni yoyote ambayo ingehitaji ujuzi wake hata kama ni kwa kadiri ndogo sana. Alifuatilia majibu yote aliyopokea na kujitayarisha kwa ajili ya mahojiano yote, akiwa amesadiki kwamba “mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.” (Methali 21:5) Fred anasema, “Kwenye kampuni moja, nilihojiwa mara mbili na meneja wakuu.” Lakini Fred alipata matokeo mazuri kwa sababu ya bidii yake. Anasema hivi, “Mwishowe niliajiriwa!”

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

      Jambo Muhimu Kuliko Mshahara

      Ni nini muhimu zaidi—utu wako au mshahara wako? Hebu ona methali mbili za Biblia.

      “Afadhali maskini anayetembea katika utimilifu wake kuliko mtu yeyote aliyepotoka katika njia zake, ingawa ni tajiri.”—Methali 28:6.

      “Afadhali chakula cha mboga za majani mahali penye upendo kuliko ng’ombe-dume aliyenoneshwa pamoja na chuki.”—Methali 15:17.

      Sifa zako nzuri na thamani yako haipotei unapopoteza kazi. Hivyo, mume wa Renée alipoachishwa kazi, aliwaambia hivi watoto wake: “Akina baba wengi wameacha familia zao. Lakini baba yenu bado yuko. Mnajua kwamba anawapenda na amewasaidia mlipokuwa na matatizo. Hamwezi kupata baba mzuri kuliko yeye!”

  • Jinsi ya Kupunguza Gharama
    Amkeni!—2010 | Julai
    • Jinsi ya Kupunguza Gharama

      ILI upunguze gharama zako unahitaji kupanga mambo kwa uangalifu. Yesu alikazia umuhimu wa jambo hilo. Aliuliza hivi: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” (Luka 14:28, 29) Kwa kutumia kanuni hiyo, unaweza “kuhesabu gharama” ya kuishi kulingana na mapato yako ikiwa utapanga bajeti. Kwa njia gani? Hebu jaribu kufanya hivi:

      Unapopata mshahara wako, tenga pesa hususa katika vikundi tofauti ili kushughulikia gharama za sasa au za wakati ujao. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 8.) Unapopanga gharama zako, unaweza kuona mahali pesa zako zinaenda na unatumia kiasi gani kununua vitu visivyo vya lazima. Kufanya hivyo kutakusaidia kuamua jinsi unavyoweza kupunguza gharama zako.

      Ili upange bajeti inayokufaa, jaribu kutumia mapendekezo yafuatayo.

      Tumia Busara Unaponunua Vitu

      Raúl alipoachishwa kazi, mke wake Bertha, alibadili mbinu yake ya kununua vitu. Anasema, “Niliangalia matangazo yaliyoonyesha mahali ambapo bidhaa zimepunguzwa bei na maduka ya mboga yaliyouza vitu viwili kwa bei ya kimoja.” Zifuatazo ni mbinu nyingine:

      ● Pika vyakula vinavyopatikana kwa wingi.

      ● Jipikie chakula badala ya kununua kilichopikwa na kupakiwa.

      ● Nunua bidhaa za ziada zinapopatikana kwa wingi au kwa bei ya chini.

      ● Nunua vitu kwa jumla, lakini jihadhari usijaze vitu vinavyoweza kuharibika upesi.

      ● Punguza gharama kwa kununua mavazi mazuri yaliyotumika.

      ● Safiri hadi maeneo ambako bei ni za chini, ikiwa hutatumia pesa nyingi kwa ajili ya usafiri.

      ● Punguza safari za kwenda dukani.a

      Andika

      Fred anasema, “Tulilazimika kupanga bajeti, kwa hiyo, niliandika gharama ambazo tulihitaji kulipa mara moja na pesa za matumizi ya mwezi mzima.” Mke wake, Adele, anasema hivi: “Nilijua ni pesa ngapi nitakazotumia ninapoenda sokoni. Nyakati nyingine nilipohitaji kununua kitu cha nyumbani au kwa ajili ya watoto, niliitazama bajeti na kujiambia, ‘Sina pesa za kukinunua, kwa hiyo, tutasubiri hadi mwezi ujao.’ Kuandika kulinisaidia sana!”

      Fikiria Kabla ya Kununua

      Uwe na zoea la kujiuliza: ‘Je, kweli ninahitaji kitu hiki? Je, kweli kile cha zamani kimechakaa, au ninataka tu kitu kipya?’ Ikiwa hutumii kitu fulani kwa ukawaida, je, si afadhali tu kukodi kitu hicho? Au ikiwa unafikiri kwamba utakitumia mara nyingi, je, unaweza kununua kilichotumika?

      Ingawa huenda ikaonekana kuwa jambo dogo kufanya mambo yaliyotajwa hapa juu, yanapofanywa yote yanaweza kusaidia sana! Jambo kuu ni, ukiwa na zoea la kuokoa pesa unazotumia kwa ajili ya vitu vidogovidogo, utafanya hivyo pia unaposhughulikia mambo makubwa.

      Tafuta Njia za Kupunguza Gharama

      Ili uokoe pesa unazotumia kununua vitu visivyo vya lazima, uwe mbunifu. Kwa mfano, Adele anasema hivi: “Tulikuwa na magari mawili lakini tukauza moja na kutumia hilo lingine. Ili tuokoe pesa tulizotumia kununua petroli, tulipanga kufanya shughuli nyingi kwa wakati mmoja. Tulitumia pesa kwa ajili tu ya vitu vya lazima.” Zifuatazo ni njia nyingine zinazoweza kukusaidia kupunguza gharama:

      ● Kuza mboga zako nyumbani.

      ● Fuata maagizo ya watengenezaji wa vifaa, ili vidumu kwa muda mrefu.

      ● Badili mavazi yako mazuri mara tu unapofika nyumbani kwani kufanya hivyo kutayafanya yadumu yakiwa mapya kwa muda mrefu zaidi.

      Usijitenge!

      Watu wengi ambao hupoteza kazi hujitenga na wengine. Lakini Fred hakujitenga! Alitegemezwa kwa fadhili na watu wa familia yake, kutia ndani watoto wake wakubwa. Anasema hivi: “Tulijifunza kushirikiana katika mambo mengi na hilo lilitufanya tuwe na uhusiano wa karibu. Sote tulijiambia hivi, ‘Hili ni tatizo letu sisi sote.’”

      Pia, Fred aliimarishwa na Wakristo wenzake alipokutana nao kwa ukawaida kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Anasema hivi: “Kila wakati baada ya mikutano yetu ya Kikristo, nilihisi nimetiwa moyo. Kila mtu alikuwa mwenye fadhili na ufikirio. Faraja na msaada wao ulitufanya tutambue kwamba hatuko peke yetu.”—Yohana 13:35.

      Manufaa za Kuwa na Imani

      Kuachishwa kazi kumewafanya mamilioni ya watu wahisi wakiwa wamechukizwa na kusalitiwa na waajiri wao. Raúl aliyetajwa hapo awali, alivunjwa moyo alipopoteza kazi mara mbili, kwanza katika nchi ya nyumbani ya Peru na kisha huko New York City. Baada ya kuachishwa kazi mara ya pili, Raúl alisema, “Katika ulimwengu wa leo, huwezi kutegemea kitu chochote.” Kwa miezi mingi, hakufanikiwa kupata kazi. Ni nini kilichomsaidia kukabiliana na hali hiyo? Raúl alisema, “Nilisitawisha urafiki wa karibu pamoja na Mungu na nikatambua kwamba ninaweza kumtegemea kikamili.”

      Raúl ni Shahidi wa Yehova, na kujifunza Biblia kumemsaidia asitawishe imani yenye nguvu katika Baba wa mbinguni mwenye kujali ambaye anaahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Waebrania 13:5) Hali zilikuwa ngumu. Raúl anasema, “Sikuzote tulisali ili tupate mahitaji ya lazima, na tulijifunza kuridhika na kile ambacho Mungu alituandalia.” Bertha, mke wa Raúl, anasema hivi: “Nyakati nyingine nilikuwa na wasiwasi mwingi nikijiuliza ikiwa Raúl atapata kazi. Lakini tuliona kwamba Yehova alijibu sala zetu kwa kutuandalia mahitaji yetu kila siku. Hata ingawa hatukuwa na vitu vingi kama hapo awali, maisha yetu yalikuwa rahisi zaidi sasa.”

      Kwa kuwa Fred ni Shahidi wa Yehova kujifunza Biblia kumemsaidia sana kukabiliana na hali yake. Anasema hivi: “Nyakati nyingine, tunategemea sana kazi, cheo, au pesa tulizo nazo kwenye benki. Lakini nilijifunza kwamba ni Yehova Mungu peke yake anayeweza kumtegemeza kikweli, na uhusiano wetu pamoja naye ndio unaoweza kutuletea utegemezo huo.”b

      [Maelezo ya Chini]

      a Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 60 hivi ya bidhaa zote zilizonunuliwa hazikuwa zimepangiwa.

      b Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kutumia pesa vizuri, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2009 (1/8/2009) ukurasa wa 10-12.

      [Blabu katika ukurasa wa 9]

      “Sikuzote tulisali ili tupate mahitaji ya lazima, na tulijifunza kuridhika na kile ambacho Mungu alituandalia”

      [Sanduku/Ramani katika ukurasa wa 8]

      Jinsi ya Kupanga Bajeti

      (1) Andika gharama za lazima za kila mwezi. Weka rekodi ya pesa zote unazotumia mwezi mzima kwa chakula, nyumba, malipo ya huduma mbalimbali, gharama za gari, na kadhalika. Kwa ajili ya gharama zinazolipiwa kila mwaka, gawa gharama hizo mara 12 ili uhifadhi pesa hizo kila mwezi.

      (2) Orodhesha gharama katika vikundi mbalimbali. Chakula, nyumba, gari, usafiri, na kadhalika.

      (3) Tambua ni pesa ngapi ulizohifadhi utakazotumia kila mwezi kulipia matumizi ya kila kikundi kwenye orodha yako. Kwa ajili ya gharama za kila mwaka, “piga hesabu” ni pesa ngapi unazopaswa kuhifadhi kila mwezi.

      (4) Andika jumla ya mapato yote ya kila mtu nyumbani. Ondoa malipo kama vile kodi. Linganisha na gharama.

      (5) Tenga kiasi unachohitaji kila mwezi ili kulipia kila kikundi. Ikiwa unatumia pesa taslimu, njia rahisi ni kuwa na bahasha iliyo na alama ya kila kikundi. Kisha, tia pesa zinazohitajika ili kugharimia mahitaji hayo ndani ya kila bahasha.

      Tahadhari: Ikiwa unatumia kadi ya mkopo, fanya hivyo kwa hekima! Bajeti za watu wengi zimevurugwa na tamaa ya ‘kununua sasa, kulipia baadaye.’

      [Chati]

      (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

      Mapato ya Mwezi

      MSHAHARA WA MWEZI Sh.․․․․․ MAPATO MENGINE Sh.․․․․․

      MSHAHARA WA WATU

      WENGINE NYUMBANI Sh.․․․․․ JUMLA YA MAPATO HALISI

      Sh.․․․․․

      Gharama za Mwezi Pesa

      Ulizopangia Ulizotumia

      Sh.․․․․․ Kodi ya Nyumba Sh.․․․․․

      Sh.․․․․․ Bima/Kodi Nyingine Sh.․․․․․

      Sh.․․․․․ Gharama za Huduma Sh.․․․․․

      Sh.․․․․․ Gharama za Gari Sh.․․․․․

      Sh.․․․․․ Burudani/Usafiri Sh.․․․․․

      Sh.․․․․․ Simu Sh.․․․․․

      Sh.․․․․․ Chakula Sh.․․․․․

      Sh.․․․․․ Gharama Nyingine Sh.․․․․․

      JUMLA JUMLA

      Sh.․․․․․ Sh.․․․․․

      Linganisha na Matumizi

      MAPATO YA MWEZI Sh.․․․․․

      ONDOA− SALIO

      MATUMIZI YA MWEZI Sh.․․․․․ Sh.․․․․․

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki