-
Je, Kweli Una Imani Katika Habari Njema?Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 15
-
-
Je, Kweli Una Imani Katika Habari Njema?
“Ufalme wa Mungu umekaribia. Iweni wenye kutubu, nyinyi watu, na iweni na imani katika habari njema.”—MARKO 1:15.
1, 2. Unaweza kuelezaje andiko la Marko 1:14, 15?
ULIKUWA mwaka wa 30 W.K. naye Yesu Kristo alikuwa ameanza huduma yake ya pekee huko Galilaya. Alikuwa akihubiri “habari njema ya Mungu,” naye aliwachochea Wagalilaya wengi kwa maneno haya: “Wakati uliowekwa umetimizwa, na ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni, na kuwa na imani katika habari njema.”—Marko 1:14, 15.
2 “Wakati uliowekwa” ulikuwa umefika kwa Yesu kuanza huduma yake, na kwa watu kufanya uamuzi ambao ungewawezesha kupata kibali cha Mungu. (Luka 12:54-56) ‘Ufalme wa Mungu ulikuwa umekaribia’ kwa sababu Yesu alikuwa miongoni mwao akiwa Mfalme-Mteule. Kazi yake ya kuhubiri iliwachochea watu wenye mioyo minyofu watubu. Lakini watu hao walionyeshaje “imani katika habari njema,” nasi tunaionyeshaje?
3. Watu wameonyeshaje kwamba wana imani katika habari njema?
3 Kama Yesu, mtume Petro aliwatia watu moyo watubu. Akiwahutubia Wayahudi huko Yerusalemu siku ya Pentekoste 33 W.K., Petro alisema: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu, nanyi mtapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.” Maelfu walitubu, wakabatizwa na kuwa wafuasi wa Yesu. (Matendo 2:38, 41; 4:4) Katika mwaka wa 36 W.K., watu wasio Wayahudi pia walichukua hatua hizohizo. (Matendo 10:1-48) Leo imani katika habari njema inawachochea maelfu watubu dhambi zao, wajiweke wakfu kwa Mungu, na kubatizwa. Watu hao wamekubali habari njema za wokovu na wanadhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Isitoshe, wanafuata uadilifu na wanaunga mkono Ufalme wa Mungu.
4. Imani ni nini?
4 Lakini imani ni nini? Mtume Paulo aliandika: “Imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.” (Waebrania 11:1) Imani yetu hutufanya tuwe na uhakika kabisa kwamba kila ahadi ambayo Mungu ametoa katika Neno lake itatimizwa. Ni kana kwamba tayari tuna hati ya kumiliki inayothibitisha tunamiliki mali fulani. Imani pia ni “wonyesho dhahiri,” au uthibitisho wa mambo yasiyoonekana. Ufahamu wetu na pia moyo uliojaa shukrani hufanya tuwe na uhakika kwamba mambo hayo ni halisi, ingawa hatujayaona.—2 Wakorintho 5:7; Waefeso 1:18.
Tunahitaji Imani!
5. Kwa nini imani ni muhimu sana?
5 Ingawa tulizaliwa tukiwa na uhitaji wa kiroho, hatukuzaliwa tukiwa na imani. Kwa kweli “imani si miliki ya watu wote.” (2 Wathesalonike 3:2) Hata hivyo, ni lazima Wakristo wawe na imani ili kurithi ahadi za Mungu. (Waebrania 6:12) Baada ya kutaja mifano mingi ya imani, Paulo aliandika: “Kwa sababu tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi likituzingira, acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu, tumkaziapo macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.” (Waebrania 12:1, 2) Ni ‘dhambi gani ambayo hututatanisha kwa urahisi’? Dhambi hiyo ni ukosefu wa imani, au hata kupoteza imani ambayo mtu alikuwa nayo hapo awali. Ili kudumisha imani yenye nguvu, ni lazima ‘tumkazie macho Yesu’ na kufuata kielelezo chake. Tunahitaji pia kukataa ukosefu wa maadili, kupambana na matendo ya mwili, na kuepuka falsafa za ulimwengu, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, na mapokeo yasiyopatana na Maandiko. (Wagalatia 5:19-21; Wakolosai 2:8; 1 Timotheo 6:9, 10; Yuda 3, 4) Zaidi ya hayo, ni lazima tuamini kwamba Mungu yu pamoja nasi na kwamba ushauri wa Neno lake unafaa.
6, 7. Kwa nini inafaa tusali ili tupewe imani?
6 Hatuwezi kusitawisha imani kwa nguvu zetu wenyewe. Imani ni mojawapo ya matunda ya roho takatifu ya Mungu, au nguvu ya utendaji. (Wagalatia 5:22, 23) Namna gani iwapo imani yetu inahitaji kutiwa nguvu? Yesu alisema: “Ikiwa nyinyi . . . mwajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, si zaidi sana yule Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:13) Naam, na tusali tupate roho takatifu, kwa kuwa inaweza kufanya tuwe na imani tunayohitaji ili kufanya mapenzi ya Mungu hata katika hali ngumu sana.—Waefeso 3:20.
7 Inafaa tusali ili tupewe imani zaidi. Kabla Yesu hajamfukuza roho mwovu kutoka kwa mvulana mmoja, baba yake alisihi hivi: “Nina imani! Unisaidie ambapo nahitaji imani!” (Marko 9:24) Nao wanafunzi wa Yesu wakamwambia hivi: “Tupe sisi imani zaidi.” (Luka 17:5) Kwa hiyo, na tusali ili tupewe imani, tukiwa na uhakika kwamba Mungu hujibu sala hizo.—1 Yohana 5:14.
Ni Muhimu Kuwa na Imani Katika Neno la Mungu
8. Imani katika Neno la Mungu inaweza kutusaidiaje?
8 Muda mfupi kabla ya kifo chake cha kidhabihu, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Msiache mioyo yenu itaabishwe. Dhihirisheni imani katika Mungu, dhihirisheni imani pia katika mimi.” (Yohana 14:1) Tukiwa Wakristo tuna imani katika Mungu na katika Mwana wake. Lakini je, tuna imani katika Neno la Mungu? Neno la Mungu linaweza kutunufaisha tukilisoma na kulifuata tukiwa na uhakika kabisa kwamba litatupatia ushauri na mwongozo bora.—Waebrania 4:12.
9, 10. Ungeelezaje yale ambayo andiko la Yakobo 1:5-8 linasema kuhusu imani?
9 Maisha yetu yamejaa matatizo kwa kuwa sisi ni wanadamu wasio wakamilifu. Hata hivyo, imani katika Neno la Mungu inaweza kwa kweli kutusaidia. (Ayubu 14:1) Kwa mfano, tuseme kwamba hatujui jinsi ya kushughulika na jaribu fulani. Neno la Mungu hutupatia ushauri huu: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo. Lakini acheni afulize kuomba katika imani, bila kutia shaka hata kidogo, kwa maana yeye atiaye shaka ni kama wimbi la bahari liendeshwalo na upepo na kupeperushwa huku na huku. Kwa kweli, acheni mtu huyo asidhani kwamba atapokea kitu chochote kutoka kwa Yehova; yeye ni mtu wa kusitasita kuamua, asiye imara katika njia zake zote.”—Yakobo 1:5-8.
10 Yehova Mungu hatatushutumu kwa kukosa hekima au kwa kusali tuipate. Badala yake, atatusaidia tulione jaribu hilo kwa njia inayofaa. Huenda tukapata msaada wa Kimaandiko kutoka kwa waamini wenzetu au tunapojifunza Biblia. Au huenda roho takatifu ya Yehova ikatuongoza kwa njia nyingine. Baba yetu wa mbinguni atatupatia hekima ya kukabiliana na majaribu ‘tukifuliza kuomba katika imani, bila kutia shaka hata kidogo.’ Hatungetazamia Mungu atupatie hekima hiyo ikiwa tungekuwa kama wimbi la bahari linaloendeshwa na upepo. Kwa nini? Kwa sababu ingemaanisha kwamba tunasitasita na kuyumbayumba katika sala au katika njia nyingine—naam, hata katika kuonyesha imani. Kwa hiyo, tunahitaji kuwa na imani thabiti katika Neno la Mungu na katika mwongozo anaotoa. Hebu tuone mifano fulani inayoonyesha jinsi Neno lake linavyotoa msaada na mwongozo.
Imani na Riziki
11. Imani katika Neno la Mungu hutupatia uhakika gani kuhusu mahitaji yetu ya kila siku?
11 Namna gani ikiwa kwa sasa hatuna chakula cha kutosha wala makao, au sisi ni maskini? Imani katika Neno la Mungu hutupatia taraja lililo hakika kwamba Yehova atatimiza mahitaji yetu ya kila siku na hatimaye atahakikisha kwamba amewaandalia kwa wingi wote wampendao. (Zaburi 72:16; Luka 11:2, 3) Huenda tukatiwa moyo kutafakari jinsi Yehova alivyomwandalia chakula nabii wake Eliya wakati wa njaa. Baadaye Mungu alitumia muujiza kuhakikisha kwamba unga na mafuta ambayo mwanamke fulani, mwanawe, na Eliya walihitaji ili kuendelea kuishi hayakwisha. (1 Wafalme 17:2-16) Vivyo hivyo, Yehova alimtimizia nabii Yeremia mahitaji yake wakati Wababiloni walipozingira Yerusalemu. (Yeremia 37:21) Ingawa Yeremia na Eliya walikuwa na chakula kidogo, Yehova aliwatunza. Yeye huwatunza pia wale wanaomwamini leo.—Mathayo 6:11, 25-34.
12. Imani itatusaidiaje kupata riziki?
12 Kuwa na imani na kufuata kanuni za Biblia hakutatutajirisha kimwili, lakini kutatusaidia kupata riziki. Kwa mfano: Biblia hutushauri tuwe wanyofu, stadi, na wenye bidii. (Mithali 22:29; Mhubiri 5:18, 19; 2 Wakorintho 8:21) Na tusipuuze kamwe umuhimu wa kuwa na sifa nzuri kazini. Wafanyakazi wanyofu, stadi, na wenye bidii hufanikiwa kupata kazi nzuri hata katika maeneo ambako ni vigumu kwa wengine kuipata. Ingawa huenda wafanyakazi hao wasiwe matajiri, kwa kawaida wao hupata riziki na wanaridhika kwa kujua kwamba wanakula chakula ambacho wamejitafutia wenyewe.—2 Wathesalonike 3:11, 12.
Imani Hutusaidia Kuvumilia Huzuni
13, 14. Imani hutusaidiaje kuvumilia huzuni?
13 Neno la Mungu linaonyesha kwamba ni jambo la kawaida kuhuzunika mtu tumpendaye anapokufa. Mzee wa ukoo Abrahamu aliomboleza kifo cha mkewe Sara. (Mwanzo 23:2) Daudi alikuwa na huzuni nyingi alipopata habari za kifo cha mwanawe Absalomu. (2 Samweli 18:33) Hata mwanadamu mkamilifu Yesu alilia rafiki yake Lazaro alipokufa. (Yohana 11:35, 36) Tunaweza kuhuzunika sana mtu tumpendaye anapokufa, hata hivyo imani katika ahadi za Neno la Mungu inaweza kutusaidia kuvumilia huzuni hiyo.
14 Paulo alisema, ‘nina tumaini kuelekea Mungu kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.’ (Matendo 24:15) Tunahitaji kuwa na imani katika mpango wa Mungu wa kufufua watu wengi. (Yohana 5:28, 29) Miongoni mwao watakuwapo Abrahamu na Sara, Isaka na Rebeka, Yakobo na Lea—ambao wamelala katika kifo wakingojea kufufuliwa kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Mwanzo 49:29-32) Kutakuwa na furaha iliyoje wakati wapendwa watakapoamshwa kutoka katika usingizi wa kifo ili waishi hapa duniani! (Ufunuo 20:11-15) Wakati huu imani haiwezi kutuondolea huzuni kabisa, lakini itatuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu, ambaye hutusaidia kuvumilia tunapofiwa.—Zaburi 121:1-3; 2 Wakorintho 1:3.
Imani Huwatia Nguvu Walioshuka Moyo
15, 16. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba hata wale walio na imani hushuka moyo? (b) Ni nini kinachoweza kufanywa ili kukabiliana na mshuko-moyo?
15 Neno la Mungu pia huonyesha kwamba hata wale walio na imani wanaweza kushuka moyo. Wakati alipopatwa na jaribu kali, Ayubu alihisi kwamba Mungu alikuwa amemwacha. (Ayubu 29:2-5) Nehemia alihuzunishwa na hali ya ukiwa ya Yerusalemu na kuta zake. (Nehemia 2:1-3) Petro alifadhaika sana baada ya kumkana Yesu hivi kwamba ‘alitoa machozi kwa uchungu.’ (Luka 22:62) Naye Paulo aliwahimiza waamini wenzake katika kutaniko la Thesalonike ‘waseme kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.’ (1 Wathesalonike 5:14) Kwa hiyo, leo si ajabu kwa wale walio na imani kushuka moyo. Hivyo basi, tunaweza kufanya nini ili kukabiliana na mshuko-moyo?
16 Huenda tumeshuka moyo kwa sababu tunakabili matatizo kadhaa makubwa. Badala ya kuona matatizo hayo kama tatizo moja kubwa mno, tunaweza kuyatatua moja baada ya jingine kwa kutumia kanuni za Biblia. Hiyo inaweza kufanya hali yetu ya kushuka moyo isiwe mbaya sana. Utendaji unaofaa na kupumzika vya kutosha kunaweza pia kutusaidia. Jambo moja ni hakika: Imani katika Mungu na Neno lake huboresha hali yetu ya kiroho kwa sababu imani hiyo hutia nguvu usadikisho wetu kwamba anatujali kikweli.
17. Tunajuaje kwamba Yehova anatujali?
17 Petro anatupatia uhakikisho huu wenye kufariji: “Jinyenyekezeni chini ya mkono wa Mungu wenye uweza, ili apate kuwakweza nyinyi katika wakati upasao; huku mkitupa hangaiko lenu lote juu yake, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.” (1 Petro 5:6, 7) Mtunga-zaburi aliimba: “BWANA huwategemeza wote waangukao, huwainua wote walioinama chini.” (Zaburi 145:14) Tunapaswa kuamini uhakikisho huo kwa kuwa unapatikana katika Neno la Mungu. Ingawa huenda mshuko-moyo ukaendelea, ni jambo linalotia imani nguvu kama nini kujua kwamba tunaweza kumtwika Baba yetu wa mbinguni mahangaiko yetu yote!
Imani na Majaribu Mengine
18, 19. Imani hutusaidiaje kukabiliana na ugonjwa na kuwafariji waamini wenzetu walio wagonjwa?
18 Imani yetu inaweza kujaribiwa vikali wakati sisi au wapendwa wetu wanapopatwa na ugonjwa mbaya. Ingawa Biblia haisemi ikiwa Wakristo kama Epafrodito, Timotheo, na Trofimo waliponywa kimuujiza, hapana shaka kwamba Yehova aliwasaidia kuvumilia. (Wafilipi 2:25-30; 1 Timotheo 5:23; 2 Timotheo 4:20) Isitoshe, mtunga-zaburi aliimba hivi kumhusu yule “amkumbukaye mnyonge”: “BWANA atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia.” (Zaburi 41:1-3) Maneno hayo ya mtunga-zaburi yanaweza kutusaidiaje kuwafariji waamini wenzetu walio wagonjwa?
19 Njia moja ya kuwasaidia kiroho walio wagonjwa ni kusali pamoja nao na kwa ajili yao. Ingawa leo hatuombi waponywe kimuujiza, tunaweza kumwomba Mungu awape nguvu za kuvumilia ugonjwa wao na nguvu za kiroho wanazohitaji ili wavumilie wanapokuwa dhaifu. Yehova atawategemeza, na imani yao itatiwa nguvu na taraja la wakati ujao ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Tunapata faraja iliyoje kujua kwamba kupitia Yesu Kristo aliyefufuliwa na kupitia Ufalme wa Mungu, wanadamu watiifu watawekwa huru kabisa na dhambi, magonjwa, na kifo! Kwa matarajio hayo mazuri, tunamshukuru Yehova ambaye ‘ataponya magonjwa yetu yote.’—Zaburi 103:1-3; Ufunuo 21:1-5.
20. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba imani inaweza kututegemeza wakati wa “siku mbaya” za uzee?
20 Imani pia inaweza kutusaidia kuvumilia ‘siku mbaya’ za uzee, wakati ambapo afya na nguvu zetu zinadhoofika. (Mhubiri 12:1-7) Kwa hiyo walio wazee miongoni mwetu wanaweza kusali kama alivyosali mtunga-zaburi mzee: “Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU . . . Usinitupe wakati wa uzee, nguvu zangu zipungukapo usiniache.” (Zaburi 71:5, 9) Mtunga-zaburi aliona uhitaji wa kutegemezwa na Yehova. Hata wengi wa Wakristo wenzetu wazee ambao wamemtumikia Mungu kwa miaka mingi wana uhitaji huohuo. Kwa sababu ya imani yao, wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ataendelea kuwategemeza milele.—Kumbukumbu la Torati 33:27.
Dumisha Imani Katika Neno la Mungu
21, 22. Imani yetu huathirije uhusiano wetu pamoja na Mungu?
21 Imani katika habari njema na katika Biblia nzima hutusaidia kuendelea kumkaribia Yehova. (Yakobo 4:8) Ni kweli kwamba yeye ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu wetu na pia Muumba na Baba yetu. (Isaya 64:8; Mathayo 6:9; Matendo 4:24) Mtunga-zaburi aliimba, “Wewe baba yangu, Mungu wangu na mwamba wa wokovu wangu.” (Zaburi 89:26) Iwapo tuna imani katika Yehova na Neno lake lililoandikwa kwa roho yake, sisi pia tunaweza kumwita ‘mwamba wa wokovu wetu.’ Hilo ni pendeleo lililoje!
22 Yehova ndiye Baba wa Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao walio na tumaini la kuishi duniani. (Waroma 8:15) Hatutakatishwa tamaa kamwe tukiwa na imani katika Baba yetu wa mbinguni. Daudi alisema: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.” (Zaburi 27:10) Zaidi ya hayo, tuna uhakikisho huu: “BWANA hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu.”—1 Samweli 12:22.
23. Ni nini kinachohitajiwa ili kufurahia uhusiano wenye kudumu pamoja na Yehova?
23 Bila shaka, ili kufurahia uhusiano wenye kudumu pamoja na Yehova, ni lazima tuwe na imani katika habari njema na kukubali Maandiko kama vile yalivyo kwa kweli—Neno la Mungu. (1 Wathesalonike 2:13) Tunapaswa kumwamini Yehova kabisa na kuongozwa na nuru ya Neno lake. (Zaburi 119:105; Mithali 3:5, 6) Imani yetu itakua tunaposali kwake tukiwa na uhakika kwamba atatuonyesha huruma, rehema, na kutusaidia.
24. Tunapata wazo gani lenye kufariji kwenye Waroma 14:8?
24 Imani ilituchochea tujiweke wakfu kwa Mungu milele. Tukiwa na imani yenye nguvu, sisi watumishi wake waliojiweka wakfu tuna tumaini la ufufuo hata kama tutakufa. Naam, “tukiishi na tukifa pia, sisi ni wa Yehova.” (Waroma 14:8) Na tuliweke moyoni wazo hilo lenye kufariji huku tukiendelea kuwa na uhakika katika Neno la Mungu na imani katika habari njema.
-
-
Imani Yako Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?Mnara wa Mlinzi—2003 | Januari 15
-
-
Imani Yako Ni Yenye Nguvu Kadiri Gani?
“Ni kwa imani yenu kwamba nyinyi mnasimama.”—2 WAKORINTHO 1:24.
1, 2. Kwa nini ni lazima tuwe na imani, nayo inawezaje kuwa na nguvu zaidi?
WATUMISHI wa Yehova wanajua kwamba ni lazima wawe na imani. Kwa kweli, ‘bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu vema.’ (Waebrania 11:6) Kwa hiyo, ni jambo la hekima kusali tupewe roho takatifu na imani, ambayo ni mojawapo ya matunda yenye kuvutia ya roho hiyo. (Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23) Kuiga imani ya waamini wenzetu kunaweza pia kuitia nguvu imani yetu.—2 Timotheo 1:5; Waebrania 13:7.
2 Imani yetu itakuwa na nguvu zaidi tukiendelea kufuata mwongozo ambao Neno la Mungu hutoa kwa Wakristo wote. Tunaweza kuongeza imani yetu kwa kusoma Biblia kila siku na kujifunza Maandiko kwa bidii tukitumia vichapo vinavyotolewa kupitia “msimamizi-nyumba mwaminifu.” (Luka 12:42-44; Yoshua 1:7, 8) Tunatiana moyo kwa imani yetu tunapohudhuria mikutano na makusanyiko yetu ya Kikristo. (Waroma 1:11, 12; Waebrania 10:24, 25) Na imani yetu itatiwa nguvu tunapohubiria wengine.—Zaburi 145:10-13; Waroma 10:11-15.
3. Kwa habari ya imani, tunapata msaada gani kutoka kwa wazee Wakristo wenye upendo?
3 Wazee Wakristo wenye upendo hutusaidia kuboresha imani yetu kwa kutoa ushauri wa Kimaandiko na kitia-moyo. Wana mtazamo kama ule wa mtume Paulo, aliyewaambia Wakorintho hivi: “Sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani yenu kwamba nyinyi mnasimama.” (2 Wakorintho 1:23, 24) Andiko hilo limetafsiriwa hivi katika Biblia Habari Njema: “Nyinyi mko imara katika imani yenu.” Waadilifu huishi kwa sababu ya imani. Bila shaka, hatuwezi kutarajia mtu mwingine adhihirishe imani kwa ajili yetu, au kutufanya tuwe na uaminifu-maadili. Kuhusiana na hilo, ‘ni lazima tuchukue mzigo wetu.’—Wagalatia 3:11; 6:5.
4. Masimulizi ya Kimaandiko kuhusu watumishi waaminifu wa Mungu yanawezaje kuitia nguvu imani yetu?
4 Maandiko yana masimulizi mengi kuhusu watu waliokuwa na imani. Huenda tunajua mengi ya matendo yao yenye kutokeza, lakini namna gani imani waliyoonyesha siku kwa siku, yamkini katika maisha yao yote? Kufikiria sasa jinsi walivyoonyesha sifa hiyo katika hali zinazofanana na zetu kunaweza kuitia imani yetu nguvu.
Imani Hutupatia Ujasiri
5. Kuna uthibitisho gani wa Kimaandiko kwamba imani hututia nguvu kutangaza neno la Mungu kwa ujasiri?
5 Imani hututia nguvu kutangaza neno la Mungu kwa ujasiri. Enoki alitangaza kwa ujasiri kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu. Alisema: “Tazama! Yehova alikuja na makumi ya maelfu yake watakatifu, kutekeleza hukumu dhidi ya wote, na kuwathibitisha ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu vitendo vyao vyote vya kutomwogopa Mungu ambavyo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema dhidi yake.” (Yuda 14, 15) Bila shaka, maadui wa Enoki wasiomwogopa Mungu walitaka kumwua waliposikia maneno hayo. Hata hivyo, alisema kwa imani na ujasiri, naye Mungu “akamchukua” kwa kukomesha uhai wake alipokuwa amelala, yaonekana bila kumruhusu apatwe na maumivu ya kifo. (Mwanzo 5:24; Waebrania 11:5) Miujiza kama hiyo haitokei leo, lakini Yehova anaweza kujibu sala zetu ili tuweze kutangaza neno lake kwa imani na ujasiri.—Matendo 4:24-31.
6. Imani na ujasiri kutoka kwa Mungu zilimsaidiaje Noa?
6 Kwa imani Noa ‘alijenga safina kwa ajili ya kuokoa watu wa nyumbani kwake.’ (Waebrania 11:7; Mwanzo 6:13-22) Noa pia alikuwa “mhubiri wa uadilifu” naye aliwatangazia kwa ujasiri onyo la Mungu watu walioishi siku zake. (2 Petro 2:5) Bila shaka watu hao walidhihaki ujumbe wake kuhusu Gharika iliyokuwa inakaribia, kama vile tu watu wengine hutudhihaki tunapowatolea uthibitisho wa Kimaandiko kwamba mfumo huu wa mambo utaharibiwa hivi karibuni. (2 Petro 3:3-12) Hata hivyo, kama Enoki na Noa, tunaweza kutangaza ujumbe huo kwa sababu tuna imani na ujasiri kutoka kwa Mungu.
Imani Hutusaidia Tuwe na Subira
7. Abrahamu na wengine walionyeshaje imani na subira?
7 Tunahitaji imani na subira, hasa tunapongojea mwisho wa mfumo huu mwovu. Abrahamu, mzee wa ukoo mwenye kumwogopa Mungu, ni kati ya watu ambao ‘kupitia imani na subira watazirithi ahadi.’ (Waebrania 6:11, 12) Kwa imani aliacha jiji la Uru, na ufanisi wake, akakaa kama mgeni katika nchi ya kigeni aliyoahidiwa na Mungu. Isaka na Yakobo pia walikuwa warithi wa ahadi hiyohiyo. Hata hivyo, “katika imani wote hao walikufa, ijapokuwa hawakupata utimizo wa ahadi.” Kwa imani ‘walijitahidi kufikia mahali palipo bora, yaani, pamoja ambapo ni pa mbinguni.’ Kwa sababu hiyo, Mungu ‘amefanya jiji liwe tayari kwa ajili yao.’ (Waebrania 11:8-16) Naam, Abrahamu, Isaka, na Yakobo—na wake zao ambao walimwogopa Mungu—walingojea kwa subira Ufalme wa mbinguni wa Mungu, ambao utakuwa ukitawala duniani watakapofufuliwa.
8. Abrahamu, Isaka, na Yakobo waliendelea kuwa na subira na imani licha ya nini?
8 Abrahamu, Isaka, na Yakobo walidumisha imani yao. Hawakuimiliki Nchi ya Ahadi, wala hawakuyaona mataifa yote yakijibariki kupitia mbegu ya Abrahamu. (Mwanzo 15:5-7; 22:15-18) Ingawa ‘Mungu angejenga jiji hilo’ karne nyingi baadaye, wanaume hao waliendelea kuwa na imani na subira katika maisha yao yote. Sisi pia tunapaswa kufanya vivyo hivyo hasa wakati huu ambapo Ufalme wa Kimesiya unatawala mbinguni.—Zaburi 42:5, 11; 43:5.
Imani Hutusaidia Kuwa na Miradi Bora
9. Imani huathirije miradi?
9 Kwa kuwa wazee wa ukoo waaminifu walikuwa na miradi bora, wao hawakufuata mtindo wa maisha mapotovu ya Wakaanani. Vivyo hivyo imani hutusaidia kuwa na miradi ya kiroho ambayo hutusaidia tusimezwe na ulimwengu huu ulio katika nguvu ya yule mwovu, Shetani Ibilisi.—1 Yohana 2:15-17; 5:19.
10. Tunajuaje kwamba Yosefu alifuatia mradi bora kuliko umashuhuri wa ulimwengu?
10 Kwa mwongozo wa Mungu, Yosefu mwana wa Yakobo alitumikia huko Misri akiwa msimamizi wa chakula, lakini hakuwa na mradi wa kuwa mtu mashuhuri katika ulimwengu huu. Kwa kuwa alikuwa na imani katika ahadi za Yehova, Yosefu aliwaambia hivi ndugu zake alipokuwa na umri wa miaka 110: “Mimi ninakufa, lakini Mungu atawajia ninyi bila shaka, atawapandisha toka nchi hii, mpaka nchi aliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo.” Yosefu aliomba azikwe katika nchi ya ahadi. Alipokufa, alipakwa dawa ili asioze kisha akatiwa katika jeneza huko Misri. Lakini Waisraeli walipokombolewa kutoka utumwani Misri, nabii Musa aliagiza mifupa ya Yosefu ibebwe ili ikazikwe katika Nchi ya Ahadi. (Mwanzo 50:22-26; Kutoka 13:19) Imani kama ya Yosefu inapasa kutuchochea tufuate miradi iliyo bora kuliko umashuhuri wa ulimwengu huu.—1 Wakorintho 7:29-31.
11. Musa alithibitishaje kwamba alikuwa na miradi ya kiroho?
11 Musa ‘alichagua kutendwa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kuwa na mfurahio wa muda wa dhambi’ akiwa mshiriki mwenye elimu wa familia ya kifalme ya Misri. (Waebrania 11:23-26; Matendo 7:20-22) Kwa sababu hiyo alikosa umashuhuri wa ulimwengu na labda mazishi ya kifahari akiwa amewekwa ndani ya jeneza lililopambwa kwenye eneo fulani maarufu huko Misri. Lakini mambo hayo yangekuwa na manufaa gani yakilinganishwa na pendeleo la kuwa “mtu wa Mungu,” mpatanishi wa agano la Sheria, nabii wa Yehova, na mwandikaji wa Biblia? (Ezra 3:2) Je, unatamani kuwa na cheo mashuhuri katika ulimwengu, au imani imekusaidia kuwa na miradi bora ya kiroho?
Imani Hufanya Maisha Yawe Yenye Kuridhisha
12. Imani iliathirije maisha ya Rahabu?
12 Imani huwasaidia watu kuwa na miradi bora na pia hufanya maisha yawe yenye kuridhisha. Bila shaka, Rahabu hakuona maisha yake ya ukahaba kuwa yenye kusudi. Hata hivyo, maisha yake yalikuwa na kusudi alipoanza kuonyesha imani! ‘Alitangazwa kuwa mwadilifu kwa kazi za imani, baada ya kuwapokea wale wajumbe Waisraeli kwa ukaribishaji-wageni na kuwatoa nje kwa njia nyingine,’ na hivyo wakawaponyoka maadui wao Wakanaani. (Yakobo 2:24-26) Alipotambua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli, Rahabu alionyesha imani pia kwa kuacha maisha ya ukahaba. (Yoshua 2:9-11; Waebrania 11:30, 31) Aliolewa na mtumishi wa Yehova, wala si na Mkanaani asiyeamini. (Kumbukumbu la Torati 7:3, 4; 1 Wakorintho 7:39) Rahabu alikuwa na pendeleo la pekee la kuwa nyanya wa Mesiya. (1 Mambo ya Nyakati 2:3-15; Ruthu 4:20-22; Mathayo 1:5, 6) Kama wengine ambao waliacha maisha yasiyo ya adili, Rahabu atapokea zawadi nyingine—atafufuliwa aishi katika dunia paradiso.
13. Daudi alifanya dhambi gani kuhusiana na Bath-sheba, lakini alionyesha mtazamo gani?
13 Baada ya kuacha maisha ya ukahaba, yaelekea Rahabu aliishi maisha ya uadilifu. Hata hivyo, wengine ambao wamejitoa kwa Mungu kwa muda mrefu walifanya dhambi nzito. Mfalme Daudi alifanya uzinzi na Beth-sheba, akaagiza mume wake auawe vitani, kisha akamchukua awe mke wake. (2 Samweli 11:1-27) Daudi alijuta sana na kutubu, kisha akamwomba Yehova hivi: ‘Roho yako takatifu usiniondolee.’ Daudi hakupoteza roho ya Mungu. Alikuwa na imani kwamba Yehova ni mwenye rehema na hadharau “moyo uliovunjika” kwa sababu ya dhambi. (Zaburi 51:11, 17; 103:10-14) Kwa sababu ya imani yao, Daudi na Bath-sheba walipata pendeleo la kuwa miongoni mwa watu wa ukoo wa Mesiya.—1 Mambo ya Nyakati 3:5; Mathayo 1:6, 16; Luka 3:23, 31.
Uhakikisho Hutia Imani Nguvu
14. Gideoni alipata uhakikisho gani, na masimulizi hayo yanaweza kuwa na matokeo gani kwa imani yetu?
14 Ingawa tunatembea kwa imani, wakati mwingine tunahitaji uhakikisho wa kwamba Mungu anatusaidia. Mwamuzi Gideoni ambaye ni mmoja wa wale “ambao kupitia imani walishinda falme katika pambano,” alihitaji uhakikisho huo. (Waebrania 11:32, 33) Wamidiani na washirika wao walipovamia Israeli, roho ya Mungu ilikuja juu ya Gideoni. Akitaka uhakikisho kwamba Yehova alikuwa pamoja naye, Gideoni alipendekeza majaribio fulani kwa kutumia manyoya ya kondoo ambayo yangewekwa kwenye uwanja wa kupuria usiku kucha. Katika jaribio la kwanza, umande ulikuwa juu ya manyoya peke yake, huku nchi ikibaki kavu. Katika jaribio la pili, umande ulikuwa juu ya nchi huku manyoya yakibaki makavu. Gideoni alitiwa nguvu na uhakikisho huo, na kwa tahadhari na imani akawashinda maadui wa Israeli. (Waamuzi 6:33-40; 7:19-25) Kutafuta uhakikisho kabla ya kufanya uamuzi fulani hakumaanishi kwamba hatuna imani. Kwa kweli sisi huonyesha imani kwa kuichunguza Biblia na vichapo vya Kikristo na kwa kuomba mwongozo wa roho takatifu tunapofanya maamuzi.—Waroma 8:26, 27.
15. Tunaweza kupata msaada gani kwa kufikiria imani ya Baraki?
15 Imani ya Mwamuzi Baraki ilitiwa nguvu na uhakikisho kupitia kitia-moyo alichopokea. Nabii wa kike, Debora alimtia moyo achukue hatua ya kuwakomboa Waisraeli waliokuwa wanakandamizwa na Mfalme Yabini wa Kanaani. Akiwa na imani na uhakikisho wa kwamba Mungu atamsaidia, Baraki aliwaongoza vitani wanaume 10,000 wasiokuwa na silaha za kutosha, nao wakawashinda wanajeshi wa Sisera waliokuwa wengi sana. Ushindi huo ulisherehekewa katika wimbo wenye kusisimua wa Debora na Baraki. (Waamuzi 4:1–5:31) Debora alimtia moyo Baraki atende kama kiongozi wa Israeli aliyechaguliwa na Mungu, naye alikuwa mmoja wa watumishi wa Yehova ambao kupitia imani ‘walitimusha majeshi ya watoka-ugenini.’ (Waebrania 11:34) Tunapofikiria jinsi Mungu alivyombariki Baraki kwa kutenda kwa imani, tunaweza kuchochewa kutenda ikiwa tunasitasita kutimiza mgawo fulani mgumu katika utumishi wa Yehova.
Imani Huchangia Amani
16. Abrahamu aliweka kielelezo gani kwa kufuatia amani pamoja na Loti?
16 Mbali na kutusaidia kutimiza migawo migumu katika utumishi wetu kwa Mungu, imani huchangia amani na utulivu. Wakati wachungaji wa Abrahamu na Loti walipogombana na ikawa lazima watengane, Abrahamu aliyekuwa mzee alimruhusu Loti achague malisho yaliyokuwa bora. (Mwanzo 13:7-12) Bila shaka Abrahamu alisali kwa imani ili Mungu amsaidie kutatua tatizo hilo. Badala ya kutanguliza mapendezi yake, alisuluhisha mambo kwa amani. Iwapo tumegombana na ndugu yetu Mkristo, na tusali kwa imani na “kutafuta amani,” huku tukikumbuka jinsi Abrahamu alivyowajali wengine.—1 Petro 3:10-12.
17. Kwa nini tunaweza kusema kwamba ugomvi ambao yaonekana ulitokea kati ya Paulo, Barnaba, na Marko ulisuluhishwa kwa njia ya amani?
17 Hebu fikiria jinsi kufuata kanuni za Kikristo kwa imani kunavyoweza kutusaidia kuchangia amani. Paulo alipokuwa karibu kuanza safari yake ya pili ya umishonari, Barnaba alikubali pendekezo la Paulo kwamba watembelee tena makutaniko huko Saiprasi na Asia Ndogo. Hata hivyo, Barnaba alitaka binamu yake Marko aandamane nao, lakini Paulo akakataa kwa sababu Marko alikuwa amewaacha wakiwa huko Pamfilia. ‘Kulitokea mfoko mkali wa hasira’ uliofanya watengane. Barnaba akamchukua Marko na kwenda Saiprasi, naye Paulo akachagua Sila kuwa mwandamani wake, nao ‘wakapitia Siria na Kilikia, wakiyatia nguvu makutaniko.’ (Matendo 15:36-41) Baada ya muda, ugomvi ambao yaonekana ulitokea kati yao ulisuluhishwa, kwa kuwa mtume Paulo alimsifu Marko walipokuwa pamoja huko Roma. (Wakolosai 4:10; Filemoni 23, 24) Paulo alipokuwa mfungwa huko Roma yapata mwaka wa 65 W.K., alimwambia Timotheo hivi: ‘Mchukue Marko na kumleta pamoja nawe, kwa maana yeye ni mwenye mafaa kwangu kwa ajili ya huduma.’ (2 Timotheo 4:11) Yaonekana Paulo alisali kwa imani kuhusu uhusiano wake pamoja na Barnaba na Marko, jambo lililoleta utulivu unaohusianishwa na “amani ya Mungu.”—Wafilipi 4:6, 7.
18. Yaelekea ni nini kilitokea kati ya Euodia na Sintike?
18 Bila shaka, “sisi sote hujikwaa mara nyingi” kwa kuwa sisi si wakamilifu. (Yakobo 3:2) Kulikuwa na kutokuelewana kati ya wanawake wawili Wakristo, ambao Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Euodia namhimiza kwa bidii na Sintike namhimiza kwa bidii wawe wenye akili ileile katika Bwana. . . . Fuliza kuwasaidia wanawake hawa ambao wamepigana sambamba pamoja nami katika habari njema.” (Wafilipi 4:1-3) Inaelekea kwamba wanawake hao waliomwogopa Mungu walisuluhisha kutopatana kwao kwa njia ya amani wakitumia ushauri unaopatikana katika Mathayo 5:23, 24. Kutumia kanuni za Kimaandiko kwa imani kutachangia sana amani leo.
Imani Hutuwezesha Kuvumilia
19. Ni hali gani ngumu ambayo haikuweza kuvunja imani ya Isaka na Rebeka?
19 Kwa imani tunaweza pia kuvumilia magumu. Labda tunahuzunika kwa sababu mshiriki wa familia yetu aliyebatizwa amekataa kumtii Mungu kwa kufunga ndoa na mtu asiyeamini. (1 Wakorintho 7:39) Isaka na Rebeka waliumia sana kwa sababu mwana wao Esau alioa wanawake wasiomwogopa Mungu. Wake zake Wahiti “waliyafanya maisha ya Isaka na Rebeka kuwa machungu” sana hivi kwamba Rebeka alisema: “Sina raha kabisa maishani kwa sababu ya hawa wanawake wa Esau Wahiti. Ikiwa Yakobo ataoa mmojawapo wa wanawake hawa Wahiti, maisha yangu yana faida gani?” (Mwanzo 26:34, 35; 27:46, BHN) Hata hivyo, imani ya Isaka na Rebeka haikuvunjwa na hali hiyo ngumu. Na tudumishe imani yenye nguvu inapokuwa vigumu kushughulika na hali fulani.
20. Naomi na Ruthu wanatuwekea vielelezo gani vya imani?
20 Naomi, mjane mzee kutoka Yudea, alijua kwamba wanawake fulani wa Yuda wangeweza kuzaa wana ambao wangekuwa babu za Mesiya. Uwezekano wa familia yake kutokeza mtu ambaye angekuwa babu ya Yesu ulikuwa mdogo sana kwa kuwa wana wake walikufa kabla ya kupata watoto naye alikuwa amepita umri wa kuzaa. Hata hivyo, Ruthu, mkwe wake aliyekuwa mjane aliolewa na Boazi, akamzalia mwana, naye akawa nyanya ya Mesiya! (Mwanzo 49:10, 33; Ruthu 1:3-5; 4:13-22; Mathayo 1:1, 5) Imani ya Naomi na Ruthu iliwasaidia kuvumilia magumu na iliwaletea furaha. Tutapata furaha nyingi pia ikiwa tutadumisha imani tunapopatwa na magumu.
21. Imani hutusaidiaje, na tunapaswa kuazimia kufanya nini?
21 Tunaweza kukabiliana na magumu yoyote kwa imani ingawa hatujui maisha yetu yatakavyokuwa kesho. Imani hutupatia ujasiri na subira. Hutusaidia kuwa na miradi bora na maisha yenye kuridhisha. Imani huboresha uhusiano wetu pamoja na wengine na hutusaidia kuvumilia magumu. Kwa hiyo na tuwe “namna iliyo na imani kuelekea kuhifadhi hai nafsi.” (Waebrania 10:39) Kwa nguvu za Yehova, Mungu wetu mwenye upendo, na kwa utukufu wake, na tuendelee kuonyesha imani yenye nguvu.
-