Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Imani Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Mei 1
    • Imani Imara Ni Muhimu

      Biblia inatutia moyo tuwe na imani imara inayojengwa juu ya uthibitisho thabiti, hata ikiwa itabidi tubadili maoni yetu. Imani kama hiyo ni muhimu sana. Mtume Paulo aliandika: “Pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”—Waebrania 11:6, Union Version.

      Kuna mambo mengi yanayoweza kukuzuia usisitawishe imani imara. Lakini ukifanya mambo manne yanayozungumziwa katika kurasa zinazofuata, unaweza kufaulu.

  • 1 Jifunze Kuitegemea Biblia
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Mei 1
    • 1 Jifunze Kuitegemea Biblia

      “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.”—2 Timotheo 3:16.

      KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Watu wengi wanasema kwamba Biblia ni kitabu chenye hekima ya wanadamu tu. Baadhi yao wanaamini kwamba masimulizi ya Biblia kuhusu matukio katika historia si sahihi. Wengine wanadai kwamba mashauri ya Biblia hayafai na yamepitwa na wakati.

      UNAWEZA KUFAULU JINSI GANI? Mara nyingi watu wasioitegemea Biblia au wale wanaofikiri kwamba haifai, hawajaichunguza. Wanasema tu mambo ambayo wamesikia wengine wakisema. Hata hivyo, Biblia inaonya: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

      Badala ya kukubali bila uthibitisho mambo ambayo wengine wanasema, unaweza kufuata mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza walioishi Beroya. Jiji hilo lilikuwa katika eneo lililo kaskazini mwa Ugiriki ya sasa. Hawakukubali tu mambo waliyoambiwa na wengine. Badala yake, walikuwa na zoea la “[ku]yachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:11) Hebu tuchunguze kwa ufupi sababu mbili zinazoweza kufanya uwe na hakika kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho.

      Biblia ni sahihi kihistoria. Kwa miaka mingi, watu wametilia shaka usahihi wa majina ya watu na maeneo mbalimbali ambayo Biblia inataja. Lakini, mara nyingi uthibitisho umeonyesha kuwa madai yao hayana msingi na kwamba masimulizi ya Biblia yanategemeka.

      Kwa mfano, wakati fulani wasomi walisema kwamba Sargoni, Mfalme wa Ashuru anayetajwa katika Isaya 20:1, hakuwahi kuishi. Hata hivyo, katika miaka ya 1840, wataalamu wa vitu vya kale walianza kuchimbua jumba la mfalme huyo. Sasa, Sargoni ni mmojawapo wa wafalme Waashuru wanaojulikana sana.

      Wachambuzi hawakuamini kwamba Pontio Pilato, gavana Mroma aliyeagiza Yesu auawe, aliwahi kuishi. (Mathayo 27:1, 22-24) Lakini mwaka wa 1961 jiwe lenye jina na cheo cha Pilato lilipatikana karibu na jiji la Kaisaria nchini Israel.

      Gazeti U.S.News & World Report la Oktoba 25, 1999 (25/10/1999), linasema hivi kuhusu usahihi wa Biblia kihistoria: “Wataalamu wa vitu vya kale wa siku hizi wamethibitisha kwamba matukio muhimu katika Agano la Kale na Agano Jipya ni sahihi. Matukio hayo yanahusu mababu wa Israeli, kutoka kwa Waisraeli nchini Misri, utawala wa ukoo wa Daudi, na maisha katika siku za Yesu.” Ingawa imani katika Biblia haitegemei uvumbuzi wa vitu vya kale, ungetarajia kitabu kilichoongozwa na roho ya Mungu kiwe sahihi kihistoria.

      Hekima iliyo katika Biblia inawanufaisha watu wa aina zote. Muda mrefu kabla ya kugunduliwa kwa vijidudu na jinsi vinavyoeneza magonjwa, Biblia ilikuwa imependekeza hatua fulani za kudumisha usafi ambazo bado zinafaa leo. (Mambo ya Walawi 11:32-40; Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Watu wa familia wanaofuata mashauri ya Biblia kuhusu jinsi wanavyopaswa kutendeana wanakuwa na furaha zaidi. (Waefeso 5:28–6:4) Pia, mtu anayefuata kanuni za Biblia anaweza kuwa mfanyakazi mwenye kutegemeka au mwajiri mwenye usawaziko. (Waefeso 4:28; 6:5-9) Kufuata kanuni za Biblia kunatunufaisha kihisia na kiafya vilevile. (Methali 14:30; Waefeso 4:31, 32; Wakolosai 3:8-10) Tungetarajia mashauri mazuri kama hayo kutoka kwa Muumba wetu.

      UTAPATA THAWABU GANI? Hekima iliyo katika Biblia inaweza kumfanya hata mtu asiye na uzoefu awe na hekima. (Zaburi 19:7) Isitoshe, tukiitegemea Biblia, inaweza kutusaidia kuchukua hatua ya pili inayozungumziwa hapa chini ili kusitawisha imani imara. Hakuna kitabu kingine chochote kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo.

      Ili kupata habari zaidi, ona sura ya 2, “Biblia—Kitabu Kutoka kwa Mungu,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?a

      [Maelezo ya chini]

      a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • 2 Pata Ujuzi Sahihi Kumhusu Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Mei 1
    • 2 Pata Ujuzi Sahihi Kumhusu Mungu

      “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli.”—Yohana 17:3.

      KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Watu fulani wanasema kwamba hakuna Mungu. Wengine wanaamini Mungu ni nguvu tu. Wale wanaoamini kwamba kuna Mungu wanafundisha mambo yanayopingana kumhusu na kuhusu sifa zake.

      UNAWEZA KUFAULU JINSI GANI? Njia moja ya kumjua Mungu ni kutazama vitu alivyoviumba. Mtume Paulo alisema: “Sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Waroma 1:20) Unapotazama uumbaji kwa makini unaweza kujifunza mambo mengi kuhusu hekima na uwezo wa Muumba wetu.—Zaburi 104:24; Isaya 40:26.

      Hata hivyo, ili kupata ujuzi sahihi kumhusu Mungu, kila mtu anahitaji kulichunguza kibinafsi Neno la Mungu, Biblia. Usiwaruhusu wengine wakuamulie mambo unayopaswa kuamini. Badala yake, fuata shauri hili la Biblia: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Kwa mfano, fikiria mambo yafuatayo ambayo Biblia inafunua kumhusu Mungu.

      Mungu ana jina. Jina la kibinafsi la Mungu lilipatikana mara 7,000 hivi katika Biblia za awali. Katika tafsiri nyingi za Biblia, jina hilo linapatikana katika andiko la Zaburi 83:18 linalosema: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”—UV.

      Yehova Mungu ana hisia, na matendo ya wanadamu yanaweza kumhuzunisha au kumfurahisha. Baada ya Yehova kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri, nyakati nyingine walipuuza mashauri yake ya hekima. Mwenendo wao wa uasi ‘ulimhuzunisha.’ Matendo yao yalimtia “uchungu Mtakatifu wa Israeli.”—Zaburi 78:40, 41.

      Yehova anamjali kila mtu binafsi. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.”—Mathayo 10:29-31.

      Mungu hapendelei watu wa jamii au utamaduni fulani. Mtume Paulo aliwaambia Wagiriki huko Athene kwamba Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima.” Pia alisema kwamba Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:26, 27) Mtume Petro alisema: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

      UTAPATA THAWABU GANI? Watu fulani wana “bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Ikiwa unajua Biblia inafundisha nini hasa kumhusu Mungu, utaepuka kupotoshwa na utaweza ‘kumkaribia Mungu.’—Yakobo 4:8.

      Ili kupata habari zaidi, ona sura ya 1, “Ukweli Kumhusu Mungu,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?a

      [Maelezo ya chini]

      a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Njia moja ya kumjua Mungu ni kutazama vitu alivyoviumba

  • 3 Jifunze Ukweli Kumhusu Yesu
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Mei 1
    • 3 Jifunze Ukweli Kumhusu Yesu

      “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

      KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Watu fulani wanasema kwamba Yesu hakuwa mtu halisi. Wengine wanakubali kwamba Yesu alipata kuishi lakini wanasema alikuwa mtu wa kawaida tu ambaye alikufa zamani.

      UNAWEZA KUFAULU JINSI GANI? Unaweza kufaulu kwa kumwiga mwanafunzi Nathanaeli.a Rafiki yake Filipo alimwambia kwamba alifikiri alikuwa amempata Masihi—“Yesu, mwana wa Yosefu, kutoka Nazareti.” Lakini Nathanaeli hakuyaamini tu maneno ya Filipo, badala yake, alimuuliza: “Je, kitu chochote kilicho chema kinaweza kutoka Nazareti?” Lakini Filipo alipomwambia, ‘Njoo ujionee’ mwenyewe, Nathanaeli alikubali. (Yohana 1:43-51) Wewe pia utanufaika kwa kujichunguzia mwenyewe uthibitisho uliopo kumhusu Yesu. Unaweza kufanya nini?

      Chunguza habari za kihistoria zinazothibitisha kwamba Yesu alikuwa mtu halisi. Yosefo na Tasito ni wanahistoria wa karne ya kwanza wenye kuheshimiwa ambao hawakuwa Wakristo. Wanamtaja Yesu Kristo kuwa mtu halisi aliyepata kuishi. Tasito aliandika hivi alipoeleza jinsi Maliki Mroma Nero alivyowalaumu Wakristo kwamba walianzisha moto jijini Roma mwaka wa 64 W.K.: “Nero aliwalaumu watu walioitwa Wakristo ambao walichukiwa na Waroma kwa sababu ya mazoea yao, naye aliwatesa kikatili sana. Jina Wakristo linatokana na jina la Kristo, ambaye gavana wetu Pontio Pilato alimhukumia kifo, wakati wa utawala wa Tiberio.”

      Kitabu Encyclopædia Britannica, Chapa ya 2002, kinasema hivi kuhusiana na mambo ambayo wanahistoria wa karne ya kwanza na ya pili walisema kumhusu Yesu na Wakristo wa mapema: “Masimulizi hayo mbalimbali yanathibitisha kwamba zamani za kale hata wapinzani wa Ukristo hawakutilia shaka kwamba Yesu alikuwa mtu halisi. Jambo hilo lilibishaniwa kwa mara ya kwanza na bila sababu nzuri mwishoni mwa karne ya 18, katika karne ya 19, na mwanzoni mwa karne ya 20.” Mnamo 2002, gazeti The Wall Street Journal lilisema: “Wasomi wengi, isipokuwa wale wachache ambao wanaamini kwamba hakuna Mungu, wamekubali Yesu wa Nazareti kuwa mtu halisi.”

      Fikiria uthibitisho wa kwamba Yesu alifufuliwa. Yesu alipokamatwa na wapinzani wake, marafiki wake wa karibu walimwacha na kutawanyika, na rafiki yake Petro alikana kumjua kwa sababu ya woga. (Mathayo 26:31, 55, 56, 69-75) Kisha kwa ghafula, wanafunzi wake wakaanza kutenda kwa bidii. Petro na Yohana waliwakabili kwa ujasiri watu walewale waliopanga njama ya kumuua Yesu. Wanafunzi wa Yesu walichochewa kiasi cha kwamba walieneza mafundisho yake kotekote katika Milki ya Roma, wakiona ni afadhali kufa kuliko kutenda kinyume cha mambo waliyoamini.

      Ni nini kilichowachochea wanafunzi hao wabadili mtazamo wao jinsi hiyo? Mtume Paulo anaeleza kwamba Yesu alifufuliwa na “alimtokea Kefa [Petro], kisha wale kumi na wawili.” Paulo anaendelea kusema: “Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mmoja.” Watu wengi waliojionea kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa walikuwa bado hai wakati Paulo alipoandika maneno hayo. (1 Wakorintho 15:3-7) Ingekuwa rahisi kwa watu wenye shaka kupuuza ushuhuda wa mtu mmoja au wawili. (Luka 24:1-11) Lakini ushuhuda wa watu zaidi ya 500 ulithibitisha kwamba Yesu alifufuliwa.

      UTAPATA THAWABU GANI? Wale wanaomwamini Yesu na kumtii wanaweza kusamehewa dhambi zao na wanaweza kuwa na dhamiri safi. (Marko 2:5-12; 1 Timotheo 1:19; 1 Petro 3:16-22) Wakifa, Yesu anaahidi atawafufua “katika siku ya mwisho.”—Yohana 6:40.

      Ili kupata habari zaidi, ona sura ya 4, “Yesu Kristo Ni Nani?,” na sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?b

      [Maelezo ya chini]

      a Katika vitabu vya Injili vya Mathayo, Marko, na Luka yaonekana Nathanaeli anaitwa Bartholomayo.

      b Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Kama Nathanaeli, chunguza mambo yanayothibitisha kwamba Yesu alikuwa mtu halisi

  • 4 Ondoa Shaka
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Mei 1
    • 4 Ondoa Shaka

      “Wewe mwenye imani kidogo, kwa nini umekuwa na shaka?”—Mathayo 14:31.

      KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Nyakati nyingine hata wanafunzi wa Yesu walikuwa na shaka. (Mathayo 14:30; Luka 24:36-39; Yohana 20:24, 25) Biblia inaeleza ukosefu wa imani kuwa “dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi.” (Waebrania 12:1) Mtume Paulo aliandika: “Imani si mali ya watu wote.” (2 Wathesalonike 3:2) Hiyo haimaanishi kwamba watu fulani hawawezi kuwa na imani, bali inamaanisha kuwa wengi hawajitahidi kuisitawisha. Mungu atawabariki wale wanaojitahidi kusitawisha imani.

      UNAWEZA KUFAULU JINSI GANI? Tambua mambo yanayokufanya uwe na shaka. Kwa mfano, mwanafunzi Tomasi alikuwa na shaka kwamba Yesu alifufuliwa hata ingawa wanafunzi wengine walisema walikuwa wamemwona. Tomasi alitaka uthibitisho. Matokeo yakawa nini? Yesu alimpa uthibitisho aliohitaji ili awe na imani yenye nguvu.—Yohana 20:24-29.

      Kupitia Biblia, Yehova Mungu anatupa majibu tunayohitaji ili kuondoa shaka. Kwa mfano, wengi wanaacha kumwamini Mungu kwa sababu kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja wanamlaumu kwa vita, jeuri, na mateso yanayowapata wanadamu. Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo?

      Mungu hatawali kupitia serikali za wanadamu. Yesu alisema kwamba Shetani ambaye ni kiumbe wa roho asiyeonekana, ndiye “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Shetani alimwambia Yesu atampa mamlaka juu ya falme zote za dunia ikiwa atamfanyia tendo moja tu la ibada. Alisema: “Hakika nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wake, kwa sababu nimepewa, na yeyote ninayetaka mimi humpa.” Yesu hakukana kwamba Shetani ana mamlaka kama hiyo. Badala yake alisema: “Imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” (Luka 4:5-8) Shetani na serikali za wanadamu ndizo zinazopaswa kulaumiwa kwa mateso yanayowapata watu ulimwenguni, bali si Mungu.—Ufunuo 12:9, 12.

      Hivi karibuni Yehova Mungu ataondoa mambo yote yanayosababisha kuteseka. Tayari amepanga kuwe na Ufalme, au serikali, chini ya Mwana wake Kristo Yesu, ambao utawatawala wanadamu. (Mathayo 6:9, 10; 1 Wakorintho 15:20-28) Kazi ya kuhubiri habari njema kuhusu Ufalme huo inaendelea duniani kote na hivyo kutimiza unabii wa Biblia. (Mathayo 24:14) Punde si punde, Ufalme huo utaondoa watu wote wanaoupinga na mambo yote yanayosababisha kuteseka.—Danieli 2:44; Mathayo 25:31-33, 46; Ufunuo 21:3, 4.

      UTAPATA THAWABU GANI? Wale wanaoendelea kuwa na shaka wanakuwa kama mawimbi yanayorushwa huku na huku na “kila upepo wa fundisho kupitia udanganyifu wa watu.” (Waefeso 4:14; 2 Petro 2:1) Lakini wale wanaojibiwa maswali yao kwa njia yenye kuridhisha wanaweza ‘kusimama imara katika imani.’—1 Wakorintho 16:13.

      Mashahidi wa Yehova ambao ni wachapishaji wa gazeti hili, wangependa kukusaidia kupata majibu kwa maswali ambayo huenda yanakufanya uwe na shaka. Wanakualika ushirikiane nao na ujichunguzie mwenyewe mafundisho yao. Kufanya hivyo kutaimarisha imani yako sana katika Mungu.

      Ili kupata habari zaidi, ona sura ya 8, “Ufalme wa Mungu Ni Nini?,” na sura ya 11, “Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?a

      [Maelezo ya chini]

      a Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Imani ya wale wanaojibiwa maswali yao kwa njia yenye kuridhisha inakuwa na msingi imara

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki