-
“Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye BusaraMnara wa Mlinzi—2004 | Machi 1
-
-
“Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye Busara
“Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani?”—MATHAYO 24:45.
1, 2. Kwa nini ni muhimu tupate chakula cha kiroho kwa ukawaida leo?
JUMANNE alasiri, Nisani 11, 33 W.K., wanafunzi wa Yesu waliuliza swali lenye maana kubwa sana kwetu leo. Walimwuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Yesu aliwajibu kwa kutoa unabii muhimu sana. Alitaja kipindi chenye msukosuko cha vita, njaa, matetemeko ya nchi, na magonjwa. Kipindi hicho kingekuwa tu “mwanzo wa maumivu ya taabu.” Hali zingezidi kuwa mbaya. Hayo ni matazamio yenye kuogopesha kama nini!—Mathayo 24:3, 7, 8, 15-22; Luka 21:10, 11.
2 Tangu mwaka wa 1914 sehemu kubwa ya unabii huo wa Yesu imetimizwa. Wanadamu wamepatwa na “maumivu ya taabu” kwa kiwango kikubwa. Hata hivyo, Wakristo wa kweli hawahitaji kuogopa. Yesu aliahidi kwamba angewategemeza kwa chakula cha kiroho chenye kujenga. Kwa kuwa sasa Yesu yuko mbinguni, amefanya mipango gani ili tupate chakula cha kiroho hapa duniani?
3. Yesu amefanya mipango gani ili tupate ‘chakula kwa wakati unaofaa’?
3 Yesu mwenyewe alionyesha jibu la swali hilo. Alipokuwa akitoa unabii wake mkuu, aliuliza: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa?” Kisha akasema: “Mtumwa huyo atakuwa mwenye furaha ikiwa bwana wake atakapofika atamkuta akifanya hivyo! Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamweka juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:45-47) Naam, kungekuwa na “mtumwa” ambaye angepewa mgawo wa kuandaa chakula cha kiroho, “mtumwa” ambaye angekuwa mwaminifu na mwenye busara. Je, mtumwa huyo alikuwa mtu mmoja tu, watu mmoja-mmoja wenye kufuatana, au kitu kingine tofauti? Kwa kuwa mtumwa mwaminifu huandaa chakula cha kiroho kinachohitajiwa sana, ingefaa tujue jibu la swali hilo.
Je, “Mtumwa” Huyo Ni Mtu Mmoja au Ni Kikundi cha Watu?
4. Tunajuaje kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hawezi kuwa mtu mmoja?
4 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hawezi kuwa mtu mmoja. Kwa nini? Kwa sababu mtumwa huyo alianza kuandaa chakula cha kiroho katika karne ya kwanza, na kulingana na Yesu, angekuwa akifanya hivyo wakati Bwana wake angewasili 1914. Hiyo ingemaanisha kwamba mtu mmoja angetumikia kwa uaminifu kwa miaka 1,900 hivi. Hata Methusela hakuishi muda mrefu hivyo!—Mwanzo 5:27.
5. Eleza kwa nini maneno “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hayarejelei Mkristo mmoja-mmoja.
5 Hivyo basi, je, huenda maneno “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” yakarejelea kiujumla kwa kila Mkristo? Ni kweli kwamba Wakristo wote wanapaswa kuwa waaminifu na wenye busara; hata hivyo, ni wazi kwamba Yesu alikuwa akifikiria jambo lingine aliposema juu ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Tunajuaje? Kwa sababu alisema kwamba wakati ambapo ‘bwana angefika’ angemweka mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” Mkristo mmoja-mmoja angewezaje kuwekwa juu ya kila kitu, yaani, juu ya mali “zote” za Bwana? Haiwezekani!
6. Taifa la Israeli lilikusudiwaje kuwa “mtumishi,” au “mtumwa” wa Mungu?
6 Hivyo, kauli pekee inayopatana na akili ni kwamba Yesu alikuwa akirejelea kikundi fulani cha Wakristo kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Je, inawezekana kwamba maneno hayo yanarejelea kikundi cha mtumwa? Ndiyo. Miaka elfu saba kabla ya Kristo, Yehova aliliita taifa zima la Israeli “mashahidi wangu” na “mtumishi wangu ambaye nimemchagua.” (Isaya 43:10) Kuanzia wakati Sheria ya Musa ilipotolewa mwaka wa 1513 K.W.K. hadi Pentekoste 33 W.K., kila Mwisraeli alikuwa mshiriki wa jamii hiyo ya mtumishi. Waisraeli wengi hawakushiriki moja kwa moja kusimamia mambo ya taifa au kuratibu mpango wa ulishaji wa kiroho wa taifa hilo. Yehova alitumia wafalme, waamuzi, makuhani, manabii na Walawi kufanya kazi hizo. Hata hivyo, taifa la Israeli lilipaswa kuwakilisha enzi kuu ya Yehova na kumsifu kati ya mataifa. Kila Mwisraeli alipaswa kuwa shahidi wa Yehova.—Kumbukumbu la Torati 26:19; Isaya 43:21; Malaki 2:7; Waroma 3:1, 2.
“Mtumishi” Afukuzwa
7. Kwa nini taifa la kale la Israeli halikustahili kuwa “mtumishi” wa Mungu?
7 Kwa kuwa taifa la Israeli lilikuwa “mtumishi” wa Mungu karne nyingi zilizopita, je, taifa hilo ndilo pia lililokuwa mtumwa ambaye Yesu alizungumzia? La, kwa kuwa inasikitisha kwamba Israeli la kale liliacha kuwa taifa lenye uaminifu au lenye busara. Paulo anaeleza kwa ufupi hali hiyo anaponukuu maneno haya ya Yehova kwa taifa hilo: “Jina la Mungu linafanyiwa makufuru katikati ya mataifa kwa sababu yenu.” (Waroma 2:24) Naam, Israeli lilifikia kilele cha historia yake ndefu ya uasi kwa kumkataa Yesu, naye Yehova akalikataa.—Mathayo 21:42, 43.
8. “Mtumishi” aliwekwa rasmi lini kuchukua mahali pa Israeli, na chini ya hali gani?
8 Ingawa “mtumishi” huyo, yaani, Israeli, alikosa uaminifu, hiyo haikumaanisha kwamba waabudu waaminifu hawangepata tena chakula cha kiroho. Kwenye Pentekoste 33 W.K., siku 50 baada ya ufufuo wa Yesu, wanafunzi wake 120 hivi walimwagiwa roho takatifu wakiwa katika chumba cha juu huko Yerusalemu. Wakati huo taifa jipya lilizaliwa. Kwa kufaa, kuzaliwa huko kulitangazwa wakati washiriki wa taifa hilo walipoanza kuwatangazia kwa ujasiri wakaaji wa Yerusalemu “mambo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:11) Hivyo, taifa hilo jipya, taifa la kiroho, likawa “mtumishi” ambaye angetangaza utukufu wa Yehova kwa mataifa na kuandaa chakula kwa wakati unaofaa. (1 Petro 2:9) Kwa kufaa, taifa hilo lilikuja kuitwa “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16.
9. (a) Ni nani ambao hufanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (b) Ni nani ‘watumishi wa nyumbani’?
9 Kila mshiriki wa “Israeli wa Mungu” ni Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa kwa roho takatifu na ana tumaini la kwenda mbinguni. Kwa hiyo, maneno “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hurejelea washiriki wote wa taifa hilo la kiroho lililotiwa mafuta ambao wameishi duniani kipindi chochote kile tangu mwaka wa 33 W.K. hadi leo, kama vile tu Mwisraeli yeyote aliyeishi kipindi chochote tangu mwaka wa 1513 K.W.K. hadi Pentekoste 33 W.K., alivyokuwa mshiriki wa jamii ya mtumishi kabla ya Ukristo. Hata hivyo, ni nani walio ‘watumishi wa nyumbani,’ ambao hupokea chakula cha kiroho chenye kujenga kutoka kwa mtumwa huyo? Katika karne ya kwanza W.K., kila Mkristo alikuwa na tumaini la kwenda mbinguni. Kwa hiyo, watumishi wa nyumbani walikuwa pia Wakristo watiwa-mafuta wakiwa mtu mmoja-mmoja bali si wakiwa kikundi. Wote, kutia ndani wale waliokuwa na madaraka kutanikoni, walihitaji chakula cha kiroho kutoka kwa mtumwa huyo.—1 Wakorintho 12:12, 19-27; Waebrania 5:11-13; 2 Petro 3:15, 16.
“Kila Mmoja Kazi Yake”
10, 11. Tunajuaje kwamba washiriki wote wa jamii ya mtumwa hawana mgawo uleule?
10 Ingawa “Israeli wa Mungu” ni jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambayo imepewa mgawo fulani, kila mshiriki pia ana madaraka ya kibinafsi. Yesu alifafanua jambo hilo waziwazi katika Marko 13:34. Alisema: “Ni kama mtu anayesafiri kwenda ng’ambo, ambaye aliacha nyumba yake na kuwapa mamlaka watumwa wake, kila mmoja kazi yake, na kumwamuru mtunza-mlango aendelee kukesha.” Kwa hiyo, kila mshiriki wa jamii ya mtumwa amepewa mgawo wa kuzidisha mali za Kristo duniani. Kila mshiriki wa jamii ya mtumwa hutimiza mgawo huo kulingana na hali na uwezo wake.—Mathayo 25:14, 15.
11 Isitoshe, mtume Petro aliwaambia hivi Wakristo watiwa-mafuta wa siku zake: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.” (1 Petro 4:10) Hivyo, watiwa-mafuta wana daraka la kuhudumiana kwa kutumia zawadi walizopewa na Mungu. Isitoshe, maneno ya Petro yanaonyesha kwamba Wakristo wote hawangekuwa na uwezo, madaraka, au mapendeleo yaleyale. Hata hivyo, kila mshiriki wa jamii ya mtumwa anaweza kusaidia kwa njia fulani ukuzi wa taifa hilo la kiroho. Jinsi gani?
12. Kila mshiriki wa jamii ya mtumwa, awe mwanamume au mwanamke, alisaidiaje ukuzi wa mtumwa huyo?
12 Kwanza, kila mmoja wao alikuwa na daraka la kuwa shahidi wa Yehova na kuhubiri habari njema ya Ufalme. (Isaya 43:10-12; Mathayo 24:14) Punde tu kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwaamuru wanafunzi wake wote waaminifu, wanaume kwa wanawake, wawe walimu. Alisema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 28:19, 20.
13. Watiwa-mafuta wote walifurahia pendeleo gani?
13 Wanafunzi wapya walipopatikana, walipaswa kufundishwa kwa makini kufuata mambo yote ambayo Kristo aliwaamuru wanafunzi wake. Baada ya muda, wale waliokubali kufundishwa walikuwa na sifa za kustahili kuwafundisha wengine. Chakula cha kiroho chenye kujenga kiliandaliwa kwa ajili ya wale ambao wangekuwa washiriki wa jamii ya mtumwa katika mataifa mengi. Wakristo wote, wanaume kwa wanawake, walishiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. (Matendo 2:17, 18) Kazi hiyo ingeendelea kuanzia wakati mtumwa huyo alipoanza kazi yake hadi mwisho wa mfumo huu wa mambo.
14. Ni nani tu waliokuwa na pendeleo la kufundisha kutanikoni, nao wanawake waaminifu waliotiwa mafuta walihisije kuhusu jambo hilo?
14 Watiwa-mafuta waliokuwa tu wamebatizwa walipata kuwa sehemu ya mtumwa huyo, na bila kujali walikuwa wamefundishwa na nani kwanza, waliendelea kupokea mafundisho kutoka kwa washiriki wa kutaniko wenye sifa za Kimaandiko zilizowastahilisha kutumikia wakiwa wanaume wazee. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:6-9) Hivyo, wanaume hao waliowekwa rasmi walikuwa na pendeleo la kusaidia ukuzi wa taifa hilo kwa njia ya kipekee. Wanawake Wakristo waaminifu waliotiwa mafuta hawakuudhika kuona kwamba wanaume Wakristo tu ndio waliopewa mgawo wa kufundisha kutanikoni. (1 Wakorintho 14:34, 35) Badala yake, walifurahia manufaa iliyotokana na kazi ya bidii ya washiriki wanaume wa kutaniko, nao walishukuru kwa mapendeleo ambayo wanawake wangepata, kutia ndani kuwatangazia wengine habari za furaha. Leo, dada watiwa-mafuta huonyesha mtazamo huohuo wa unyenyekevu, hata kama wazee waliowekwa rasmi ni watiwa-mafuta au la.
15. Ni ipi iliyokuwa mojawapo ya vyanzo vikuu vya chakula cha kiroho katika karne ya kwanza, na ni nani walioongoza kukiandaa?
15 Chakula muhimu cha kiroho kilichoandaliwa katika karne ya kwanza kilitokana moja kwa moja na barua za mitume na wanafunzi wengine waliokuwa wakiongoza. Barua walizoandika—hasa zile zinazopatikana kati ya vile vitabu 27 vilivyoongozwa na roho ya Mungu, na ambavyo hufanyiza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo—zilisambazwa katika makutaniko na bila shaka wazee walizitumia kufundisha. Kwa njia hiyo, wawakilishi wa mtumwa mwaminifu waligawanya chakula cha kiroho chenye kujenga kwa Wakristo wanyoofu. Jamii ya mtumwa ya karne ya kwanza ilitimiza kwa uaminifu mgawo iliyopewa.
Yule “Mtumwa” Baada ya Miaka 1,900 Hivi
16, 17. Jamii ya mtumwa ilionyeshaje uaminifu katika kutimiza mgawo wake katika miaka iliyotangulia mwaka wa 1914?
16 Namna gani leo? Kuwapo kwa Yesu kulipoanza mwaka wa 1914, je, alipata kikundi cha Wakristo watiwa-mafuta ambao walikuwa wakigawanya kwa uaminifu chakula kwa wakati unaofaa? Bila shaka. Kikundi hicho kingeweza kutambuliwa waziwazi kwa sababu ya matunda yake mazuri. (Mathayo 7:20) Tangu wakati huo, historia imethibitisha kwamba kikundi hicho ndicho kimekuwa kikigawanya chakula cha kiroho.
17 Wakati Yesu alipofika, watumishi wa nyumbani wapatao 5,000 walikuwa wakieneza kweli ya Biblia kwa bidii. Wafanyakazi walikuwa wachache, lakini mtumwa alibuni njia kadhaa za kueneza habari njema. (Mathayo 9:38) Kwa mfano, mipango ilifanywa ili vichwa vya mazungumzo ya Biblia vichapishwe katika magazeti-habari 2,000 hivi. Kwa njia hiyo, ukweli wa Neno la Mungu uliwafikia makumi ya maelfu ya wasomaji kwa wakati mmoja. Isitoshe, programu ya sinema na slaidi za rangi iliyochukua muda wa saa nane, ilitayarishwa. Kwa sababu ya mbinu hiyo ya kuhubiri, watu zaidi ya milioni tisa katika mabara matatu walitangaziwa ujumbe wa Biblia, kuanzia Uumbaji hadi mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Njia nyingine iliyotumiwa ni vichapo. Kwa mfano, mwaka wa 1914 nakala 50,000 za jarida hili zilichapishwa.
18. Yesu alimweka rasmi mtumwa juu ya mali zake zote wakati gani, na kwa nini?
18 Naam, Bwana alipowasili alimpata mtumwa wake mwaminifu akiwalisha kwa bidii watumishi wa nyumbani na pia kuhubiri habari njema. Sasa mtumwa huyo angepewa madaraka makubwa zaidi. Yesu alisema: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamweka juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:47) Yesu alifanya hivyo mwaka wa 1919, baada ya mtumwa huyo kupitia kipindi cha ukaguzi. Hata hivyo, kwa nini “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alipewa madaraka makubwa zaidi? Kwa sababu mali za Bwana zilikuwa zimeongezeka. Yesu alipewa utawala mwaka wa 1914.
19. Eleza jinsi mahitaji ya kiroho ya “umati mkubwa” yametimizwa.
19 Bwana aliyekuwa tu ametawazwa alimweka rasmi mtumwa wake mwaminifu juu ya mali zipi? Juu ya mali Zake zote za kiroho duniani. Kwa mfano, miaka 20 baada ya Kristo kutawazwa mwaka wa 1914, “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” ulitambulishwa. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Hawa hawakuwa washiriki watiwa-mafuta wa “Israeli wa Mungu,” lakini walikuwa wanaume na wanawake wanyoofu wenye tumaini la kuishi duniani, ambao walimpenda Yehova nao walitaka kumtumikia kama walivyofanya watiwa-mafuta. Kwa kweli, walimwambia hivi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) Wakristo hao waliokuwa tu wamebatizwa na pia watumishi wa nyumbani waliotiwa mafuta, walikula chakula kilekile chenye kujenga kiroho, na tangu wakati huo jamii hizo mbili zimekuwa zikila pamoja kwenye meza hiyo ya kiroho. Washiriki wa “umati mkubwa” wamepata baraka iliyoje!
20. “Umati mkubwa” umetimiza daraka gani katika kuzidisha mali za Bwana?
20 Kwa furaha, washiriki wa “umati mkubwa” walijiunga na jamii ya mtumwa iliyotiwa mafuta wakiwa wahubiri wa habari njema. Kadiri walivyohubiri ndivyo mali za duniani za Bwana zilivyoongezeka, na hivyo kumwongezea “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” madaraka. Hesabu ya watu waliotaka kujifunza kweli ilipoongezeka, ilibidi viwanda vya uchapishaji vipanuliwe ili kutosheleza mahitaji ya vichapo vya Biblia. Ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova zilianzishwa katika nchi moja baada ya nyingine. Mishonari walitumwa kwenda “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Katika mwaka wa 1914, kulikuwa na wasifaji wa Mungu waliotiwa mafuta elfu tano hivi, lakini leo idadi hiyo imeongezeka hadi wasifaji zaidi ya milioni sita ambao wengi wao ni wa “umati mkubwa.” Naam, mali za Mfalme zimeongezeka sana tangu atawazwe mwaka wa 1914!
21. Tutazungumzia mifano gani miwili katika funzo letu linalofuata?
21 Yote hayo yanaonyesha kwamba mtumwa amekuwa “mwaminifu na mwenye busara.” Baada tu ya kuzungumza kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yesu alitoa mifano miwili inayokazia sifa hizo: mfano wa mabikira wenye busara na mabikira wapumbavu, na ule wa talanta. (Mathayo 25:1-30) Mifano hiyo inatuvutia sana! Mifano hiyo inamaanisha nini kwetu leo? Tutazungumzia swali hilo katika makala inayofuata.
-
-
‘Yule Mtumwa Mwaminifu’ Apita Mtihani wa Ukaguzi!Mnara wa Mlinzi—2004 | Machi 1
-
-
‘Yule Mtumwa Mwaminifu’ Apita Mtihani wa Ukaguzi!
“Ni wakati uliowekwa wa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu.” —1 Petro 4:17.
1. Yesu alikuta hali gani alipokagua yule “mtumwa”?
SIKU ya Pentekoste 33 W.K., Yesu alimweka rasmi “mtumwa” ili awaandalie chakula “watumishi wake wa nyumbani” wakati unaofaa. Katika mwaka wa 1914, Yesu alitawazwa kuwa Mfalme, na punde wakati ukafika wa kumkagua “mtumwa” huyo. Alikuta kwamba wengi wa jamii hiyo ya “mtumwa” walikuwa ‘waaminifu na wenye busara.’ Hivyo, akaiweka rasmi jamii hiyo “juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, kulikuwa pia na mtumwa mwovu ambaye hakuwa mwaminifu wala mwenye busara.
“Mtumwa Huyo Mwovu”
2, 3. Jamii ya “mtumwa huyo mwovu” ilitoka wapi, nayo ilisitawi jinsi gani?
2 Yesu alimtaja mtumwa mwovu mara tu baada ya kuzungumza kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Alisema: “Mtumwa huyo mwovu akisema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia,’ naye aanze kuwapiga watumwa wenzake na kula na kunywa pamoja na walevi wa kupindukia, bwana wa mtumwa huyo atakuja katika siku ambayo hatazamii na katika saa ambayo hajui, naye atamwadhibu kwa ukali mkubwa zaidi na kumgawia sehemu yake pamoja na wanafiki. Huko ndiko atalia na kusaga meno.” (Mathayo 24:48-51) Maneno “mtumwa huyo mwovu” yanakazia maneno ya Yesu yaliyotangulia kuhusu mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Naam, wale wanaofanyiza “mtumwa huyo mwovu” walitoka miongoni mwa jamii ya mtumwa mwaminifu.a Jinsi gani?
3 Kabla ya mwaka wa 1914 washiriki wengi wa jamii ya mtumwa mwaminifu walikuwa na matazamio makubwa ya kukutana na Bwana-arusi mbinguni mwaka huo, lakini matazamio yao hayakutimizwa. Kwa sababu hiyo na hali nyingine, wengine walikata tamaa na wachache wakawa wenye uchungu. Baadhi yao walianza ‘kuwapiga’ kwa maneno ndugu zao wa zamani na kushirikiana na “walevi wa kupindukia,” yaani, vikundi vya dini zinazojiita za Kikristo.—Isaya 28:1-3; 32:6.
4. Yesu alishughulikaje na yule ‘mtumwa mwovu’ na wote ambao wameonyesha mtazamo kama wake?
4 Mwishowe, watu hao ambao walikuwa Wakristo walikuja kutambulishwa kuwa ‘mtumwa mwovu,’ naye Yesu akawaadhibu “kwa ukali mkubwa zaidi.” Jinsi gani? Aliwakataa, nao wakapoteza tumaini lao la kwenda mbinguni. Hata hivyo, hawakuharibiwa mara moja. Kwanza, walihitaji kupitia kipindi cha kulia na kusaga meno ‘katika giza lililo nje’ ya kutaniko la Kikristo. (Mathayo 8:12) Tangu siku hizo za mapema watiwa-mafuta wengine wachache wameonyesha mtazamo mbaya kama huo, na kujiunga na yule ‘mtumwa mwovu.’ Baadhi ya “kondoo wengine” wameiga ukosefu wao wa uaminifu. (Yohana 10:16) Adui hao wote wa Kristo wanaishia huko “nje katika giza” hilohilo la kiroho.
5. Mtumwa mwaminifu na mwenye busara alitendaje tofauti na ‘mtumwa mwovu’?
5 Hata hivyo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara na ‘mtumwa mwovu’ walipitia ukaguzi uleule. Hata hivyo, badala ya mtumwa mwaminifu kuwa mwenye uchungu, alikubali kurekebishwa upya. (2 Wakorintho 13:11) Upendo wao kwa Yehova na kwa ndugu zao uliimarishwa. Kwa sababu hiyo, wamekuwa “nguzo na tegemezo la ile kweli” katika ‘siku hizi za mwisho’ zenye msukosuko.—1 Timotheo 3:15; 2 Timotheo 3:1.
Mabikira Wenye Busara na Mabikira Wapumbavu
6. (a) Yesu alitoa mfano gani kuonyesha busara ya jamii yake ya mtumwa mwaminifu? (b) Wakristo watiwa-mafuta walitangaza ujumbe gani kabla ya mwaka wa 1914?
6 Baada ya kuzungumza juu ya “mtumwa huyo mwovu,” Yesu alitoa mifano miwili kuonyesha kwa nini Wakristo fulani waliotiwa mafuta wangekuwa waaminifu na wenye busara huku wengine wakikosa sifa hizo.b Yesu alitoa mfano huu ili kuonyesha busara hiyo: “Ufalme wa mbinguni utakuwa kama mabikira kumi waliochukua taa zao na kwenda kumpokea bwana-arusi. Watano kati yao walikuwa wapumbavu, na watano walikuwa wenye busara. Kwa maana wale wapumbavu walichukua taa zao lakini hawakuchukua mafuta pamoja nao, lakini wale wenye busara walichukua mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao.” (Mathayo 25:1-4) Mabikira hao kumi hutukumbusha Wakristo watiwa-mafuta kabla ya mwaka wa 1914. Walikuwa wamepiga hesabu na kujua kwamba bwana-arusi, Yesu Kristo, alikuwa karibu kutokea. Hivyo ‘wakaenda’ kumpokea, huku wakihubiri kwa ujasiri kwamba “nyakati zilizowekwa za mataifa” zingeisha mwaka wa 1914.—Luka 21:24.
7. Wakristo watiwa-mafuta ‘walilala’ kwa njia ya mfano lini na kwa nini?
7 Walipiga hesabu kwa usahihi. Nyakati zilizowekwa za mataifa ziliisha mwaka wa 1914, nao Ufalme wa Mungu chini ya Kristo Yesu ukaanza kufanya kazi. Lakini hilo lilitukia katika mbingu zisizoonekana. Duniani, wanadamu walianza kupatwa na “ole” uliotabiriwa. (Ufunuo 12:10, 12) Kipindi cha ukaguzi kikaanza. Kwa kutoelewa mambo vizuri, Wakristo watiwa-mafuta walifikiri kwamba ‘bwana-arusi alikuwa anakawia.’ Kwa sababu ya kuchanganyikiwa na kuchukiwa na ulimwengu, kwa ujumla watiwa-mafuta walipunguza bidii yao na karibu waache kabisa kazi ya kuhubiri hadharani kwa njia ya mpango. Kama mabikira katika mfano wa Yesu, “walisinzia na kuanza kulala” kiroho, kama vile watu wasio waaminifu waliodai kuwa Wakristo walivyofanya baada ya mitume wa Yesu kufa.—Mathayo 25:5; Ufunuo 11:7, 8; 12:17.
8. Ni nini kilichosababisha mwito: “Huyu hapa bwana-arusi!” na huo ulikuwa wakati wa Wakristo watiwa-mafuta kufanya nini?
8 Kisha mwaka wa 1919 jambo fulani lisilotazamiwa likatukia. Tunasoma: “Katikati ya usiku kukatokea mwito, ‘Huyu hapa bwana-arusi! Nendeni mkampokee.’ Ndipo mabikira wote hao wakasimama na kuzitayarisha taa zao.” (Mathayo 25:6, 7) Wakati ule tu mambo yalionekana kuwa mabaya kabisa, ndipo mwito wa kutenda ulipotokea! Katika mwaka wa 1918, Yesu, “mjumbe wa agano,” alikuja kwenye hekalu la kiroho la Yehova ili kukagua na kulisafisha kutaniko la Mungu. (Malaki 3:1) Sasa, Wakristo watiwa-mafuta walihitaji kwenda nje na kumpokea katika nyua za kidunia za hekalu. Wakati wao wa ‘kutoa nuru’ ulikuwa umefika.—Isaya 60:1; Wafilipi 2:14, 15.
9, 10. Kwa nini Wakristo fulani walikuwa “wenye busara” na wengine “wapumbavu” mwaka wa 1919?
9 Lakini ona kwamba baadhi ya wanawake hao wachanga katika mfano huo walikuwa na tatizo. Yesu aliendelea kusema: “Wale wapumbavu wakawaambia wale wenye busara, ‘Tupeni sisi kiasi fulani cha mafuta yenu, kwa sababu taa zetu zinakaribia kuzimika.’” (Mathayo 25:8) Bila mafuta, taa hizo hazingeweza kutoa nuru. Hivyo, mafuta ya taa hutukumbusha Neno la Mungu la kweli na roho yake takatifu, ambayo huwatia nguvu waabudu wa kweli wawe wachukuaji nuru. (Zaburi 119:130; Danieli 5:14) Kabla ya mwaka wa 1919, Wakristo watiwa-mafuta wenye busara walikuwa wamejitahidi kutambua mapenzi ya Mungu japo udhaifu wao wa muda. Hivyo, mwito wa kutoa nuru ulipotolewa, walikuwa tayari.—2 Timotheo 4:2; Waebrania 10:24, 25.
10 Hata hivyo, watiwa-mafuta fulani hawakuwa tayari kujidhabihu au kujikakamua, ingawa walitamani sana kuwa pamoja na Bwana-arusi. Kwa hiyo, wakati ulipofika wa kuhubiri habari njema kwa bidii, wao hawakuwa tayari. (Mathayo 24:14) Hata walijaribu kupunguza bidii ya wenzao, kwa kuwaomba wawagawie mafuta yao. Katika mfano wa Yesu, mabikira wenye busara walijibuje? Walisema: “Labda huenda tusiwe na ya kutosha kwa ajili yetu na kwa ajili yenu. Badala yake, shikeni njia mwende kwa wale wanaoyauza mkajinunulie.” (Mathayo 25:9) Vivyo hivyo, mwaka wa 1919 Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa waaminifu walikataa kufanya lolote ambalo lingepunguza uwezo wao wa kutoa nuru. Hivyo, walipita mtihani huo wa ukaguzi.
11. Mabikira wapumbavu walipatwa na nini?
11 Yesu anamalizia kwa kusema: “[Mabikira wapumbavu] walipokuwa wakienda zao kununua, bwana-arusi akafika, na wale mabikira waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya arusi; nao mlango ukafungwa. Baadaye wale mabikira wengine pia wakaja, wakisema, ‘Bwana, bwana, tufungulie!’ Akajibu, akasema, ‘Ninawaambia ninyi kweli, Siwajui ninyi.’” (Mathayo 25:10-12) Naam, baadhi yao hawakuwa tayari kumpokea Bwana-arusi alipowasili. Hivyo, wakaanguka mtihani wa ukaguzi na kupoteza nafasi ya kuhudhuria karamu ya arusi mbinguni. Ilihuzunisha kama nini!
Mfano wa Talanta
12. (a) Yesu alitumia mfano gani kuhusu sifa ya uaminifu? (b) Mtu ‘aliyeenda ng’ambo’ ni nani?
12 Baada ya kutoa mfano kuhusu busara, Yesu alitoa mfano mwingine kuhusu sifa ya uaminifu. Alisema: “Ni kama wakati ambapo mtu, akiwa karibu kusafiri ng’ambo, aliwaita watumwa wake na kuwapa mali zake. Akampa mmoja talanta tano, mwingine mbili, na mwingine moja, kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe, naye akaenda ng’ambo.” (Mathayo 25:14, 15) Mtu anayetajwa katika mfano huo ni Yesu mwenyewe, ambaye ‘alienda ng’ambo’ alipopanda mbinguni mwaka wa 33 W.K. Lakini kabla ya kupanda mbinguni, Yesu aliwapa wanafunzi wake waaminifu “mali zake.” Jinsi gani?
13. Yesu alitayarishaje shamba kubwa la utendaji na kuwapa ‘watumwa’ wake ruhusa ya kufanya biashara?
13 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alianza kutayarisha shamba kubwa la utendaji kwa kuhubiri habari njema za Ufalme katika nchi yote ya Israeli. (Mathayo 9:35-38) Kabla ya ‘kwenda ng’ambo,’ aliwapa wanafunzi waaminifu shamba hilo akisema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:18-20) Kwa maneno hayo Yesu aliwapa “watumwa” wake ruhusa ya kufanya biashara hadi atakaporudi, “kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.”
14. Kwa nini wanafunzi wote hawakutazamiwa wafanye biashara kwa kiwango kilekile?
14 Maneno hayo yanaonyesha kwamba hali za Wakristo wote wa karne ya kwanza hazikufanana. Hali za wengine, kama vile Paulo na Timotheo, ziliwawezesha kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. Huenda hali za wengine zilifanya iwe vigumu sana kushiriki katika kazi hiyo. Kwa mfano, Wakristo fulani walikuwa watumwa, wengine walikuwa wagonjwa, wazee, au wenye madaraka ya familia. Bila shaka, kulikuwa na mapendeleo fulani kutanikoni ambayo baadhi ya wanafunzi hawakuyapata. Baadhi ya wanawake na wanaume watiwa-mafuta hawakufundisha kutanikoni. (1 Wakorintho 14:34; 1 Timotheo 3:1; Yakobo 3:1) Hata hivyo, bila kujali hali zao, wanafunzi wote wa Kristo waliotiwa mafuta, wanaume kwa wanawake, walipewa mgawo wa kufanya biashara, nao walitumia vizuri nafasi na hali zao katika huduma ya Kikristo. Leo wanafunzi wa Kristo hufanya vivyo hivyo.
Wakati wa Ukaguzi Waanza!
15, 16. (a) Wakati wa kufanya hesabu ulifika lini? (b) Ni nafasi gani mpya za “kufanya biashara” ambazo wale walio waaminifu walipewa?
15 Katika mfano huo Yesu anaendelea kusema: “Baada ya muda mrefu bwana wa watumwa hao alikuja na kufanya hesabu pamoja nao.” (Mathayo 25:19) Katika mwaka wa 1914—bila shaka muda mrefu baada ya 33 W.K.—kuwapo kwa Kristo Yesu akiwa mfalme kulianza. Mnamo mwaka wa 1918, miaka mitatu na nusu baadaye, alikuja kwenye hekalu la Mungu la kiroho na kutimiza maneno haya ya Petro: “Ni wakati uliowekwa wa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu.” (1 Petro 4:17; Malaki 3:1) Ulikuwa wakati wa kufanya hesabu.
16 Watumwa, yaani, ndugu za Yesu watiwa-mafuta, wamefanyaje na “talanta” za Mfalme? Kuanzia mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, kutia ndani miaka iliyotangulia mwaka wa 1914, wengi walikuwa wakifanya “biashara” ya Yesu kwa bidii. (Mathayo 25:16) Hata wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, walionyesha tamaa kubwa ya kumtumikia Bwana. Wakati huo ilifaa wale walio waaminifu wapewe nafasi mpya za “kufanya biashara.” Mwisho wa mfumo huu wa mambo ulikuwa umefika. Habari njema ilipaswa kuhubiriwa duniani kote. “Mavuno ya dunia” yalipaswa kuvunwa. (Ufunuo 14:6, 7, 14-16) Washiriki wa mwisho wa jamii ya ngano walipaswa kutafutwa na “umati mkubwa” kukusanywa.—Ufunuo 7:9; Mathayo 13:24-30.
17. Wakristo waaminifu waliotiwa mafuta ‘waliingiaje katika shangwe ya bwana wao’?
17 Wakati wa mavuno ni wakati wa furaha. (Zaburi 126:6) Hivyo, inafaa kwamba Yesu alipowapa madaraka zaidi ndugu zake watiwa-mafuta mwaka wa 1919, alisema: ‘Mlikuwa waaminifu juu ya mambo machache. Nitawaweka juu ya mambo mengi. Ingieni katika shangwe ya bwana wenu.’ (Mathayo 25:21, 23) Isitoshe, hatuwezi kuwazia furaha ambayo Bwana alipata alipotawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. (Zaburi 45:1, 2, 6, 7) Jamii ya mtumwa mwaminifu inapata furaha hiyo pia kwa kumwakilisha Mfalme na kuzidisha mambo yanayohusu ufalme wake. (2 Wakorintho 5:20) Furaha yao inaonyeshwa katika maneno haya ya kinabii ya Isaya 61:10: “Hakika nitafurahi katika Yehova. Nafsi yangu itakuwa na shangwe katika Mungu wangu. Kwa maana amenivika mavazi ya wokovu.”
18. Kwa nini wengine hawakupita mtihani wa ukaguzi, na ilikuwaje?
18 Inasikitisha kwamba wengine hawakupita mtihani wa ukaguzi. Tunasoma: “Yule aliyekuwa amepokea talanta moja akaja na kusema, ‘Bwana nilijua wewe ni mtu mwenye kudai, ambaye huvuna mahali ambapo hukupanda na kukusanya mahali ambapo hukupepeta. Kwa hiyo nikaogopa na kwenda zangu na kuficha talanta yako katika udongo. Tazama, hiki hapa kilicho chako.’” (Mathayo 25:24, 25) Vivyo hivyo, Wakristo fulani watiwa-mafuta hawakufanya “biashara.” Kabla ya mwaka wa 1914 hawakuwa na bidii ya kuwaeleza wengine tumaini lao, nao hawakutaka kuanza kufanya hivyo mwaka wa 1919. Yesu alitendaje kuhusiana na dharau yao? Aliwanyang’anya mapendeleo yao yote. ‘Walitupwa nje katika giza ambako walilia na kusaga meno yao.’—Mathayo 25:28, 30.
Ukaguzi Unaendelea
19. Ukaguzi unaendelea katika njia gani, nao Wakristo wote watiwa-mafuta wameazimia kufanya nini?
19 Bila shaka, wengi wa wale ambao wangekuwa watumwa watiwa-mafuta wa Kristo wakati wa mwisho hawakuwa wakimtumikia Yehova wakati Yesu alipoanza ukaguzi mwaka wa 1918. Je, walikaguliwa? Ndiyo. Ukaguzi ulianza tu mwaka wa 1918/1919, wakati mtumwa mwaminifu na mwenye busara akiwa jamii alipopita mtihani wa ukaguzi. Wakristo mmoja-mmoja waliotiwa mafuta wanaendelea kukaguliwa hadi watiwe muhuri wa kudumu. (Ufunuo 7:1-3) Kwa kutambua jambo hilo, ndugu za Kristo watiwa-mafuta wameazimia kuendelea “kufanya biashara” kwa uaminifu. Wameazimia pia kuwa wenye busara na kuweka mafuta mengi vya kutosha ili nuru iendelee kung’aa zaidi. Wanajua kwamba kila mmoja wao anapokufa akiwa mwaminifu, Yesu atampokea na kukaa naye mbinguni.—Mathayo 24:13; Yohana 14:2-4; 1 Wakorintho 15:50, 51.
20. (a) Leo kondoo wengine wameazimia kufanya nini? (b) Wakristo watiwa-mafuta wanajua nini?
20 Umati mkubwa wa kondoo wengine wamewaiga ndugu zao watiwa-mafuta. Wanajua kwamba ujuzi wao wa makusudi ya Mungu huwafanya wawe na daraka kubwa. (Ezekieli 3:17-21) Hivyo, kwa msaada wa Neno la Yehova na roho yake takatifu, wao pia huweka mafuta mengi vya kutosha kupitia funzo na mikutano ya Kikristo. Nao huangaza nuru yao kwa kuhubiri na kufundisha na hivyo “kufanya biashara” pamoja na ndugu zao watiwa-mafuta. Hata hivyo, Wakristo watiwa-mafuta wanafahamu vizuri kwamba wao ndio waliopewa talanta. Lazima watoe hesabu kuhusu jinsi mali za Bwana zinavyosimamiwa duniani. Ingawa wao ni wachache, hawawezi kuwatwika umati mkubwa daraka lao. Kwa kuzingatia hilo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara anaendelea kuongoza katika kutunza biashara ya Mfalme na kushukuru kwa msaada wa washiriki wenye bidii wa umati mkubwa. Washiriki wa umati mkubwa wanatambua daraka la ndugu zao watiwa-mafuta nao huona ni pendeleo kufanya kazi chini ya usimamizi wao.
21. Ni himizo gani linalowahusu Wakristo wote kabla ya mwaka wa 1919 hadi siku zetu?
21 Hivyo, ingawa mifano hiyo miwili inafafanua matukio ya mwaka wa 1919 au karibu na wakati huo, kanuni za mifano hiyo zinahusu Wakristo wote wa kweli katika siku zote za mwisho. Kwa njia hiyo, ingawa himizo ambalo Yesu alitoa mwishoni mwa mfano wa mabikira kumi kwanza linahusu Wakristo watiwa-mafuta kabla ya mwaka wa 1919, bado kanuni zake zinahusu kila Mkristo. Sote na tutii maneno haya ya Yesu: “Endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”—Mathayo 25:13.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa njia inayofanana na hiyo, baada ya mitume kufa, “mbwa-mwitu wenye kukandamiza” walitoka miongoni mwa wazee Wakristo waliotiwa mafuta.—Matendo 20:29, 30.
-