-
Kumpendeza Yehova Ndilo Hangaikio Langu KuuMnara wa Mlinzi—1998 | Novemba 1
-
-
Mlango wangu wa seli ulifunguka, ofisa akapaaza sauti: “Neros ni nani?” Nilipojitambulisha, aliamuru hivi: “Simama. Tunaenda kukuua.” Jambo hilo lilitokea katika kambi ya kijeshi huko Korintho, Ugiriki, 1952. Kwa nini maisha yangu yalikuwa mashakani? Kabla sijaeleza hayo, acheni niwaambie kuhusu malezi yangu.
-
-
Kumpendeza Yehova Ndilo Hangaikio Langu KuuMnara wa Mlinzi—1998 | Novemba 1
-
-
Kutokuwamo Kwangu kwa Kikristo Kwajaribiwa
Nilipokuwa nimezuiliwa katika kambi za kijeshi huko Mesolóngion na Korintho, nilikuwa na fursa ya kueleza makomanda wa jeshi kwamba dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia haingeniruhusu kuwa askari-jeshi katika kutegemeza mambo ya kisiasa. “Mimi tayari ni askari-jeshi wa Yesu,” nikaelezea, nikionyesha 2 Timotheo 2:3. Niliposihiwa nifikirie hilo, nilisema kwamba uamuzi wangu haukuwa umefanywa kwa ghafula tu bali ulikuwa umefanywa baada ya kufikiria kwa uzito, na kwa kuzingatia wakfu wangu kwa Mungu kufanya mapenzi yake.
Tokeo likawa kwamba, nililazimika kufanya kazi ya kulazimishwa, kukosa chakula kila baada ya siku moja kwa siku 20, na kulala kwenye sakafu ya sementi ya seli yenye ukubwa wa futi tatu kwa sita. Nilikuwa katika seli hiyo pamoja na Mashahidi wengine wawili! Wakati huo, nilipokuwa ningali katika kambi ya Korintho, ndipo nilipoitwa kutoka seli ili nikauawe.
Tulipokuwa tukienda mahali pa kuuawa ofisa aliuliza, “Je, husemi chochote?”
“La,” nikajibu.
“Hutaandikia familia yako?”
“La,” nikajibu tena. “Tayari wanajua kwamba huenda nikauawa hapa.”
Tulifika kwenye ua, nami nikaamuriwa kusimama nikiangalia ukuta. Kisha, badala ya kuamuru askari-jeshi wafyatue risasi, huyo ofisa aliagiza, “Mpelekeni ndani.” Ulikuwa uuaji wa kusingizia tu, uliokusudiwa kujaribu azimio langu.
-