-
Familia Kubwa Zilizoungana Katika Utumishi wa MunguMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 15
-
-
Kama vile mti uzaavyo matunda mazuri ukimwagiliwa maji kwa ukawaida, ndivyo pia familia zilizolishwa vizuri kiroho huzaa matunda ya kimungu, ili jina la Yehova lisifiwe. Familia ya Uwadiegwu, anayeishi Afrika Magharibi ni mfano mmoja. Ijapokuwa Uwadiegwu na mke wake wana watoto wanane, wote wawili wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida, au wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Yeye asema: “Familia yetu imedumisha funzo la Biblia la ukawaida kwa zaidi ya miaka 20. Tumefundisha watoto Neno la Mungu tangu walipokuwa watoto wadogo, si wakati wa funzo la familia tu, bali pia katika huduma na nyakati nyinginezo. Watoto wetu wote ni wapiga-mbiu wa habari njema za Ufalme, na yule ambaye hajabatizwa bado ni yule mdogo zaidi tu aliye na umri wa miaka sita.”
-
-
Familia Kubwa Zilizoungana Katika Utumishi wa MunguMnara wa Mlinzi—1999 | Februari 15
-
-
Kazi ya pamoja hutia ndani kuwapa watoto madaraka ya kiroho wanapokuwa tayari kufanya hivyo. Baba mmoja, mzee Mkristo mwenye watoto 11, huamka asubuhi na mapema ili kuongoza mafunzo na watoto kadhaa kabla ya kwenda kazini. Wale wakubwa, wanapobatizwa, huwasaidia ndugu na dada zao wachanga kwa zamu, hiyo yatia ndani kushiriki katika kuwafundisha Biblia. Baba huwasimamia, akiwapongeza kwa jitihada zao. Sita kati ya watoto hao wamebatizwa, na wengine wanaendelea kujitahidi kufikia mradi huo.
Mawasiliano Mazuri, Miradi ya Pamoja
Lililo muhimu katika familia zilizoungana ni mawasiliano yenye upendo na miradi ya kiroho ya pamoja. Gordon, mzee Mkristo anayeishi Nigeria, ni baba ya watoto saba wenye umri wa kati ya miaka 11 hadi miaka 27. Sita kati yao ni mapainia, kama vile wazazi wao. Yule mdogo zaidi, aliyebatizwa hivi majuzi, hushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kufanya wanafunzi na wale wengine katika familia. Wana wawili ambao ni watu wazima ni watumishi wa huduma katika kutaniko.
Gordon aliongoza mwenyewe mafunzo ya Biblia pamoja na kila mmoja wa watoto wake. Mbali na hilo, familia hiyo ina programu yenye mambo mengi ya elimu ya Biblia. Wao hukutana kila asubuhi ili kuchunguza andiko la Biblia kisha kujitayarisha kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.
Mojawapo ya miradi iliyowekwa kwa kila mshiriki wa familia ni kusoma makala zote katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hivi majuzi, waliongezea usomaji wa Biblia wa kila siku katika kawaida yao ya usomaji. Kwa kuzungumzia yale wanayosoma, washiriki wa familia hutiana moyo kuendeleza zoea hilo.
Funzo la Biblia la familia la kila juma limeimarika vizuri sana hivi kwamba hakuna mtu ambaye huhitaji kikumbusha—kila mtu hulitazamia. Kwa miaka kadhaa, mambo yaliyomo, muundo wake, na urefu wa funzo la familia, yametofautiana kulingana na umri na mahitaji ya watoto. Familia hiyo imekuwa na ukaribu pamoja na watumishi wengine waaminifu wa Mungu, na hilo limekuwa na matokeo yenye kunufaisha watoto.
Wakiwa familia, wao hufanya mambo pamoja na kutenga wakati wa tafrija. Mara moja kwa juma wao hufurahia “tafrija ya jioni ya familia,” ambayo huwa na maswali ya kutahini, mizaha ifaayo, kupiga piano, kusimulia hadithi, na kupumzika tu. Mara nyingine, wao huenda pwani na sehemu nyingine zenye kupendeza.
Kumtegemea Yehova
Hakuna moja kati ya mambo yaliyotajwa juu ambayo hurahisisha ugumu wa kulea familia kubwa. “Ni vigumu sana kuwa baba mzuri wa watoto wanane,” Mkristo mmoja asema. “Hali hiyo hutaka chakula kingi cha kimwili na cha kiroho kuweza kuwatosha; lazima nifanye kazi kwa bidii ili kupata fedha za kutosha kuwategemeza. Watoto walio wakubwa kidogo kwa umri wako katika miaka yao ya utineja, na wote wanane huenda shuleni. Najua kwamba mazoezi ya kiroho ni muhimu, lakini baadhi ya watoto wangu ni watundu na wasiotii. Wao hunihuzunisha, lakini najua nyakati nyingine mimi hufanya mambo ambayo huhuzunisha moyo wa Yehova, naye hunisamehe. Kwa hiyo, lazima niendelee kuwasahihisha watoto wangu kwa subira hadi warekebike.
“Najaribu kufuata kielelezo cha Yehova kwa kuwa yeye ni mwenye subira kutuelekea kwa sababu hutaka wote wafikie toba. Najifunza na familia yangu, na baadhi ya watoto wangu wanajitahidi kufikia mradi wa ubatizo. Sitegemei nguvu zangu mwenyewe ili kupata matokeo haya; nguvu zangu haziwezi kutimiza mengi. Najaribu kumkaribia Yehova katika sala na kutumia mithali isemayo: ‘Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.’ Yehova atanisaidia nitimize mazoezi ya watoto wangu.”—Mithali 3:5, 6.
Usikate Tamaa!
Nyakati nyingine kuzoeza watoto huonekana kuwa kazi ngumu isiyothaminiwa, lakini usikate tamaa! Vumilia! Watoto wako wakikosa kuitikia kwa njia inayofaa au kuthamini jitihada zako sasa, huenda wakafanya hivyo baadaye. Huchukua muda mrefu ili mtoto akue kufikia kuwa Mkristo mwenye kuzaa matunda ya roho.—Wagalatia 5:22, 23.
Monica, anayeishi Kenya, ni mmoja wa watoto kumi. Yeye asema: “Wazazi wangu walitufunza kweli ya Biblia tangu utotoni. Baba alikuwa akitufunza vichapo vya Kikristo kila juma. Kwa sababu ya kazi yake, funzo halikuwa siku ileile sikuzote. Nyakati nyingine, alipokuwa akirudi nyumbani kutoka kazini, angetuona tukicheza nje na kutuambia kwamba baada ya dakika tano ilitupasa tuingie ndani kwa ajili ya funzo letu la Biblia. Baada ya funzo letu la Biblia, tulikuwa tukitiwa moyo kuuliza maswali na kuzungumzia matatizo yetu.
“Alihakikisha kwamba tulishirikiana na watoto wenye kumhofu Mungu. Baba alitembelea shule yetu kwa ukawaida na kuuliza walimu kuhusu mwenendo wetu. Katika ziara moja alisikia kwamba kaka zangu watatu walikuwa wamepigana na wavulana wengine na kwamba nyakati nyingine walikuwa wajeuri. Baba aliwaadhibu kwa kukosa adabu, lakini pia alichukua wakati kueleza kutoka katika Maandiko sababu waliyohitaji kujiendesha wenyewe katika njia ya kimungu.
“Wazazi wetu walituonyesha manufaa za kuhudhuria mikutano kwa kutayarisha sehemu za mkutano pamoja nasi. Tulizoezwa kuwa wahudumu kwa kujizoeza nyumbani. Kuanzia utotoni tuliandamana na wazazi wetu katika utumishi wa shambani.
“Leo, kaka zangu wawili ni mapainia wa pekee, dada mmoja ni painia wa kawaida, na dada mwingine, ambaye ameolewa ana familia, naye ni Shahidi mwenye bidii. Dada zangu wawili wachanga, mmoja mwenye umri wa miaka 18 na yule mwingine miaka 16, ni wahubiri waliobatizwa. Wavulana wawili wachanga wanazoezwa. Nimekuwa nikitumikia katika ofisi ya tawi ya Kenya ya Mashahidi wa Yehova kwa miaka mitatu. Nawapenda na kuwathamini wazazi wangu kwa sababu wao ni watu wa kiroho; walituwekea kielelezo chema.”
-