Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 15
    • Kwa hiyo ukimshawishi mtu akubali fundisho fulani la Biblia, umemsadikisha akutumaini, na hivyo aamini kwamba fundisho hilo ni la kweli. Bila shaka, haitoshi tu kumweleza mtu yale ambayo Biblia husema ili aiamini na kutenda kupatana nayo. Lazima msikilizaji wako asadiki kwamba yale unayosema ni ya kweli, hata kama yeye ni mtoto, jirani, mfanyakazi mwenzako, mwanafunzi mwenzako, au mtu wa ukoo.—2 Timotheo 3:14, 15.

      8. Ni nini kinachohusika katika kumsadikisha mtu ukweli fulani wa Biblia?

      8 Unawezaje kumsadikisha mtu kwamba yale unayosema kutoka katika Neno la Mungu ni kweli? Paulo alijitahidi kubadili maoni ya watu aliozungumza nao kwa kujadiliana nao kupatana na akili, kutoa hoja zinazofaa, na kuwasihi kwa bidii.a Kwa hiyo, badala tu ya kusema kwamba jambo fulani ni kweli, unahitaji kutoa uthibitisho wenye kuridhisha kuunga mkono maneno yako. Unawezaje kufanya hivyo? Hakikisha kwamba maneno yako yanategemea kabisa Neno la Mungu wala si maoni yako mwenyewe. Pia, toa uthibitisho zaidi ili kuunga mkono maneno yako ya kutoka moyoni yanayotegemea Biblia. (Methali 16:23) Kwa mfano, ukisema kwamba wanadamu watiifu watafurahia maisha katika dunia paradiso, tumia Maandiko kama vile Luka 23:43 au Isaya 65:21-25 kuunga mkono maneno hayo. Unawezaje kutoa uthibitisho zaidi ili kuunga mkono hoja yako ya Kimaandiko? Unaweza kutumia mifano inayotegemea mambo ambayo yamempata msikilizaji wako. Unaweza kumkumbusha mambo fulani madogo anayofurahia bila malipo yoyote, kama vile machweo ya jua yenye kupendeza, harufu nzuri ya ua, ladha nzuri ya tunda, au furaha unayopata kwa kumtazama ndege akilisha makinda yake. Msaidie aone kwamba mambo hayo yenye kufurahisha yanathibitisha kwamba Muumba wetu anataka tufurahie maisha duniani.—Mhubiri 3:11, 12.

      9. Tunawezaje kuonyesha busara tunapohubiri?

      9 Unapojaribu kumshawishi mtu akubali fundisho fulani la Biblia, jihadhari shauku yako isifanye uonekane kama unashikilia maoni yako tu, na hivyo kutofikia akili na moyo wa msikilizaji wako. Kitabu Shule ya Huduma kinatoa tahadhari hii: ‘Kwa kawaida ukifichua kwa dharau fundisho fulani la uwongo ambalo mtu anapenda sana, mtu huyo hatakubali kweli hata umsomee Maandiko mangapi. Kwa mfano, ukishutumu tu sherehe zinazopendwa kwamba ni za kipagani, huenda watu wasibadili maoni yao kuzihusu. Kwa kawaida unaweza kufanikiwa kwa kujadiliana nao.’ Kwa nini ujitahidi sana kuwa mwenye busara? Kitabu hicho kinasema: ‘Kujadiliana hufanya watu wachangie mazungumzo, huwasaidia kufikiria mambo hayo baadaye, na kuwafanya waweze kusikiliza wakati ujao. Kusababu kunaweza kushawishi sana.’—Wakolosai 4:6.

  • Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 15
    • Tumia Neno la Mungu kwa Ustadi

      13. Unawezaje kuwachochea wasikilizaji wako kama Paulo?

      13 Paulo alitamani kuwachochea wasikilizaji wake watende kupatana na habari njema. (1 Wathesalonike 1:5-7) Ili kutimiza hilo, aliuchochea moyo wao wa mfano ambao ni chanzo cha msukumo wa kutenda. Tunapochunguza zaidi namna Paulo alivyojitetea mbele ya Agripa, ona jinsi Paulo ‘alivyotumia neno la Mungu sawasawa’ kwa kurejelea mambo yaliyosemwa na Musa na manabii.—2 Timotheo 2:15.

      14. Eleza jinsi Paulo alivyotumia ushawishi alipokuwa mbele ya Agripa.

      14 Paulo alijua kwamba Agripa alikuwa Myahudi kwa jina tu. Alitaja ujuzi wa Agripa kuhusu Dini ya Kiyahudi na kusema kwamba mahubiri yake yalihusu hasa ‘kutosema lolote ila mambo ambayo Manabii na vilevile Musa walisema yatatukia’ kuhusu kifo na ufufuo wa Masihi. (Matendo 26:22, 23) Akizungumza na Agripa moja kwa moja, Paulo aliuliza: “Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii?” Agripa alitatanika. Kama angesema kwamba hakuwaamini manabii, sifa yake akiwa mwamini Myahudi ingeharibika. Na kama angekubaliana na hoja ya Paulo, angekuwa anakiri hadharani kwamba anakubaliana na maoni ya mtume huyo na hivyo kuitwa Mkristo, jambo ambalo lilikuwa hatari. Paulo alijibu swali lake mwenyewe kwa hekima, akisema: “Ninajua unawaamini.” Moyo wa Agripa ulimchochea kujibuje? Alijibu: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Matendo 26:27, 28) Ingawa Agripa hakupata kuwa Mkristo, ni wazi kwamba Paulo alimgusa moyo kwa kadiri fulani kwa ujumbe wake.—Waebrania 4:12.

      15. Paulo aliwezaje kuanzisha kutaniko huko Thesalonike?

      15 Je, umeona kwamba mazungumzo ya Paulo kuhusu habari njema yalihusisha kutangaza ujumbe na kushawishi? Kwa kuwa Paulo alitumia njia hiyo ‘alipolitumia neno la Mungu sawasawa,’ baadhi ya watu waliomsikiliza waliacha kuwa wasikilizaji tu na wakawa waamini. Hivyo ndivyo ilivyotukia huko Thesalonike ambako Paulo alitafuta katika sinagogi Wayahudi na watu wa mataifa waliomwogopa Mungu. Andiko la Matendo 17:2-4 linasema: “Kulingana na desturi ya Paulo akaingia ndani walimokuwa, na kwa sabato tatu akajadiliana nao kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu . . . Ikawa kwamba baadhi yao wakawa waamini.” Paulo alikuwa mwenye kushawishi. Alitoa hoja, akaeleza, na kuthibitisha kupitia Maandiko kwamba Yesu ndiye Masihi aliyekuwa ameahidiwa kwa muda mrefu. Ikawaje? Kutaniko la waamini lilianzishwa.

      16. Unawezaje kupata furaha kubwa zaidi katika kuhubiri juu ya Ufalme?

      16 Je, unaweza kuwa mwenye ustadi zaidi katika kushawishi unapofafanua Neno la Mungu? Ikiwa ndivyo, utapata uradhi na furaha zaidi katika kazi yako ya kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. Wahubiri wa habari njema wamepata uradhi na furaha zaidi kwa kufuata madokezo ya kuitumia Biblia zaidi katika kazi ya kuhubiri.

      17. Ili kuonyesha manufaa ya kutumia Biblia katika huduma, simulia jambo ulilojionea au uonyeshe umuhimu wa kufanya hivyo kama inavyoonyeshwa katika fungu hili.

      17 Kwa mfano, mwangalizi mmoja asafiriye wa Mashahidi wa Yehova aliandika hivi: “Sasa ndugu na dada wengi hubeba Biblia mkononi wanapohubiri nyumba kwa nyumba. Kufanya hivyo kumewasaidia wahubiri kuwasomea andiko fulani baadhi ya watu wengi wanaokutana nao. Kumemsaidia mwenye nyumba na pia mhubiri kuihusianisha huduma yetu na Biblia, wala si magazeti na vitabu tu.” Bila shaka, kubeba Biblia mkononi tunapohubiri kunategemea mambo kadhaa, kutia ndani desturi za eneo tunalohubiri. Hata hivyo, tunahitaji kutamani kuwa na sifa ya kutumia Neno la Mungu kwa ustadi ili kushawishi wengine wakubali ujumbe wa Ufalme.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki