-
Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia HabariFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari
IWE unazungumza na mtu mmoja au watu wengi, si vizuri kudhani wasikilizaji watapenda habari yako eti kwa sababu unaipenda. Ingawa ujumbe wako ni muhimu, baada ya muda watu wanaweza kuacha kukusikiliza ikiwa huwaonyeshi faida yake.
Ndivyo ilivyo pia na wasikilizaji katika Jumba la Ufalme. Wanaweza kusikiliza unapotumia mfano au unaposimulia tukio ambalo hawajasikia. Lakini wanaweza kuacha kukusikiliza unapozungumzia mambo ambayo tayari wanajua, hasa ukikosa kujenga hotuba yako juu ya mambo hayo. Unahitaji kuwasaidia waone kwa nini habari hiyo ina faida na pia inawafaidi kwa njia gani.
Biblia inatuhimiza tufikiri kwa njia inayofaa. (Mit. 3:21) Yehova alimtumia Yohana Mbatizaji kuwaonyesha watu “hekima itumikayo ya walio waadilifu.” (Luka 1:17) Hekima hii inategemea kumcha Yehova. (Zab. 111:10) Wale wanaotambua hekima hii husaidiwa kukabiliana kwa mafanikio na maisha wakati huu, na kushika uhai halisi na wa milele wa wakati ujao.—1 Tim. 4:8; 6:19.
-
-
Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia HabariFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Kuwasaidia Wengine Kuona Faida ya Ujumbe Wetu. Unapohubiri, usisahau kuonyesha faida ya habari njema maishani mwao. Ili ufaulu, unahitaji kufahamu mambo yanayowahangaisha watu katika eneo lenu. Unawezaje kujua mambo hayo? Sikiliza habari kwenye redio au televisheni. Tazama ukurasa wa mbele wa gazeti la habari. Pia jaribu kuwafanya watu wazungumze, na uwasikilize wanapoongea. Unaweza kugundua wana matatizo makubwa kama vile kupoteza kazi, kulipa kodi ya nyumba, ugonjwa, kifo cha mshiriki wa familia, kupatwa na uhalifu, kutendwa isivyofaa na mtu mwenye mamlaka, kuvunjika kwa ndoa, kuwadhibiti watoto, na kadhalika. Je, Biblia inaweza kuwasaidia? Bila shaka, ndiyo.
Inaelekea kwamba unapoanzisha mazungumzo utakuwa na jambo fulani akilini unalotaka kusema. Lakini ukiona kwamba mtu huyo ana jambo jingine linalomhangaisha sana, usisite kuzungumza naye jambo hilo ikiwezekana, au mwambie utamletea habari ambazo zinaweza kumsaidia. Ingawa tunaepuka ‘kujiingiza katika lile lisilotuhusu,’ tunafurahi kuwapa wengine mashauri ya Biblia ambayo wanaweza kutumia. (2 The. 3:11) Ni wazi kwamba jambo linalowavutia watu zaidi ni shauri la Biblia linalohusu maisha yao.
Watu wasipoona jinsi ujumbe wetu unavyowahusu, wanaweza kukatiza mazungumzo haraka. Hata wakituruhusu tuendelee kuzungumza, tukikosa kuwaonyesha faida ya habari hiyo hawatafaidika. Lakini tukiwaonyesha faida ya ujumbe wetu, mazungumzo yetu yanaweza kubadili maisha yao.
Unapofundisha watu Biblia, endelea kukazia jinsi wanavyoweza kutumia habari wanayojifunza. (Mit. 4:7) Wasaidie wanafunzi waelewe shauri, kanuni, na mifano inayopatikana katika Maandiko ambayo inawaonyesha jinsi ya kufuata njia za Yehova. Kazia faida ambazo watapata. (Isa. 48:17, 18) Kufanya hivyo kutawachochea wanafunzi wafanye mabadiliko yanayotakikana katika maisha yao. Wasaidie wampende Yehova na kuwa na tamaa ya kumpendeza, na pia wasaidie wachochewe na moyo wao wenyewe kutumia shauri la Neno la Mungu.
-