-
Kuzungumza kwa njia ya kawaidaFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
SOMO LA 14
Kuzungumza kwa njia ya kawaida
KUONGEA kwa njia ya kawaida hufanya wengine wakuamini. Je, unaweza kuamini maneno ya mtu ambaye amefunika uso wake kwa kitu fulani? Na je, ungeamini maneno yake kama kitu hicho kinavutia kuliko sura yake halisi? Hapana. Basi uwe jinsi ulivyo kwa kawaida badala ya kuiga usemi mwingine.
Kuzungumza kwa njia ya kawaida si uzembe. Kutotumia lugha sanifu, kutamka maneno vibaya, na kutosema maneno yanayosikika wazi hakufai. Tuepuke lugha ya mtaani. Nyakati zote maneno yetu na tabia zetu ziwe na adabu. Mtu ambaye anaongea kwa njia ya kawaida haongei kwa njia rasmi kupita kiasi wala hafikirii tu kuvutia watu.
Katika Huduma ya Shambani. Unapokaribia nyumba au unapoelekea kukutana na mtu hadharani ili umhubirie, je, unakuwa na wasiwasi? Wengi wetu huwa na wasiwasi, lakini wengine huwa na wasiwasi zaidi. Wasiwasi unaweza kufanya sauti ibadilike au itetemeke, au unaweza kufanya utoe ishara isiyofaa kwa mikono na kichwa.
Kuna sababu kadhaa zinazoweza kumfanya mhubiri apate tatizo hilo. Labda anafikiria watu watamwonaje au anafikiria iwapo atafanikiwa kutoa ushahidi. Hiyo ni kawaida, lakini matatizo hutokea tunapofikiria mambo hayo kupita kiasi. Ukishikwa na wasiwasi kabla ya kuanza huduma, ni nini kinachoweza kukusaidia? Jitayarishe vizuri na usali sana kwa Yehova. (Mdo. 4:29) Fikiria rehema kubwa ambayo Yehova anaonyesha kwa kuwaalika watu wafurahie afya kamilifu na uhai wa milele katika Paradiso. Wafikirie wale unaojaribu kuwasaidia na uhitaji wao wa kusikia habari njema.
Ukumbuke pia kwamba watu wana hiari, kwa hiyo ama wanaweza kukubali ujumbe wako ama waukatae. Ndivyo ilivyokuwa Yesu alipohubiri katika Israeli la kale. Mgawo wako ni kuhubiri tu. (Mt. 24:14) Hata kama watu hawakupi nafasi ya kuzungumza, unatoa ushahidi unapowatembelea. Utakuwa umefaulu kwa sababu umemruhusu Yehova akutumie kutimiza mapenzi yake. Na ukipata fursa za kuongea, utazungumzaje? Ukijifunza kufikiria mahitaji ya wengine, utaongea kwa njia ya kuvutia na ya kawaida.
Ukitenda na kuzungumza kama kawaida unapohubiri, wale wanaokusikiliza watastarehe. Hata wanaweza kukubali kwa urahisi zaidi Maandiko ambayo unataka kuwaeleza. Badala ya kuwahutubia, zungumza nao. Uwe mwenye urafiki. Pendezwa nao, na uwaruhusu wajieleze. Kama kuna desturi fulani katika lugha ama jamii ya kuonyesha adabu unapoongea na watu usiowajua, ni vizuri kuzifuata. Lakini, uwe tayari nyakati zote kutabasamu kirafiki.
-