Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Tumia Sawasawa Neno la Mungu’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 15
    • ‘Tumia Sawasawa Neno la Mungu’

      “Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, ukilitumia sawasawa neno la kweli.”—2 TIMOTHEO 2:15.

      1, 2. (a) Kwa nini wafanyakazi huhitaji vifaa? (b) Wakristo wanashiriki kazi gani, nao huonyeshaje kwamba wanatafuta kwanza Ufalme?

      WAFANYAKAZI wanahitaji vifaa ili viwasaidie kufanya kazi yao. Lakini haitoshi tu kuwa na kifaa chochote. Mfanyakazi anahitaji kifaa kinachofaa, na anapaswa kukitumia kwa njia inayofaa. Kwa mfano, ikiwa unajenga kibanda na unataka kuunganisha mbao mbili, hungehitaji tu nyundo na misumari. Ungehitaji kujua jinsi ya kupigilia msumari kwenye mbao bila kuupinda. Ni jambo gumu na hata lenye kukatisha tamaa kujaribu kuupigilia msumari kwenye mbao ikiwa hujui jinsi ya kutumia nyundo. Lakini vifaa vinapotumiwa sawasawa vinatusaidia kutimiza kazi kwa njia yenye kuridhisha.

      2 Tukiwa Wakristo tuna kazi muhimu sana ya kufanya. Yesu Kristo aliwahimiza wafuasi wake ‘watafute kwanza ufalme.’ (Mathayo 6:33) Tunawezaje kufanya hivyo? Njia moja ni kuwa wenye bidii katika kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Njia nyingine ni kutegemea kabisa Neno la Mungu katika huduma yetu. Nayo njia ya tatu ni kuwa na mwenendo mzuri. (Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 8:25; 1 Petro 2:12) Ili tuwe na matokeo na kufurahia kazi hiyo ya Kikristo, tunahitaji vifaa vinavyofaa na kujua jinsi ya kuvitumia sawasawa. Kuhusiana na kazi hiyo, mtume Paulo aliweka kielelezo bora akiwa mfanyakazi Mkristo, naye aliwatia moyo waamini wenzake wamwige. (1 Wakorintho 11:1; 15:10) Hivyo basi, tunaweza kujifunza nini kutoka kwa mfanyakazi mwenzetu, Paulo?

      Paulo, Mtangazaji wa Ufalme Mwenye Bidii

      3. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba mtume Paulo alikuwa mfanyakazi wa Ufalme mwenye bidii?

      3 Paulo alikuwa mfanyakazi wa aina gani? Bila shaka, Paulo alikuwa mwenye bidii naye alijikakamua kabisa kueneza habari njema katika eneo kubwa la Mediterania. Akieleza sababu iliyofanya awe na shauku katika kazi ya kutangaza Ufalme, mtume huyo asiyechoka alisema hivi: “Ikiwa, sasa, ninatangaza habari njema, hiyo si sababu ya mimi kujisifu, kwa maana nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!” (1 Wakorintho 9:16) Je, Paulo alitaka tu kuokoa uhai wake? La. Yeye hakuwa mwenye ubinafsi. Badala yake, alitaka wengine pia wanufaike na habari njema. Aliandika hivi: “Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.”—1 Wakorintho 9:23.

      4. Wafanyakazi Wakristo huthamini zaidi kifaa gani?

      4 Mtume Paulo alikuwa mfanyakazi mwenye kiasi ambaye alitambua kwamba hangeweza kutegemea ustadi wake tu. Kama vile seremala huhitaji nyundo, Paulo alihitaji kifaa kinachofaa ili kukazia kweli ya Mungu katika mioyo ya wasikilizaji wake. Alitumia kifaa gani hasa? Alitumia Neno la Mungu, Maandiko Matakatifu. Vivyo hivyo, Biblia nzima ndicho kifaa kikuu tunachotumia kutusaidia kufanya wanafunzi.

      5. Ili tuwe wahudumu wenye matokeo, tunahitaji kufanya nini zaidi ya kunukuu tu maandiko?

      5 Paulo alijua kwamba kutumia sawasawa Neno la Mungu kulihusisha mengi zaidi ya kulinukuu tu. Alitumia “ushawishi.” (Matendo 28:23) Jinsi gani? Paulo alitumia kwa mafanikio Neno la Mungu lililoandikwa ili kuwasadikisha wengi wakubali kweli ya Ufalme. Alijadiliana nao. Kwa miezi mitatu, Paulo ‘alitoa hotuba na kutumia ushawishi kuhusu ufalme wa Mungu’ katika sinagogi moja huko Efeso. Baadhi ya watu walisikiliza ingawa ‘wengine waliendelea kujifanya wenyewe wagumu na kutoamini.’ Kwa sababu ya huduma ya Paulo huko Efeso ‘neno la Yehova lilizidi kukua na kusitawi.’—Matendo 19:8, 9, 20.

      6, 7. Paulo aliitukuzaje huduma yake, nasi tunawezaje kufanya hivyo?

      6 Paulo alikuwa mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii naye ‘aliitukuza huduma yake.’ (Waroma 11:13) Jinsi gani? Hakutaka kujitukuza wala hakuona aibu kujulikana hadharani kuwa mmoja wa wafanyakazi wenzi wa Mungu. Badala yake, aliiona huduma yake kuwa pendeleo lenye kuheshimika sana. Paulo alitumia Neno la Mungu kwa ustadi na kwa matokeo. Utendaji wake wenye matokeo uliwatia wengine moyo na kuwachochea watimize huduma yao kikamili zaidi. Katika njia hiyo pia, huduma yake ilitukuzwa.

      7 Kama Paulo, tunaweza kutukuza kazi yetu tukiwa wahudumu kwa kutumia Neno la Mungu mara nyingi na kwa matokeo. Katika sehemu zote za huduma yetu, lengo letu linapaswa kuwa kuzungumzia jambo fulani katika Maandiko pamoja na watu wengi iwezekanavyo. Tunawezaje kufanya hivyo kwa ushawishi? Fikiria njia tatu muhimu (1) Elekeza fikira za wengine kwenye Neno la Mungu katika njia inayofanya liheshimiwe. (2) Eleza kwa busara yale ambayo Biblia husema kisha uonyeshe jinsi yanavyotumika. (3) Tumia Maandiko kueleza mambo katika njia yenye kusadikisha.

      8. Leo tuna vifaa gani vya kuhubiri Ufalme, nawe umevitumiaje?

      8 Leo watangazaji wa Ufalme wana vifaa ambavyo Paulo hakuwa navyo wakati wa huduma yake. Vifaa hivyo vinatia ndani, vitabu, magazeti, broshua, vikaratasi vya ukaribishaji, trakti, kaseti, na video. Katika karne iliyopita, kadi za kutoa ushahidi, santuri, magari yenye vikuza-sauti, na matangazo ya redio yalitumiwa. Bila shaka, kifaa chetu bora zaidi ni Biblia, nasi tunapaswa kutumia kifaa hicho muhimu kwa njia nzuri na inayofaa.

      Lazima Huduma Yetu Itegemee Neno la Mungu

      9, 10. Tunaweza kujifunza nini kutokana na shauri la Paulo kwa Timotheo kuhusiana na kulitumia Neno la Mungu?

      9 Tunawezaje kutumia Neno la Mungu kwa matokeo? Kwa kufuata maneno haya ya Paulo kwa mfanyakazi mwenzake Timotheo: “Fanya kabisa yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, ukilitumia sawasawa neno la kweli.” (2 Timotheo 2:15) ‘Kulitumia sawasawa neno la kweli’ kunahusisha nini?

      10 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kutumia sawasawa’ kihalisi linamaanisha “kukata kwa kunyooka” au “kupasua njia iliyonyooka.” Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno hilo limetumiwa tu katika himizo la Paulo kwa Timotheo. Neno hilohilo linaweza kutumiwa kufafanua jinsi ya kukata mtaro ulionyooka kutoka upande mmoja wa shamba hadi mwingine. Bila shaka, mkulima mwenye uzoefu angeona aibu kama angekata mtaro uliojipinda. Ili Timotheo awe “mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu,” alikumbushwa kwamba hangepaswa kukengeuka kutoka kwenye mafundisho ya kweli ya Neno la Mungu. Timotheo hakupaswa kuruhusu maoni yake ya kibinafsi yaathiri mafundisho yake. Mahubiri na mafundisho yake yalipaswa kutegemea kabisa Maandiko. (2 Timotheo 4:2-4) Katika njia hiyo, watu wenye mioyo minyoofu wangesaidiwa kuona mambo jinsi Yehova anavyoyaona, badala ya kufuata falsafa za kilimwengu. (Wakolosai 2:4, 8) Ndivyo ilivyo leo.

      Lazima Tuwe na Mwenendo Mzuri

      11, 12. Mwenendo wetu unahusianaje na kulitumia sawasawa Neno la Mungu?

      11 Tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kulitumia sawasawa Neno la Mungu kwa kutangaza kweli zake. Lazima mwenendo wetu upatane na Neno hilo. “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu,” kwa hiyo hatupaswi kuwa wafanyakazi wanafiki. (1 Wakorintho 3:9) Neno la Mungu linasema: “Hata hivyo, je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba? Wewe, unayesema ‘Usifanye uzinzi,’ je, wewe hufanya uzinzi? Wewe, unayechukizwa na sanamu, je, wewe huiba katika mahekalu?” (Waroma 2:21, 22) Kwa hiyo, tukiwa wafanyakazi wa Mungu leo, njia moja ambayo tunaweza kulitumia Neno la Mungu sawasawa ni kwa kufuata himizo hili: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

      12 Tunaweza kutarajia matokeo gani tunapolitumia sawasawa Neno la Mungu? Fikiria uvutano wa Neno la Mungu lililoandikwa juu ya maisha ya watu wenye mioyo minyoofu.

      Neno la Mungu Lina Nguvu za Kubadili Watu

      13. Mtu anaweza kufanya mabadiliko gani anapotumia Neno la Mungu?

      13 Watu wanapokubali kwamba Neno la Mungu linategemeka, ujumbe wake unakuwa na uvutano wenye nguvu ambao huwasaidia kufanya mabadiliko makubwa maishani mwao. Paulo alikuwa ameona neno la Mungu likitenda kazi na alikuwa ameshuhudia matokeo yake mazuri juu ya wale ambao waligeuka na kuwa Wakristo katika Thesalonike la kale. Kwa hiyo, aliwaambia: “Sisi tunamshukuru Mungu pia bila kuacha, kwa sababu mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu, ambalo pia linafanya kazi ndani yenu waamini.” (1 Wathesalonike 2:13) Wakristo hao na pia wafuasi wote wa kweli wa Kristo, wanajua kwamba akili ndogo ya mwanadamu haiwezi kulinganishwa na hekima ya juu ya Mungu. (Isaya 55:9) Wathesalonike ‘walilipokea neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu,’ wakawa vielelezo kwa waamini wengine.—1 Wathesalonike 1:5-7.

      14, 15. Ujumbe wa Neno la Mungu una nguvu kadiri gani, na kwa nini?

      14 Neno la Mungu lina nguvu kama Yehova, aliye Chanzo chake. Linatoka kwa “Mungu aliye hai,” ambaye kwa neno lake “mbingu zilifanywa,” na sikuzote neno hilo ‘hufanikiwa katika yale ambayo limetumwa.’ (Waebrania 3:12; Zaburi 33:6; Isaya 55:11) Msomi mmoja wa Biblia alisema: “Mungu hajitengi na Neno lake. Halikani kana kwamba halihusiani naye. . . . Kwa hiyo, sikuzote li hai, na kamwe halikosi kuwa na matokeo linapotamkwa; kwa kuwa linatuunganisha na Mungu aliye hai.”

      15 Ujumbe wa Neno la Mungu una nguvu kadiri gani? Una nguvu nyingi sana. Kwa kufaa, Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.”—Waebrania 4:12.

      16. Neno la Mungu linawezaje kumbadili mtu kikamili?

      16 Ujumbe wa Neno la Mungu lililoandikwa ni ‘wenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili.’ Kwa hiyo, una nguvu nyingi sana zinazopenya zaidi kuliko kifaa chochote cha mwanadamu. Neno la Mungu huchoma sehemu za ndani kabisa za mtu nalo linaweza kumbadili kindani, kuwa na uvutano kuhusu jinsi anavyofikiri na mambo anayopenda, na kumfanya awe mfanyakazi anayemwogopa Mungu na mwenye kukubalika. Neno hilo lina nguvu kama nini!

      17. Eleza jinsi nguvu za Neno la Mungu zinavyobadili watu.

      17 Neno la Mungu hufunua jinsi mtu alivyo kindani kinyume na anavyofikiri alivyo au jinsi anavyotaka wengine wamwone. (1 Samweli 16:7) Wakati mwingine, hata mtu mwovu anaweza kuficha jinsi alivyo kindani kwa kujifanya kuwa mwenye fadhili au mwenye kumcha Mungu. Waovu hutenda kwa unafiki wakiwa na nia mbaya. Watu wenye kiburi hujifanya kuwa wanyenyekevu huku wakitamani kusifiwa na watu. Hata hivyo, kwa kufunua waziwazi yaliyo moyoni, Neno la Mungu linaweza kumchochea kwa nguvu mtu mnyenyekevu avue utu wa kale na “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Waefeso 4:22-24) Mafundisho ya Neno la Mungu yanaweza pia kumbadili mtu mwenye haya akawa Shahidi wa Yehova mwenye ujasiri na mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii.—Yeremia 1:6-9.

      18, 19. Ukitumia habari iliyo kwenye mafungu haya au jambo ulilojionea katika utumishi wa shambani, eleza jinsi kweli ya Biblia inavyoweza kubadili mtazamo wa mtu.

      18 Nguvu za Neno la Mungu za kubadili watu zina matokeo mazuri juu ya watu kila mahali. Kwa mfano, watangazaji wa Ufalme kutoka Phnom Penh, Kambodia, walihubiri mkoa wa Kompong Cham mara mbili kwa mwezi. Baada ya kusikia makasisi wengine wakiongea vibaya kuhusu Mashahidi wa Yehova, kasisi mmoja mwanamke ambaye ni mwenyeji, alipanga kukutana na Mashahidi hao wakati ambapo wangetembelea tena mkoa huo. Aliwarushia maswali mengi kuhusu kusherehekea sikukuu naye alisikiliza kwa makini walipojadiliana naye wakitumia Maandiko. Kisha akasema: “Sasa ninajua yale ambayo makasisi wenzangu walisema kuwahusu si ya kweli! Walidai kwamba hamtumii Biblia, lakini ninyi mmeitumia asubuhi yote!”

      19 Mwanamke huyo aliendelea kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na Mashahidi na hakuruhusu vitisho vya kuachishwa ukasisi vimzuie. Alimweleza rafiki yake kuhusu mazungumzo hayo ya Biblia, naye pia akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Rafiki huyo alifurahia sana mambo aliyokuwa akijifunza hivi kwamba kwenye mojawapo ya ibada za kanisa analohudhuria, alichochewa kusema, “Njooni, mjifunze Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova!” Muda mfupi baadaye, mwanamke huyo aliyekuwa kasisi, na pia wengineo walianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.

      20. Kisa cha mwanamke fulani anayeishi nchini Ghana kinaonyeshaje nguvu za Neno la Mungu?

      20 Kisa cha Paulina, mwanamke anayeishi nchini Ghana, kinaonyesha pia jinsi Neno la Mungu lilivyo na nguvu. Mtangazaji mmoja wa Ufalme wa wakati wote alijifunza Biblia pamoja naye akitumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele.a Paulina alikuwa katika ndoa ya wake wengi naye aliona uhitaji wa kufanya mabadiliko, lakini mume wake na watu wake wote wa ukoo wakampinga vikali. Babu yake, ambaye ni jaji wa mahakama kuu na mzee wa kanisa, alijaribu kumzuia kwa kutumia vibaya andiko la Mathayo 19:4-6. Jaji huyo alizungumza kwa mamlaka, lakini Paulina akatambua mara moja kwamba hivyo ndivyo Shetani alivyopotosha Maandiko alipomjaribu Yesu Kristo. (Mathayo 4:5-7) Alikumbuka jinsi Yesu alivyozungumza waziwazi kuhusu ndoa, aliposema kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa mwanamume na mwanamke, si mwanamume na wanawake, na kwamba hao wawili, wala na si watatu wangekuwa mwili mmoja. Alishikilia uamuzi wake na mwishowe, kulingana na desturi za kwao, akapewa talaka kutokana na ndoa hiyo ya wake wengi. Muda mfupi baadaye, alikuwa mtangazaji wa Ufalme aliyebatizwa mwenye furaha.

      Endelea Kulitumia Sawasawa Neno la Mungu

      21, 22. (a) Tunataka kuazimia kufanya nini tukiwa watangazaji wa Ufalme? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

      21 Kwa kweli, Neno la Mungu lililoandikwa ni kifaa chenye nguvu tunachoweza kutumia kuwasaidia wengine wafanye mabadiliko maishani mwao ili wamkaribie Yehova. (Yakobo 4:8) Kama vile wafanyakazi stadi hutumia vifaa ili kupata matokeo mazuri, na tuazimie kujitahidi kutumia kwa ustadi Neno la Mungu, Biblia, katika kazi yetu tuliyopewa na Mungu tukiwa watangazaji wa Ufalme.

      22 Tunawezaje kutumia Maandiko kwa njia yenye matokeo zaidi katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi? Njia moja ni kusitawisha uwezo mbalimbali tukiwa walimu wenye kusadikisha. Tafadhali kazia fikira makala inayofuata, kwa kuwa inadokeza njia mbalimbali za kufundisha na kuwasaidia wengine waukubali ujumbe wa Ufalme.

  • Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 15
    • Wasaidie Wengine Wakubali Ujumbe wa Ufalme

      “Agripa akamwambia Paulo: ‘Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.’”—MATENDO 26:28.

      1, 2. Kwa nini mtume Paulo alisimama mbele ya Gavana Festo na Mfalme Agripa wa Pili?

      KATIKA mwaka wa 58 W.K., Mfalme Herode Agripa wa Pili na dada yake Bernike walimtembelea Gavana Mroma, Porkio Festo, huko Kaisaria. Walikuwa wamealikwa na Gavana huyo, nao ‘wakaingia kwa fahari nyingi katika chumba cha baraza pamoja na viongozi wa kijeshi na vilevile wanaume waheshimiwa katika jiji.’ Ndipo Festo akaamuru mtume Mkristo Paulo aletwe mbele zao. Kwa nini mfuasi huyo wa Yesu Kristo alisimama mbele ya kiti cha hukumu cha Gavana Festo?—Matendo 25:13-23.

      2 Mambo ambayo Festo aliwaeleza wageni wake yanajibu swali hilo. Alisema: “Mfalme Agripa na ninyi wanaume wote mliopo pamoja nasi, ninyi mnaona mtu huyu ambaye kuhusu yeye umati wote wa Wayahudi ukiwa pamoja umepeleka ombi kwangu katika Yerusalemu na hapa pia, ukipaaza sauti kwamba hapaswi kuishi tena kamwe. Lakini mimi nikaona hakuwa amefanya jambo lolote linalostahili kifo. Kwa hiyo mwanamume huyu mwenyewe alipokata rufani kwa Mheshimiwa, niliamua kumpeleka. Lakini kuhusu yeye sina jambo hakika la kumwandikia Bwana wangu. Kwa hiyo nikamleta mbele yenu, na hasa mbele yako wewe, Mfalme Agripa, ili, baada ya kumhoji kihukumu, nipate jambo fulani la kuandika. Kwa maana linaonekana kuwa jambo lisilo la akili kwangu kumpeleka mfungwa bila kuonyesha mashtaka juu yake.”—Matendo 25:24-27.

      3. Kwa nini viongozi wa kidini walimshtaki Paulo?

      3 Maneno ya Festo yanaonyesha kwamba Paulo alikuwa ameshtakiwa kwa uwongo kwamba alikuwa mchochezi, kosa ambalo lilistahili hukumu ya kifo. (Matendo 25:11) Lakini Paulo hakuwa na hatia. Mashtaka hayo yalitokana na wivu wa viongozi wa kidini wa Yerusalemu. Walipinga kazi ya Paulo ya kutangaza Ufalme nao walichukizwa sana kuona kwamba aliwasaidia wengine wawe wafuasi wa Yesu Kristo. Chini ya ulinzi mkali, Paulo alisafirishwa kutoka Yerusalemu hadi jiji la bandarini la Kaisaria, ambako alikata rufani kwa Kaisari. Kutoka hapo angepelekwa Roma.

      4. Mfalme Agripa alisema maneno gani yenye kushangaza?

      4 Wazia Paulo akiwa katika jumba la gavana mbele ya watu ambao walitia ndani mtawala wa eneo muhimu la Miliki ya Roma. Mfalme Agripa anamgeukia Paulo na kusema: “Unaruhusiwa kujitetea.” Paulo anapozungumza, jambo la kustaajabisha linatukia. Mfalme anaanza kuguswa moyo na mambo ambayo Paulo anasema. Naam, Mfalme Agripa anasema: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.”—Matendo 26:1-28.

      5. Kwa nini maneno ya Paulo kwa Agripa yalikuwa yenye matokeo sana?

      5 Hebu wazia! Kwa sababu Paulo alijitetea kwa njia ya ustadi, mtawala huyo aliguswa moyo na nguvu zenye kupenya za Neno la Mungu. (Waebrania 4:12) Kwa nini njia ya Paulo ya kujitetea ilikuwa yenye matokeo sana? Nasi tunaweza kujifunza jambo gani kutoka kwa Paulo ambalo linaweza kutusaidia katika kazi yetu ya kufanya wanafunzi? Tunapochanganua njia yake ya kujitetea, mambo mawili makuu yanadhihirika: (1) Paulo alikuwa mwenye ushawishi katika mazungumzo yake. (2) Alitumia ujuzi wake wa Neno la Mungu kwa ustadi, kama vile msanii hutumia kifaa fulani kwa njia yenye matokeo.

      Tumia Ustadi wa Kushawishi

      6, 7. (a) Neno “ushawishi” linamaanisha nini kama linavyotumiwa katika Biblia? (b) Ushawishi ni muhimu kadiri gani katika kuwasaidia wengine wakubali mafundisho ya Biblia?

      6 Katika kitabu cha Matendo, maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa ushawishi yametumiwa mara nyingi kumhusu Paulo. Kutumia ushawishi kunahusianaje na kazi yetu ya kufanya wanafunzi?

      7 Katika lugha ya awali ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno “shawishi” linamaanisha “kusadikisha” au kumfanya mtu “abadili maoni yake kwa kujadiliana naye au kwa kuchunguza pamoja naye kanuni za maadili,” chasema kichapo Expository Dictionary of New Testament Words cha Vine. Tunaelewa zaidi maana ya neno hilo tunapochunguza maana ya msingi. Maana hiyo ya msingi inatoa wazo la kumtumaini mtu. Kwa hiyo ukimshawishi mtu akubali fundisho fulani la Biblia, umemsadikisha akutumaini, na hivyo aamini kwamba fundisho hilo ni la kweli. Bila shaka, haitoshi tu kumweleza mtu yale ambayo Biblia husema ili aiamini na kutenda kupatana nayo. Lazima msikilizaji wako asadiki kwamba yale unayosema ni ya kweli, hata kama yeye ni mtoto, jirani, mfanyakazi mwenzako, mwanafunzi mwenzako, au mtu wa ukoo.—2 Timotheo 3:14, 15.

      8. Ni nini kinachohusika katika kumsadikisha mtu ukweli fulani wa Biblia?

      8 Unawezaje kumsadikisha mtu kwamba yale unayosema kutoka katika Neno la Mungu ni kweli? Paulo alijitahidi kubadili maoni ya watu aliozungumza nao kwa kujadiliana nao kupatana na akili, kutoa hoja zinazofaa, na kuwasihi kwa bidii.a Kwa hiyo, badala tu ya kusema kwamba jambo fulani ni kweli, unahitaji kutoa uthibitisho wenye kuridhisha kuunga mkono maneno yako. Unawezaje kufanya hivyo? Hakikisha kwamba maneno yako yanategemea kabisa Neno la Mungu wala si maoni yako mwenyewe. Pia, toa uthibitisho zaidi ili kuunga mkono maneno yako ya kutoka moyoni yanayotegemea Biblia. (Methali 16:23) Kwa mfano, ukisema kwamba wanadamu watiifu watafurahia maisha katika dunia paradiso, tumia Maandiko kama vile Luka 23:43 au Isaya 65:21-25 kuunga mkono maneno hayo. Unawezaje kutoa uthibitisho zaidi ili kuunga mkono hoja yako ya Kimaandiko? Unaweza kutumia mifano inayotegemea mambo ambayo yamempata msikilizaji wako. Unaweza kumkumbusha mambo fulani madogo anayofurahia bila malipo yoyote, kama vile machweo ya jua yenye kupendeza, harufu nzuri ya ua, ladha nzuri ya tunda, au furaha unayopata kwa kumtazama ndege akilisha makinda yake. Msaidie aone kwamba mambo hayo yenye kufurahisha yanathibitisha kwamba Muumba wetu anataka tufurahie maisha duniani.—Mhubiri 3:11, 12.

      9. Tunawezaje kuonyesha busara tunapohubiri?

      9 Unapojaribu kumshawishi mtu akubali fundisho fulani la Biblia, jihadhari shauku yako isifanye uonekane kama unashikilia maoni yako tu, na hivyo kutofikia akili na moyo wa msikilizaji wako. Kitabu Shule ya Huduma kinatoa tahadhari hii: ‘Kwa kawaida ukifichua kwa dharau fundisho fulani la uwongo ambalo mtu anapenda sana, mtu huyo hatakubali kweli hata umsomee Maandiko mangapi. Kwa mfano, ukishutumu tu sherehe zinazopendwa kwamba ni za kipagani, huenda watu wasibadili maoni yao kuzihusu. Kwa kawaida unaweza kufanikiwa kwa kujadiliana nao.’ Kwa nini ujitahidi sana kuwa mwenye busara? Kitabu hicho kinasema: ‘Kujadiliana hufanya watu wachangie mazungumzo, huwasaidia kufikiria mambo hayo baadaye, na kuwafanya waweze kusikiliza wakati ujao. Kusababu kunaweza kushawishi sana.’—Wakolosai 4:6.

      Ushawishi Unaochochea Moyo

      10. Paulo alianzishaje mazungumzo yake ya kujitetea mbele ya Agripa?

      10 Sasa na tuchunguze kwa makini maneno ambayo Paulo alitumia kujitetea katika Matendo sura ya 26. Ona jinsi alivyoanza mazungumzo yake. Katika utangulizi wake, Paulo alitafuta sababu nzuri ya kumpongeza Agripa, hata ingawa mfalme huyo alikuwa na uhusiano wenye aibu pamoja na dada yake Bernike. Paulo alisema: “Kuhusu mambo yote ninayoshtakiwa na Wayahudi, Mfalme Agripa, ninajihesabu mwenyewe kuwa mwenye furaha kwamba ninajitetea mbele yako leo, hasa kwa kuwa wewe una ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kwa hiyo ninakuomba unisikie kwa subira.”—Matendo 26:2, 3.

      11. Maneno ya Paulo kwa Agripa yalionyeshaje heshima, nayo yalikuwa na manufaa gani?

      11 Je, umeona kwamba Paulo alitambua cheo cha juu cha Agripa kwa kumwita Mfalme, jina lake la cheo? Kwa kufanya hivyo na pia kwa kuchagua maneno yake kwa hekima, Paulo alimwonyesha Agripa heshima. (1 Petro 2:17) Mtume huyo alikiri kwamba Agripa alijua desturi na sheria za raia zake Wayahudi ambazo zilikuwa ngumu kueleweka, na kusema kwamba alikuwa mwenye furaha kwa kuwa aliweza kujitetea mbele ya mtawala kama huyo mwenye ujuzi. Paulo, aliyekuwa Mkristo, hakutenda kana kwamba alikuwa mtu bora kuliko Agripa ambaye hakuwa Mkristo. (Wafilipi 2:3) Badala yake, Paulo alimwomba mfalme huyo amsikilize kwa subira. Hivyo, Paulo akatokeza hali ambayo yaelekea ingemfanya Agripa, na pia wasikilizaji wengine, wakubali mambo aliyotaka kusema. Alikuwa anaweka msingi wa kutegemeza hoja zake kwa kuzungumzia mambo ambayo wote walikubaliana.

      12. Tunawezaje kuchochea mioyo ya wasikilizaji wetu tunapofanya kazi ya kutangaza Ufalme?

      12 Acheni tuchochee mioyo ya wasikilizaji wetu tangu mwanzo hadi mwisho wa mazungumzo yetu kuhusu ujumbe wa Ufalme kama vile Paulo alivyofanya mbele ya Agripa. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuonyesha tunamheshimu kikweli mtu tunayemhubiria na kwamba tunapendezwa kikweli na malezi na maoni yake.—1 Wakorintho 9:20-23.

      Tumia Neno la Mungu kwa Ustadi

      13. Unawezaje kuwachochea wasikilizaji wako kama Paulo?

      13 Paulo alitamani kuwachochea wasikilizaji wake watende kupatana na habari njema. (1 Wathesalonike 1:5-7) Ili kutimiza hilo, aliuchochea moyo wao wa mfano ambao ni chanzo cha msukumo wa kutenda. Tunapochunguza zaidi namna Paulo alivyojitetea mbele ya Agripa, ona jinsi Paulo ‘alivyotumia neno la Mungu sawasawa’ kwa kurejelea mambo yaliyosemwa na Musa na manabii.—2 Timotheo 2:15.

      14. Eleza jinsi Paulo alivyotumia ushawishi alipokuwa mbele ya Agripa.

      14 Paulo alijua kwamba Agripa alikuwa Myahudi kwa jina tu. Alitaja ujuzi wa Agripa kuhusu Dini ya Kiyahudi na kusema kwamba mahubiri yake yalihusu hasa ‘kutosema lolote ila mambo ambayo Manabii na vilevile Musa walisema yatatukia’ kuhusu kifo na ufufuo wa Masihi. (Matendo 26:22, 23) Akizungumza na Agripa moja kwa moja, Paulo aliuliza: “Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii?” Agripa alitatanika. Kama angesema kwamba hakuwaamini manabii, sifa yake akiwa mwamini Myahudi ingeharibika. Na kama angekubaliana na hoja ya Paulo, angekuwa anakiri hadharani kwamba anakubaliana na maoni ya mtume huyo na hivyo kuitwa Mkristo, jambo ambalo lilikuwa hatari. Paulo alijibu swali lake mwenyewe kwa hekima, akisema: “Ninajua unawaamini.” Moyo wa Agripa ulimchochea kujibuje? Alijibu: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Matendo 26:27, 28) Ingawa Agripa hakupata kuwa Mkristo, ni wazi kwamba Paulo alimgusa moyo kwa kadiri fulani kwa ujumbe wake.—Waebrania 4:12.

      15. Paulo aliwezaje kuanzisha kutaniko huko Thesalonike?

      15 Je, umeona kwamba mazungumzo ya Paulo kuhusu habari njema yalihusisha kutangaza ujumbe na kushawishi? Kwa kuwa Paulo alitumia njia hiyo ‘alipolitumia neno la Mungu sawasawa,’ baadhi ya watu waliomsikiliza waliacha kuwa wasikilizaji tu na wakawa waamini. Hivyo ndivyo ilivyotukia huko Thesalonike ambako Paulo alitafuta katika sinagogi Wayahudi na watu wa mataifa waliomwogopa Mungu. Andiko la Matendo 17:2-4 linasema: “Kulingana na desturi ya Paulo akaingia ndani walimokuwa, na kwa sabato tatu akajadiliana nao kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu . . . Ikawa kwamba baadhi yao wakawa waamini.” Paulo alikuwa mwenye kushawishi. Alitoa hoja, akaeleza, na kuthibitisha kupitia Maandiko kwamba Yesu ndiye Masihi aliyekuwa ameahidiwa kwa muda mrefu. Ikawaje? Kutaniko la waamini lilianzishwa.

      16. Unawezaje kupata furaha kubwa zaidi katika kuhubiri juu ya Ufalme?

      16 Je, unaweza kuwa mwenye ustadi zaidi katika kushawishi unapofafanua Neno la Mungu? Ikiwa ndivyo, utapata uradhi na furaha zaidi katika kazi yako ya kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. Wahubiri wa habari njema wamepata uradhi na furaha zaidi kwa kufuata madokezo ya kuitumia Biblia zaidi katika kazi ya kuhubiri.

      17. Ili kuonyesha manufaa ya kutumia Biblia katika huduma, simulia jambo ulilojionea au uonyeshe umuhimu wa kufanya hivyo kama inavyoonyeshwa katika fungu hili.

      17 Kwa mfano, mwangalizi mmoja asafiriye wa Mashahidi wa Yehova aliandika hivi: “Sasa ndugu na dada wengi hubeba Biblia mkononi wanapohubiri nyumba kwa nyumba. Kufanya hivyo kumewasaidia wahubiri kuwasomea andiko fulani baadhi ya watu wengi wanaokutana nao. Kumemsaidia mwenye nyumba na pia mhubiri kuihusianisha huduma yetu na Biblia, wala si magazeti na vitabu tu.” Bila shaka, kubeba Biblia mkononi tunapohubiri kunategemea mambo kadhaa, kutia ndani desturi za eneo tunalohubiri. Hata hivyo, tunahitaji kutamani kuwa na sifa ya kutumia Neno la Mungu kwa ustadi ili kushawishi wengine wakubali ujumbe wa Ufalme.

      Uwe na Maoni ya Mungu Kuhusu Huduma

      18, 19. (a) Mungu huionaje huduma yetu, na kwa nini tusitawishe maoni kama yake? (b) Ni nini kitakachotusaidia tufanikiwe kufanya ziara za kurudia? (Ona sanduku lenye kichwa “Jinsi ya Kufanikiwa Kufanya Ziara za Kurudia,” kwenye ukurasa wa 16.)

      18 Njia nyingine ya kufikia mioyo ya wasikilizaji wetu inahusisha kuiona huduma jinsi Mungu anavyoiona na kuwa wenye subira. Mapenzi ya Mungu ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na “kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Je, sisi tuna tamaa kama hiyo? Yehova pia ni mwenye subira, na subira yake huwapatia wengi nafasi ya kufikia toba. (2 Petro 3:9) Kwa hiyo, tunapopata mtu anayetaka kusikiliza ujumbe wa Ufalme, huenda ikawa lazima kumrudia tena na tena ili kukuza upendezi huo. Inachukua muda na subira kungojea mbegu za kweli zikue. (1 Wakorintho 3:6) Sanduku lililo katika makala hii lenye kichwa, “Jinsi ya Kufanikiwa Kufanya Ziara za Kurudia” lina madokezo ya kukuza upendezi huo. Kumbuka kwamba maisha ya watu—matatizo na hali zao—hubadilika daima. Huenda ukahitaji kuwatembelea mara nyingi ili kuwapata nyumbani, lakini jitihada hizo zinafaa. Tunataka kuwapa nafasi ya kusikia ujumbe wa Mungu wa wokovu. Kwa hiyo, mwombe Yehova Mungu akupatie hekima ya kusitawisha ustadi wa ushawishi katika kazi yako ya kuwasaidia wengine waukubali ujumbe wa Ufalme.

      19 Wafanyakazi Wakristo wanaweza kufanya jambo gani jingine wanapompata mtu anayetaka kusikia mengi zaidi kuhusu ujumbe wa Ufalme? Tutapata madokezo katika makala yetu inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu ushawishi, ona somo la 48 na 49 katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • Hubiri Ili Kufanya Wanafunzi
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 15
    • Hubiri Ili Kufanya Wanafunzi

      “Prisila na Akila walipomsikia [Apolo], wakamchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.” —Matendo 18:26.

      1. Ingawa Apolo alikuwa “amewaka roho,” alihitaji nini?

      PRISILA na Akila, wenzi wa ndoa Wakristo wa karne ya kwanza, walimsikia Apolo akitoa hotuba kwenye sinagogi moja katika jiji la Efeso. Apolo alikuwa amenasa fikira za wasikilizaji wake kwa ufasaha na uwezo wake wa kushawishi. Alikuwa “amewaka roho,” naye alikuwa ‘akifundisha kwa usahihi mambo juu ya Yesu.’ Hata hivyo, ilikuwa wazi kwamba Apolo ‘alifahamu ubatizo wa Yohana tu.’ Yale ambayo Apolo alihubiri kumhusu Kristo yalikuwa ya kweli lakini hayakutosha. Tatizo lilikuwa kwamba hakuwa na ujuzi wa kutosha kumhusu Kristo. Apolo alihitaji kuongeza ujuzi wake kuhusu daraka la Yesu Kristo katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova.—Matendo 18:24-26.

      2. Prisila na Akila walikabili jambo gani gumu?

      2 Bila kukawia, Prisila na Akila walijitoa kumsaidia Apolo aweze kushika “mambo yote” ambayo Kristo aliamuru. (Mathayo 28:19, 20) Masimulizi hayo yanasema kwamba ‘walimchukua Apolo na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.’ Hata hivyo, kuna mambo fulani kumhusu Apolo ambayo yangewafanya Wakristo fulani wasite kumfundisha. Ni mambo gani hayo? Nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jitihada za Prisila na Akila za kuzungumzia Maandiko pamoja na Apolo? Kuchunguza masimulizi hayo ya zamani kunaweza kutusaidiaje kuelekeza juhudi zetu katika kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani?

      Kazia Fikira Juu ya Mahitaji ya Watu

      3. Kwa nini malezi ya Apolo hayakuwazuia Prisila na Akila wasimfundishe?

      3 Akiwa Myahudi wa asili, yaelekea kwamba Apolo alilelewa katika jiji la Aleksandria. Wakati huo Aleksandria ulikuwa mji mkuu wa Misri na kituo cha elimu ya juu, kilichokuwa mashuhuri kwa sababu ya maktaba yake kubwa. Mji huo ulikuwa na wakaaji wengi Wayahudi, kutia ndani wasomi. Hivyo, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania inayojulikana kuwa Septuagint ilitafsiriwa huko. Si ajabu kwamba Apolo alikuwa “mwenye ujuzi mwingi sana wa Maandiko”! Akila na Prisila walikuwa watengenezaji wa mahema. Je, ufasaha wa Apolo uliwaogopesha? La. Kwa upendo walimwona kama mtu tu, wakafikiria mahitaji yake, na jinsi ambavyo wangeweza kumsaidia.

      4. Apolo alipata wapi msaada aliohitaji na kwa njia gani?

      4 Hata ingawa Apolo alikuwa msemaji mwenye ufasaha sana alihitaji kufundishwa. Msaada aliohitaji haungepatikana kwenye chuo kikuu chochote bali ungepatikana miongoni mwa washiriki wenzake katika kutaniko la Kikristo. Apolo angenufaika na habari ambazo zingetokana na uelewaji sahihi zaidi wa mpango wa Mungu wa wokovu. Prisila na Akila ‘walimchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.’

      5. Hali ya kiroho ya Prisila na Akila ilikuwaje?

      5 Prisila na Akila walikuwa wenye nguvu kiroho na wenye imani thabiti. Yaelekea ‘sikuzote walikuwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye alitaka kutoka kwao sababu ya tumaini lao,’ hata kama mtu huyo alikuwa tajiri, maskini, msomi, au mtumwa. (1 Petro 3:15) Akila na mke wake waliweza ‘kulitumia sawasawa neno la kweli.’ (2 Timotheo 2:15) Ni wazi kwamba walikuwa wanafunzi wenye bidii wa Maandiko. Apolo alichochewa sana na mafundisho yaliyotegemea ‘neno la Mungu lililo hai na lenye nguvu,’ ambalo hugusa moyo.—Waebrania 4:12.

      6. Tunajuaje kwamba Apolo alithamini msaada aliopata?

      6 Apolo alithamini kielelezo cha walimu wake naye akawa mwenye ustadi zaidi katika kufanya wanafunzi. Alitumia ujuzi wake kikamili katika kazi ya kutangaza habari njema, hasa kwa Wayahudi. Apolo alisaidia kwa njia ya pekee kuwashawishi Wayahudi wamwamini Kristo. ‘Kwa kuwa alikuwa hodari katika Maandiko,’ aliweza kuwathibitishia kwamba manabii wote wa zamani walitazamia kuja kwa Kristo. (Matendo 18:24, Union Version) Masimulizi hayo yanaongeza kusema kwamba baadaye Apolo alienda Akaya, ambako ‘aliwasaidia sana wale waliokuwa wameamini kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu; kwa maana kwa juhudi nyingi alithibitisha kikamili hadharani kuwa Wayahudi ni wenye makosa, huku akionyesha kwa Maandiko kwamba Yesu alikuwa ndiye Kristo.’—Matendo 18:27, 28.

      Jifunze Kutokana na Kielelezo cha Walimu Wengine

      7. Akila na Prisila walipataje kuwa walimu stadi?

      7 Akila na Prisila walipataje kuwa walimu stadi wa Neno la Mungu? Mbali na bidii yao katika funzo la kibinafsi na kuhudhuria mikutano, bila shaka, kushirikiana kwa ukaribu na mtume Paulo kuliwasaidia sana. Paulo alikaa nyumbani kwa Prisila na Akila huko Korintho kwa miezi 18. Walifanya kazi pamoja ya kutengeneza na kurekebisha mahema. (Matendo 18:2, 3) Wazia jinsi mazungumzo yao kuhusu Maandiko yalivyokuwa yenye kina! Bila shaka, walinufaika sana kiroho kwa kushirikiana na Paulo. Andiko la Methali 13:20 linasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” Mashirika mazuri yaliwasaidia kuwa na mazoea mazuri ya kiroho.—1 Wakorintho 15:33.

      8. Prisila na Akila walijifunza nini kwa kumtazama Paulo akihubiri?

      8 Wakati Prisila na Akila walipomtazama Paulo akitangaza Ufalme, walitambua kwamba alikuwa mwalimu bora. Masimulizi katika Matendo yanasema kwamba Paulo “alikuwa akitoa hotuba katika sinagogi [huko Korintho] kila sabato na alikuwa akiwashawishi Wayahudi na Wagiriki.” Baadaye, Sila na Timotheo walipojiunga naye, Paulo ‘alianza kushughulika sana na lile neno, akiwatolea Wayahudi ushahidi ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Kristo.’ Prisila na Akila waliona kwamba Paulo alihamia nyumba iliyokuwa karibu na sinagogi ambapo watu waliitikia vizuri zaidi alipoona kwamba washiriki wa sinagogi hawakupendezwa sana na ujumbe wake. Huko Paulo aliweza kumsaidia Krispo “ofisa-msimamizi wa sinagogi,” kuwa mwanafunzi. Yaelekea Prisila na Akila walitambua kwamba kumfanya mtu huyo mmoja kuwa mwanafunzi kulikuwa na matokeo makubwa sana katika eneo hilo. Masimulizi hayo yanasema: “Krispo . . . akawa mwamini katika Bwana, na ndivyo na watu wote wa nyumba yake. Na wengi kati ya Wakorintho waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa.”—Matendo 18:4-8.

      9. Prisila na Akila walifanyaje baada ya kutazama kielelezo cha Paulo?

      9 Prisila na Akila na watangazaji wengine wa Ufalme waliiga kielelezo cha Paulo katika kuhubiri. Mtume huyo aliwahimiza hivi Wakristo wengine: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Kwa kuiga kielelezo cha Paulo, Prisila na Akila walimsaidia Apolo kuelewa mafundisho ya Kikristo kwa usahihi zaidi. Naye Apolo akawasaidia wengine. Bila shaka, Prisila na Akila walisaidia kufanya wanafunzi huko Roma, Korintho, na Efeso.—Matendo 18:1, 2, 18, 19; Waroma 16:3-5.

      10. Umejifunza mambo gani katika Matendo sura ya 18 yatakayokusaidia katika kazi ya kufanya wanafunzi?

      10 Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza Matendo sura ya 18? Kama vile yaelekea Akila na Prisila walijifunza kutoka kwa Paulo, tunaweza kuboresha uwezo wetu wa kufanya wanafunzi kwa kuiga kielelezo cha walimu wazuri wa Neno la Mungu. Tunaweza kushirikiana na wale ambao ‘hushughulika sana na lile neno’ na ambao ‘huwatolea wengine ushahidi kamili.’ (Matendo 18:5, Kingdom Interlinear Translation) Tunaweza kuchunguza jinsi wanavyoifikia mioyo ya watu kwa kufundisha kwa ustadi na kwa ushawishi. Ustadi huo unaweza kutusaidia kufanya wanafunzi. Tunapojifunza Biblia na mtu fulani, tunaweza kumwomba awaalike washiriki wengine wa familia yake au majirani wajiunge naye. Au tunaweza kumwomba atueleze ikiwa kuna wengine ambao tunaweza kujifunza Biblia pamoja nao.—Matendo 18:6-8.

      Tafuta Nafasi za Kufanya Wanafunzi

      11. Wanafunzi wapya wanaweza kupatikana wapi?

      11 Paulo na Wakristo wenzake walijitahidi kufanya wanafunzi kwa kuhubiri nyumba kwa nyumba, sokoni, na waliposafiri—naam, kila mahali. Ukiwa mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii unayetaka kufanya wanafunzi, je, unaweza kupanua utumishi wako wa shambani? Je, unaweza kutumia ifaavyo nafasi za kutafuta watu wanaostahili na kuwahubiria? Ni kwa kutumia njia gani watangazaji wa habari njema wenzetu wamepata wanafunzi? Kwanza na tuchunguze kuhubiri kwa njia ya simu.

      12-14. Ili kuonyesha manufaa ya mahubiri ya simu, simulia jambo ulilojionea au mojawapo ya mambo yaliyotajwa kwenye mafungu haya.

      12 Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba huko Brazili, Mkristo tutakayemwita Maria alimpa trakti mwanamke mmoja kijana aliyekuwa anaondoka katika jengo fulani. Maria alitumia kichwa cha trakti hiyo kama utangulizi, na kumwuliza, “Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu Biblia?” Mwanamke huyo akamjibu: “Ningependa. Lakini tatizo ni kwamba mimi ni mwalimu, na hutumia wakati wangu wote kufundisha.” Maria alimweleza kwamba wangeweza kuzungumzia habari za Biblia kupitia simu. Mwanamke huyo alimpa Maria namba yake ya simu, kisha jioni hiyohiyo akaanza kujifunza broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?a kupitia simu.

      13 Alipokuwa akihubiri kupitia simu, dada mmoja ambaye ni mhudumu wa wakati wote huko Ethiopia alishangaa alipozungumza na mwanamume mmoja na kusikia kelele fulani. Mwanamume huyo alimwomba ampigie simu baadaye. Dada huyo alipompigia simu, mwanamume huyo aliomba msamaha na kusema kwamba wakati simu hiyo ilipopigwa mara ya kwanza, yeye na mke wake walikuwa wakigombana vikali. Aliposikia hivyo, dada huyo alitumia nafasi hiyo kueleza kwamba Biblia ina mwongozo wa hekima wa kutatua matatizo ya familia. Alimwambia kwamba familia nyingi zimesaidiwa na kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Siku chache baada ya kumpelekea kitabu hicho, dada huyo alimpigia simu tena mwanamume huyo. Alisema: “Kitabu hiki kimeokoa ndoa yangu!” Mwanamume huyo alifanya mkutano na familia yake na kuieleza mambo mazuri aliyokuwa amesoma katika kitabu hicho. Baada ya muda mfupi, funzo la Biblia la nyumbani lilianzishwa, na mtu huyo akaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida.

      14 Mtangazaji mmoja wa Ufalme huko Denmark ambaye alianzisha funzo la Biblia kwa kuhubiri kupitia simu anasema: “Mwangalizi wa utumishi alinitia moyo nishiriki katika mahubiri ya kutumia simu. Mwanzoni nilisita nikisema: ‘Sipendelei mahubiri hayo.’ Hata hivyo, siku moja nilipiga moyo konde na nikampigia simu mwenye-nyumba wa kwanza. Sonja alijibu simu hiyo, na baada ya mazungumzo mafupi akakubali vichapo vinavyozungumzia Biblia. Jioni moja tulizungumza kuhusu uumbaji, na mwanamke huyo akataka kusoma kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation.b Nilimwambia kwamba ingekuwa vema kama tungekutana uso kwa uso na kuzungumzia habari hiyo. Alikubali. Nilipofika, Sonja alikuwa tayari kujifunza na tangu wakati huo tumekuwa tukijifunza kila juma.” Dada yetu Mkristo anamalizia: “Nilikuwa nimesali kwa miaka mingi ili nipate funzo la Biblia, lakini sikutazamia kupata funzo kupitia mahubiri ya simu.”

      15, 16. Unaweza kusimulia mambo gani yaliyoonwa ili kuonyesha manufaa ya kuwa macho kutumia njia mbalimbali za kuanzisha mafunzo ya Biblia?

      15 Wengi wanapata mafanikio kwa sababu ya kutumia madokezo ya kuhubiria watu mahali popote wanapopatikana. Mwanamke mmoja Mkristo huko Marekani alisimamisha gari lake karibu na gari la biashara kwenye sehemu ya kuegesha magari. Mwanamke aliyekuwa ndani ya gari hilo alipomwona, dada huyo alimweleza kuhusu kazi yetu ya kufundisha watu Biblia. Mwanamke huyo alisikiliza, akatoka nje ya gari, na kukaribia gari la dada huyo. Kisha akasema: “Nimefurahi sana kwamba umeegesha gari lako ili kuzungumza nami. Kwa muda mrefu sijapokea vichapo vyenu vinavyozungumzia Biblia. Isitoshe, ningependa kujifunza Biblia tena. Je, utajifunza pamoja nami?” Kwa hiyo, dada yetu alitafuta nafasi inayofaa ya kuhubiri habari njema.

      16 Dada mmoja huko Marekani anasimulia jinsi alivyofanya alipotembelea hospitali moja ya kibinafsi: Alizungumza na mkurugenzi aliyesimamia kazi fulani katika hospitali hiyo na kumwambia kwamba angependa kujitolea kusaidia kutimiza mahitaji ya kiroho ya watu walioishi huko. Dada yetu aliongeza kusema kwamba angependa kujifunza Biblia kila juma bila malipo pamoja na wote waliotaka kuhudhuria funzo hilo. Mkurugenzi huyo alimpa ruhusa ya kutembelea vyumba vya wakaaji mbalimbali. Baada ya muda mfupi, alikuwa akiongoza funzo la Biblia mara tatu kwa juma pamoja na wakaaji 26, na mmoja wao anahudhuria mikutano yetu kwa ukawaida.

      17. Ni njia gani ambayo mara nyingi inakuwa na matokeo katika kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani?

      17 Watangazaji fulani wa Ufalme hupata matokeo mazuri kwa kuanzisha funzo la Biblia moja kwa moja. Asubuhi moja, kutaniko lenye wahubiri 105 walifanya jitihada ya pekee ili kumtolea kila mwenye nyumba waliyekutana naye nafasi ya kujifunza Biblia. Wahubiri 86 walishiriki katika kazi ya kuhubiri, na baada ya kuhubiri kwa muda wa saa mbili, walianzisha mafunzo mapya ya Biblia yapatayo 15.

      Endelea Kuwatafuta Wanaostahili

      18, 19. Tunapaswa kukumbuka agizo gani muhimu la Yesu, na tunapaswa kuazimia kufanya nini ili kulitimiza?

      18 Ukiwa mtangazaji wa Ufalme, huenda ukataka kujaribu kutumia madokezo yaliyotajwa katika makala hii. Bila shaka, lingekuwa jambo la hekima kuzingatia desturi za kwenu unapofikiria njia za kuhubiri. Zaidi ya yote, na tukumbuke agizo la Yesu la kutafuta wanaostahili na kuwasaidia wawe wanafunzi.—Mathayo 10:11; 28:19.

      19 Ili kutimiza kusudi hilo, na ‘tulitumie sawasawa neno la kweli.’ Tunaweza kufanya hivyo kwa kutumia ushawishi unaotegemea kabisa Maandiko. Hilo litatusaidia kufikia mioyo ya wenye kusikiliza na kuwachochea kutenda. Tunapomtegemea Yehova katika sala, tunaweza kushiriki katika kuwasaidia wengine wawe wanafunzi wa Yesu Kristo. Kazi hiyo inathawabisha sana. Kwa hiyo, acheni ‘tufanye yote tuwezayo ili tujitoe kwa Mungu tukiwa watu waliokubaliwa,’ sikuzote tukimheshimu Yehova tukiwa watangazaji wa Ufalme wenye bidii, ambao huhubiri wakiwa na kusudi la kufanya wanafunzi.—2 Timotheo 2:15.

      [Maelezo ya Chini]

      a Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      b Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki