Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wahudumu wa Habari Njema
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • kuonyesha imani yake kwa kuwahubiria wengine habari njema, anaweza kusaidiwaje?

      14 Ni vizuri wazazi wazungumze na mmoja wa wazee wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ili kuona ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri. Mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili (mmoja wao akiwa mshiriki wa halmashauri ya utumishi) wakutane na mtoto huyo na mzazi mmoja au wote wawili ambao ni waamini, au mlezi wake. Ikiwa mtoto ana ujuzi wa msingi wa kweli za Biblia na anaonyesha wazi kwamba anataka kushiriki katika utumishi, jambo hilo litathibitisha kwamba amefanya maendeleo. Baada ya kufikiria mambo hayo na mengine yanayowahusu watu wazima, wazee hao wanaweza kuamua ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. (Luka 6:45; Rom. 10:10) Wanapokutana na mtoto, hakuna haja ya kuzungumzia baadhi ya mambo ambayo kwa kawaida yanawahusu watu wazima tu.

      15 Wakati wa mazungumzo, wazee wanapaswa kumpongeza mtoto kwa maendeleo yake na kumtia moyo ajitahidi kufikia ubatizo. Kwa kuwa wazazi wamejitahidi kumfundisha mtoto wao kweli, wao pia wanastahili kupongezwa. Ili kuwasaidia wazazi kumsaidia zaidi mtoto wao, wazee wanapaswa kuwaonyesha habari yenye kichwa “Ujumbe kwa Wazazi Wakristo,” kwenye ukurasa wa 179-181.

      WAKFU NA UBATIZO

      16 Ikiwa umemjua na kumpenda Yehova kwa kupatanisha maisha yako na matakwa yake na kwa kushiriki katika huduma ya shambani, unahitaji kuimarisha uhusiano wako pamoja naye. Jinsi gani? Kwa kujiweka wakfu kwake na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji.—Mt. 28:19, 20.

      17 Kuweka wakfu humaanisha kutenga kwa ajili ya kusudi takatifu. Kujiweka wakfu kwa Mungu kunamaanisha kusali kwake na kumwahidi kwamba utatumia maisha yako kumtumikia na kutembea katika njia zake. Humaanisha kumwabudu yeye peke yake milele. (Kum. 5:9) Hilo ni jambo la kibinafsi unalofanya faraghani. Hakuna mtu anayeweza kufanya hivyo kwa niaba yako.

      18 Hata hivyo, haitoshi tu kumwambia Yehova faraghani kwamba unataka kuwa mali yake. Unahitaji kuwaonyesha wengine kwamba umejiweka wakfu kwa Mungu. Unafanya hivyo kwa kubatizwa katika maji, kama Yesu alivyofanya. (1 Pet. 2:21; 3:21) Ikiwa umeamua kumtumikia Yehova na unataka kubatizwa, unapaswa kufanya nini? Unapaswa kumwambia mratibu wa baraza la wazee. Atapanga wazee kadhaa wazungumze nawe ili kuhakikisha kwamba unatimiza matakwa ya Mungu kwa ajili ya wale wanaotaka kubatizwa. Kwa habari zaidi, tafadhali soma “Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa,” kwenye ukurasa wa 182-184 wa kitabu hiki na “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” kwenye ukurasa wa 185-207.

      RIPOTI YA MAENDELEO YA HUDUMA

      19 Kwa miaka mingi, ripoti za maendeleo ya ibada safi ulimwenguni pote zimewatia moyo watu wa Yehova. Tangu Yesu Kristo alipowaambia wanafunzi wake kwamba habari njema ingehubiriwa duniani kote, Wakristo wa kweli wametamani sana kujua jinsi ambavyo kazi hiyo ingetimizwa.—Mt. 28:19, 20; Marko 13:10; Mdo. 1:8.

      20 Wafuasi wa Yesu walifurahia kusikiliza ripoti za maendeleo ya kazi ya kuhubiri. (Marko 6:30) Kitabu cha Biblia cha Matendo kinatuambia kwamba kulikuwa na watu 120 hivi roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Muda mfupi baadaye idadi ya wanafunzi iliongezeka hadi 3,000 hivi, kisha 5,000 hivi. Iliripotiwa kwamba ‘Yehova aliendelea kuwaongezea kila siku watu waliokuwa wakiokolewa’ na kwamba “umati mkubwa wa makuhani wakawa waamini.” (Mdo. 1:15; 2:5-11, 41, 47; 4:4; 6:7) Habari hizo za ongezeko ziliwatia moyo sana wanafunzi! Ripoti hizo zenye kusisimua ziliwachochea kuendelea kufanya kazi waliyopewa na Mungu, licha ya mateso makali yaliyoanzishwa na viongozi wa dini ya Kiyahudi!

      21 Karibu mwaka wa 60 na 61 W.K., Paulo katika barua yake kwa Wakolosai aliandika kwamba habari njema ilikuwa ikizaa “matunda na kuongezeka ulimwenguni kote” na “ilihubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.” (Kol. 1:5, 6, 23) Wakristo wa karne ya kwanza walitii Neno, na roho takatifu iliwatia nguvu kutimiza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kabla ya mfumo wa mambo wa Kiyahudi kufikia mwisho wake mwaka wa 70 W.K. Wakristo hao waaminifu walitiwa moyo kwelikweli kusikia ripoti za matokeo ya kazi hiyo!

      Je, unajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja?

      22 Vivyo hivyo, tengenezo la Yehova la kisasa hujitahidi kuweka rekodi sahihi za kazi inayofanywa ili kutimiza Mathayo 24:14 inayosema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna kazi inayopaswa kufanywa haraka. Kila mmoja wetu anapaswa ajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja. Yehova atahakikisha kwamba kazi hiyo inakamilika, na tukishiriki kuifanya, tutapata kibali chake.—Eze. 3:18-21.

      RIPOTI YAKO YA UTUMISHI WA SHAMBANI

      23 Tunapaswa kuripoti nini? Fomu ya Ripoti ya Utumishi wa Shambani inayochapishwa na tengenezo ina mambo yanayopaswa kuripotiwa. Hata hivyo, maelezo na ufafanuzi ufuatao, utakusaidia sana.

      24 Katika safu ya “Machapisho (Yaliyochapishwa na ya Kielektroniki),” andika jumla ya machapisho yote iwe ni yaliyochapishwa au ya kielektroniki uliyowapa watu ambao si Mashahidi waliobatizwa. Katika safu ya “Video Ambazo Zilionyeshwa” andika jumla ya video zote ambazo ulionyesha.

      25 Unaporipoti “Ziara za Kurudia,” jumlisha ziara zote za kurudia ulizofanya kwa kusudi la kuchochea upendezi ulioonyeshwa na mtu ambaye si Shahidi aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Ziara ya kurudia inaweza kufanywa kwa kumtembelea mtu kibinafsi, kwa kuandika barua, kupiga simu, kutuma ujumbe kupitia simu au barua pepe, au kumpelekea chapisho fulani. Kila mara unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani, unaweza kuhesabu ziara ya kurudia. Mzazi anaweza kuhesabu ziara moja ya kurudia kila juma anapoongoza ibada ya familia ikiwa kuna mtoto ambaye hajabatizwa.

      26 Ingawa funzo la Biblia huongozwa kila juma, huripotiwa kama funzo moja tu kwa mwezi. Wahubiri wanapaswa kuandika idadi ya mafunzo ya Biblia yaliyoongozwa katika mwezi. Mafunzo ya Biblia ambayo yanaweza kuripotiwa yanatia ndani watu wote ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Unaweza kuhesabu funzo la Biblia unapojifunza na ndugu au dada asiyetenda unapoombwa na mshiriki wa halmashauri ya utumishi au unapojifunza na mhubiri aliyebatizwa karibuni ambaye hajamaliza kitabu Furahia Maisha Milele!

      27 Ni muhimu kutoa ripoti sahihi ya “Saa.” Kwa kawaida huo ni muda unaotumia unapohubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, unapofanya ziara za kurudia, unapoongoza mafunzo ya Biblia, au unapowahubiria rasmi au isivyo rasmi watu ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Wahubiri wawili wanapohubiri pamoja, wote wanaweza kuhesabu saa, lakini mmoja tu ndiye atakayehesabu ziara ya kurudia au funzo la Biblia litakaloongozwa. Wazazi wawili wanaoshirikiana kuwafundisha watoto wao wakati wa Ibada ya Familia wanaweza kuhesabu saa moja kwa juma. Ndugu wanaweza kuhesabu muda wanaotumia kutoa hotuba za watu wote. Mkalimani wa hotuba ya watu wote anaweza pia kuhesabu muda huo. Muda unaotumiwa kwa shughuli nyingine muhimu kama vile, kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani, kuhudhuria mkutano wa utumishi, shughuli za kibinafsi wakati wa utumishi, na kadhalika hauhesabiwi.

      28 Kila mhubiri atatumia dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kusali na kuamua muda aliotumia kutoa ushahidi. Baadhi ya wahubiri wanahubiri katika maeneo yenye watu wengi, na wengine huhubiri katika maeneo yasiyo na watu wengi hivyo wanatumia muda mwingi kusafiri. Maeneo yanatofautiana; maoni ya wahubiri kuhusu huduma yao hutofautiana. Baraza Linaloongoza haliweki sheria jinsi makutaniko yanavyohesabu muda uliotumika katika utumishi wa shambani, wala hakuna mtu aliyeteuliwa ili kuwahukumu wengine kuhusu jambo hilo.—Mt. 6:1; 7:1; 1 Tim. 1:5.

      29 Muda unaotumia katika utumishi wa shambani unapaswa kuripotiwa saa nzima-nzima. Hata hivyo, mhubiri asiyejiweza kwa sababu ya uzee, ulemavu, ugonjwa au udhaifu mwingine wowote, anaweza kuripoti utumishi wa dakika 15, 30, na 45. Hata ikiwa alitoa ushahidi kwa dakika 15 tu kwa mwezi, anaweza kuripoti muda huo. Atahesabiwa kuwa mhubiri wa Ufalme anayetenda. Mhubiri ambaye hajiwezi kwa mwezi mmoja au miezi kadhaa, labda kwa sababu ya ugonjwa au jeraha kubwa, anaweza pia kuhusishwa katika mpango huo. Mpango huo unawahusu wale tu wenye udhaifu mkubwa wa kimwili. Halmashauri ya utumishi itaamua ikiwa mhubiri anastahili kuhusishwa katika mpango huo.

      REKODI YA KUTANIKO YA MHUBIRI

      30 Ripoti yako ya utumishi wa shambani ya kila mwezi huandikwa kwenye Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri. Rekodi hizo ni za kutaniko unaloshirikiana nalo. Ukitaka kuhamia kutaniko lingine, hakikisha unawajulisha wazee. Mwandishi atahakikisha kwamba rekodi zako zinatumwa kwenye kutaniko unalohamia. Kwa kufanya hivyo, wazee wa kutaniko unalohamia watakukaribisha na wataendelea kukusaidia kiroho. Ikiwa utakuwa mbali na kutaniko lako kwa muda usiozidi miezi mitatu, tafadhali endelea kutuma ripoti yako ya utumishi katika kutaniko lako.

      KWA NINI TUNARIPOTI UTUMISHI WETU WA SHAMBANI?

      31 Je, nyakati nyingine wewe husahau kutoa ripoti yako ya utumishi wa shambani? Bila shaka sote tunahitaji kukumbushwa mara kwa mara. Lakini tukisitawisha mtazamo unaofaa na tukielewa umuhimu wa kuripoti utumishi wetu wa shambani, inaweza kuwa rahisi kukumbuka kufanya hivyo.

      32 Wengine wameuliza: “Kwa kuwa Yehova anajua yale ambayo ninafanya katika utumishi wake, kwa nini nitoe ripoti kutanikoni?” Ni kweli kwamba Yehova anajua yale tunayofanya, naye anajua ikiwa tunamtumikia kwa nafsi yote au tunafanya kidogo kwa kulinganisha na uwezo wetu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova alirekodi siku ambazo Noa alikaa ndani ya safina na miaka ambayo Waisraeli walisafiri jangwani. Mungu aliweka rekodi ya wale waliokuwa waaminifu na wale ambao hawakutii. Alirekodi jinsi nchi ya Kanaani ilivyotekwa hatua kwa hatua na mambo yaliyotimizwa na waamuzi waaminifu wa Israeli. Naam, alirekodi habari nyingi sana kuhusu matendo ya watumishi wake. Alitumia roho yake kuongoza kuandikwa kwa matukio hayo, na hivyo kutuonyesha umuhimu wa kuandika rekodi sahihi.

      33 Matukio ya kihistoria yaliyoandikwa katika Biblia yanaonyesha usahihi wa ripoti na rekodi za watu wa Yehova. Katika visa vingi, masimulizi ya Biblia hayangekuwa yenye kuchochea ikiwa hesabu kamili haingetajwa. Fikiria mifano ifuatayo: Mwanzo 46:27; Kutoka 12:37; Waamuzi 7:7; 2 Wafalme 19:35; 2 Mambo ya Nyakati 14:9-13; Yohana 6:10; 21:11; Matendo 2:41; 19:19.

      34 Ingawa ripoti hizo hazionyeshi kila jambo tunalofanya katika utumishi wetu kwa Yehova, zinatimiza kusudi muhimu katika tengenezo la Yehova. Katika karne ya kwanza, baada ya kuhubiri, mitume wa Yesu waliripoti “mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.” (Marko 6:30) Nyakati nyingine, ripoti zinaweza kuonyesha mambo hususa yanayohitaji kushughulikiwa katika sehemu fulani ya huduma yetu. Takwimu zinaweza kuonyesha kama kuna maendeleo katika utendaji fulani, na vilevile ikiwa hakuna ongezeko kubwa la wahubiri. Huenda wahubiri wanahitaji kutiwa moyo au kuna matatizo yanayopaswa kushughulikiwa. Waangalizi wanaohusika watachunguza ripoti hizo na kujitahidi kurekebisha hali yoyote ambayo huenda inazuia maendeleo ya mtu mmoja-mmoja au ya kutaniko lote.

      35 Pia, ripoti hulisaidia tengenezo kujua maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Ni maeneo gani yenye matokeo mazuri? Ni maeneo gani yenye ukuzi mdogo? Ni machapisho gani yanayohitajiwa ili kuwasaidia watu wajifunze kweli? Ripoti husaidia tengenezo kujua machapisho yanayohitajiwa katika maeneo mbalimbali ulimwenguni na kisha huhakikisha kwamba yanapatikana.

      36 Wengi wetu hutiwa moyo na ripoti. Je, hatusisimuki tunaposikia kuhusu mambo ambayo ndugu zetu wanatimiza wanapohubiri habari njema ulimwenguni pote? Ripoti za ongezeko hutusaidia kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyopanuka. Mambo yaliyoonwa huchangamsha moyo, huzidisha bidii yetu na kutuchochea tushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri. (Mdo. 15:3) Ni muhimu kila mmoja wetu atoe ripoti ya utumishi wa shambani na hilo huonyesha kwamba tunawajali ndugu zetu ulimwenguni pote. Kupitia jambo hilo dogo tunaonyesha kwamba tunatii mipango ya tengenezo la Yehova.—Luka 16:10; Ebr. 13:17.

      KUJIWEKEA MALENGO

      37 Hatuna sababu yoyote ya kulinganisha utumishi wetu wa shambani na wa mtu mwingine. (Gal. 5:26; 6:4) Hali za watu hutofautiana sana. Kwa upande mwingine, tunaweza kupata faida nyingi sana tukiweka malengo halisi tunayoweza kufikia ili kupima maendeleo yetu katika huduma. Tukifikia malengo hayo tutaridhishwa na mambo tuliyotimiza.

      38 Ni wazi kwamba sasa Yehova anaharakisha kazi ya kukusanya watu watakaookoka ile “dhiki kuu.” Tunaishi wakati ambapo unabii huu wa Isaya unatimia: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” (Ufu. 7:9, 14; Isa. 60:22) Ni heshima kubwa sana kuwa wahudumu wa habari njema katika siku hizi za mwisho!—Mt. 24:14.

  • Njia za Kuhubiri Habari Njema
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • SURA YA 9

      Njia za Kuhubiri Habari Njema

      YESU KRISTO alihubiri habari njema kwa bidii, akiwawekea mfano mzuri wafuasi wake. Alichukua hatua ya kuwatafuta watu, akizungumza nao na kuwafundisha nyumbani kwao na hadharani. (Mt. 9:35; 13:36; Luka 8:1) Yesu alizungumza na watu binafsi, aliwafundisha wanafunzi wake faraghani, na hata alihutubia maelfu ya watu. (Marko 4:10-13; 6:35-44; Yoh. 3:2-21) Alitumia kila pindi aliyopata kuwatia watu moyo na kuwapa tumaini. (Luka 4:16-19) Hakuacha nafasi ya kuhubiri impite hata alipohitaji kupumzika au kula. (Marko 6:30-34; Yoh. 4:4-34) Tunaposoma masimulizi ya huduma ya Yesu yaliyoongozwa na roho, je, hatuchochewi kuiga mfano wake? Bila shaka tunachochewa kumwiga, kama mitume walivyochochewa.—Mt. 4:19, 20; Luka 5:27, 28; Yoh. 1:43-45.

      2 Fikiria nafasi ambazo Wakristo wanazo za kushiriki katika kazi iliyoanzishwa na Yesu Kristo miaka 2,000 hivi iliyopita.

      KUHUBIRI NYUMBA KWA NYUMBA

      3 Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunatambua umuhimu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa utaratibu, yaani, nyumba kwa nyumba. Tumetumia sana njia hiyo hivi kwamba ni alama inayotutambulisha. Faida za kutumia njia hii ili kuwafikia mamilioni ya watu katika muda mfupi zimeonyeshwa pia na ongezeko kubwa tunalopata. (Mt. 11:19; 24:14) Kuhubiri nyumba kwa nyumba hutupatia fursa ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova na jirani zetu.—Mt. 22:34-40.

      4 Mahubiri ya nyumba kwa nyumba hayakubuniwa hivi karibuni na Mashahidi wa Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba aliwafundisha watu nyumbani kwao. Akiwaeleza waangalizi huko Efeso kuhusu huduma yake, alisema hivi: “Tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia, . . . sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida na kuwafundisha . . . nyumba kwa nyumba.” Kupitia njia hiyo na nyinginezo, Paulo alitoa “ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Mdo. 20:18, 20, 21) Wakati huo, watawala Waroma walichochea ibada ya sanamu na watu wengi ‘walionekana kuwa wanaogopa sana miungu.’ Watu walihitaji kumtafuta kwa haraka “Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo,” ambaye wakati huo alikuwa “anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.”—Mdo. 17:22-31.

      5 Leo kuna uhitaji mkubwa hata zaidi wa kuwapelekea watu habari njema haraka. Mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unakaribia kwa kasi sana. Tunachochewa kuongeza bidii yetu tunapotambua uhitaji huo. Hakuna njia nyingine bora ya kuwatafuta watu wenye njaa ya kiroho kuliko njia ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ambayo imetumiwa kwa muda mrefu. Bado ina matokeo mazuri leo kama ilivyokuwa katika siku za Yesu na mitume.—Marko 13:10.

      6 Je, unashiriki kikamili katika huduma ya nyumba kwa nyumba? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba unamfurahisha Yehova. (Eze. 9:11; Mdo. 20:35) Huenda isiwe rahisi kwako kuhubiri nyumba kwa nyumba. Labda una udhaifu wa kimwili au watu wengi katika eneo lenu hawataki kusikiliza. Au kuna vizuizi vya serikali. Huenda wewe ni mwenye haya, na unaogopa kuzungumza na watu usiowafahamu. Kwa sababu hiyo, kila mara unapohubiri nyumba kwa nyumba unakuwa na wasiwasi. Usikate tamaa. (Kut. 4:10-12) Ndugu zako pia wanakabili hali kama hizo katika maeneo mengine.

      7 Yesu aliwaahidi wanafunzi wake hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Ahadi hiyo hutuimarisha tunapofanya kazi ya kuhubiri na kufundisha. Tunahisi kama mtume Paulo aliyesema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.” (Flp. 4:13) Unga mkono kikamili mipango ya kutaniko ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Unapohubiri na wengine, watakutia moyo na kukusaidia kuboresha ustadi wako. Sali ili ushinde vizuizi ambavyo huenda ukakabili, na ujitahidi kuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii.—1 Yoh. 5:14.

      8 Unapowatangazia wengine habari njema, utapata nafasi za kuwaeleza ‘sababu ya tumaini ulilo nalo.’ (1 Pet. 3:15) Utafahamu vizuri zaidi tofauti kati ya wale walio na tumaini la Ufalme na wale wasio na tumaini. (Isa. 65:13, 14) Utaridhika kwa kujua kwamba umetii amri ya Yesu ya ‘kuacha nuru yako iangaze,’ na huenda hata ukawa na pendeleo la kuwasaidia wengine wamjue Yehova na wapate kweli inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Mt. 5:16; Yoh. 17:3; 1 Tim. 4:16.

      9 Mipango hufanywa ili kuhubiri nyumba kwa nyumba katikati ya juma na pia mwisho juma. Makutaniko fulani hupanga kuhubiri jioni katika maeneo ambayo ni vigumu kuwapata watu nyumbani mchana. Huenda watu wakawa tayari kuwakaribisha wageni alasiri au jioni badala ya asubuhi.

      KUWATAFUTA WALE WANAOSTAHILI

      10 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake ‘wawatafute’ wale wanaostahili. (Mt. 10:11) Hakuwatafuta watu wenye mwelekeo unaofaa kwa kuhubiri tu nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, alitumia kila nafasi aliyopata ili kuhubiri rasmi au isivyo rasmi. (Luka 8:1; Yoh. 4:7-15) Pia, mitume waliwahubiria watu katika maeneo mbalimbali.—Mdo. 17:17; 28:16, 23, 30, 31.

      Lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana

      11 Vivyo hivyo, lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana. Hiyo inamaanisha kwamba tunapaswa kuiga njia ambazo Yesu na wanafunzi wake walitumia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha na vilevile kubadilikana kulingana na nyakati na hali za watu katika eneo letu. (1 Kor. 7:31) Kwa mfano, wahubiri wamefanikiwa kuwapata watu katika sehemu zao za biashara. Katika nchi nyingi, wahubiri wamepata matokeo kwa kuhubiri barabarani, bustani za kupumzikia, maegesho ya magari, au popote pale watu wanapopatikana. Makutaniko fulani yamepanga kuhubiri kwa kutumia meza au vigari vyenye machapisho katika eneo lao. Isitoshe, ofisi ya tawi inaweza kupanga mahubiri ya pekee ya hadharani katika barabara zenye watu wengi sana katika majiji, kwa kutumia wahubiri wa makutaniko mbalimbali. Matokeo ni kwamba watu wasiopatikana nyumbani wanaweza kupata habari njema mahali pengine.

      12 Tunapokutana na watu wanaopendezwa na ujumbe wa Biblia katika maeneo ya umma, tunaweza kuwapa chapisho linalowafaa. Ili kusitawisha upendezi, unaweza kumpa anwani au namba yako ya simu na kupanga kumrudia, au umwonyeshe tovuti ya jw.org, au umwelekeze kwenye eneo lililo karibu naye ambapo mikutano ya kutaniko hufanywa. Huenda kuwahubiria watu katika maeneo ya umma ikawa njia nzuri ya kupanua huduma yako na utakayofurahia.

      13 Hata hivyo, kazi ya Wakristo leo haihusu tu kutangaza habari njema. Ili ufanikiwe kuwasaidia wengine waikubali kweli inayoongoza kwenye uzima, unahitaji kuwarudia tena na tena watu waliopendezwa ili wafanye maendeleo na kuwa Wakristo wakomavu.

      KUFANYA ZIARA ZA KURUDIA

      14 Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Lakini pia aliwaambia: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.” (Mt. 28:19, 20) Unaweza kupata shangwe katika utumishi wa Yehova ukifanya ziara za kurudia. Huenda watu uliowahubiria habari njema wakafurahi ukiwatembelea tena. Unapozungumza nao habari zaidi kuhusu Biblia, unaweza kuimarisha imani yao katika Mungu na kuwasaidia kutambua uhitaji wao wa kiroho. (Mt. 5:3) Ukipanga kurudi wakati unaofaa na ukijitayarisha vizuri, huenda ukaanzisha funzo la Biblia. Unapaswa kuwa na lengo hilo unapofanya ziara za kurudia. Sisi hupanda mbegu ya kweli na vilevile kuitia maji.—1 Kor. 3:6.

      15 Huenda ikawa vigumu kwa wengine kufanya ziara za kurudia. Labda umezoea kuhubiri kifupi habari njema na unafurahia kufanya hivyo. Lakini huenda ukaogopa kumrudia mwenye nyumba ili kuendeleza mazungumzo ya Biblia. Matayarisho mazuri yatakusaidia kuwa na ujasiri. Tumia mapendekezo yanayotolewa katika mkutano wa katikati ya juma. Pia, unaweza kupanga kuhubiri na mhubiri mwenye uzoefu ili akusaidie.

      KUONGOZA MAFUNZO YA BIBLIA

      16 Alipokuwa akizungumza na mtu aliyegeuzwa imani na kuwa Myahudi ambaye alikuwa akisoma Neno la Mungu, mweneza-injili Filipo alimwuliza hivi: “Je, kweli unajua unayosoma?” Mwanamume huyo alijibu: “Kwa kweli, ninawezaje kuyaelewa mtu fulani asiponiongoza?” Masimulizi ya Biblia kwenye Matendo sura ya 8 yanaeleza kwamba Filipo ‘alimtangazia habari njema kumhusu Yesu,’ akianza na andiko ambalo mtu huyo alikuwa akisoma. (Mdo. 8:26-36) Hatujui Filipo alizungumza naye kwa muda gani, lakini Filipo alimweleza waziwazi habari njema hivi kwamba mtu huyo akaamini na akaomba kubatizwa. Kisha akawa mwanafunzi wa Yesu Kristo.

      17 Watu wengi leo hawajui mafundisho ya Biblia, na huenda tukahitaji kuwarudia mara nyingi na kujifunza nao kwa majuma au miezi kadhaa, au hata mwaka mmoja au zaidi ili wawe na imani na wastahili kubatizwa. Hata hivyo, ukiwasaidia kwa subira na upendo watu wanyofu wawe wanafunzi, utapata thawabu kama Yesu alivyosema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Mdo. 20:35.

      18 Bila shaka, ungependa kuongoza funzo la Biblia ukitumia machapisho yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo. Kwa kutumia maagizo yanayotolewa kwenye mkutano wa katikati ya juma na kwa kuhubiri na walimu wenye uzoefu kutanikoni, utafaulu kuongoza mafunzo yenye matokeo, na kuwasaidia wengine wawe wanafunzi wa Yesu Kristo.

      19 Ikiwa unahitaji kusaidiwa kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia, zungumza na mzee yeyote au Shahidi mwenye ustadi wa kuongoza mafunzo ya Biblia. Mapendekezo yanayopatikana katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha na ambayo huzungumziwa kwenye mkutano huo yatakusaidia pia. Mtegemee Yehova na usali kuhusu tamaa yako ya kuongoza funzo. (1 Yoh. 3:22) Kwa hiyo, jitahidi kuongoza angalau funzo moja la Biblia mbali na funzo ambalo huenda unaongoza katika familia yako. Ukiongoza mafunzo ya Biblia, utapata shangwe zaidi katika huduma.

      KUWAELEKEZA WANAOPENDEZWA KWENYE TENGENEZO LA YEHOVA

      20 Tunapowasaidia watu wamjue Yehova Mungu na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo, wanajiunga na kutaniko. Wanafunzi wa Biblia watafanya maendeleo ya kiroho na kukomaa ikiwa watalifahamu tengenezo la Yehova na kushirikiana nalo. Ni muhimu tuwafundishe jinsi ya kufanya hivyo. Unaweza kuwasaidia kwa kutumia broshua Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo? na video zilizotayarishwa kwa kusudi hilo. Unaweza pia kutumia habari iliyo katika Sura ya 4 ya kitabu hiki.

      21 Mara tu mnapoanza kujifunza Biblia, msaidie mwanafunzi aone kwamba Yehova anatumia tengenezo kutimiza kazi ya kuhubiri inayoendelea duniani. Mweleze faida za machapisho ya kujifunzia Biblia na jinsi yanavyotayarishwa na kusambazwa ulimwenguni pote na wafanyakazi wa kujitolea ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu. Mwalike mwanafunzi wako wa Biblia mwende pamoja kwenye Jumba la Ufalme. Mweleze jinsi mikutano inavyofanywa na umtambulishe kwa akina ndugu na dada. Msaidie pia afahamiane na Mashahidi wengine kwenye makusanyiko. Katika pindi hizo, mwache mwanafunzi ajionee jinsi waabudu wa Yehova wanavyopendana, jambo linalowatambulisha Wakristo wa kweli. (Yoh. 13:35) Mtu anayependezwa akiendelea kulithamini tengenezo la Yehova, atazidi kumkaribia Yehova.

      KUTUMIA MACHAPISHO YA BIBLIA

      22 Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri kwa bidii Neno la Mungu. Walinakili kwa mkono Maandiko waliyotumia kujifunza wao binafsi na kutanikoni. Waliwahimiza watu wasome Neno la Mungu la kweli. Nakala walizonakili zilikuwa chache na hivyo walizithamini sana. (Kol. 4:16; 2 Tim. 2:15; 3:14-17; 4:13; 1 Pet. 1:1) Leo, Mashahidi wa Yehova hutumia mbinu za kisasa kuchapisha mamia ya mamilioni ya Biblia na machapisho ya kujifunzia Biblia. Machapisho hayo yanatia ndani trakti, broshua, vitabu, na magazeti katika lugha nyingi.

      23 Unapowahubiria wengine habari njema, tumia machapisho ya kujifunzia Biblia yanayoandaliwa na tengenezo la Yehova. Unapotafakari jinsi ambavyo umefaidika kwa kusoma na kujifunza machapisho ya Mashahidi wa Yehova, utachochewa kuwapa wengine pia.—Ebr. 13:15, 16.

      24 Watu wengi sana hutegemea kupata habari katika Intaneti. Kwa hiyo, mbali na machapisho ya Biblia, tovuti yetu rasmi ya jw.org ni njia nyingine nzuri ya kutangaza habari njema. Watu ulimwenguni pote wanaweza kutumia kompyuta zao kusoma au kusikiliza Biblia na machapisho ya Biblia yakisomwa katika mamia ya lugha. Watu wanaosita kuzungumza nasi au wanaoishi katika maeneo ambayo hayana Mashahidi wengi wa Yehova wanaweza kuchunguza mambo tunayoamini kwa kutumia jw.org wakiwa nyumbani kwao.

      25 Kwa hiyo, tunawajulisha watu kuhusu jw.org kila tunapopata fursa. Mwenye nyumba anapouliza swali kuhusu imani yetu, tunaweza kutumia simu au kompyuta kumwonyesha jibu papo hapo. Tunapokutana na mtu anayezungumza lugha nyingine, kutia ndani lugha ya alama, tunaweza kumwelekeza kwenye tovuti yetu ili asome Biblia na machapisho ya Biblia katika lugha yake. Wahubiri wengi wametumia mojawapo ya video zilizo kwenye tovuti hiyo kuanzisha mazungumzo ya Biblia.

      MAHUBIRI YASIYO RASMI

      26 Yesu aliwaambia hivi wale waliokuwa wakimsikiliza: “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu. . . . Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:14-16) Wanafunzi hao waliishi kulingana na viwango vya Mungu kwa kumwiga Yesu aliyesema: “Mimi ndiye nuru ya ulimwengu.” Yesu aliwawekea Wakristo mfano kwa kuacha “nuru ya uzima” iangaze kwa faida ya wote ambao wangesikiliza.—Yoh. 8:12.

      27 Mtume Paulo pia alituwekea mfano mzuri. (1 Kor. 4:16; 11:1) Alipokuwa Athene, kila siku aliwahubiria watu aliokutana nao sokoni. (Mdo. 17:17) Wakristo huko Filipi waliiga mfano wake. Kwa sababu hiyo, Paulo aliwaandikia hivi: Mnaishi “katikati ya kizazi kilicho kombo na kilichopotoka, ambao kati yao mnaangaza kama mianga katika ulimwengu.” (Flp. 2:15) Sisi pia tunaweza kuacha kweli ya Ufalme iangaze kupitia maneno na matendo yetu tunapopata nafasi ya kuwaambia wengine habari njema. Ni kweli kwamba mfano wetu mzuri wa kuwa wanyofu na waadilifu unaweza kuonyesha sisi ni tofauti na ulimwengu. Hata hivyo, tukizungumza na watu kuhusu habari njema, watajua sababu inayotufanya tuwe tofauti.

      28 Mashahidi wengi wa Yehova huwahubiria habari njema watu wanaokutana nao kila siku kazini, shuleni, kwenye usafiri wa umma, au katika shughuli zao za kila siku. Tunaposafiri, tunaweza kuzungumza na wasafiri wenzetu. Kila mmoja wetu anapaswa kuwa tayari kutoa ushahidi katika mazungumzo yoyote ya kawaida. Acheni tuwe tayari kuzungumza na wengine wakati wowote.

      29 Tutachochewa kuzungumza na wengine tukikumbuka kwamba kwa kufanya hivyo tunamsifu Muumba wetu na kuliheshimu jina lake. Isitoshe, tunaweza kuwasaidia watu wenye moyo mnyoofu wamjue Yehova ili wao pia wamtumikie na kuwa na tumaini la kupata uzima kwa msingi wa imani katika Yesu Kristo. Yehova hupendezwa sana na jitihada hizo na kuuona huo kuwa utumishi mtakatifu.—Ebr. 12:28; Ufu. 7:9,10.

      ENEO

      30 Mapenzi ya Yehova ni kwamba ujumbe wa Ufalme uhubiriwe kwa utaratibu ulimwenguni pote, mijini na vijijini. Ili kutimiza hilo, makutaniko na watu binafsi wanaohubiri maeneo ya mbali hupewa eneo na ofisi ya tawi. (1 Kor. 14:40) Hilo linapatana na mpango wa Mungu uliofuatwa katika karne ya kwanza. (2 Kor. 10:13; Gal. 2:9) Kazi ya kuhubiri Ufalme inapopanuka haraka katika siku hizi za mwisho, tutapata matokeo mazuri ikiwa kuna utaratibu mzuri wa kuhubiri maeneo ya kutaniko.

      31 Mwangalizi wa utumishi ndiye anayesimamia mipango hiyo. Mtumishi wa huduma anaweza kuwagawia wahubiri maeneo. Kuna aina mbili za maeneo, maeneo ya vikundi na maeneo ya kibinafsi ya wahubiri. Katika kutaniko lenye eneo dogo, waangalizi wa vikundi huwa na maeneo ambayo huhubiriwa na wahubiri wa vikundi vyao. Katika kutaniko lenye eneo kubwa, wahubiri wanaweza kupewa eneo la kibinafsi.

      32 Mhubiri aliye na eneo la kibinafsi anaweza kuhubiri eneo hilo wakati ambapo hakuna mpango wa mkutano wa utumishi wa shambani au kama hawezi kufika kwenye kikundi. Kwa mfano, wahubiri fulani huchukua eneo lililo karibu na mahali wanapofanya kazi nao huhubiri wakati wa mapumziko ya mchana au baada ya kazi. Familia fulani huchukua eneo la kibinafsi karibu na nyumbani kwao na kuhubiri wakati wa jioni. Kuwa na eneo la kibinafsi lililo karibu humsaidia mhubiri atumie wakati mwingi zaidi katika utumishi wa shambani. Eneo la kibinafsi linaweza pia kuhubiriwa na kikundi. Kama ungependa kuwa na eneo la kibinafsi unaweza kumwomba mtumishi wa maeneo.

      33 Iwe ni eneo la kikundi lililopewa mwangalizi wa kikundi au eneo la kibinafsi lililopewa mhubiri, mtu aliyepewa eneo hilo atajitahidi kadiri awezavyo kuzungumza na mtu fulani katika kila nyumba. Mipango ya kuhubiri eneo kikamili inapaswa kufuata sheria za kulinda taarifa zinazotumiwa. Kila mwangalizi wa kikundi au mhubiri anayepewa eneo anapaswa kujitahidi kulikamilisha kwa miezi minne. Mara tu anapomaliza, anapaswa kumjulisha mtumishi wa maeneo. Ikitegemea na hali, mwangalizi wa kikundi au mhubiri anaweza kubaki na eneo hilo ili alihubiri tena au anaweza kumrudishia mtumishi wa maeneo.

      34 Wahubiri wote kutanikoni wakishirikiana, eneo linaweza kuhubiriwa kikamili. Pia, eneo moja halitahubiriwa na wahubiri tofauti-tofauti wakati uleule, jambo linaloweza kuwaudhi wenye nyumba. Tukifanya hivyo, tutaonyesha kwamba tunawajali ndugu zetu na watu walio katika eneo.

      KUSHIRIKIANA KUWAHUBIRIA WATU WA KILA LUGHA

      35 Wanadamu wote wanahitaji kujifunza kumhusu Yehova Mungu, Mwana wake, na Ufalme. (Ufu. 14:6, 7) Tungependa kuwasaidia watu wa lugha zote waliitie jina la Yehova ili waokolewe na wavae utu mpya wa Kikristo. (Rom. 10:12, 13; Kol. 3:10, 11) Tunakabili changamoto gani tunapohubiri maeneo yenye watu wanaozungumza lugha mbalimbali? Tunawezaje kukabiliana na hali hizo ili watu wengi iwezekanavyo wasikie ujumbe wa Ufalme katika lugha wanayoelewa vizuri?—Rom. 10:14.

      36 Maeneo hupangwa kulingana na lugha. Kwa hiyo, wahubiri wa makutaniko yenye maeneo ya lugha tofauti-tofauti wanaweza kuhubiri eneo lilelile. Katika maeneo hayo, ni vizuri wahubiri wa kila kutaniko wajitahidi kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kutaniko lao. Hilo linahusika pia wakati wa kampeni za kila mwaka za kugawa mialiko. Hata hivyo, wahubiri wanapohubiri hadharani na isivyo rasmi, wanaweza kuzungumza na mtu yeyote na kutoa machapisho ya lugha yoyote.

      37 Katika visa fulani, makutaniko ya lugha tofauti yanaweza kushindwa kuhubiri kikamili maeneo yao kwa ukawaida. Katika visa kama hivyo, waangalizi wa utumishi wa makutaniko yanayohusika wanapaswa kuwasiliana ili kupanga utaratibu unaofaa wa kuhubiri eneo lote. Hilo litampa kila mtu nafasi ya kusikia ujumbe wa Ufalme na kuzuia makutaniko tofauti kuhubiri eneo lilelile kwa wakati mmoja.—Met. 15:22.

      38 Tunapaswa kufanya nini ikiwa mwenye nyumba anazungumza lugha tofauti? Tusifikiri kwamba wahubiri wanaozungumza lugha yake watamtembelea. Wahubiri fulani wamejifunza utangulizi mfupi wa lugha zinazozungumzwa katika eneo lao. Tunaweza kumwonyesha mtu jinsi ya kusoma au kupakua machapisho ya lugha yake kwenye tovuti yetu rasmi ya jw.org, au tunaweza kupanga kumletea machapisho ya lugha yake.

      39 Mwenye nyumba akionyesha upendezi, tunapaswa kujaribu kumtafuta mhubiri anayezungumza lugha anayoelewa. Pia tunaweza kumwelekeza kwenye kutaniko la karibu linalofanya mikutano kwa lugha yake. Ikiwa anapenda kuwasiliana na mhubiri anayezungumza lugha yake, tunaweza kumwelekeza jinsi ya kujaza habari zake za mawasiliano kwenye Tovuti ya jw.org. Kisha, ofisi ya tawi itajitahidi kupata mhubiri aliye karibu, kikundi, au kutaniko linaloweza kumsaidia zaidi.

      40 Tunapaswa kuendelea kumtembelea mtu huyo anayependezwa mpaka atakapotembelewa na mhubiri anayezungumza lugha yake. Katika visa fulani, huenda ofisi ya tawi ikawajulisha wazee kwamba hawakumpata mhubiri anayezungumza lugha ya mtu huyo. Ikiwa ndivyo, tunapaswa kujitahidi kuendeleza upendezi wa mwenye nyumba. Ikiwezekana tunaweza kujifunza naye Biblia, labda kwa kutumia machapisho ya lugha yake. Tukitumia vizuri picha na kumwomba mtu huyo asome maandiko yaliyonukuliwa, atapata ujuzi fulani wa msingi wa Biblia. Labda ana mtu wa ukoo anayejua lugha yake na lugha ya kutaniko ambaye anaweza kumtafsiria ujumbe.

      41 Ili kumwelekeza mtu anayependezwa kwenye tengenezo la Mungu, tunapaswa kumwalika ahudhurie mikutano yetu, ingawa huenda asielewe kikamili mambo yanayozungumziwa. Maandiko yanaposomwa, tunaweza kumsaidia kuyapata katika Biblia ya lugha yake ikiwa inapatikana. Anaposhirikiana na wengine kutanikoni, anaweza kuimarishwa na kusaidiwa kufanya maendeleo zaidi ya kiroho.

      42 Vikundi vidogo: Kikundi kidogo hufanyizwa na wahubiri wanaotumia lugha tofauti na ile inayotumiwa na kutaniko lao, ingawa hakuna mzee au mtumishi wa huduma anayestahili kuongoza mikutano katika lugha hiyo kila juma. Ofisi ya tawi inaweza kutambua kutaniko kuwa linalosimamia kikundi kidogo ikiwa matakwa yafuatayo yametimizwa:

      1. (1) Kuna idadi ya kutosha ya watu katika eneo ambao wanazungumza lugha nyingine tofauti na lugha ya kutaniko.

      2. (2) Angalau kuna wahubiri wachache wanaojua au wako tayari kujifunza lugha hiyo.

      3. (3) Baraza la wazee liko tayari kuongoza mipango ya mahubiri katika lugha hiyo.

      Ikiwa baraza la wazee liko tayari kusimamia kikundi kidogo, wazee wanapaswa kuwasiliana na mwangalizi wa mzunguko. Huenda anajua makutaniko mengine yanayojitahidi kuwahubiria watu wa lugha hiyo na anaweza kuandaa habari muhimu itakayowasaidia kujua kutaniko linaloweza kusimamia kikundi hicho kidogo kwa njia bora zaidi. Baada ya kuamua ni kutaniko gani litakalosimamia, wazee wanaweza kuandika barua kwa ofisi ya tawi na kuomba idhini ya kutambuliwa rasmi kama kutaniko linalosimamia kikundi kidogo.

      43 Vikundi: Ofisi ya tawi inaweza kutambua kutaniko kuwa linalosimamia kikundi ikiwa matakwa yafuatayo yametimizwa:

      1. (1) Kuwe na idadi ya kutosha ya watu wanaopendezwa na uwezekano wa ongezeko katika eneo la lugha hiyo.

      2. (2) Angalau idadi ndogo ya wahubiri wanaozungumza au wanaojifunza lugha hiyo.

      3. (3) Mzee au mtumishi wa huduma anayestahili anapatikana ili kusimamia na kuongoza angalau mkutano mmoja katika juma​​—au sehemu ya mkutano wa kila juma, kama vile hotuba ya watu wote au Funzo la Mnara wa Mlinzi​​—katika lugha hiyo.

      Matakwa hayo yanapotimizwa kwa kiwango kinachofaa, baraza la wazee litaandikia ofisi ya tawi barua yenye habari kamili na kuomba kutambuliwa rasmi kuwa kutaniko linalosimamia kikundi. Mzee au mtumishi wa huduma anayesimamia kikundi hicho ataitwa “mwangalizi wa kikundi” au “mtumishi wa kikundi” akiwa na jukumu la kutunza kikundi hicho.

      44 Baada ya kikundi kuanzishwa, baraza la wazee la kutaniko linalosimamia kikundi hicho litaamua ikiwa sehemu nyingine za mikutano ya kutaniko zinapaswa kuongezwa na ni mara ngapi kwa mwezi zinapaswa kufanywa. Mikutano ya utumishi wa shambani inaweza pia kupangwa kwa ajili ya kikundi hicho. Washiriki wote watakuwa chini ya usimamizi wa baraza la wazee linalotegemeza kikundi hicho. Wazee watatoa mwongozo wenye usawaziko na kuchukua hatua zifaazo ili kushughulikia mahitaji ya kikundi hicho. Mwangalizi wa mzunguko anapohubiri pamoja na kikundi hicho katika juma la ziara yake kwa kutaniko linalotegemeza, ataandikia ofisi ya tawi ripoti fupi kuhusu maendeleo ya kikundi hicho na kutaja mahitaji hususa. Baada ya muda, huenda kikundi hicho kikastahili kuwa kutaniko. Ikiwa wote wanaohusika wanafuata miongozo ya kitheokrasi, Yehova atafurahi.—1 Kor. 1:10; 3:5, 6.

      MAHUBIRI YA VIKUNDI

      45 Kila Mkristo aliyejiweka wakfu ana wajibu wa kuwahubiria wengine habari njema. Kuna njia nyingi za kufanya hivyo, lakini wengi wetu hufurahia kuhubiri pamoja na wahubiri wengine. (Luka 10:1) Kwa hiyo, makutaniko hukutana kwa ajili ya utumishi wa shambani katika mwisho juma na pia katikati ya juma. Kunapokuwa na sikukuu, tunapata pia nafasi za kuhubiri tukiwa kikundi, kwa kuwa ndugu wengi hawaendi kazini. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko hupanga mahali pa mikutano ya utumishi wa shambani na wakati unaowafaa wengi wakati wa mchana na jioni.

      46 Mahubiri ya vikundi huwasaidia wahubiri kufanya kazi pamoja na hivyo ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:12) Wahubiri wapya wanaweza kuhubiri na wahubiri wenye ustadi na uzoefu ili wasaidiwe. Katika maeneo fulani huenda ikawa jambo la hekima kwa wahubiri wawili au zaidi kuhubiri pamoja kwa sababu ya usalama. Hata ikiwa unapanga kuhubiri peke yako katika eneo, kukutana na wengine katika kikundi kunaweza kuwatia moyo. Kujua tu kwamba wengine wanahubiri katika eneo lilelile kunaweza kukupa ujasiri. Mapainia na wengine hawapaswi kuhisi kwamba ni lazima wahudhurie kila mkutano wa utumishi wa shambani uliopangwa na kutaniko, hasa ikiwa mikutano hiyo hufanywa kila siku. Hata hivyo, inaelekea kwamba wanaweza kuunga mkono angalau mikutano kadhaa ya utumishi wa shambani kila juma.

      47 Acheni sote tuige mfano uliowekwa na Yesu na mitume wake! Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kushiriki kikamili katika kazi muhimu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme.—Luka 9:57-62.

  • Njia za Kupanua Huduma Yako
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • SURA YA 10

      Njia za Kupanua Huduma Yako

      YESU alipowaagiza wanafunzi wake wahubiri Ufalme, aliwaambia hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” Kulikuwa na kazi nyingi, basi akaongeza hivi: “Mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo ya kutimiza huduma yao. Alionyesha umuhimu wa kazi hiyo aliposema: “Hamtamaliza kamwe kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika.”—Mt. 10:23.

      2 Leo pia, kuna kazi nyingi ya kufanya katika huduma ya shambani. Lazima habari njema ya Ufalme ihubiriwe kabla ya mwisho kuja, na muda unayoyoma! (Marko 13:10) Kwa kuwa shamba ni ulimwengu, tunakabili hali kama ya Yesu na wanafunzi wake, ingawa kwa kiwango kikubwa zaidi. Idadi yetu ni ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya wanadamu ulimwenguni, lakini tuna hakika kwamba Yehova atatusaidia. Habari njema ya Ufalme itahubiriwa ulimwenguni pote, na wakati uliowekwa na Yehova utakapofika, mwisho utakuja. Je, tutatanguliza Ufalme wa Mungu maishani ili tutimize huduma yetu kikamili? Tunaweza kujiwekea malengo gani ya kitheokrasi?

      3 Akieleza matakwa ya Yehova kwa watumishi wake waliojiweka wakfu, Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Tunapaswa kumtumikia Mungu kwa nafsi yote. Hilo linamaanisha kuwa tunaonyesha kwamba tumejiweka wakfu na tumejitoa kikamili kwa kufanya yote tunayoweza katika utumishi wa Yehova. (2 Tim. 2:15) Kila mmoja wetu anaweza kupanua utumishi wake katika njia mbalimbali ikitegemea hali na uwezo wake. Hebu fikiria baadhi ya njia hizo, na uamue malengo ya kitheokrasi unayoweza kujiwekea unapotimiza huduma yako.

      KUWA MHUBIRI WA KUTANIKO

      4 Wote wanaokubali kweli wana pendeleo la kutangaza habari njema. Hiyo ndiyo kazi kuu ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kwa kawaida, mwanafunzi wa Yesu Kristo huanza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema mara tu anaposikia ujumbe huo. Hivyo ndivyo Andrea, Filipo, Kornelio, na wengine walivyofanya. (Yoh. 1:40, 41, 43-45; Mdo. 10:1, 2, 24; 16:14, 15, 25-34) Je, inamaanisha kwamba mtu anaweza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema kabla hajabatizwa? Ndiyo! Mara tu mtu anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa kutanikoni, anaweza kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Anaweza pia kushiriki katika sehemu mbalimbali za huduma ikitegemea hali na uwezo wake.

      5 Mhubiri anapobatizwa, bila shaka yuko tayari kufanya yote anayoweza ili awasaidie wengine wajifunze habari njema. Wanaume na wanawake wana pendeleo la kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Ni pendeleo kushiriki hata kwa sehemu ndogo katika kuendeleza kazi ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, tukipanua huduma yetu na kufikia mapendeleo zaidi ya utumishi tutakuwa na furaha sana.

      KUTUMIKIA KATIKA MAENEO YENYE UHITAJI MKUBWA

      6 Huenda eneo la kutaniko lenu huhubiriwa kwa ukawaida na ushahidi mzuri unatolewa. Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kwamba unaweza kupanua huduma yako kwa kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. (Mdo. 16:9) Ikiwa unatumikia ukiwa mzee au mtumishi wa huduma, huenda kuna kutaniko lingine ambalo litathamini msaada wako. Mwangalizi wenu wa mzunguko anaweza kukupendekezea jinsi ya kusaidia kutaniko lingine katika mzunguko wenu. Ikiwa ungependa kutumikia katika eneo lingine nchini kwenu, ofisi ya tawi inaweza kukupatia habari zaidi.

      7 Je, ungependa kutumikia katika nchi nyingine? Ikiwa ndivyo, unapaswa kufikiria jambo hilo kwa makini. Kwa nini usizungumzie jambo hilo na wazee wa kutaniko lenu? Bila shaka, hilo litakuwa badiliko kubwa kwako na kwa wale watakaoenda nawe. (Luka 14:28) Hata hivyo, ikiwa hukusudii kukaa kwa muda mrefu, huenda ikafaa ufikirie kutumikia katika eneo lililo nchini kwenu.

      8 Katika nchi fulani, ndugu wanaosimamia kazi ni wapya katika kweli. Kwa unyenyekevu, ndugu wenyeji wako tayari kuwaachia wazee wenye uzoefu wanaohamia katika makutaniko yao waongoze mambo. Ikiwa wewe ni mzee na unafikiria kuhamia katika nchi kama hizo, kumbuka kwamba lengo lako si kuchukua mapendeleo ya ndugu wenyeji. Badala yake, tumikia pamoja nao. Watie moyo wafanye maendeleo na wakubali majukumu kutanikoni. (1 Tim. 3:1) Uwe na subira ikiwa mambo fulani hayafanywi kama yanavyofanywa katika nchi yenu. Tumia uzoefu wako ukiwa mzee kuwasaidia akina ndugu. Kisha, ikiwa wakati fulani utalazimika kurudi katika nchi yenu, wazee wenyeji watakuwa na uwezo wa kusimamia kutaniko.

      9 Kabla ofisi ya tawi haijakupa majina ya makutaniko yanayoweza kufaidika na msaada wako, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lenu itahitaji kutuma barua ya kukupendekeza. Barua hiyo inahitajiwa hata kama wewe ni mzee, mtumishi wa huduma, painia, au mhubiri. Halmashauri ya utumishi itatuma barua ya kukupendekeza pamoja na ombi lako moja kwa moja kwenye ofisi ya tawi ya nchi unayotaka kutumikia.

      KUHUBIRI KATIKA LUGHA NYINGINE

      10 Ili upanue huduma yako, huenda ukafikiria kujifunza lugha nyingine, kutia ndani lugha ya alama. Kama una lengo la kujifunza kuhubiri katika lugha nyingine, unaweza kuzungumza na wazee na mwangalizi wa mzunguko. Wanaweza kukupa madokezo na kukutia moyo. Kupitia mwelekezo wa ofisi ya tawi, mizunguko fulani imepanga madarasa ya lugha ili kuwazoeza wahubiri wenye uwezo na mapainia kuhubiri katika lugha nyingine.

      UTUMISHI WA PAINIA

      11 Wahubiri wote wanapaswa kujua matakwa ya msingi ya utumishi wa painia msaidizi, wa kawaida, na wa pekee na pia utumishi mwingine wa wakati wote. Painia anapaswa kuwa Mkristo aliyebatizwa mwenye mfano

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki