-
Jua Jinsi Unavyopaswa KujibuFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Jua Jinsi Unavyopaswa Kujibu
MASWALI fulani ni kama miamba ya barafu. Sehemu kubwa zaidi imefichika chini ya maji. Sehemu iliyofichika huwa muhimu kuliko swali lenyewe.
Hata kama anayeuliza swali anataka sana kujibiwa, kujua jinsi unavyopaswa kumjibu kunatia ndani kufahamu kadiri utakavyojibu na jinsi utakavyojibu. (Yn. 16:12) Katika hali fulani, kama Yesu alivyoonyesha mitume wake, mtu anaweza kutaka habari ambayo hastahili kujua au ambayo kwa kweli haimfaidi.—Mdo. 1:6, 7.
Maandiko yanatushauri hivi: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.” (Kol. 4:6) Kwa hiyo, kabla ya kujibu, tunahitaji kufikiria yale tutakayosema na jinsi tutakavyoyasema.
Fahamu Maoni ya Anayeuliza Swali
Masadukayo walijaribu kumnasa Yesu walipomwuliza swali la ufufuo wa mwanamke fulani aliyeolewa mara nyingi. Lakini, Yesu alijua kwamba kwa hakika wao hawaamini ufufuo. Basi alipowajibu, alizingatia maoni yao yenye makosa yaliyochochea swali hilo. Yesu alisababu nao kwa ustadi akitumia simulizi wanalofahamu katika Maandiko, akawaonyesha jambo ambalo hawakupata kamwe kulifikiria awali—uthibitisho wa wazi kwamba kwa kweli Mungu atafufua wafu. Jibu lake liliwashangaza sana wapinzani wake hivi kwamba wakaogopa kumwuliza maswali mengine zaidi.—Luka 20:27-40.
Ili ujue jinsi unavyopaswa kujibu, ni lazima pia ufahamu maoni na mahangaiko ya wale wanaokuuliza maswali. Kwa mfano, mwanafunzi wa darasa lenu au mfanyakazi mwenzako anaweza kukuuliza mbona husherehekei Krismasi. Kwa nini anauliza? Je, kweli anataka kujua sababu, au anauliza tu ili ajue kama unaruhusiwa kujifurahisha? Ili ujue, unaweza kumwuliza kwa nini ameuliza swali hilo. Kisha ujibu kulingana na hali. Kuhusu sherehe hiyo, pia unaweza kutumia fursa hiyo kuonyesha jinsi kufuata mwongozo wa Biblia kunavyotulinda dhidi ya mambo fulani ambayo yamefadhaisha watu na kuwatweza.
Tuseme umealikwa uhutubie kikundi cha wanafunzi juu ya Mashahidi wa Yehova. Baada ya hotuba yako, huenda wakauliza maswali. Maswali yakionekana kuwa manyofu na ya waziwazi, ni bora kutoa majibu rahisi na ya moja kwa moja. Ikiwa wanauliza maswali kuhusu jinsi watu wanavyosema vibaya juu yetu, inaweza kuwa bora kuzungumzia kwanza kwa ufupi mambo yanayoweza kuathiri maoni ya wengi juu ya masuala kama hayo na sababu inayofanya Mashahidi wa Yehova watumie Biblia kuwa kanuni yao. Mara nyingi, kuna faida ya kuyaona maswali hayo kama masuala yanayowahangaisha badala ya kuyaona kuwa vipingamizi—hata kama huenda yamezushwa kwa njia hiyo. Basi, jibu lako linakupa fursa ya kuwaelewesha wasikilizaji, kuwapa habari sahihi, na kuonyesha Maandiko yanayounga mkono imani yetu.
-
-
Jua Jinsi Unavyopaswa KujibuFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Anayeuliza Maswali Anaonaje Maandiko?
Unapofikiria jinsi ya kujibu, pia unaweza kufikiria anayeuliza maswali anaonaje Maandiko Matakatifu. Yesu alifanya hivyo alipokuwa akijibu swali la Masadukayo juu ya ufufuo. Kwa kuwa alijua kwamba wao wanakubali tu maandishi ya Musa, Yesu alisababu nao juu ya simulizi fulani la vitabu vya Torati, akianza na maneno haya: “Lakini kwamba wafu wafufuliwa hata Musa alifunua.” (Luka 20:37) Wewe pia unaweza kuona faida ya kunukuu sehemu za Biblia ambazo yule unayeongea naye anakubali na anafahamu.
Lakini namna gani kama yule unayeongea naye haamini Biblia? Ona jinsi mtume Paulo alivyofanya alipotoa hotuba kule Areopago, kama ilivyoandikwa katika Matendo 17:22-31. Aliwaeleza kweli za Kimaandiko bila kunukuu Biblia moja kwa moja. Unaweza kufanya hivyo ikiwa inawezekana. Katika maeneo mengine huenda ikahitajika kuzungumza na mtu mara kadhaa kabla ya kunukuu Biblia moja kwa moja. Unapoelekeza kwenye Biblia, inaweza kuwa jambo la hekima kuonyesha kwanza sababu zinazofanya istahili kuzingatiwa, badala ya kukazia tu kishupavu kwamba ni Neno la Mungu. Lakini, kusudia kutoa ushahidi wa wazi juu ya kusudi la Mungu, na baadaye, kumwacha yule unayeongea naye ajionee mwenyewe mambo yanayosemwa na Biblia. Biblia inagusa moyo kuliko jambo lolote ambalo sisi wenyewe huenda tukasema.—Ebr. 4:12.
Usemi Wako na ‘Upendeze Sikuzote’
Yehova ni mwenye neema, na kwa kufaa watumishi wake wanaambiwa wawe na usemi ‘unaopendeza sikuzote, uliokolezwa chumvi’! (Kol. 4:6; Kut. 34:6) Hiyo inamaanisha kwamba tunapaswa kusema kwa fadhili, hata kama inaonekana haistahili. Usemi wetu unapaswa kuwa mzuri, si mbaya wala usio na busara.
Watu wengi wana mikazo sana, na wanatukanwa kila siku. Tunapowatembelea watu kama hao, huenda wakaongea kwa ukali. Tuwajibuje? Biblia inasema: “Jawabu la upole hugeuza hasira.” Jibu kama hilo linaweza kumtuliza mtu ambaye anapinga. (Mit. 15:1; 25:15) Tabia na sauti yenye fadhili zinaweza kuwavutia sana watu ambao wanapatwa na magumu kila siku hata waweze kusikiliza habari njema tunazowapelekea.
Hatuna haja ya kubishana na watu ambao hawaiheshimu kweli. Badala yake, tamaa yetu ni kutumia Maandiko kusababu na watu ambao watakubali. Hata tukabili hali ipi, tukumbuke kwamba tunapaswa kujibu kwa fadhili na kwa usadikisho kwamba ahadi za Mungu zenye thamani zinategemeka.—1 The. 1:5.
-