-
Wahudumu wa Habari NjemaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
Halmashauri ya utumishi itaamua ikiwa mhubiri anastahili kuhusishwa katika mpango huo.
REKODI YA KUTANIKO YA MHUBIRI
30 Ripoti yako ya utumishi wa shambani ya kila mwezi huandikwa kwenye Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri. Rekodi hizo ni za kutaniko unaloshirikiana nalo. Ukitaka kuhamia kutaniko lingine, hakikisha unawajulisha wazee. Mwandishi atahakikisha kwamba rekodi zako zinatumwa kwenye kutaniko unalohamia. Kwa kufanya hivyo, wazee wa kutaniko unalohamia watakukaribisha na wataendelea kukusaidia kiroho. Ikiwa utakuwa mbali na kutaniko lako kwa muda usiozidi miezi mitatu, tafadhali endelea kutuma ripoti yako ya utumishi katika kutaniko lako.
KWA NINI TUNARIPOTI UTUMISHI WETU WA SHAMBANI?
31 Je, nyakati nyingine wewe husahau kutoa ripoti yako ya utumishi wa shambani? Bila shaka sote tunahitaji kukumbushwa mara kwa mara. Lakini tukisitawisha mtazamo unaofaa na tukielewa umuhimu wa kuripoti utumishi wetu wa shambani, inaweza kuwa rahisi kukumbuka kufanya hivyo.
32 Wengine wameuliza: “Kwa kuwa Yehova anajua yale ambayo ninafanya katika utumishi wake, kwa nini nitoe ripoti kutanikoni?” Ni kweli kwamba Yehova anajua yale tunayofanya, naye anajua ikiwa tunamtumikia kwa nafsi yote au tunafanya kidogo kwa kulinganisha na uwezo wetu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova alirekodi siku ambazo Noa alikaa ndani ya safina na miaka ambayo Waisraeli walisafiri jangwani. Mungu aliweka rekodi ya wale waliokuwa waaminifu na wale ambao hawakutii. Alirekodi jinsi nchi ya Kanaani ilivyotekwa hatua kwa hatua na mambo yaliyotimizwa na waamuzi waaminifu wa Israeli. Naam, alirekodi habari nyingi sana kuhusu matendo ya watumishi wake. Alitumia roho yake kuongoza kuandikwa kwa matukio hayo, na hivyo kutuonyesha umuhimu wa kuandika rekodi sahihi.
33 Matukio ya kihistoria yaliyoandikwa katika Biblia yanaonyesha usahihi wa ripoti na rekodi za watu wa Yehova. Katika visa vingi, masimulizi ya Biblia hayangekuwa yenye kuchochea ikiwa hesabu kamili haingetajwa. Fikiria mifano ifuatayo: Mwanzo 46:27; Kutoka 12:37; Waamuzi 7:7; 2 Wafalme 19:35; 2 Mambo ya Nyakati 14:9-13; Yohana 6:10; 21:11; Matendo 2:41; 19:19.
34 Ingawa ripoti hizo hazionyeshi kila jambo tunalofanya katika utumishi wetu kwa Yehova, zinatimiza kusudi muhimu katika tengenezo la Yehova. Katika karne ya kwanza, baada ya kuhubiri, mitume wa Yesu waliripoti “mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.” (Marko 6:30) Nyakati nyingine, ripoti zinaweza kuonyesha mambo hususa yanayohitaji kushughulikiwa katika sehemu fulani ya huduma yetu. Takwimu zinaweza kuonyesha kama kuna maendeleo katika utendaji fulani, na vilevile ikiwa hakuna ongezeko kubwa la wahubiri. Huenda wahubiri wanahitaji kutiwa moyo au kuna matatizo yanayopaswa kushughulikiwa. Waangalizi wanaohusika watachunguza ripoti hizo na kujitahidi kurekebisha hali yoyote ambayo huenda inazuia maendeleo ya mtu mmoja-mmoja au ya kutaniko lote.
35 Pia, ripoti hulisaidia tengenezo kujua maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Ni maeneo gani yenye matokeo mazuri? Ni maeneo gani yenye ukuzi mdogo? Ni machapisho gani yanayohitajiwa ili kuwasaidia watu wajifunze kweli? Ripoti husaidia tengenezo kujua machapisho yanayohitajiwa katika maeneo mbalimbali ulimwenguni na kisha huhakikisha kwamba yanapatikana.
36 Wengi wetu hutiwa moyo na ripoti. Je, hatusisimuki tunaposikia kuhusu mambo ambayo ndugu zetu wanatimiza wanapohubiri habari njema ulimwenguni pote? Ripoti za ongezeko hutusaidia kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyopanuka. Mambo yaliyoonwa huchangamsha moyo, huzidisha bidii yetu na kutuchochea tushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri. (Mdo. 15:3) Ni muhimu kila mmoja wetu atoe ripoti ya utumishi wa shambani na hilo huonyesha kwamba tunawajali ndugu zetu ulimwenguni pote. Kupitia jambo hilo dogo tunaonyesha kwamba tunatii mipango ya tengenezo la Yehova.—Luka 16:10; Ebr. 13:17.
KUJIWEKEA MALENGO
37 Hatuna sababu yoyote ya kulinganisha utumishi wetu wa shambani na wa mtu mwingine. (Gal. 5:26; 6:4) Hali za watu hutofautiana sana. Kwa upande mwingine, tunaweza kupata faida nyingi sana tukiweka malengo halisi tunayoweza kufikia ili kupima maendeleo yetu katika huduma. Tukifikia malengo hayo tutaridhishwa na mambo tuliyotimiza.
38 Ni wazi kwamba sasa Yehova anaharakisha kazi ya kukusanya watu watakaookoka ile “dhiki kuu.” Tunaishi wakati ambapo unabii huu wa Isaya unatimia: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” (Ufu. 7:9, 14; Isa. 60:22) Ni heshima kubwa sana kuwa wahudumu wa habari njema katika siku hizi za mwisho!—Mt. 24:14.
-
-
Njia za Kuhubiri Habari NjemaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 9
Njia za Kuhubiri Habari Njema
YESU KRISTO alihubiri habari njema kwa bidii, akiwawekea mfano mzuri wafuasi wake. Alichukua hatua ya kuwatafuta watu, akizungumza nao na kuwafundisha nyumbani kwao na hadharani. (Mt. 9:35; 13:36; Luka 8:1) Yesu alizungumza na watu binafsi, aliwafundisha wanafunzi wake faraghani, na hata alihutubia maelfu ya watu. (Marko 4:10-13; 6:35-44; Yoh. 3:2-21) Alitumia kila pindi aliyopata kuwatia watu moyo na kuwapa tumaini. (Luka 4:16-19) Hakuacha nafasi ya kuhubiri impite hata alipohitaji kupumzika au kula. (Marko 6:30-34; Yoh. 4:4-34) Tunaposoma masimulizi ya huduma ya Yesu yaliyoongozwa na roho, je, hatuchochewi kuiga mfano wake? Bila shaka tunachochewa kumwiga, kama mitume walivyochochewa.—Mt. 4:19, 20; Luka 5:27, 28; Yoh. 1:43-45.
2 Fikiria nafasi ambazo Wakristo wanazo za kushiriki katika kazi iliyoanzishwa na Yesu Kristo miaka 2,000 hivi iliyopita.
KUHUBIRI NYUMBA KWA NYUMBA
3 Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunatambua umuhimu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa utaratibu, yaani, nyumba kwa nyumba. Tumetumia sana njia hiyo hivi kwamba ni alama inayotutambulisha. Faida za kutumia njia hii ili kuwafikia mamilioni ya watu katika muda mfupi zimeonyeshwa pia na ongezeko kubwa tunalopata. (Mt. 11:19; 24:14) Kuhubiri nyumba kwa nyumba hutupatia fursa ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova na jirani zetu.—Mt. 22:34-40.
4 Mahubiri ya nyumba kwa nyumba hayakubuniwa hivi karibuni na Mashahidi wa Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba aliwafundisha watu nyumbani kwao. Akiwaeleza waangalizi huko Efeso kuhusu huduma yake, alisema hivi: “Tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia, . . . sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida na kuwafundisha . . . nyumba kwa nyumba.” Kupitia njia hiyo na nyinginezo, Paulo alitoa “ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Mdo. 20:18, 20, 21) Wakati huo, watawala Waroma walichochea ibada ya sanamu na watu wengi ‘walionekana kuwa wanaogopa sana miungu.’ Watu walihitaji kumtafuta kwa haraka “Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo,” ambaye wakati huo alikuwa “anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.”—Mdo. 17:22-31.
5 Leo kuna uhitaji mkubwa hata zaidi wa kuwapelekea watu habari njema haraka. Mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unakaribia kwa kasi sana. Tunachochewa kuongeza bidii yetu tunapotambua uhitaji huo. Hakuna njia nyingine bora ya kuwatafuta watu wenye njaa ya kiroho kuliko njia ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ambayo imetumiwa kwa muda mrefu. Bado ina matokeo mazuri leo kama ilivyokuwa katika siku za Yesu na mitume.—Marko 13:10.
6 Je, unashiriki kikamili katika huduma ya nyumba kwa nyumba? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba unamfurahisha Yehova. (Eze. 9:11; Mdo. 20:35) Huenda isiwe rahisi kwako kuhubiri nyumba kwa nyumba. Labda una udhaifu wa kimwili au watu wengi katika eneo lenu hawataki kusikiliza. Au kuna vizuizi vya serikali. Huenda wewe ni mwenye haya, na unaogopa kuzungumza na watu usiowafahamu. Kwa sababu hiyo, kila mara unapohubiri nyumba kwa nyumba unakuwa na wasiwasi. Usikate tamaa. (Kut. 4:10-12) Ndugu zako pia wanakabili hali kama hizo katika maeneo mengine.
7 Yesu aliwaahidi wanafunzi wake hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Ahadi hiyo hutuimarisha tunapofanya kazi ya kuhubiri na kufundisha. Tunahisi kama mtume Paulo aliyesema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.” (Flp. 4:13) Unga mkono kikamili mipango ya kutaniko ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Unapohubiri na wengine, watakutia moyo na kukusaidia kuboresha ustadi wako. Sali ili ushinde vizuizi ambavyo huenda ukakabili, na ujitahidi kuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii.—1 Yoh. 5:14.
8 Unapowatangazia wengine habari njema, utapata nafasi za kuwaeleza ‘sababu ya tumaini ulilo nalo.’ (1 Pet. 3:15) Utafahamu vizuri zaidi tofauti kati ya wale walio na tumaini la Ufalme na wale wasio na tumaini. (Isa. 65:13, 14) Utaridhika kwa kujua kwamba umetii amri ya Yesu ya ‘kuacha nuru yako iangaze,’ na huenda hata ukawa na pendeleo la kuwasaidia wengine wamjue Yehova na wapate kweli inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Mt. 5:16; Yoh. 17:3; 1 Tim. 4:16.
9 Mipango hufanywa ili kuhubiri nyumba kwa nyumba katikati ya juma na pia mwisho juma. Makutaniko fulani hupanga kuhubiri jioni katika maeneo ambayo ni vigumu kuwapata watu nyumbani mchana. Huenda watu wakawa tayari kuwakaribisha wageni alasiri au jioni badala ya asubuhi.
KUWATAFUTA WALE WANAOSTAHILI
10 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake ‘wawatafute’ wale wanaostahili. (Mt. 10:11) Hakuwatafuta watu wenye mwelekeo unaofaa kwa kuhubiri tu nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, alitumia kila nafasi aliyopata ili kuhubiri rasmi au isivyo rasmi. (Luka 8:1; Yoh. 4:7-15) Pia, mitume waliwahubiria watu katika maeneo mbalimbali.—Mdo. 17:17; 28:16, 23, 30, 31.
Lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana
11 Vivyo hivyo, lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana. Hiyo inamaanisha kwamba tunapaswa kuiga njia ambazo Yesu na wanafunzi wake walitumia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha na vilevile kubadilikana kulingana na nyakati na hali za watu katika eneo letu. (1 Kor. 7:31) Kwa mfano, wahubiri wamefanikiwa kuwapata watu katika sehemu zao za biashara. Katika nchi nyingi, wahubiri wamepata matokeo kwa kuhubiri barabarani, bustani za kupumzikia, maegesho ya magari, au popote pale watu wanapopatikana. Makutaniko fulani yamepanga kuhubiri kwa kutumia meza au vigari vyenye machapisho katika eneo
-