-
“Kutafuta Kwanza Ufalme”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Mapema zaidi, The Watch Tower la Julai 1, 1920, lilikuwa limechunguza unabii mkubwa wa Yesu kuhusu ‘ishara ya kuwapo kwake na ya mwisho wa ulimwengu.’ (Mt. 24:3, KJ) Lilikazia fikira kazi ya kuhubiri ambayo lazima ifanywe kwa utimizo wa Mathayo 24:14 na likatambulisha ujumbe utakaotangazwa, likisema: “Habari njema hapa zinahusu mwisho wa utaratibu wa mambo wa kale na kusimamishwa kwa ufalme wa Mesiya.” The Watch Tower lilieleza kwamba kwa msingi wa mahali Yesu aliposema hayo kuhusiana na sehemu nyinginezo za ile ishara, kazi hii ingetimizwa “kati ya wakati wa vita ile kuu ya ulimwengu [Vita ya Ulimwengu 1] na wakati wa ‘dhiki kubwa’ iliyotajwa na Bwana-Mkubwa katika Mathayo 24:21, 22.” Hiyo kazi ilikuwa ya haraka. Ni nani angeifanya?
Kwa wazi daraka hilo lilikuwa juu ya washiriki wa “kanisa,” kutaniko la kweli la Kikristo. Hata hivyo, katika 1932, kupitia toleo la Agosti 1 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), hao walishauriwa watie moyo “jamii ya Kiyehonadabu” kushiriki nao katika kazi, kwa kupatana na roho ya Ufunuo 22:17. Jamii ya Kiyehonadabu—ambayo tumaini layo ni uhai wa milele katika dunia-Paradiso—iliitikia, na wengi wao walifanya hivyo kwa bidii.
Umaana mkubwa wa kazi hii umekaziwa sana: “Ni jambo la maana kushiriki katika utumishi wa Bwana kama vile ilivyo kuhudhuria mkutano,” likasema The Watch Tower katika 1921. “Kila mmoja lazima awe mhubiri wa gospeli,” likaonyesha katika 1922. “Yehova amefanya kuhubiri kuwe kazi ya maana sana awezayo yeyote kati yetu kufanya katika ulimwengu huu,” likasema katika 1949. Julisho rasmi la mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 9:16 (NW), limenukuliwa mara nyingi: “Nimewekewa sharti. Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sikutangaza habari njema!” Andiko hilo limetumiwa kuhusu kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
-
-
“Kutafuta Kwanza Ufalme”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Je, Mashahidi wa Yehova hufikiri kwamba kwa njia fulani wanastahili wokovu kwa utendaji wao wa kuhubiri? La hasha! Kitabu Wenye Umoja Katika Ibada ya Mungu wa Pekee wa Kweli, ambacho kimetumiwa tangu 1983 kusaidia wanafunzi kuendelea kufikia ukomavu wa Kikristo, kinazungumzia jambo hilo. Kinasema: “Vilevile dhabihu ya Yesu imetufungulia nafasi ya kupata uzima wa milele . . . Hiyo si thawabu tunayojipatia kwa ustahili wa kufanya kazi. Hata tufanye mengi namna gani katika utumishi wa Yehova, hatuwezi kamwe kujifanyia ustahili huo hata Mungu awe na deni kwetu la kutulipa uzima. Uzima wa milele ni ‘zawadi anayotoa Mungu . . . kwa njia ya Kristo Yesu, Bwana wetu.’ (Rum. 6:23; Efe. 2:8-10, NW) Hata hivyo, tukiwa na imani katika zawadi hiyo na kuthamini ni kwa jinsi gani ilifanywa iwezekane, tutaonyesha hilo. Kwa kufahamu namna Yehova ametumia Yesu kwa njia ya ajabu katika kutimiza mapenzi Yake na namna lilivyo jambo la maana sana kwetu sote kufuata sana hatua za Yesu, tutaifanya huduma ya Kikristo iwe mojapo mambo ya maana zaidi katika maisha zetu.”
Je, yaweza kusemwa kwamba Mashahidi wa Yehova wote ni watangazaji wa Ufalme wa Mungu? Ndiyo! Kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwamaanisha hivyo. Zaidi ya nusu karne iliyopita, kuna wale waliohisi kwamba haikuwa lazima kwao kushiriki katika utumishi wa shambani, kwenda hadharani na nyumba hadi nyumba. Lakini leo hakuna yeyote kati ya Mashahidi wa Yehova anayedai asihusishwe na utumishi huo kwa sababu ya daraka lake katika kutaniko la mahali au katika tengenezo la ulimwenguni pote. Wanaume na wanawake pamoja na wachanga na wazee hushiriki. Wao huuona kuwa pendeleo lenye thamani, utumishi mtakatifu. Watu wengi hupiga mbiu wajapokuwa na udhaifu mbaya. Na kwa wowote ambao hawawezi kimwili kwenda nyumba hadi nyumba, wao hupata njia nyinginezo za kuwafikia watu na kuwapa ushahidi kibinafsi.
Nyakati nyingine zamani, kulikuwa na mwelekeo wa kuruhusu wapya zaidi washiriki katika utumishi wa shambani mapema mno. Lakini katika miongo ya hivi karibuni, mkazo mkubwa umewekwa juu ya kustahili kabla ya kualikwa. Hilo linamaanisha nini? Halimaanishi kwamba ni lazima waweze kueleza kila kitu katika Biblia. Lakini, kama vile kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu kinavyofafanua, ni lazima wajue na waamini mafundisho ya msingi ya Biblia. Ni lazima pia wawe wanaishi maisha safi, kupatana na viwango vya Biblia. Ni lazima kila mmoja atake kikweli kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
-