Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Endelea Kuangalia Huduma Ambayo Uliikubali Katika Bwana”
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Januari 15
    • Kwa Nini Watu Wengi Hawana Tumaini?

      4, 5. Wanadamu wanakumbwa na nini, na watu wengi wanahisi namna gani?

      4 Matukio ya ulimwengu yanaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” na mwisho uko karibu sana. Wanadamu wanakumbwa na matukio na hali ambazo Yesu na wanafunzi wake walisema zingekuwapo katika “siku za mwisho.” “Maumivu ya taabu,” kutia ndani vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya nchi, na misiba mingine inawakumba wanadamu. Uasi-sheria, uchoyo, na mitazamo ya kutomwogopa Mungu imeenea sana. Hata watu ambao wanajitahidi kuishi kupatana na viwango vya Biblia wanakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”—Mt. 24:3, 6-8, 12; 2 Tim. 3:1-5.

      5 Hata hivyo, wanadamu wengi hawajui matukio ya ulimwengu yanamaanisha nini. Kwa sababu hiyo, wanahangaikia usalama wao na wa familia zao. Wengi wanafadhaika sana wanapofiwa na wapendwa wao au wanapopata misiba mingine. Watu hao hawana tumaini kwa sababu hawana ujuzi sahihi kuhusu kwa nini mambo kama hayo yanatukia na suluhisho ni nini.—Efe. 2:12.

      6. Kwa nini “Babiloni Mkubwa” ameshindwa kuwasaidia wafuasi wake?

      6 “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, haijawafariji wanadamu. Badala yake, kupitia “divai ya uasherati wake” imefanya watu wengi wayumbe-yumbe na kuvurugika kiroho. Zaidi ya hayo, kama kahaba, dini ya uwongo imewashawishi na kuwaongoza “wafalme wa dunia.” Inatumia mafundisho ya uwongo na mazoea ya kuwasiliana na pepo kuwafanya wanadamu wengi wajitiishe kabisa kwa viongozi wao wa kisiasa. Kwa hiyo, dini ya uwongo imekuwa na nguvu na uvutano, hata hivyo, imekataa kabisa kweli ya kidini.—Ufu. 17:1, 2, 5; 18:23.

      7. Wanadamu wengi watapatwa na nini, lakini baadhi yao wanaweza kusaidiwa jinsi gani?

      7 Yesu alifundisha kwamba wanadamu wengi wanatembea katika barabara pana ambayo inaongoza kwenye uharibifu. (Mt. 7:13, 14) Watu fulani wako kwenye barabara hiyo pana kwa sababu wameamua kukataa kimakusudi mafundisho ya Biblia, lakini wengine wengi wako kwenye barabara hiyo kwa sababu wamedanganywa, au wako gizani kwa sababu hawajafundishwa na viongozi wao wa kidini mambo ambayo kwa kweli Yehova anataka wafanye. Labda wengine wangebadili maisha yao ikiwa wangeonyeshwa waziwazi sababu za Kimaandiko za kufanya hivyo. Lakini wale ambao wanabaki ndani ya Babiloni Mkubwa na kuendelea kukataa viwango vya Biblia hawataokolewa wakati wa “ile dhiki kuu.”—Ufu. 7:14.

  • “Endelea Kuangalia Huduma Ambayo Uliikubali Katika Bwana”
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Januari 15
    • “Endelea Kuangalia Huduma” Yako

      14. Mtume Paulo aliwawekea Wakristo wenzake mfano gani, naye alitoa shauri gani?

      14 Mtume Paulo aliitimiza huduma yake kwa bidii sana, naye aliwatia moyo waamini wenzake wafanye hivyo. (Mdo. 20:20, 21; 1 Kor. 11:1) Mtu mmoja ambaye Paulo alimtia moyo sana ni Arkipo, Mkristo aliyeishi katika karne ya kwanza. Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Wakolosai: “Mwambieni Arkipo hivi: ‘Endelea kuangalia huduma ambayo uliikubali katika Bwana, ili uitimize.’” (Kol. 4:17) Hatujui Arkipo alikuwa nani au alikabili hali gani, lakini tunajua kwamba aliikubali huduma. Ikiwa wewe ni Mkristo aliyejiweka wakfu, wewe pia umeikubali huduma. Je, unaendelea kuiangalia huduma hiyo ili uitimize?

      15. Wakfu wa Mkristo unahusisha nini, na ni maswali gani yanayotokea?

      15 Kabla ya kubatizwa, tulisali kutoka moyoni na kuweka wakfu maisha yetu kwa Yehova. Hivyo, tuliazimia kufanya mapenzi yake. Kwa hiyo basi, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, kweli kufanya mapenzi ya Mungu ndilo jambo la maana zaidi maishani mwangu?’ Huenda tukawa na wajibu mbalimbali ambao Yehova anatutazamia tutimize, kama vile kuandaa mahitaji ya familia yetu. (1 Tim. 5:8) Lakini tunatumia namna gani nguvu na wakati wetu unaobaki? Tunatanguliza nini maishani?—Soma 2 Wakorintho 5:14, 15.

      16, 17. Vijana Wakristo au wale ambao hawana madaraka mengi wanaweza kufikiria mapendeleo gani?

      16 Je, wewe ni Mkristo kijana aliyejiweka wakfu ambaye amemaliza au anakaribia kumaliza masomo? Inaelekea kwamba kwa sasa huna madaraka mazito ya familia. Basi, unapanga kutumia maisha yako jinsi gani? Ni maamuzi gani ambayo yatakusaidia zaidi kutimiza ahadi yako ya kufanya mapenzi ya Yehova? Vijana wengi wamepanga mambo yao ili wafanye upainia, na wamepata uradhi na shangwe kubwa sana.—Zab. 110:3; Mhu. 12:1.

      17 Labda wewe ni kijana. Umeajiriwa kazi ya wakati wote lakini huna madaraka mengi isipokuwa kutimiza mahitaji yako. Bila shaka, unafurahi kushiriki katika utendaji wa kutaniko kadiri hali zako zinavyokuruhusu. Je, unaweza kupata shangwe zaidi? Je, umefikiria kupanua huduma yako? (Zab. 34:8; Met. 10:22) Katika maeneo fulani, bado kuna kazi nyingi ya kumtangazia kila mtu ujumbe wa kweli unaoleta uzima. Je, unaweza kufanya mabadiliko fulani katika maisha yako ili utumike katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme?—Soma 1 Timotheo 6:6-8.

      18. Wenzi fulani wa ndoa ambao ni vijana walifanya mabadiliko gani, na matokeo yalikuwa nini?

      18 Kwa mfano, mfikirie Kevin na Elena, kutoka Marekani.a Walitaka sana kununua nyumba kama wenzi wengi wa ndoa wanavyofanya katika eneo lao baada ya kufunga ndoa. Wote wawili walifanya kazi ya wakati wote na waliishi maisha ya starehe. Lakini, hawakuwa na wakati wa kutosha wa kushiriki katika utumishi wa shambani kwa sababu ya kazi zao za kuajiriwa na kazi nyingine za nyumbani. Walitambua kwamba walikuwa wakitumia wakati na nguvu nyingi kutunza mali yao. Hata hivyo, Kevin na Elena walipoona maisha rahisi na yenye furaha ya wenzi fulani wa ndoa mapainia, waliamua kubadili mambo wanayotanguliza maishani. Baada ya kutafuta mwongozo wa Yehova kupitia sala, waliuza nyumba yao na kuhamia kwenye nyumba ya kupanga. Elena aliamua kufanya kazi kwa saa chache na akawa painia. Kevin alichochewa na matokeo mazuri ambayo mke wake alikuwa akipata katika huduma, akaacha kazi yake ya wakati wote na akawa painia. Punde si punde, walihamia nchi moja ya Amerika Kusini ili watumike katika eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Kevin anasema hivi: “Ndoa yetu ilikuwa yenye furaha sikuzote, lakini tulipojitahidi kufikia miradi ya kiroho, furaha yetu iliongezeka zaidi.”—Soma Mathayo 6:19-22.

      19, 20. Kwa nini kuhubiri habari njema ndiyo kazi ya maana zaidi leo?

      19 Kuhubiri habari njema ndiyo kazi ya maana zaidi inayofanywa duniani leo. (Ufu. 14:6, 7) Inachangia kutakaswa kwa jina la Yehova. (Mt. 6:9) Ujumbe wa Biblia unaboresha maisha ya maelfu ya watu ambao wanaukubali kila mwaka, na hilo linaweza kuwaongoza kwenye wokovu. Hata hivyo, “watasikiaje bila mtu wa kuhubiri?” akauliza mtume Paulo. (Rom. 10:14, 15) Kwa kweli watasikiaje tusipohubiri? Kwa nini usiazimie kufanya yote unayoweza ili utimize huduma yako?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki