Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Usitawi wa Muundo wa Tengenezo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kupanga Mambo Kitengenezo ili Habari Njema Zipate Kuhubiriwa

      Katika hatua ya mapema sana, Ndugu Russell alitambua kwamba mojapo madaraka ya maana sana kwa kila mshiriki wa kutaniko la Kikristo lilikuwa kazi ya kueneza evanjeli. (1 Pet. 2:9) Watch Tower lilieleza kwamba maneno ya kiunabii ya Isaya 61:1 hayakuhusu Yesu pekee bali pia wafuasi wake wote watiwa-mafuta kwa roho, yaani: “Bwana amenitia mafuta, niwahubiri wanyenyekevu habari njema,” au, kama vile King James Version hutafsiri nukuu la Yesu la fungu hilo, ‘Amenitia mafuta kuhubiri gospeli.’—Luka 4:18.

      Mapema sana kama 1881, Watch Tower lilikuwa na makala “Wahubiri 1,000 Watakwa.” Hiyo ilikuwa sihi kwa kila mshiriki wa kutaniko atumie wakati wowote ambao angeweza (nusu saa, saa moja, au mbili, au tatu) kushiriki katika kueneza kweli ya Biblia. Wanaume na wanawake ambao hawakuwa na familia zilizowategemea na ambao wangeweza kutoa kabisa nusu au zaidi ya wakati wao kwa kazi ya Bwana walitiwa moyo waanze kazi wakiwa waeneza-evanjeli makolpota. Idadi hiyo ilitofautiana sana mwaka mmoja na mwingine, lakini kufikia 1885 kulikuwa tayari kama 300 waliokuwa wakishiriki kazi hiyo wakiwa makolpota. Baadhi yao pia walishiriki lakini kwa kadiri ndogo zaidi. Madokezo yalitolewa kwa makolpota kuhusu jinsi ya kufanya kazi yao. Lakini shamba lilikuwa kubwa, na angalau mwanzoni, waliteua eneo lao wenyewe na kwenda toka eneo moja hadi jingine sanasana kama walivyoona kuwa vema. Halafu walipokutana kwenye mikusanyiko, walikuwa wakifanya marekebisho yaliyohitajiwa ili kuratibu jitihada zao.

      Mwaka huohuo ambao utumishi wa kolpota ulianza, Ndugu Russell alichapisha idadi fulani ya trakti (au vijitabu) vigawanywe bila malipo. Chenye kutokeza miongoni mwazo kilikuwa kile kijitabu Food for Thinking Christians, kilichogawanywa kufikia idadi ya nakala 1,200,000 katika miezi minne ya kwanza. Kazi iliyohusika katika kupanga uchapaji na ugawanyaji huo ndiyo iliyosababisha kufanyizwa kwa Zion’s Watch Tower Tract Society ili kuangalia mambo ya muhimu. Kuzuia kukatizwa kwa kazi ikiwa kifo chake chatukia, na ili kurahisisha kushughulikiwa kwa michango ipaswayo kutumiwa katika kazi, Ndugu Russell aliomba Sosaiti isajiliwe kisheria, na jambo hilo lilitiwa katika rekodi Desemba 15, 1884. Jambo hilo lilitokeza chombo cha kisheria kilichohitajiwa.

      Uhitaji ulipozuka, ofisi za tawi za Watch Tower Society zilianzishwa katika nchi nyinginezo. Ya kwanza ilikuwa katika London, Uingereza, katika Aprili 23, 1900. Nyingine, katika Elberfeld, Ujerumani, katika 1902. Miaka miwili baadaye, kwenye ule upande mwingine wa dunia, tawi lilipangwa kitengenezo katika Melbourne, Australia. Wakati wa kuandika kitabu hiki, kuna matawi 99 ulimwenguni pote.

      Ijapokuwa mipango ya kitengenezo iliyohitajiwa ili kutayarisha kiasi kikubwa cha fasihi ya Biblia ilikuwa ikisitawishwa, mwanzoni makutaniko yaliachwa yafanye mipango yao ya kugawanya hadharani habari hiyo. Katika barua yenye tarehe ya Machi 16, 1900, Ndugu Russell alieleza jinsi alivyoliona jambo hilo. Barua hiyo aliyopelekewa “Alexander M. Graham, na Kanisa katika Boston, Mass[achusetts],” ilisema hivi: “Kama vile nyinyi nyote mjuavyo, kusudi langu thabiti ni kuacha kila kampuni ya watu wa Bwana kusimamia mambo yao wenyewe, kulingana na maamuzi yao wenyewe, nikitoa madokezo, si kwa njia ya kuingilia [mambo], bali kwa njia tu ya shauri.” Hilo lilitia ndani si mikutano yao tu bali pia njia ambayo waliendesha huduma yao ya shambani. Hivyo, baada ya kuwapa akina ndugu shauri fulani litumikalo, alimalizia kwa elezo hili: “Hili ni dokezo tu.”

      Utendaji fulani ulitaka mwelekezo hususa zaidi kutoka kwa Sosaiti. Kuhusiana na kuonyeshwa kwa ile “Photo-Drama of Creation,” kila kutaniko liliachwa liamue kama walikuwa na nia na uwezo wa kukodi jumba la maonyesho au jumba jingine katika mahali pao la kuionyeshea. Hata hivyo, ilikuwa lazima kuhamisha vifaa toka jiji hadi jiji, na ilikuwa lazima kufuata ratiba; hivyo, kwa sababu hizo mwelekezo kutoka makao makuu ulitolewa na Sosaiti. Kila kutaniko lilitiwa moyo liwe na Halmashauri ya Drama ya kushughulikia mipango ya kwao. Lakini msimamizi aliyepelekwa na Sosaiti alishughulikia kwa uangalifu yale mambo madogo-madogo ili kuhakikisha kwamba kila jambo limefanywa kwa utaratibu.

      Kadiri miaka 1914 na kisha 1915 ilivyopita, Wakristo hao watiwa-mafuta kwa roho walingojea kwa hamu utimizo wa tumaini lao la kimbingu. Wakati uleule, walitiwa moyo waendelee kujishughulisha na utumishi wa Bwana. Hata ingawa waliona wakati wao uliobaki katika mwili kuwa mfupi, ilipata kuwa wazi kwamba ili kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema kwa njia ya utaratibu, mwelekezo zaidi ulihitajiwa kuliko wakati ambao walikuwa na idadi ya mamia wachache tu. Muda mfupi baada ya J. F. Rutherford kuwa msimamizi wa pili wa Watch Tower Society, mwelekezo huo ulianza kuwa na sura mpya. Toleo la Machi 1, 1917, la The Watch Tower lilitangaza kwamba, kuanzia hapo na kuendelea, ofisi ya Sosaiti itakuwa ikiwagawia makolpota na wafanyakazi wa uchungajie katika makutaniko maeneo yote ya kufanyia kazi. Mahali palipokuwa na wafanyakazi wenyeji na makolpota pia wakishiriki katika utumishi kama huo wa shambani katika jiji au wilaya, eneo liligawanywa miongoni mwao na halmashauri ya wilaya ya mahali iliyowekwa. Mpango huo ulichangia ugawanyaji wenye kutokeza kikweli wa The Finished Mystery katika muda wa miezi michache tu katika 1917-1918. Mpango huo ulikuwa wenye thamani pia katika kupata ugawanyaji wa kasi wa nakala 10,000,000 za ufichuo wenye nguvu wa Jumuiya ya Wakristo katika trakti iliyozungumzia habari “Kuanguka kwa Babiloni.”

      Muda mfupi baada ya hilo, washiriki wa wafanyakazi wa usimamizi wa Sosaiti walikamatwa, na Juni 21, 1918, wakahukumiwa vifungo vya miaka 20 gerezani. Kazi ya kuhubiri habari njema ikakaribia sana kukoma. Je, huo ulikuwa ndio wakati ambao hatimaye wangeunganishwa na Bwana katika utukufu wa kimbingu?

      Miezi michache baadaye, vita ikaisha. Mwaka uliofuata wakuu wa Sosaiti wakafunguliwa. Walikuwa wangali katika mwili. Hawakuwa wametarajia hilo, lakini walikata kauli kwamba lazima Mungu awe na kazi aliyotaka waifanye hapa duniani.

      Walikuwa ndipo wametoka tu katika mitihani mikali ya imani yao. Hata hivyo, katika 1919, The Watch Tower liliwaimarisha kwa mafunzo ya Kimaandiko yenye kuwachochea juu ya kichwa “Wabarikiwa Ni Wasioogopa.” Hayo yalifuatwa na makala “Fursa za Utumishi.” Lakini ndugu hawakuwazia usitawi mkubwa wa kitengenezo ambao ungetukia wakati wa miongo ambayo ingefuata.

      Kielelezo Kifaacho kwa Kundi

      Ndugu Rutherford alijua kwamba ili kazi iendelee kusonga mbele kwa njia ya utaratibu na ya umoja, hata wakati uwe mfupi kadiri gani, kielelezo kifaacho kwa kundi ni cha muhimu. Yesu alikuwa amewaeleza wafuasi wake kuwa kama kondoo, na kondoo hufuata mchungaji wao. Bila shaka, Yesu mwenyewe ndiye Mchungaji Mwema, lakini yeye hutumia pia wanaume wazee, au wazee, wakiwa wachungaji wadogo wa watu wake. (1 Pet. 5:1-3) Wazee hao lazima wawe wanaume ambao wao wenyewe hushiriki katika kazi ambayo Yesu aliwagawia na ambao huwatia wengine moyo wafanye hivyo. Ni lazima wawe kikweli na roho ya kueneza evanjeli. Hata hivyo, wakati wa ugawanyaji wa The Finished Mystery, baadhi ya wazee walikuwa wamekataa; wengine hata walisema waziwazi sana wakiwavunja wengine moyo wasishiriki.

      Hatua ya maana sana kuelekea kusahihishwa kwa hali hiyo ilichukuliwa katika 1919 gazeti The Golden Age lilipoanza kutangazwa. Hilo lingekuwa kifaa chenye nguvu cha kutangaza Ufalme wa Mungu kuwa utatuzi pekee wenye kudumu kwa matatizo ya wanadamu. Kila kutaniko ambalo lilitaka kushiriki katika utendaji huo lilialikwa liombe kwamba lisajiliwe na Sosaiti kuwa “tengenezo la utumishi.” Halafu mwelekezi, au mwelekezi wa utumishi kama alivyokuja kujulikana, ambaye hakulazimika kuchaguliwa kila mwaka, aliwekwa na Sosaiti.f Akiwa ndiye mwakilishi wa Sosaiti mwenyeji, alipaswa kupanga kazi, kutoa migawo ya eneo, na kutia kutaniko moyo lishiriki katika utumishi wa shambani. Hivyo, sambamba na wazee na mashemasi waliochaguliwa kidemokrasi, mpango wa kitengenezo wa aina nyingine ulianza kufanya kazi, ambao ulitambua mamlaka yenye kuweka rasmi yaliyo nje ya kutaniko la mahali na ambao ulitia mkazo mwingi zaidi katika kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu.g

      Wakati wa miaka iliyofuata, kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme ilipewa msukumo mkubwa, kana kwamba kwa kani isiyoweza kukinzwa. Matukio ya 1914 na baada ya hapo yalikuwa yameonyesha wazi kwamba ule unabii mkubwa ambao katika huo Bwana Yesu Kristo alikuwa ameueleza umalizio wa mfumo wa kale ulikuwa ukitimizwa. Kukiwa na maoni hayo, katika 1920, The Watch Tower lilionyesha kwamba kama ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24:14, huu ndio wakati wa kupiga mbiu ya habari njema kuhusu “mwisho wa utaratibu wa mambo wa kale na kusimamishwa kwa ufalme wa Mesiya.”h (Mt. 24:3-14) Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia katika Cedar Point, Ohio, katika 1922, wajumbe waliondoka shime hii ikiwa inalia masikioni mwao: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Daraka la Wakristo wa kweli lilipata kutambuliwa wazi zaidi na likakaziwa zaidi katika 1931 wakati jina Mashahidi wa Yehova lilipokubaliwa.

      Ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa amegawia watumishi wake kazi ambayo wote wangeweza kushiriki. Kulikuwa itikio lenye idili. Wengi walifanya marekebisho katika maisha zao ili kutumia wakati wao wote katika kazi hiyo. Hata miongoni mwa wale waliotumia sehemu tu ya wakati, idadi kubwa ilitumia siku nzimanzima katika utumishi wa shambani mwishoni mwa juma. Wakiitikia kitia-moyo kilichokuwa katika Mnara wa Mlinzi na Informant (Mpasha-Habari) katika 1938 na 1939, wengi kati ya Mashahidi wa Yehova wakati huo walijitahidi kwa kudhamiria kutumia saa 60 kila mwezi katika utumishi wa shambani.

      Miongoni mwa Mashahidi hao wenye bidii, walikuwamo watumishi wa Yehova wengi wanyenyekevu na waliojitoa, ambao walikuwa wazee katika makutaniko. Hata hivyo, katika sehemu nyingine, wakati wa miaka ya 1920 na mapema katika miaka ya 1930, kulikuwako pia ukinzani mwingi kwa wazo la kila mtu kushiriki katika utumishi wa shambani. Wazee waliochaguliwa kidemokrasi mara nyingi walisema waziwazi wakipinga yale ambayo The Watch Tower lilisema juu ya daraka la kuhubiria watu walio nje ya kutaniko. Kukataa kusikiliza yale ambayo roho ya Mungu ilihitaji kuliambia kutaniko juu ya jambo hilo kwa njia ya Maandiko Matakatifu, kulizuia umiminikaji wa roho ya Mungu katika vikundi hivyo.—Ufu. 2:5, 7.

      Hatua zilichukuliwa katika 1932 kusahihisha hali hiyo. Jambo la kuhangaikiwa zaidi halikuwa kama baadhi ya wazee mashuhuri wangeudhiwa au kama baadhi ya wale walioshirikiana na makutaniko wangeondoka. Bali, tamaa ya akina ndugu ilikuwa kumpendeza Yehova na kufanya mapenzi yake. Kwa kusudi hilo, matoleo ya Agosti 15 na Septemba 1 ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) mwaka huo yalizungumzia habari “Tengenezo la Yehova.”

      Makala hizo zilionyesha waziwazi kwamba wote ambao walikuwa sehemu ya tengenezo la Yehova kwelikweli wangeshiriki kazi ambayo Neno lake lilisema lazima ifanywe katika pindi hii ya wakati. Makala hizo zilitetea maoni ya kwamba uzee wa Kikristo si cheo ambacho kwacho mtu angeweza kuchaguliwa bali ilikuwa hali ifikiwayo kwa ukuzi wa kiroho. Mkazo wa pekee ulitolewa kwenye sala ya Yesu kwamba wafuasi wake wangeweza ‘wote kuwa mmoja’—katika muungano na Mungu na Kristo, na hivyo kuwa na umoja mtu na mwenzake katika kufanya mapenzi ya Mungu. (Yn. 17:21, NW) Nayo matokeo yakawa nini? Makala ya pili ilijibu hivi kwamba “kila mmoja wa mabaki lazima awe shahidi kwa jina na ufalme wa Yehova Mungu.” Wowote walioshindwa au waliokataa kufanya yale ambayo wangeweza kwa kadiri fulani kushiriki katika kutoa ushahidi hadharani hawangepewa uangalizi.

      Kwenye umalizio wa funzo la makala hizo, makutaniko yalialikwa yapitishe azimio yakionyesha kukubali kwao. Hivyo uchaguzi wa kila mwaka wa kutaniko wa wanaume kuwa wazee na mashemasi ukaondolewa. Katika Belfast, Ireland Kaskazini, kama kwingineko, baadhi ya wale waliokuwa hapo kwanza “wazee wa kuchaguliwa” waliondoka; wengine mmoja-mmoja walioshiriki maoni yao waliondoka pamoja nao. Hilo lilitokeza upungufu wa idadi lakini kuimarishwa kwa tengenezo zima. Wale waliobaki walikuwa watu waliokuwa tayari kubeba daraka la Kikristo la kutoa ushahidi. Badala ya kupigia wazee kura, makutaniko—yakiwa bado yanatumia njia ya kidemokrasi—yaliteua halmashauri ya utumishii ambayo washiriki wayo walikuwa wanaume wakomavu kiroho walioshiriki kwa bidii kutoa ushahidi hadharani. Washiriki wa kutaniko pia walipiga kura kuchagua mwenyekiti wa kusimamia mikutano yao pamoja na mwandishi na mweka-hazina. Wote hao walikuwa wanaume waliokuwa mashahidi wa Yehova watendaji.

      Wanaume waliopendezwa si na cheo chao binafsi bali na kufanya kazi ya Mungu wakiwa sasa wamepewa uangalizi wa kutaniko—kutoa ushahidi kwa jina na Ufalme wake—na ambao walikuwa wakiweka kielelezo kwa kuishiriki wao wenyewe, kazi ilisonga mbele kwa utaratibu zaidi. Ijapokuwa hawakuwa wakijua wakati ule, kulikuwa mengi ya kufanywa, ushahidi ulioenezwa zaidi kuliko ule uliokuwa tayari umetolewa, kukusanya ndani ambako hawakuwa wametarajia. (Isa. 55:5) Kwa wazi Yehova alikuwa akiwatayarisha kwa ajili ya kazi hiyo.

      Wachache wenye tumaini la uhai wa milele duniani walikuwa wameanza kushirikiana nao.j Hata hivyo, Biblia ilitabiri kukusanywa kwa halaiki kubwa (au, umati mkubwa) kwa kusudi la kuhifadhiwa kwao kuipita dhiki kubwa. (Ufu. 7:9-14) Katika 1935 utambulisho wa hii halaiki kubwa ulielezwa wazi. Mabadiliko katika kuteuliwa kwa waangalizi wakati wa miaka ya 1930 yalilitayarisha tengenezo liweze kutunza vizuri zaidi kazi ya kuwakusanya, kuwafundisha, na kuwazoeza.

      Kwa walio wengi kati ya Mashahidi wa Yehova, kazi hiyo iliyopanuka ilikuwa usitawi wenye kusisimua. Huduma yao ya shambani ilichukua umaana mpya. Hata hivyo, baadhi yao hawakuwa na hamu ya kuhubiri. Walijizuia kushiriki kazi, nao walijaribu kutetea kutotenda kwao kwa kutoa hoja kwamba hakuna halaiki kubwa ambayo ingekusanywa mpaka baada ya Har–Magedoni. Lakini walio wengi walitambua fursa iliyoongezwa ya kuonyesha uaminifu-mshikamanifu wao kwa Yehova na upendo wao kwa wanadamu wenzao.

      Wale wa umati mkubwa walifaanaje na muundo wa tengenezo? Walionyeshwa daraka ambalo Neno la Mungu liligawia lile “kundi dogo” la watiwa-mafuta kwa roho, nao walifanya kazi kwa nderemo kupatana na mpango huo. (Luka 12:32-44, NW) Pia walijifunza kwamba, kama vile watiwa-mafuta kwa roho, walikuwa na daraka la kushiriki habari njema na wengine. (Ufu. 22:17) Kwa kuwa walitaka kuwa raia za kidunia za Ufalme wa Mungu, Ufalme huo ulipaswa kutangulizwa maishani mwao, nao walipaswa kuwa wenye bidii katika kuambia wengine juu yao. Ili wafaane na elezo la Biblia la wale ambao wangehifadhiwa kuipita ile dhiki kubwa kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu, lazima wawe watu ambao ‘hufuliza kulia kwa sauti kubwa, wakisema: “Sisi tunawiwa wokovu na Mungu wetu, aketiye juu ya hicho kiti cha ufalme, na kwa Mwana-Kondoo.”’ (Ufu. 7:10, 14, NW) Katika 1937, idadi zao zilipoanza kukua na bidii yao kwa ajili ya Bwana ikadhihirika, walialikwa pia wasaidie kuchukua furushi la daraka katika uangalizi wa kutaniko.

      Hata hivyo, walikumbushwa kwamba tengenezo ni la Yehova, si la mwanadamu yeyote. Hakukupaswa kuwe na mgawanyiko kati ya mabaki ya watiwa-mafuta kwa roho na wale wa umati mkubwa wa kondoo wengine. Walipaswa kufanya kazi pamoja wakiwa ndugu na dada katika utumishi wa Yehova. Kama vile Yesu alivyokuwa amesema, “Nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia lazima niwalete, nao watasikiliza sauti yangu, nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.” (Yn. 10:16, NW) Uhalisi wa jambo hilo ulikuwa ukidhihirika.

  • Usitawi wa Muundo wa Tengenezo
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 215]

      Maswali ya V.D.M.

      Herufi V.D.M. huwakilisha maneno ya Kilatini “Verbi Dei Minister,” au Mhudumu wa Neno la Mungu.

      Katika 1916 orodha ya maswali juu ya mambo ya Kimaandiko ilitayarishwa na Sosaiti. Wale ambao wangewakilisha Sosaiti wakiwa wasemaji waliombwa wajibu kila moja la maswali hayo kwa kuandika. Hilo liliwezesha Sosaiti kujua mawazo, maoni, na uelewevu wa ndugu hao kwa habari ya kweli za Biblia za msingi. Majibu yaliyoandikwa yalichunguzwa kwa uangalifu na baraza la kutahini katika ofisi za Sosaiti. Wale waliotambuliwa kuwa wastahili kuwa wasemaji walipaswa kuwa na gredi ya asilimia 85 au zaidi.

      Baadaye, wengi kati ya wazee, mashemasi, na Wanafunzi wa Biblia wengine waliomba kama wangeweza kuwa na orodha ya maswali hayo. Baada ya wakati, ilitaarifiwa kwamba ingefaa ikiwa madarasa yangeteua wawakilishi wao kuwa watu wale tu waliokuwa wamestahili kuwa V.D.M.

      Sosaiti ilipotoa shahada (digrii) ya Mhudumu wa Neno la Mungu, hiyo haikumaanisha kuwa mtu huyo alikuwa akiagizwa rasmi. Ilionyesha tu kwamba baraza la kutahini katika ofisi za Sosaiti lilikuwa limepitia ukuzi wa kimafundisho wa mtu huyo, na sifa yake kwa kadiri ifaayo, na kukata kauli kwamba alikuwa amestahili kuitwa Mhudumu wa Neno la Mungu.

      Maswali ya V.D.M. ni kama yafuatavyo:

      (1) Ni nini lililokuwa tendo la kwanza la uumbaji wa Mungu?

      (2) Ni nini maana ya neno “Logosi,” kama lishirikishwavyo na Mwana wa Mungu? na ni nini linalomaanishwa na maneno Baba na Mwana?

      (3) Ni lini na jinsi gani dhambi ilipoingia ulimwenguni?

      (4) Ni nini adhabu ya Kimungu ya dhambi juu ya watenda dhambi? na watenda dhambi ni nani?

      (5) Kwa nini ilihitajiwa “Logosi” afanywe kuwa mwili? na je, Yeye “alivikwa mwili”?

      (6) Mwanadamu Kristo Yesu alikuwa wa asili gani kutoka utoto hadi kifo?

      (7) Yesu alikuwa wa asili gani tangu ufufuo; na ni upi ulio uhusiano Wake rasmi na Yehova?

      (8) Ni nini iliyo kazi ya Yesu wakati wa hii Enzi ya Gospeli—katika pindi ya tangu wakati wa Pentekoste mpaka sasa?

      (9) Kufikia hapo ulimwengu wa wanadamu umefanyiwa nini na Yehova Mungu? na Yesu?

      (10) Ni nini lililo kusudi la Kimungu kwa habari ya Kanisa likamilishwapo?

      (11) Ni nini lililo kusudi la Kimungu kwa habari ya wanadamu?

      (12) Ni nini yatakayokuwa matokeo kwa wale ambao hatimaye watakuwa wasiobadilika?

      (13) Ni nini zitakazokuwa thawabu au baraka zitakazoujia ulimwengu wa wanadamu kupitia utii kwa Ufalme wa Mesiya?

      (14) Ni kwa kuchukua hatua zipi mtenda dhambi aweza kuja katika uhusiano ulio muhimu pamoja na Kristo na pamoja na Baba wa Kimbingu?

      (15) Baada ya Mkristo kuzaliwa kwa Roho Takatifu, mwendo wake ni upi, kama ielekezwavyo katika Neno la Mungu?

      (16) Je, wewe umegeuka kutoka katika dhambi umtumikie Mungu aliye hai?

      (17) Je, umetakasa kabisa maisha yako na uwezo wako na vipawa vyako kwa Bwana na utumishi Wake?

      (18) Je, umefananisha utakaso huo kwa uzamisho wa maji?

      (19) Je, umechukua Nadhiri ya I.B.S.A. [International Bible Students Association] ya utakatifu wa uhai?

      (20) Je, umesoma kikamili na kwa uangalifu yale mabuku sita ya STUDIES IN THE SCRIPTURES?

      (21) Je, umepata nuru nyingi ya elimu na manufaa kutokana nayo?

      (22) Je, wewe unaamini kwamba una ujuzi wa Biblia wa kutosha na wenye kudumu utakaokufanya uwe mwenye mafanikio zaidi ukiwa mtumishi wa Bwana muda wote ubakio wa maisha yako?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki