-
Kutumia MuhtasariFaidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
-
-
Je, unajitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani? Panga mkoba wako na ufikirie mambo utakayosema. Ukiamua kutumia mmojawapo wa utangulizi katika Huduma Yetu ya Ufalme, uusome mara kadhaa ili ukumbuke vizuri mambo makuu. Taja mambo hayo katika sentensi moja au mbili. Tumia maneno ya utangulizi huo kwa kupatana na hali zako na hali za eneo lenu. Inafaa kuwa na muhtasari fulani akilini. Muhtasari huo unaweza kuwa na nini? (1) Kwenye utangulizi, unaweza kutaja jambo ambalo linawahangaisha watu wengi katika eneo lenu. Mpe nafasi mwenye nyumba atoe maoni yake. (2) Fikiria jambo fulani hususa ambalo unaweza kuzungumza naye kuhusu habari hiyo, pamoja na andiko moja au maandiko mawili yanayoonyesha ahadi ya Mungu ya kusuluhisha tatizo hilo. Ukipata fursa, kazia kwamba Yehova atatatua tatizo hilo kupitia Ufalme wake, serikali yake ya mbinguni. (3) Mtie moyo mwenye nyumba achukue hatua juu ya jambo ambalo umezungumzia. Unaweza kumtolea kichapo au Funzo la Biblia na kufanya mipango hususa ya kuendeleza mazungumzo.
Katika hali hizo utahitaji tu muhtasari ambao umeshika akilini. Ukitaka kuangalia muhtasari ulioandika kabla ya kufanya ziara ya kwanza, muhtasari huo uwe na utangulizi mfupi tu, andiko moja au mawili, na umalizio mfupi. Kutayarisha muhtasari kama huo na kuutumia hutusaidia tusitangetange katika mazungumzo. Pia kunatusaidia kumwachia mwenye nyumba ujumbe ulio wazi ambao anaweza kukumbuka kwa urahisi.
Ikiwa swali fulani au kipingamizi fulani huzushwa katika eneo lenu, inaweza kufaa kufanya utafiti kulihusu. Kwa kawaida, unahitaji tu mambo makuu mawili au matatu pamoja na maandiko yanayoyaunga mkono. “Vichwa vya Biblia vya Mazungumzo” au vichwa vidogo vyenye maandishi mazito vinavyopatikana katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko vinaweza kuwa na muhtasari hususa unaohitaji. Unaweza kupata mnukuo mzuri katika kichapo kingine ambao unaweza kutumia pia. Tayarisha muhtasari mfupi, ambatanisha nakala ya mnukuo huo, kisha uziweke pamoja na vifaa unavyotumia katika utumishi wa shambani. Mwenye nyumba anapozusha swali lile au kipingamizi kile, mjulishe kwamba ungefurahi kumwambia sababu zinazokufanya uamini jambo hilo. (1 Pet. 3:15) Tumia muhtasari huo kumjibu.
-