-
Belize2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
“VITISHO VYAKE HAVINGEWEZA KUNIZUIA”
Upesi, kikundi cha wanafunzi wa Biblia huko San Antonio walianza kufanya maendeleo, na ilivutia kuona jinsi walivyoipenda kweli. Frank anaeleza: “Vijijini, wanawake hasa wana haya sana, na kulingana na mila zao wanajitiisha kwa baba na waume zao. Ni kinyume cha utamaduni wao kuzungumza na watu wasiowajua. Kwa hiyo, ilikuwa vigumu sana kwao kuhubiri nyumba kwa nyumba.”
Priscilian Sho aliyekuwa na miaka 20 wakati huo na ambaye hakuwa amebatizwa, alitaka sana kuwahubiria jirani zake. Pindi moja, Priscilian na shemeji yake Amalia Sho walikuwa wakifanya ziara za kurudia, walipokabili tatizo fulani wasilotazamia.
Priscilian anasema: “Sikuwa nimemwambia baba yangu ninaenda kuhubiri, kwa sababu alikuwa amenikataza na nilimwogopa. Jumapili hiyo asubuhi, tulipokuwa tukihubiri, tulimwona baba yangu mbele ya kanisa lake la Baptisti. Mwanzoni, tulijificha kwenye nyasi kwa kuwa hatukutaka atuone. Lakini nikasema, ‘Wajua nini Amalia, Yehova anatuona. Hatupaswi kumwogopa baba yangu. Tunapaswa kumwogopa Yehova.’”
Baba yake alikasirika sana, lakini Priscilian alikabili tatizo kubwa hata zaidi. Baba yake hakutaka kwa vyovyote Priscilian awe Shahidi wa Yehova. Baada ya kusali kuhusu tatizo hilo hadi mkesha wa kusanyiko ambapo angebatizwa, Priscilian alizungumza na baba yake bila kumwogopa.
Alimwambia, “Kesho ninaenda Belize City.”
“Unaenda kufanya nini?” baba akamuuliza.
“Ninaenda kubatizwa,” Priscilian akamjibu. “Ninaenda kufanya yale ambayo Yehova anataka nifanye. Ninakupenda, lakini ninapaswa kumpenda Yehova pia.”
“Je, kwa kweli unaenda kubatizwa?” akamuuliza kwa hasira.
“Ndiyo,” Priscilian akamjibu. “Matendo 5:29 linasema lazima nimtii Mungu kuliko mwanadamu.”
Baba ya Priscilian aliondoka kwa hasira. Priscilian anasema: “Sikuhisi nikiwa salama hadi pale nilipopanda gari, tayari kwenda kusanyikoni. Sikujua angefanya nini wakati ambapo ningerudi nyumbani baada ya kusanyiko. Lakini nilijua kuwa wakati huo ningekuwa nimebatizwa, kwa hiyo, hata kama angeniua, ningekuwa nimefanya jambo linalofaa.”
Ingawa baba ya Priscilian hakumuumiza aliporudi nyumbani, baadaye alitisha kumuua. Priscilian anasema, “Lakini alitambua kwamba vitisho vyake havingeweza kunizuia, na tangu wakati huo, yeye si mkali sana kwangu.”
-
-
Belize2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 235, 236]
Wamaya Wanaompenda Yehova
JORGE NA NICOLAS SHO (PAMOJA NA DADA YAO, PRISCILIAN)
WALIZALIWA 1969 na 1971
WALIBATIZWA 1997
MALEZI Kupatana na mila za Wamaya, watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao kikamili, hata kama watoto hao ni watu wazima waliofunga ndoa.
◼ NICOLAS na Jorge walipomjua na kumpenda Yehova, baba yao alipinga vikali utendaji wao wa Kikristo.
Nicolas anasema, “Nilimweleza baba yangu kwamba nilikuwa nikijifunza mambo yenye faida, lakini kwa kuwa alikuwa mfuasi wa Kanisa la Baptisti hakufurahia mambo niliyomweleza. Niliacha kujifunza Biblia kwa mara kadhaa kwa sababu sikutaka kumuumiza. Lakini nilijua kwamba kwa kunywa pombe pamoja na baba yangu sikuwa nikiwawekea watoto wangu mfano mzuri. Mke na watoto wangu walihuzunika sana hivi kwamba hawakuwa wanatabasamu kamwe.
“Nilipoanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, kweli niliyojifunza ilinisaidia kuacha mwenendo mbaya. Nilifanya kazi kwa bidii na nilitumia mapato yangu kuisaidia familia yangu. Sasa, mimi na familia yangu tunamtumikia Yehova kwa bidii, na kuna furaha na shangwe nyumbani kwetu.”
Kisa cha Jorge kilikuwa sawa na cha Nicolas. Alikuwa na matatizo ya familia kwa sababu alikunywa pombe na kutumia lugha chafu, na hakuwa anapatikana nyumbani mwishoni mwa juma. Lakini alipojifunza Biblia, mwenendo wake ulibadilika sana.
Jorge anaeleza, “Nilipofanya maendeleo, baba alizidi kunipinga. Alituita manabii wa uwongo. Alitisha kutushambulia kwa upanga wake mara kadhaa. Ndugu Cardoza, ambaye alinifundisha Biblia, alikuwa amejitahidi kututayarisha mapema kuhusu upinzani. Alituuliza: ‘Tuseme baba yenu atawaambia mwondoke nyumbani, mtafanya nini?’ Nilimjibu, ‘Baba yangu ananipenda na hawezi kufanya hivyo.’ Lakini inasikitisha kwamba hivyo ndivyo alivyofanya.
“Hata hivyo,” Jorge anaendelea kusema, “nilipenda mambo niliyokuwa nikijifunza, na maisha yangu yalikuwa yanaboreka. Familia yangu ilifaidika kwa sababu nilikuwa nikisitawisha sifa za Kikristo. Tuliheshimiana na kufurahia kuwa pamoja. Leo, kazi ya kuhubiri inaniletea shangwe nyingi, na kwa msaada wa Yehova, mimi ni painia wa kawaida.”
-