-
Tahiti2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kweli ya Biblia Yahubiriwa Gerezani
Kama katika nchi nyingine nyingi, watu kadhaa huko Polinesia ya Ufaransa wamepata kujua kweli za Biblia wakiwa gerezani. Kwa mfano, Alexandre Tetiarahi alikuwa mhalifu tangu ujanani na alifungwa kwa miaka saba. Alitoroka angalau mara sita na hivyo akaitwa Butterfly (Kipepeo), jina la mfungwa mtoro anayesimuliwa katika hadithi fulani maarufu.
Alexandre alipata Biblia na kitabu “Mambo Mawili Yasiyobadilika Asiyoweza Mungu Kusema Uongo” mahali alipokuwa akijificha kwenye kisiwa cha Raïatéa. Alisoma Biblia nzima na akasoma kitabu hicho mara kadhaa. Alisadikishwa kwamba amepata kweli, kwa hiyo, dhamiri yake ikaanza kumsumbua. Alifanya nini?
Ingawa hakuwasiliana moja kwa moja na Mashahidi wa Yehova ambao ni wachapishaji wa kitabu hicho, Alexandre alijisalimisha kwa polisi, nao wakamrudisha gerezani Tahiti. Colson Deane alikuwa mlinzi kwenye gereza alimofungwa Alexandre. Muda mfupi baada ya kufika, Alexandre alimsikia Colson akimhubiria mfanyakazi mwenzake na mara moja akayatambua mafundisho hayo. Hivyo, alimwendea Colson faraghani na kumwomba amfundishe mengi zaidi.
Ndugu Deane alimwomba msimamizi wa gereza ruhusa ya kumfundisha Alexandre. Punde si punde, wafungwa wengine pia walitaka kujifunza. Msimamizi wa gereza alimruhusu Colson kujifunza na wafungwa wakati wa mapumziko ya mchana pia. Baadaye ilionwa kuwa afadhali wazee wengine wawili waongoze funzo hilo. Kwa muda wa miaka kadhaa, wafungwa 30 hadi 50 hivi walisikiliza hotuba ya Biblia kila juma, kisha ndugu waliongoza funzo la Biblia pamoja na kila mmoja aliyetaka.
Alexandre alifanya maendeleo kwa haraka na maafisa wa gereza wakatambua jambo hilo. Kwa hiyo, walimpa mtoro huyo bingwa ruhusa ya kipekee ya kuhudhuria kusanyiko lake la kwanza la wilaya, chini ya usimamizi wa Ndugu Deane. Alexandre alibatizwa kwenye kusanyiko hilo. Sasa ameachiliwa na anaendelea kumtumikia Yehova.
-
-
Tahiti2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 122]
Alexandre Tetiarahi pamoja na mkewe Elma, na binti zao, Rava (kushoto) na Riva
-