-
Biblia Inabadili MaishaMnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
-
-
“Situmikii Sanamu Tena.”—ABA DANSOU
MWAKA WA KUZALIWA: 1938
NCHI: BENIN
HISTORIA: MWABUDU SANAMU
MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika kijiji kinachoitwa So-Tchahoué, kilicho katika eneo lenye majimaji karibu na ziwa. Wanakijiji huvua samaki na kufuga ng’ombe, mbuzi, kondoo, nguruwe, na ndege. Eneo hilo halina barabara, hivyo watu wanasafiri kwa mashua na mitumbwi. Kwa kawaida, wao hujenga nyumba kwa mbao na nyasi, ingawa wengine hujenga kwa matofali. Watu wengi katika eneo hilo ni maskini. Hata hivyo, hakuna uhalifu mwingi kama ilivyo mijini.
Nilipokuwa mdogo, mimi na dada yangu tulipelekwa na baba yetu katika makao ya waabudu wa sanamu zinazoaminika kuwa na nguvu za pepo, ambako tulifundishwa mapokeo ya ibada hiyo ya sanamu. Nilipokuwa mtu mzima nilimchagua Dudua (Oduduwa), mungu wa Wayoruba, kuwa mungu wangu. Nilimjengea madhabahu na kutoa kwa ukawaida dhabihu za viazi vikuu, mafuta ya mawese, konokono, kuku, njiwa, na aina nyingine za wanyama. Dhabihu hizo zilikuwa za bei ya juu na mara nyingi nilitumia karibu mapato yangu yote.
JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipoanza kujifunza Biblia, nilijua kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Nilijifunza pia kwamba hapendezwi na ibada ya sanamu. (Kutoka 20:4, 5; 1 Wakorintho 10:14) Nilielewa ninachopaswa kufanya. Hivyo, nilitupa sanamu zangu zote na kuondoa nyumbani kwangu kila kitu kilichohusiana na ibada ya sanamu. Niliacha kutafuta habari kupitia uaguzi na sikushiriki tena katika matambiko na desturi za mazishi.
Haikuwa rahisi kwangu—mwanamke mwenye umri wa miaka 60 hivi—kufanya mabadiliko hayo. Rafiki, watu wa familia, na jirani zangu walinipinga na kunicheka. Lakini nilisali kwa Yehova ili nipate nguvu za kufanya yaliyo sawa. Nilifarijiwa sana na andiko la Methali 18:10, linalosema hivi: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.”
Jambo lingine lililonisaidia sana ni kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Katika mikutano hiyo nilijionea upendo wa Kikristo, na nilivutiwa sana kwa sababu watu hao wanajitahidi kuishi kulingana na viwango vya juu vya Biblia vya maadili. Mambo niliyoona yalinisadikisha kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaofuata dini ya kweli.
JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kufuata kanuni za Biblia kumenisaidia kuboresha uhusiano wangu pamoja na watoto wangu. Pia, ninahisi kuwa mzigo mkubwa umeondolewa mabegani mwangu. Nilikuwa nikipoteza mapato yangu kwa ajili ya sanamu zisizo na uhai ambazo hazikuninufaisha kwa vyovyote. Sasa ninamwabudu Yehova, ambaye hutoa suluhisho la kudumu kwa matatizo yetu yote. (Ufunuo 21:3, 4) Ninafurahi sana kwamba situmikii sanamu tena, badala yake, ninamtumikia Yehova! Yeye ananipa ulinzi na usalama wa kweli.
-
-
Biblia Inabadili MaishaMnara wa Mlinzi—2011 | Julai 1
-
-
[Picha katika ukurasa wa 12]
Nimejionea upendo wa Kikristo kati ya Mashahidi wa Yehova
-