Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Uweke Pesa Akiba Badala ya Kuzitumia?
    Amkeni!—2011 | Septemba
    • Kwa Nini Uweke Pesa Akiba Badala ya Kuzitumia?

      “KUWEKA akiba kunachosha,” ndivyo watu wengi wanavyosema. “Lakini inafurahisha kununua nguo, vifaa vya elektroniki, na vitu kama hivyo.”

      Iwe umeathiriwa na kushuka kwa uchumi wa ulimwengu au la, unaweza kufaidika kwa kufikiria njia mbalimbali ambazo unaweza kuhifadhi pesa na njia za kuzitumia kwa hekima. Chunguza mashauri kutoka katika chanzo kinachotegemeka ambacho kimewasaidia mamilioni ya watu katika karne nyingi kushughulikia matatizo yao ya kifedha.

      Misemo Mitatu ya Kale Yenye Hekima

      Katika moja ya mifano yake, Yesu wa Nazareti alitaja kanuni fulani muhimu inayohusiana na mambo ya kiuchumi. Katika mfano huo bwana mkubwa alimwambia mtumishi wake hivi: “Ilikupasa basi, kuiweka fedha yangu katika benki, nami ningelichukua mtaji wangu na faida yake!” (Mathayo 25:27, Biblia Habari Njema) Maneno ambayo Yesu alisema wakati huo ni muhimu sana leo. Acheni tuone sababu.

      Hivi karibuni katika nchi fulani, faida iliyopatikana baada ya miaka kumi hivi, ilizidi kiasi cha pesa ambacho mtu alikuwa ameweka katika benki. Ingawa leo benki nyingi haziwapi watu faida kubwa hivyo, na faida inayopatikana kutokana na vitu ambavyo mtu huwekeza si ya kiasi kikubwa kama ile inayotazamiwa na wawekezaji, ni jambo la hekima kuweka pesa akiba kwa ajili ya mambo ya dharura.

      Biblia inakazia jambo hilo inaposema: “Hekima ni ulinzi, kama vile pesa ni ulinzi.” (Mhubiri 7:12) Lakini pesa haziwezi kukulinda ikiwa huna zozote akibani! “Kila mmoja wenu,” Biblia inasema, “aweke kando kitu fulani katika akiba kulingana na anavyofanikiwa.”—1 Wakorintho 16:2.

      Jinsi Unavyoweza Kuweka Pesa Akiba

      Kwanza, kabla ya kununua kitu cha bei ghali, fikiria ikiwa kwa kweli unakihitaji.

      Pili, ikiwa unahitaji kitu fulani, tafuta vitu vipya ambavyo vinauzwa kwa bei iliyopunguzwa au vitu vya mtumba vilivyo katika hali nzuri. Espen na Janne, wazazi fulani wanaoishi huko Norway, walihitaji kigari cha kumbebea mwana wao, Daniel. Walinunua kigari cha mtumba kilichokuwa katika hali nzuri kwa nusu ya bei ya kawaida. Espen anasema hivi: “Daniel atakapokuwa mkubwa aache kukitumia, nina hakika kwamba tutaweza kukiuza kwa bei nzuri.” Lakini anaonya: “Unaweza kutumia wakati mwingi kutafuta kitu cha bei nafuu.”a

      Tatu, usinunue vitu bila kupangia; tumia wakati wa kutosha kufikiria kuhusu bidhaa unayotaka kununua. Ukihisi kwamba bado unahitaji sana bidhaa hiyo, unaweza kuitafuta katika duka linalouza vitu kwa bei ya chini au bidhaa za mtumba. Pia, mara nyingi unaweza kuokoa pesa iwapo hutahisi unalazimika kununua bidhaa zenye majina ya watengenezaji maarufu. Isitoshe, badala ya kununua nguo za kisasa zaidi za watoto kutoka kwenye maduka yanayouza vitu kwa bei ya juu, mbona usitumie nguo zilizotumiwa hapo awali na watoto wengine?

      Vivyo hivyo, mama aliyejifungua kwa mara ya kwanza anaweza kutumia nepi zinazoweza kufuliwa. Kitabu Budgeting—Personal Spending and Money Management a Key to Weathering the Storm, kilichoandikwa na Denise Chambers, kinasema hivi: “Nepi zinazotupwa baada ya kutumiwa zitagharimu dola 2,000 au zaidi katika muda wa miaka 2. Nepi za kitambaa . . . zitagharimu dola 300 hadi 500 katika kipindi hichohicho cha miaka 2.” Akaongezea hivi: “Nepi za kisasa za kitambaa ni rahisi zaidi kutumia na haziharibu mazingira!”

      Nne, kumbuka kwamba kununua vitu na kupika nyumbani hakugharimu sana kama kula kwenye mkahawa. Ikiwa una watoto wanaoenda shuleni, mbona usiwafundishe kubeba chakula kilichotayarishwa nyumbani badala ya kuwapa pesa za kununua chakula cha bei ghali? Na badala ya kununua vinywaji vya bei ghali, kunywa maji. Yana afya zaidi na si bei ghali.

      Muda fulani uliopita familia zilikuwa zikikuza mboga kwenye bustani zao. Je, umewahi kufikiria kukuza chakula chako? Watu wengi, kutia ndani wale wanaoishi katika nyumba za orofa au nyumba ndogo, wana eneo fulani wanaloweza kutumia kukuza vitu. Utashangaa kuona kiasi cha chakula ambacho unaweza kukuza ukiwa na sehemu ndogo tu!

      Fikiria hili pia: Ikiwa unahitaji kuwa na simu ya mkononi, je, unaweza kuitumia tu kwa ajili ya hali za dharura na ulipie mapema muda fulani wa maongezi? Au ikiwa una mashini ya kukausha nguo, je, umewahi kufikiria kupunguza matumizi yake? Labda unaweza kuanika nguo fulani—au zote—nje kwenye kamba. Pia unaweza kupunguza muda unaotumia vifaa vya kuondoa hewa yenye joto, vipasha-joto, au kifaa kingine cha kielektroniki. Kabla ya kuwasha vifaa hivyo, jiulize, ‘Je, hali ya hewa ni mbaya kiasi hicho?’ Pia unaweza kuzungumza na wengine ili ufahamu jinsi wanavyodhibiti matumizi yao ya umeme.

      Pia ingefaa kufungua akaunti ya kuweka pesa akiba au uwekeze pesa zako katika mpango wa bima unaolipa faida. Kwa kuongezea, Hilton, mfanyakazi wa kujitolea nchini Afrika Kusini, anaeleza hivi: “Si jambo la hekima kuweka vitu vyako vyote vyenye thamani mahali pamoja. Nyakati nyingine, benki na mashirika mengine ya kifedha hufilisika. Tumewahi kujionea jambo hilo.” Kwa hiyo, weka akiba katika benki ambayo serikali itakurudishia pesa zako iwapo benki hiyo itafilisika.

      Jinsi ya Kumaliza Deni

      Kwanza, jaribu kulipa zaidi ya kiasi unachodaiwa kila mwezi kwenye kadi ya mkopo au deni lingine.

      Pili, jitahidi kulipa deni linalodai ulipe riba ya kiasi cha juu zaidi.

      Tatu, dhibiti jinsi unavyotumia pesa. Hilo ni jambo muhimu sana.

      Je, umewahi kushawishiwa na matangazo ya kibiashara? Danny, mwanamume fulani mwenye familia nchini Sweden anakiri kwamba amewahi. Alikuwa na biashara nzuri lakini alilazimika kuiuza ili alipie deni la kadi yake ya mkopo. Alijifunza kutokana na hilo na sasa anadhibiti pesa zake. Anatoa ushauri huu: “Jihadhari na pupa. Jifunze kuishi kulingana na mapato yako.”

      Deni la Lazima

      Ni watu wachache wanaoweza kulipa pesa taslimu kwa ajili ya nyumba wanayonunua. Kwa hiyo, wengi huchukua mkopo kwenye benki ili kununua nyumba. Kiasi wanacholipa kila mwezi ili kurudisha pesa hizo huonwa ni kana kwamba wanalipa kodi ya nyumba. Lakini baada ya kulipa mkopo huo kwa muda mrefu, wanamiliki nyumba hiyo!

      Pia watu wengi huona kuwa inafaa kuchukua mkopo ili kununua gari ambalo halitumii petroli nyingi. Wanapolipa mkopo huo upesi iwezekanavyo, gari hilo huwa na faida, na hiyo ni njia nyingine ya kuokoa pesa.b Wengine wameona ni jambo la hekima kununua gari la mtumba lililo katika hali nzuri na ambalo halijatumiwa sana. Wengine huokoa pesa kwa kutumia usafiri wa umma au hata kuendesha baiskeli.

      Vyovyote vile, uwe na kiasi na uone mambo kihalisi kuhusiana na vitu unavyonunua na ufanye maamuzi ukiwa makini. Unaweza kukuza tabia ya kutumia pesa bila hekima na hilo litakuletea matatizo. Kwa hiyo, jitahidi kutumia pesa kwa uangalifu na kwa busara, na huenda ukafaulu kuwa na furaha ya kudumu.

      Mbali na hilo, ili ufurahie kuhifadhi pesa, unapaswa kujua jinsi ya kuzitumia kwa hekima. Habari inayofuata itazungumzia jambo hilo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ili uwe na hakika kwamba hununui bidhaa zilizoibiwa, ni jambo la hekima kumwuliza muuzaji jina lake, anwani yake na kumwomba risiti.

      b Kumbuka kwamba ukipoteza kazi yako na ushindwe kulipia mkopo, huenda ukapoteza nyumba au gari lako na pesa zote ulizokuwa umelipa kufikia wakati huo. Ingawa hivyo, wengi huamua kuwa na bima ya kuzuia hilo.

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      NJIA ZA KUOKOA PESA

      Tafuta vitu vinavyouzwa kwa bei iliyopunguzwa

      Nunua nguo kwenye maduka yanayopunguza bei au nguo za mtumba

      Wafundishe watoto wako kujitayarishia chakula nyumbani

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Punguza gharama za chakula kwa kukuza bustani ndogo ya mboga nyumbani. Punguza gharama kwa kuanika nguo nje

  • Jinsi ya Kupangia Matumizi ya Pesa Zako
    Amkeni!—2011 | Septemba
    • Jinsi ya Kupangia Matumizi ya Pesa Zako

      KUNA njia tatu za kupangia matumizi ya pesa: (1) Kuzitumia, (2) kuziweka akiba, au (3) kuwapa watu. Acheni kwanza tuzungumzie jinsi unavyoweza kutumia pesa kwa hekima.

      Poromoko Kubwa la Uchumi limeonyesha wazi kwamba ni jambo la hekima kuwa na bajeti iliyopangwa vizuri. Bajeti ni nini? Kwa ufupi, ni makadirio ya jinsi mapato yatakavyotumiwa na mtu binafsi, familia, biashara, au serikali.

      Ushirikiano wa Familia

      Unaweza kupanga bajeti jinsi gani? Kitabu Budgeting, cha Denise Chambers kinasema kwamba “watu wote katika familia wanapaswa kuhusishwa katika kupanga bajeti ili wote waweze kuifuata.” Mara kwa mara, wote wanapaswa kukutana ili kuona jinsi bajeti yao inavyoendelea. Wote wanaweza kunufaika wanaposhirikiana kupanga bajeti nzuri na kila mmoja anapojitahidi kuishi kulingana na mapato ya familia.

      Watu fulani hutumia programu ya kompyuta kupanga bajeti. Wengine hutumia tu penseli na karatasi iliyochorwa safu mbili. Safu moja inaonyesha mapato, ile nyingine inaonyesha matumizi. Pia ni muhimu kutia katika bajeti kiasi fulani kila mwezi cha kushughulikia gharama zinazolipiwa mara moja kwa mwaka, kama vile kodi ya mapato au hata likizo.

      Njia ambayo watu wametumia kwa muda mrefu ni ile ya kutia pesa katika bahasha au vikasha vilivyoandikwa “Chakula,” “Kodi ya Nyumba,” “Usafiri,” “Umeme,” “Gharama za Matibabu,” na kadhalika. Zamani, watu walitia pesa za matumizi hayo ndani ya bahasha kila mwezi. Leo wengi huona kuwa ni salama na rahisi zaidi kuweka pesa katika akaunti ya benki na kuzitoa wanapozihitaji.

      Mara nyingi, Jonathan na Anne, wanaoishi nchini Afrika Kusini pamoja na binti zao wawili, hutumia mbinu ya kupanga bajeti kwa kutumia bahasha. Jonathan anasema hivi: “Ikiwa mshahara wako unatumwa katika akaunti ya benki, ni muhimu sana uwe mwangalifu kuhusu unavyogawa pesa hizo. Kwa mfano, ikiwa pesa ulizotenga kwa ajili ya kununua nyama kila mwezi zimeisha, hupaswi kununua nyama kwa kutumia pesa zilizotengwa kwa ajili ya kuwekwa akiba.”

      Jonathan alikuwa na biashara, lakini sasa yeye na familia yake wameamua kutumikia wakiwa wafanyakazi wa kujitolea kujenga majengo ya ibada. Kwa kuwa wangependa kuendelea katika utumishi huo wa kujitolea, wanahitaji kufuata kwa makini bajeti nzuri. Familia yao hujadiliana kwa ukawaida kuhusu bajeti yao ili waone mabadiliko wanayopaswa kufanya.

      Furaha Kubwa Zaidi

      Uchunguzi unaonyesha kwamba kuwapa watu wengine mali, kutia ndani wakati na nguvu na vilevile kiasi fulani cha pesa, kunaleta furaha kubwa sana. Kwa kadiri ambavyo uwezo wako utaruhusu, huenda hiyo ikawa ndiyo njia bora zaidi ya kutumia pesa zako kati ya zile zilizotajwa katika utangulizi.

      Katika kitabu chake The New Frugality, Chris Farrell anasema kwamba “unapoweka pesa akiba, unapata nafasi ya kufurahia kuzitumia.” Naye anapendekeza: “Jambo lenye faida zaidi na la hekima zaidi unaloweza kufanya na pesa zako ni kuwapa watu wengine.”a Farrell anaongezea hivi: “Unapofikiria jambo lililo muhimu zaidi maishani, mara nyingi utapata ni kuwa na uhusiano mzuri na watu, kujionea mambo, na kuhisi kwamba umesaidia kwa njia fulani, bali si kuwa na pesa au mali.”

      Michael Wagner, ambaye ni mtaalamu wa uchumi, anakubaliana na maneno hayo. Katika kitabu chake, Your Money, Day One, ambacho kimekusudiwa kuwatia moyo vijana waweke pesa akiba, anasema hivi: “Unapochukua hatua ya kwanza kuwasaidia watu wenye uhitaji, utapata faida kwa njia mbalimbali kwa sababu ya kuonyesha fadhili na ukarimu, lakini faida kubwa zaidi itakuwa hisia ambayo utapata moyoni kwa kumsaidia mwanadamu mwenzako.”

      Biblia inaonyesha kwamba kutoa huleta furaha. Kama ilivyozungumziwa hapo awali, Biblia ina semi zinazoweza kukusaidia kutumia pesa kwa hekima. Sasa, acheni tuchunguze semi nyingine saba.

      [Maelezo ya Chini]

      a Pesa zinaweza kutolewa kama zawadi au zitumiwe kuwaonyesha watu ukarimu kwa kutayarisha chakula kwa ajili ya marafiki na watu wa familia.

  • Semi Saba Zenye Hekima
    Amkeni!—2011 | Septemba
    • Semi Saba Zenye Hekima

      SEMI zilizo hapa chini zimetolewa katika kitabu cha kale kilicho na semi nyingi ambazo zina faida na zinatumika leo. Fikiria jinsi semi hizo zinavyoweza kukusaidia kutumia pesa zako kwa njia ya hekima.

      1. “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.” (Mhubiri 5:10) Hayo si maneno ya mtu mwenye wivu ambaye alikuwa maskini. Yaliandikwa na Mfalme Sulemani aliyekuwa mmoja wa watu matajiri zaidi, naye aliyaandika kwa kutegemea mambo yaliyompata na aliyojionea. Matajiri wa leo wamesema maneno kama hayo pia.

      2. “Kama tunacho chakula na mavazi, tunapaswa kuridhika navyo. Lakini wale wanaotaka kutajirika huanguka katika majaribu.” (1 Timotheo 6:8, 9, Biblia Habari Njema) Maneno hayo yaliandikwa na mtume Paulo, ambaye aliacha kazi maarufu ili awe mfuasi wa Yesu Kristo. Tofauti na viongozi fulani wa kidini leo, Paulo alikataa kabisa kufaidika kifedha kutoka kwa wale aliowafundisha au rafiki zake. Badala yake, alisema hivi kwa unyoofu: “Sikutamani fedha au dhahabu au vazi la mtu. Ninyi wenyewe mnajua kwamba mikono hii imehudumia mahitaji yangu na ya wale walio pamoja nami.”—Matendo 20:33, 34.

      3. “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” (Luka 14:28) Mfano huo wa Yesu unaweza kutumiwa katika hali fulani unayoweza kukabili: Unapotaka kununua kitu, hasa unapotumia kadi ya mkopo, je, utanunua vitu ambavyo hukupangia au utakuwa na subira na kuhesabu gharama? Je, kweli unahitaji kitu unachotaka kununua, na unaweza kukigharimia?

      4. “Mkopaji ni mtumwa wa mkopeshaji.” (Methali 22:7, BHN) Kuporomoka kwa uchumi ambako kulitokea hivi karibuni kumeonyesha wazi madhara ya kutumia kadi za mikopo na kurundika madeni kwa njia nyingine. “Ni jambo la kawaida kwa mtu leo kuwa na deni la kadi ya mkopo la dola 9,000 au zaidi kwenye kadi kama nne hivi za mkopo,” anasema Michael Wagner katika kitabu chake Your Money, Day One cha mwaka wa 2009.

      5. “Mwovu anakopa lakini halipi, lakini mwadilifu anaonyesha kibali na anatoa zawadi.” (Zaburi 37:21) Watu fulani huona kwamba kusema wamefilisika ni njia rahisi ya kutolipa pesa wanazodaiwa. Lakini wale wanaothamini uhusiano wao mzuri pamoja na Mungu, wanaongozwa na dhamiri kulipa madeni ikiwa wanaweza kufanya hivyo, nao pia hutumia mali zao kwa ukarimu.

      6. “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.” (Zaburi 37:25) Maneno hayo yaliandikwa na mtu aliyetendewa kwa njia isiyo ya haki. Kwa miaka mingi alikuwa mkimbizi, nyakati nyingine aliishi katika mapango na nyakati nyingine alikimbilia nchi jirani. Mwishowe, mkimbizi huyo, Daudi, akawa mfalme wa Israeli la kale. Maishani mwake alijionea ukweli wa maneno hayo yaliyotajwa.

      7. “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Maneno hayo yalisemwa na yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi. “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake,” Yesu alitumia maisha yake duniani kuwatumikia wengine. Sasa akiwa kiumbe wa roho asiyeweza kufa, anafurahia uhai mbinguni akiwa kwenye mkono wa kulia wa yule “Mungu mwenye furaha,” Yehova.—Waebrania 12:2; 1 Timotheo 1:11.

      Kusudi kubwa zaidi maishani mwetu ni kuiga mfano wa Yesu kwa kufanya yote tunayoweza ili kuwatumikia wengine. Bila shaka utakubali kwamba ni afadhali mtu awe makini kuweka pesa akiba ili aweze kuwapa wengine vitu kwa ukarimu, badala ya kutumia pesa kwa ubinafsi.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki