-
Kitu Ambacho Kinadumu Kuliko SanaaAmkeni!—2007 | Aprili
-
-
Nilipaswa kujiunga na Anja Keto, ambaye nimemzidi umri kwa miaka 17. Ingawa sikumjua Anja, nilikubali mgawo huo na tukaanza kuishi pamoja. Mimi na yeye ndio tuliokuwa Mashahidi pekee katika eneo hilo, kwa hiyo karibu kila wakati tulihubiri pamoja. Muda si muda, tukawa marafiki wa chanda na pete.
Kuhamia huko Jalasjärvi kulimaanisha kwamba nijifunze tena kuishi maisha ya vijijini kama nilivyokuwa nimezoea kabla ya kuanza kusomea usanii kwenye jiji kuu miaka 20 iliyotangulia. Hali ilikuwa ngumu sana wakati wa majira ya baridi kali, na nyakati nyingine tulihitaji kutembea kwenye theluji iliyofika hadi kwenye mapaja yetu. Tuliishi katika nyumba ndogo ya mbao ambayo haikuwa nzuri sana. Tulichota maji kutoka kwenye chemchemi iliyokuwa karibu, na mara kwa mara maji tuliyoteka na kuweka ndani ya nyumba yetu yaliganda usiku. Lakini tulikuwa na kila kitu tulichohitaji. (1 Timotheo 6:8) Hizo zilikuwa siku zenye furaha sana zilizokuwa na shughuli nyingi.
Mengi ya Kufanya Katika Kazi Yenye Kuthawabisha
Mwanzoni, jitihada zetu hazikuonekana kuwa na matokeo kwa sababu wenyeji wa eneo hilo walitubagua sana. Ili kuwasaidia waelewe kazi yetu, tulipanga kuwaonyesha sinema zilizotayarishwa na Mashahidi wa Yehova, kama vile The New World Society in Action na The Happiness of the New World Society. Sinema hizo ziliwasaidia kutuelewa na kuelewa tengenezo letu, na hivyo kuona jinsi utendaji wetu unavyowafaidi watu ulimwenguni pote. Watu wengi walihudhuria maonyesho hayo.
Kwenye pindi fulani, Eero Muurainen, mwangalizi anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova, alionyesha sinema The New World Society in Action katika ukumbi wa starehe wa eneo hilo. Ukumbi huo ulijaa sana watu hivi kwamba ilikuwa shida kupata nafasi katika kona niliyosimama. Ilinibidi kusimama kwa mguu mmoja nikiegemea ukutani kwani ule mguu mwingine haukuwa na mahali pa kukanyaga. Sinema hiyo ilipokwisha, watu wengi walitujia na kutuomba tuwatembelee.
Pia tulitumia redio kubwa kucheza hotuba za Biblia katika nyumba za mashambani. Pindi moja, tulikubali kucheza hotuba fulani saa moja jioni katika nyumba ya familia moja, nasi tulikuwa tumekaribisha kijiji kizima. Mapema asubuhi hiyo, tuliondoka kwa baiskeli zetu tukahubiri katika kijiji kilichokuwa umbali wa kilomita 25 hivi, tukifikiri kwamba tungerudi kabla ya jioni. Lakini wakati wa kurudi, barabara zilikuwa zimejaa matope kwa sababu ya mvua iliyonyesha.
Mwishowe, baiskeli zetu zilijaa matope hivi kwamba magurudumu hayangeweza kuzunguka na hivyo tukalazimika kuzibeba hadi nyumbani. Kwa sababu hiyo, hatungeweza kutoka nyumbani kwa ajili ya mkutano tuliopangia hadi baadaye usiku. Tulibeba redio yetu nzito na kufika huko mwendo wa saa nne usiku. Tulikuwa na hakika kwamba kila mtu alikuwa ameondoka. Lakini tulishangaa kukuta nyumba imefurika wanakijiji wakitusubiri! Baada ya hotuba hiyo, mazungumzo yenye kusisimua yalianza. Mwishowe tulipofika nyumbani usiku wa manane, tulikuwa tumechoka sana lakini tulikuwa na furaha tele!
Umbali kutoka kijiji kimoja hadi kingine ulikuwa mrefu sana hivi kwamba Mashahidi katika eneo hilo walitusaidia kununua gari fulani la zamani lililotengenezewa Urusi. Hilo lilifanya kazi yetu ya kuhubiri iwe rahisi. Baada ya muda, gari hilo likawa limejulikana sana hivi kwamba askofu wa dayosisi alipozuru, aliwaambia waumini wasitukaribishe katika nyumba zao. Alizungumza kuhusu wanawake wawili walio na gari la bluu. Mara moja maonyo hayo yakawachochea watu. Walitaka kujua wanawake hao wawili walikuwa akina nani na kilichowafanya kuwa hatari! Udadisi wao ulitusaidia kuwa na mazungumzo mazuri ya Biblia. Maneno ya nabii Isaya yalithibitika kuwa kweli: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.”—Isaya 54:17.
Baada ya muda, kazi yetu ilizaa matunda. Tulianza kuongoza mikutano ya kila juma na kikundi kidogo cha watu wanaopendezwa. Mwishowe kikundi chetu kiliongezeka, na katika mwaka wa 1962 kutaniko lenye Mashahidi 18, wengi wao wakiwa wanawake, lilianzishwa. Miaka miwili baadaye, mimi na Anja tulihamishwa hadi mji wa Ylistaro katika eneo hilohilo.
Eneo Lenye Kuchochea
Tulifurahia sana mandhari ya vijijini iliyokuwa maridadi na tulivu katika mgawo huo mpya, lakini tulipendezwa hasa na watu wa huko. Kwa ujumla, walikuwa wakarimu na wenye urafiki. Ni kweli kwamba, wengi wao walikuwa watu wa dini sana na wazalendo, na nyakati nyingine walitufokea kwa ukali; lakini kuna wengine walioistahi sana Biblia. Mara nyingi tulipotoa Biblia, wanawake waliacha kazi zao za nyumbani ili wasikilize na wanaume walivua kofia zao, kofia ambazo kwa kawaida hazingevuliwa hata kidogo. Nyakati nyingine tulipojifunza Biblia, nyumba nzima, na hata majirani, wangekuja na kusikiliza.
Watu wanyoofu niliokutana nao katika utumishi walichochea usanii wangu. Nilipokuwa na wakati, ningechukua udongo na kuanza kuufinyanga. Kwa kuwa mimi huvutiwa hasa na sifa za wanadamu zenye uchangamfu na zinazofurahisha, vitu vingi nilivyotengeneza vilihusiana na watu. Vingi vilionyesha wanawake wakifanya kazi zao. Makala moja ya gazeti ilisema hivi kuhusu vitu nilivyotengeneza: “Mtu anapotazama sanaa hizo anahisi amani na usalama, na pia ucheshi na utulivu . . . Kupendezwa sana na watu pamoja na ustadi wa kisanii ndio humsaidia kutokeza sanaa hizo.” Hata hivyo, nilijitahidi sana nisikengeushwe na sanaa. Nilishikamana na uamuzi wangu wa kumtumikia Yehova wakati wote.
Mnamo 1973, nilipewa kazi ambayo singeweza kukataa. Niliombwa nitengeneze sanaa kubwa kwa kutumia udongo kwa ajili ya eneo la mapokezi la ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Finland huko Vantaa. Andiko la Zaburi 96:11-13 lilichaguliwa kuwa kichwa cha sanaa hiyo. Nilifurahi kama nini kutumia kipawa changu kumsifu Yehova!
Kwa kuwa nilifanya kazi ya usanii hasa kwa ajili ya kujifurahisha tu nilipokuwa nikifanya upainia, nilishangaa sana katika miaka ya mwishomwisho ya 1970 nilipokabidhiwa malipo ya uzeeni ya wasanii. Bila shaka, nilithamini kupata utegemezo huo wa kifedha, lakini nilijiuliza, ‘Je, ni hili tu ambalo ningekuwa nimetimiza ikiwa ningetumia maisha yangu katika sanaa? Yaani ningepata pesa kidogo tu za kunitegemeza baada ya kustaafu?’ Malipo hayo yalikuwa kitu kidogo tu yanapolinganishwa na thawabu ya uzima wa milele!—1 Timotheo 6:12.
Narudi Jijini
Mwaka wa 1974 ulileta mabadiliko makubwa katika maisha na utumishi wetu. Tulipewa mgawo mpya katika jiji kubwa la Turku. Wakati huo nyumba nyingi za ghorofa zilikuwa zikijengwa katika eneo hilo hivyo kukawa na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme kwa kuwa watu wengi walihamia huko. Mwanzoni, hatukufurahia sana mgawo wetu mpya katika jijini hilo. Ilikuwa vigumu kuwahubiria wakaaji wa jijini kwani wengi wao hawakujali. Lakini polepole tulianza kuzoea eneo hilo jipya, na tuliwapata wengi ambao walithamini kweli za Biblia.
Mimi na Anja tumepata pendeleo la kusaidia zaidi ya watu 40 kuweka maisha yao wakfu kwa Yehova. Watoto hao wa kiroho hutuletea shangwe nyingi sana! (3 Yohana 4) Katika miaka ya karibuni afya yangu imezorota, lakini nimehisi zaidi utegemezo wa Yehova, upendo wa kutaniko, na “msaada wenye kunitia nguvu” kutoka kwa Anja, painia mwenzangu mpendwa. (Wakolosai 4:11; Zaburi 55:22) Nilipokutana na Anja karibu miaka 50 iliyopita, sidhani kama kuna yeyote kati yetu aliyefikiri kwamba tungeendelea kufanya upainia pamoja maisha yetu yote.
-
-
Kitu Ambacho Kinadumu Kuliko SanaaAmkeni!—2007 | Aprili
-
-
[Picha katika ukurasa wa 21]
Nikiwa na Anja (kushoto), 1957
[Picha katika ukurasa wa 22]
Nikiwa na Anja (kulia) leo
-