-
Je, Unatambua Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu?Mnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
-
-
Je, Unatambua Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu?
WAISRAELI na hata Wamisri hawakuwa wamewahi kuona kitu kama hicho. Waisraeli walipokuwa wakitoka Misri, nguzo ya wingu ilikuwa ikielea karibu nao na kukaa pamoja nao siku baada ya siku. Usiku, ilikuwa nguzo ya moto. Lilikuwa jambo la kustaajabisha kama nini! Lakini nguzo hiyo ilitoka wapi? Ilikuwa na kusudi gani? Na sisi tunaoishi miaka 3,500 baadaye, tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Waisraeli walivyoiona ile “nguzo ya moto na wingu”?—Kut. 14:24.
Neno la Mungu linafunua chanzo na kusudi la nguzo hiyo linaposema hivi: “Yehova alikuwa akienda mbele yao wakati wa mchana katika nguzo ya wingu ili kuwaongoza njiani, na wakati wa usiku katika nguzo ya moto ili kuwapa nuru ya kwenda wakati wa mchana na wakati wa usiku.” (Kut. 13:21, 22) Yehova Mungu alitumia nguzo ya moto na wingu kuwaongoza watu wake kutoka Misri na kupitia nyikani. Walipaswa kuwa tayari kuondoka na kuifuata. Vikosi vya Misri vilivyokuwa vinawafuata vilipokuwa karibu kuwashambulia watu wa Mungu, nguzo ile ilisonga na kusimama katikati ya vikundi hivyo viwili, na kuwalinda Waisraeli. (Kut. 14:19, 20) Ingawa nguzo hiyo haikuwaongoza kufuata njia ya moja kwa moja, Waisraeli wangeweza tu kufika katika Nchi ya Ahadi kwa kuifuata nguzo hiyo.
Kuwepo kwa nguzo hiyo kuliwahakikishia watu wa Mungu kwamba Yehova alikuwa pamoja nao. Nguzo hiyo ilimwakilisha Yehova, na nyakati nyingine alizungumza kupitia nguzo hiyo. (Hes. 14:14; Zab. 99:7) Zaidi ya hayo, wingu hilo lilionyesha kwamba Musa ndiye aliyechaguliwa na Yehova kuliongoza taifa hilo. (Kut. 33:9) Vivyo hivyo, Biblia inaonyesha kwamba mara ya mwisho lilipotokea, wingu hilo lilionyesha kwamba Yehova alikuwa amemweka rasmi Yoshua kuwa kiongozi baada ya Musa. (Kum. 31:14, 15) Kwa kweli, ili Waisraeli wafanikiwe katika safari yao ya kutoka Misri, walipaswa kutambua uthibitisho wa mwongozo wa Mungu na kisha kuufuata.
Walipuuza Uthibitisho
Waisraeli walipoona nguzo hiyo kwa mara ya kwanza, bila shaka walistaajabu. Hata hivyo, inasikitisha kwamba muujiza huo ulioonekana waziwazi haukuwasaidia Waisraeli vya kutosha kuwa na uhakika wenye kudumu katika Yehova. Mara kwa mara walitilia shaka mwongozo wa Mungu. Jeshi la Misri lilipowafuata, hawakuonyesha imani katika nguvu za Yehova za kuokoa. Badala yake, walidai kwamba Musa, mtumishi wa Mungu, aliwaongoza ili wafe. (Kut. 14:10-12) Baada ya kukombolewa na kuvuka Bahari Nyekundu, walimnung’unikia Musa, Haruni, na Yehova kwa sababu walidai kwamba walikosa chakula na maji. (Kut. 15:22-24; 16:1-3; 17:1-3, 7) Na baada ya majuma machache, walimsukuma Haruni atengeneze ndama wa dhahabu. Hebu wazia! Katika sehemu moja ya kambi yao, Waisraeli waliona ile nguzo ya moto na wingu—uthibitisho wenye nguvu wa Yule ambaye alikuwa amewaongoza kutoka Misri—na karibu na mahali hapo, wakaanza kuabudu sanamu isiyo na uhai, wakisema: “Huyu ndiye Mungu wako, Ee Israeli, aliyekuongoza kutoka nchi ya Misri.” Yalikuwa “matendo makubwa ya kukosa heshima” kama nini!—Kut. 32:4; Neh. 9:18.
Matendo ya Waisraeli ya uasi yalionyesha wazi kwamba walipuuza mwongozo wa Yehova. Si kwamba walikuwa vipofu kihalisi, badala yake hawakuona mambo kwa njia ya kiroho. Waliiona ile nguzo, lakini walisahau maana ya nguzo hiyo. Ingawa matendo yao ‘yalimtia uchungu Mtakatifu wa Israeli,’ kwa rehema Yehova aliendelea kutoa mwongozo kupitia ile nguzo mpaka Waisraeli walipofika katika Nchi ya Ahadi.—Zab. 78:40-42, 52-54; Neh. 9:19.
-
-
Je, Unatambua Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu?Mnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
-
-
Fuata Mwongozo wa Mungu
Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini mwongozo wa Mungu? Mtume Paulo alisema hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee.” (Ebr. 13:17) Huenda nyakati nyingine ikawa vigumu kufanya hivyo. Kwa mfano: Jiweke katika hali ya Mwisraeli aliyeishi katika siku za Musa. Wazia kwamba baada ya wewe kutembea kwa muda fulani, ile nguzo inasimama. Itasimama mahali hapo kwa muda gani? Siku moja? Juma moja? Miezi fulani? Unajiuliza, ‘Je, ninahitaji kufungua mizigo yangu yote?’ Kwanza, huenda ukafungua vitu ambavyo unahitaji zaidi. Hata hivyo, baada ya siku chache, ukiwa umechoka kutafuta-tafuta vitu ndani ya mizigo yako, unaanza kufungua kila kitu. Lakini mara tu unapokaribia kumaliza kufungua kila kitu, unaona nguzo ikiinuka—na hivyo unalazimika kufunga mizigo yako tena! Hilo halingekuwa jambo rahisi wala lenye kupendeza. Ingawa hivyo, bado Waisraeli walipaswa ‘kuondoka mara moja baada ya’ wingu kuinuka.—Hes. 9:17-22.
Hivyo basi, tunatenda jinsi gani tunapopata mwongozo kutoka kwa Mungu? Je tunajaribu kuufuata ‘mara moja baada ya’ kutolewa? Au je, tunaendelea kufanya mambo kama vile tu tulivyozoea kufanya?
-