-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MAUA MAREFU YANAKUWA MAHALI PA KUJIFICHA
Zinaida anasema hivi: “Wakati mmoja, dada kadhaa waliziandikia familia zao barua wakiomba mbegu za mimea inayochanua maua makubwa. Tuliwaambia wasimamizi wa kambi kwamba tulitaka kupanda maua maridadi na kuomba tupewe udongo mweusi wenye rutuba kwa kusudi hilo. Tulishangaa walipokubali mara moja. Tulipanda maua ndani ya kambi na kwenye vijia vya kambi hiyo. Muda si muda kambi hiyo ilikuwa na vichaka virefu vya maua ya waridi na maua mengine maridadi na marefu. Bustani iliyokuwa katikati ya kambi ilikuwa na maua maridadi ya dalia na vichaka virefu vya maua ya daisy yenye rangi mbalimbali. Tulitembea huko, tukajifunza Biblia nyuma ya maua na kuficha vichapo vyetu katika vichaka vya waridi.
“Tulifanya mikutano yetu tulipokuwa tukitembea. Tulijigawa katika vikundi vya watu watano. Kila mmoja wa akina dada alikariri mapema fungu moja kati ya mafungu matano kutoka katika kichapo kinachozungumzia Biblia. Kisha baada ya kufungua kwa sala, tungerudia mafungu tuliyokariri na kuyazungumzia. Baada ya kumaliza kwa sala, tuliendelea na matembezi yetu. Magazeti yetu ya Mnara wa Mlinzi yalikuwa vijitabu vidogo [kama picha inayoonyeshwa kwenye ukurasa wa 161]. Kila siku tulijifunza jambo fulani, hasa andiko la siku na kukariri mafungu katika mikutano yetu ambayo tulifanya mara tatu kwa juma. Na si hayo tu, tulijitahidi kukariri sura nzima-nzima za Biblia na kuzirudia ili kutiana nguvu. Kwa njia hiyo hatukuathirika sana vichapo vyetu vilipotwaliwa wakati wa msako.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 157]
Maua marefu yalikuwa mahali pa kujificha kwa ajili ya mazungumzo na funzo la Biblia
-