-
“Wakaaji wa Muda” Waungana Katika Ibada ya KweliMnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 15
-
-
1. Baadhi ya watu wana maoni gani kuhusu watu wa nchi nyingine, lakini kwa nini maoni hayo hayafai?
KAMA makala iliyotangulia ilivyoonyesha, watu hutumia maneno “mtu wa nchi nyingine” au mgeni ili kumdharau mtu, kumdhihaki, au hata kuonyesha waziwazi kwamba wanamchukia. Si jambo la heshima kuwadharau watu wa taifa lingine. Isitoshe, mtazamo kama huo unaonyesha kwamba hatukubali ukweli wa mambo. Kitabu kimoja (The Races of Mankind) kinasema hivi: “Wanadamu wa jamii zote ni ndugu, kama Biblia inavyosema.” Kwa kawaida, ndugu wanakuwa tofauti sana, lakini vyovyote vile, wao ni ndugu.
2, 3. Yehova ana maoni gani kuhusu watu wa nchi nyingine?
2 Bila shaka, watu wa nchi nyingine wanaishi miongoni mwetu popote tulipo. Ndivyo ilivyokuwa pia kwa Waisraeli wa kale, ambao walikuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Yehova Mungu kwa msingi wa agano la Sheria. Watu hao ambao hawakuwa Waisraeli walikuwa na haki kwa kiasi fulani, hata hivyo, Waisraeli walipaswa kuwatendea kwa heshima na bila ubaguzi. Huo ni mfano mzuri kama nini wa kuiga! Wakristo wa kweli hawapaswi kamwe kuwa na ubaguzi au upendeleo. Kwa nini? Mtume Petro alisema hivi: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Mdo. 10:34, 35.
3 Wageni walioishi katika taifa la kale la Israeli walinufaika kwa kushirikiana kwa ukaribu na Waisraeli. Hilo lilionyesha maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo, maoni ambayo yaliandikwa miaka mingi baadaye na mtume Paulo alipouliza hivi kumhusu Yehova: “Je, yeye ni Mungu wa Wayahudi peke yao? Je, yeye si wa watu wa mataifa pia? Ndiyo, wa watu wa mataifa pia.”—Rom. 3:29; Yoe. 2:32.
4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba hakuna wageni katika taifa la “Israeli wa Mungu”?
4 Kwa msingi wa agano jipya, kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilichukua mahali pa taifa la asili la Israeli na kuwa na uhusiano wa pekee na Mungu. Kwa hiyo, kutaniko hilo linaitwa “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Na kama Paulo alivyoeleza, katika taifa hilo jipya, “hakuna Mgiriki wala Myahudi, tohara wala kutotahiriwa, mgeni, Msikithe, mtumwa, mtu huru, bali Kristo ni kila kitu na katika vitu vyote.” (Kol. 3:11) Basi, ni katika maana hiyo kwamba hakungekuwa na wageni katika kutaniko la Kikristo.
-
-
“Wakaaji wa Muda” Waungana Katika Ibada ya KweliMnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 15
-
-
USIWABAGUE WATU WA MATAIFA MENGINE
11. Sulemani alisema jambo gani ambalo liliwahusu watu wengine wasio Waisraeli?
11 Wakati wa uzinduzi wa hekalu mwaka wa 1026 K.W.K., na kupatana na ahadi ambayo Yehova alimpa Abrahamu, Sulemani alisema kwamba watu wa mataifa yote wangeshiriki katika kumsifu Yehova. Alisali hivi kutoka moyoni: “Pia kwa mgeni, ambaye si sehemu ya watu wako Israeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako (kwa maana watasikia habari za jina lako kuu na za mkono wako wenye nguvu na za mkono wako ulionyooshwa), naye kwa kweli aje na kusali kuelekea nyumba hii, basi na usikilize ukiwa mbinguni, makao yako yaliyofanywa imara, nawe ufanye kulingana na yote ambayo mgeni huyo anakuomba; kusudi watu wote wa dunia wajue jina lako ili wakuogope kama vile watu wako Israeli wanavyokuogopa.”—1 Fal. 8:41-43.
12. Kwa nini huenda watu fulani wanawaona Mashahidi wa Yehova kuwa watu wa ajabu au kama “wageni”?
12 Mgeni ni mtu anayeishi katika nchi ya kigeni au mtu anayejiunga na jamii au kikundi fulani. Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova walivyo. Wanawajibika kwanza kwa serikali ya kimbingu, yaani, Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo. Hivyo, hawajihusishi kamwe na mambo ya kisiasa, hata ikiwa wengine wanawaona kuwa watu wa ajabu wasiofaa katika jamii ya leo.
13. (a) Kwa nini mara nyingi maana ya neno “mgeni” inategemea maoni ya mtu binafsi? (b) Je, kusudi la Yehova la mwanzoni lilitia ndani wazo la wageni? Eleza.
13 Kwa kawaida wageni wanatambuliwa kwa sababu ya mambo fulani yanayowafanya waonekane kuwa tofauti na wengine. Wanaweza kutambuliwa kwa lugha yao, desturi zao, mwonekano au sura yao, au mavazi yao. Hata hivyo, mambo yanayowatofautisha na wengine ni machache yakilinganishwa na mambo yanayofanya wafanane na wanadamu wengine wote bila kujali ni wa taifa gani. Basi, kwa kweli mtu huonwa kuwa mgeni kwa sababu yuko tofauti katika njia fulani. Tunapojifunza kutokazia fikira mambo hayo yanayofanya mtu aonekane kuwa tofauti, inaelekea kwamba hatutamwona yeyote kuwa “mgeni” katika maana hiyo. Ikiwa watu wote duniani wangeishi chini ya serikali au chama kimoja cha kisiasa, hakungekuwa na mgeni katika maana ya kisiasa. Kwa kweli, Yehova alikusudia mwanzoni wanadamu wote waungane wakiwa familia moja chini ya utawala mmoja—utawala wake. Je, watu wa mataifa yote duniani wanaweza kuwa kama familia moja chini ya utawala mmoja leo?
14, 15. Mashahidi wa Yehova wamethamini nini wakiwa kikundi?
14 Katika ulimwengu wenye roho ya uchoyo na utaifa, inaburudisha kuona watu wasiowabagua watu wa mataifa mengine. Kwa kweli, si rahisi kuishinda roho ya ubaguzi. Mwanzilishi wa kituo cha televisheni cha CNN, Ted Turner, anaeleza jinsi alivyohisi alipofanya kazi na watu wenye vipawa kutoka katika mataifa mbalimbali: “Nilifurahi sana kukutana na watu hao. Nilijifunza kuwaona watu kutoka nchi nyingine kuwa raia wenzangu badala ya kuwaona kuwa ‘wageni.’ Nilianza kuona neno ‘mgeni’ kuwa neno la dharau na nikaweka sheria katika kituo cha CNN ya kwamba neno hilo lisitumiwe katika vipindi vya televisheni au katika mazungumzo ofisini. Badala yake, niliwaamuru watumie neno ‘kimataifa.’”
15 Katika nchi zote duniani, ni Mashahidi wa Yehova peke yao wakiwa kikundi wanaoiga njia ya Mungu ya kufikiri. Kwa sababu wamejifunza kuona mambo kama Yehova anavyoyaona, wamefanikiwa kushinda mawazo na hisia za ubaguzi kuelekea watu wa mataifa mengine. Badala ya kuwatilia shaka, kutowaamini, au hata kuwachukia watu wa mataifa mengine, wamejifunza kuthamini uwezo na sifa mbalimbali za watu hao nao wanaziona kuwa zenye kuvutia. Je, umetafakari kuhusu jambo hilo la pekee na kuona jinsi ambavyo limekunufaisha unaposhughulika na wengine?
-