-
Msamaha wa Yehova Unamaanisha Nini Kwako?Mnara wa Mlinzi—2012 | Novemba 15
-
-
SALA YA DAUDI NA MSAMAHA WA MUNGU
8, 9. Zaburi ya 51 inafunuaje hisia za moyoni za Daudi, na inatufundisha nini kumhusu Yehova?
8 Maneno ya wimbo ambao Mfalme Daudi alitunga baadaye yanafunua jinsi alivyojuta kutoka moyoni. Zaburi ya 51 ina sihi zenye kugusa moyo ambazo Daudi alimtolea Yehova na inaonyesha wazi kwamba alifanya mengi zaidi kuliko kukiri tu makosa yake. Alitubu pia dhambi zake. Daudi alihangaikia hasa uhusiano wake na Mungu. Aliungama hivi: “Dhidi yako wewe, wewe peke yako, nimetenda dhambi.” Akamsihi Yehova: “Uumbe moyo safi ndani yangu, Ee Mungu, na kuweka ndani yangu roho mpya, iliyo imara. . . . Unirudishie shangwe ya wokovu wako, nawe unitegemeze kwa roho ya kupenda.” (Zab. 51:1-4, 7-12) Je, wewe pia unazungumza na Yehova kwa unyoofu na kwa bidii kuhusu makosa yako?
9 Yehova hakuondoa matokeo yenye kuumiza ya dhambi za Daudi. Madhara hayo yangeendelea kumsumbua muda wote wa maisha yake. Hata hivyo, Yehova alimsamehe Daudi kwa sababu alionyesha toba, yaani, Daudi alikuwa na “moyo uliovunjika na kupondwa.” (Soma Zaburi 32:5; Zab. 51:17) Mungu Mweza-Yote anajua mtazamo na nia ambayo humchochea mtu kutenda dhambi. Badala ya kuagiza wazinzi hao wahukumiwe kifo na waamuzi wanadamu kulingana na Sheria ya Musa, kwa rehema Yehova aliingilia kati na kushughulikia mwenyewe kisa cha Daudi na Bath-sheba. (Law. 20:10) Mungu hata alimfanya mwana wao Sulemani kuwa mfalme wa Israeli baada ya Daudi.—1 Nya. 22:9, 10.
10. (a) Huenda Yehova alitumia msingi gani kumsamehe Daudi? (b) Ni mamb o gani yanayomchochea Yehova kusamehe?
10 Labda jambo lingine lililomfanya Yehova amsamehe Daudi ni jinsi Daudi mwenyewe alivyokuwa amemwonyesha rehema Sauli. (1 Sam. 24:4-7) Kama Yesu alivyoeleza, Yehova anatutendea kama tunavyowatendea wengine. Yesu alisema hivi: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa; na kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi.” (Mt. 7:1, 2) Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova atatusamehe dhambi zetu, hata dhambi nzito kama vile uzinzi au uuaji! Atatusamehe tukiwa na roho ya kusamehe, tukiungama dhambi zetu mbele yake, na tukionyesha kwamba tumebadili mtazamo wetu kuelekea matendo yetu mabaya. Watenda-dhambi wanapotubu kikweli wanapata “majira ya kuburudisha” kutoka kwa Yehova.—Soma Matendo 3:19.
MANASE ATENDA DHAMBI NZITO LAKINI ATUBU
11. Ni katika njia zipi Mfalme Manase alifanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Mungu?
11 Fikiria simulizi lingine la Kimaandiko linaloonyesha jinsi Yehova alivyo tayari kusamehe. Miaka 360 hivi baada ya Daudi kuanza kutawala, Manase alitawazwa kuwa mfalme wa Yuda. Uovu ulienea sana wakati wa utawala wake wa miaka 55, na mazoea yake yenye kuchukiza sana yalishutumiwa na Yehova. Kati ya mambo mengine, Manase alijenga madhabahu za Baali, akaabudu “jeshi lote la mbinguni,” akawapitisha wanawe motoni, na kuendeleza mazoea ya kuwasiliana na pepo. Kwa kweli, “alifanya kwa kiasi kikubwa yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.”—2 Nya. 33:1-6.
12. Manase alimrudiaje Yehova?
12 Hatimaye, Manase alitekwa kutoka katika nchi yake na kutupwa gerezani huko Babiloni. Akiwa huko, huenda alikumbuka maneno haya ambayo Musa aliwaambia Waisraeli: “Utakapokuwa katika dhiki kali na maneno yote haya yawe yamekupata mwishoni mwa siku hizo, basi utarudi kwa Yehova Mungu wako na kuisikiliza sauti yake.” (Kum. 4:30) Manase alimrudia Yehova. Jinsi gani? ‘Aliendelea kujinyenyekeza sana’ na ‘kuendelea kusali’ kwa Mungu (kama picha inavyoonyesha kwenye ukurasa wa 21). (2 Nya. 33:12, 13) Hatujui maneno hususa ambayo Manase alisema katika sala hizo, lakini tunaweza kuwazia kwamba huenda alisema maneno kama ya Mfalme Daudi, yaliyoandikwa katika Zaburi ya 51. Kwa vyovyote vile, moyo wa Manase ulibadilika kabisa.
13. Kwa nini Yehova alimsamehe Manase?
13 Yehova aliitikiaje sala za Manase? “Yeye akakubali kusihiwa [na Manase] kisha Yeye akasikia ombi lake la kutaka kibali.” Kama Daudi alivyofanya awali, Manase alitambua uzito wa dhambi zake naye akatubu kikweli. Kwa sababu hiyo, Mungu alimsamehe Manase na kumweka tena kuwa mfalme huko Yerusalemu. Kwa hiyo, “Manase akapata kujua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.” (2 Nya. 33:13) Inatia moyo pia kujifunza kutokana na mfano huo kwamba Mungu wetu mwenye rehema huwasamehe wale wanaotubu kikweli.
JE, MSAMAHA WA YEHOVA HAUNA MIPAKA?
14. Yehova huamuaje ikiwa atawasamehe watenda-dhambi?
14 Leo, watu wengi wa Mungu huenda wasihitaji kuomba msamaha kwa ajili ya kufanya dhambi nzito kama zile za Daudi na Manase. Hata hivyo, uhakika wa kwamba Yehova aliwasamehe wafalme hao wawili unatusaidia kutambua kwamba Mungu wetu yuko tayari kusamehe hata dhambi nzito sana ikiwa mtenda-dhambi anatubu kikweli.
-
-
Msamaha wa Yehova Unamaanisha Nini Kwako?Mnara wa Mlinzi—2012 | Novemba 15
-
-
KUFAIDIKA KUTOKANA NA MSAMAHA WA YEHOVA
17, 18. Tunawezaje kupata msamaha wa Yehova?
17 Tunapaswa kuitikiaje utayari wa Yehova wa kusamehe? Bila shaka, tunapaswa kutenda kama Daudi na Manase. Tunapaswa kutambua hali yetu ya dhambi, kutubu makosa yetu, kumsihi sana Yehova atusamehe, na kumwomba aumbe moyo safi ndani yetu. (Zab. 51:10) Ikiwa tumetenda dhambi nzito, tunapaswa pia kutafuta msaada wa kiroho kutoka kwa wazee. (Yak. 5:14, 15) Licha ya hali zetu, inafariji kukumbuka kwamba Yehova ana sifa zilezile alizomwambia Musa, yaani, yeye ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli, anayehifadhi fadhili zenye upendo kwa ajili ya maelfu, anayesamehe kosa na ubaya na dhambi.” Yehova hajabadilika.—Kut. 34:6, 7.
18 Akitumia mfano wenye nguvu, Yehova aliwaahidi Waisraeli waliotubu kwamba angeondoa kabisa doa lao la dhambi, na angefanya dhambi zao “nyekundu” ziwe nyeupe kama “theluji.” (Soma Isaya 1:18.) Kwa hiyo basi, msamaha wa Yehova unamaanisha nini kwetu? Unamaanisha kwamba anatusamehe kabisa dhambi na makosa yetu, maadamu tunaonyesha mtazamo wa shukrani na wa kutubu.
-