Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Hekima Inavyohusika
    Amkeni!—2008 | Juni
    • Uhuru Mwingi Kadiri Gani?

      Huenda kisababishi kikubwa zaidi cha matatizo kati ya wazazi na vijana wanaobalehe kikahusiana na suala la uhuru. Kijana anapaswa kupewa uhuru mwingi kadiri gani? Kuhusu uhuru, baba mmoja alisema hivi: “Mara nyingine, mimi huhisi kwamba binti yangu akionja asali atachonga mzinga.”

      Kwa wazi, kuwapa vijana uhuru usio na mipaka kutakuwa na matokeo mabaya. Kwa kweli, Biblia inaonya kwamba “mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.” (Methali 29:15) Vijana wa umri wowote ule wanahitaji mwongozo thabiti, na inapohusu kutekeleza sheria za familia wazazi wanapaswa kuwa wenye upendo lakini imara. (Waefeso 6:4) Wakati huohuo, vijana wanapaswa kupewa kiasi fulani cha uhuru ili wawe tayari zaidi kufanya maamuzi ya hekima baadaye maishani.

      Kwa mfano, fikiria jinsi ulivyojifunza kutembea. Mwanzoni, ulipokuwa mtoto mchanga, ulibebwa. Muda si muda, ulianza kutambaa kisha kutembea. Bila shaka, kutambaa au kutembea kunaweza kumhatarisha mtoto mdogo. Hivyo, wazazi wako walikuwa waangalifu sana na huenda walikuwekea vizuizi fulani ili usikaribie maeneo hatari, kama vile ngazi. Hata hivyo, walikuruhusu utembee peke yako na baada ya kuanguka mara kadhaa, hatimaye ulifaulu kutembea bila matatizo.

      Kupata uhuru kunahusisha hatua kama hizo. Mwanzoni, kwa njia ya mfano wazazi wanawabeba watoto wao wachanga kwa kuwafanyia maamuzi. Baadaye, kadiri watoto wanavyokomaa, wazazi wanawaruhusu watambae kwa kujifanyia maamuzi fulani. Wakati huohuo wanawawekea vijana vizuizi ambavyo vinawalinda kutokana na madhara. Kadiri watoto wao wanavyokomaa, ndivyo wazazi wanavyowaruhusu “watembee” peke yao. Kisha watakapokuwa watu wazima, watakuwa na uwezo kamili wa ‘kubeba mzigo wao wenyewe.’—Wagalatia 6:5.

      Kujifunza Kutokana na Mfano wa Biblia

      Kwa wazi, akiwa na umri wa miaka 12, Yesu alikuwa amepewa uhuru fulani na wazazi wake, lakini hakuutumia vibaya. Badala yake, ‘aliendelea kujitiisha’ kwa wazazi wake na “akazidi kufanya maendeleo katika hekima na ukuzi wa kimwili, akipata kibali kwa Mungu na wanadamu.”—Luka 2:51, 52.

      Ukiwa mzazi, unaweza kujifunza kutokana na mfano huo kwa kuwapa watoto wako uhuru zaidi kadiri wanavyoonyesha wanaweza kuutumia vizuri. Kuhusiana na hilo, fikiria yale ambayo wazazi fulani wamesema kuhusu mambo waliyojionea.

      “Nilikuwa nikiingilia sana shughuli za watoto wangu. Lakini baadaye, nilianza kuwafundisha kanuni mbalimbali na kuwaacha wafanye uamuzi kupatana na yale waliyojifunza. Baada ya hapo, niliona kwamba walianza kufikiria kwa makini zaidi maamuzi yao.”—Soo Hyun, Korea.

      “Nyakati zote mimi na mume wangu huwa na wasiwasi kuhusu kuwapa watoto wetu uhuru, lakini hatujaacha hilo lituzuie kuwaruhusu watumie uhuru wanaostahili kwa njia inayofaa.”—Daria, Brazili.

      “Nimegundua kwamba ni muhimu kumpongeza mwana wangu ambaye ni tineja anapotumia vizuri uhuru ninaompa. Pia mimi hufanya yale ninayomwambia afanye. Kwa mfano, mimi humwambia ninakoenda na ninachofanya. Pia ikiwa nitachelewa, mimi humjulisha.”—Anna, Italia.

      “Katika nyumba yetu tunasisitiza kwamba wana wetu hawana haki ya kujitegemea lakini wanapaswa kuthibitisha kwamba wanaweza kutegemeka.”—Peter, Uingereza.

      Kukabili Matokeo

      Biblia inasema hivi: “Ni jambo jema kwa mwanamume kuchukua nira wakati wa ujana wake.” (Maombolezo 3:27) Mojawapo ya njia bora ya kijana kujichukulia nira ya wajibu ni kujionea mwenyewe ukweli wa taarifa hii: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.”—Wagalatia 6:7.

      Wakiwa na nia nzuri, huenda wazazi fulani wakawakinga vijana wao kutokana na matokeo ya matendo yasiyo ya hekima. Kwa mfano, tuseme kwamba kwa kununua vitu asivyohitaji mvulana fulani anajiingiza katika deni. Atajifunza nini ikiwa Baba na Mama watalipa deni hilo? Kwa upande mwingine, mvulana huyo angejifunza nini ikiwa wazazi wake wangemsaidia kupanga jinsi atakavyojilipia deni hilo?

      Wazazi hawafaidi watoto wao hata kidogo wanapowakinga kutokana na matokeo ya tabia zao za kutokuwa waangalifu. Badala ya kuwatayarisha kwa ajili ya maisha ya utu uzima, kufanya hivyo kunawafundisha kwamba nyakati zote kutakuwa na mtu wa kuwaondoa matatani, kuwatatulia matatizo wanayojiletea, na kuwafunikia makosa yao. Inafaa zaidi kuwaacha vijana wavune walichopanda na wajifunze kutatua matatizo yao. Hiyo ni sehemu muhimu ya ‘kuzoeza nguvu zao za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’—Waebrania 5:14.

  • Kuwalea Vijana Wanaobalehe—Jinsi Hekima Inavyohusika
    Amkeni!—2008 | Juni
    • [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      Kuwapa Uhuru Zaidi

      Mara nyingi vijana hutaka uhuru mwingi kuliko wanavyostahili. Wakati huohuo, wazazi fulani huwapa uhuru mdogo kuliko wanavyoweza. Usawaziko unaweza kupatikana jinsi gani? Kwanza huenda ukataka kuchunguza orodha iliyo hapa chini. Mwana au binti yako ni mwenye kutegemeka katika mambo gani?

      □ Kuchagua marafiki

      □ Kuchagua mavazi

      □ Kutumia pesa vizuri

      □ Kurudi nyumbani kwa wakati uliowekwa

      □ Kumaliza kazi za nyumbani

      □ Kumaliza kazi za shule

      □ Kuomba msamaha unapokosea

      □ Mengine ․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․․

      Ikiwa tayari kijana wako anaonyesha ukomavu katika baadhi ya mambo yaliyo hapo juu, kwa nini usifikirie njia fulani za kumpa uhuru zaidi?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki