-
Utumwa Utakapokoma!Amkeni!—2002 | Juni 22
-
-
Utumwa Utakapokoma!
UHURU! Neno hilo ni mojawapo ya maneno yanayowafurahisha sana wanadamu. Watu wamepigana na kuteseka, kuishi na kufa, wakitafuta uhuru. Hata hivyo, inahuzunisha kwamba wengi wamefanya hivyo bila kufanikiwa sana. Je, kuna tumaini lolote kwamba utumwa utakoma—tumaini ambalo halitawafadhaisha wanadamu wala kuwakatisha tamaa? Naam, lipo.
Mtume Paulo aliongozwa na Mungu kuandika ahadi yake inayosema hivi: “Viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Lakini tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Mungu ataleta ‘uhuru huo wenye utukufu’? Njia moja ni kuchunguza jinsi ambavyo Mungu ameshughulika na wanadamu sikuzote.
Biblia inasema hivi: “Iliko roho ya Yehova, kuna uhuru.” (2 Wakorintho 3:17) Naam, roho ya Mungu, au nguvu yake ya utendaji, ina nguvu nyingi sana. Kwa muda mrefu, ameitumia kuwaweka watu huru kwa njia nyingi. Jinsi gani? Twapaswa kukumbuka kwamba kuna aina nyingi za utumwa. Tayari tumezungumzia aina moja yenye ukatili mwingi sana—jinsi ambavyo watu wenye uwezo huwatumikisha watu wasio na uwezo kwa nguvu au kwa ujeuri. Lakini hebu fikiria aina nyingine za utumwa.
Watu wanaweza kuwa watumwa wa mazoea mbalimbali ambayo ni vigumu sana kuyaacha. Na watu wanaweza kuwa watumwa wa uwongo na udanganyifu, wakidanganywa kuamini mafundisho ya uwongo sikuzote. Zaidi ya yote, kuna aina moja ya utumwa ambayo inatuathiri sote—iwe twajua au hatujui—na matokeo yake husababisha kifo. Hata hivyo, ni lazima tukazie kwamba ijapokuwa tunazungumzia aina mbalimbali za utumwa katika habari hii, hatumaanishi hata kidogo kwamba zote ziko sawa. Aina za utumwa zinatofautiana sana. Hata hivyo, zinafanana katika jambo moja. Hatimaye, Mungu wa uhuru atahakikisha kwamba wanadamu wamewekwa huru kutokana na aina zote hizo za utumwa.
-
-
Utumwa Utakapokoma!Amkeni!—2002 | Juni 22
-
-
Utumwa Hatari Zaidi Usioonekana Wazi
Hebu ona jinsi Yesu alivyofafanua utumwa mmoja hatari usioonekana wazi, ambao ulitajwa awali na unaathiri kila mwanamume, mwanamke, na mtoto hapa duniani: “Kwa kweli kabisa mimi nawaambia, Kila mtendaji wa dhambi ni mtumwa wa dhambi.” (Yohana 8:34) Ni nani anayeweza kudai kwamba yeye hatendi dhambi? Hata mtume Paulo alikubali hivi: “Lile jema nitakalo silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo nazoea kulifanya.” (Waroma 7:19) Ijapokuwa hakuna mtu anayeweza kujiweka huru kutokana na dhambi, bado kuna tumaini.
Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Mwana akiwaweka nyinyi huru, mtakuwa huru kikweli.” (Yohana 8:36) Utimizo wa ahadi hiyo utamaanisha uhuru wa kweli kutokana na ule utumwa hatari zaidi. Ili tuelewe namna ambavyo twaweza kuwekwa huru kutokana na utumwa huo, lazima kwanza tuone jinsi tulivyoingia utumwani.
Biblia inaeleza kwamba Mungu alimuumba mwanadamu akiwa na hiari, bila mwelekeo wa kutenda dhambi. Lakini mwana mmoja wa kiroho wa Mungu, asiyeonekana, alitaka kuwatawala wanadamu, bila kujali mateso ambayo yangewapata. Ili kufikia lengo hilo, malaika huyo mwasi, ambaye baadaye aliitwa Shetani Ibilisi, aliwafanya wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, wamwache Mungu. Adamu alipoasi kimakusudi maagizo ya Mungu yaliyokuwa wazi, akawa mtendaji wa dhambi na akapitisha kutokamilika na kifo kwa wazao wake wote. (Waroma 5:12) Hatimaye, Shetani akawa “mtawala wa ulimwengu,” na ‘dhambi imewatawala wanadamu ikiwa mfalme pamoja na kifo.’—Yohana 12:31; Waroma 5:21; Ufunuo 12:9.
Twawezaje kuwekwa huru? Tunapokuwa wanafunzi wa Yesu, twaweza kufaidika kutokana na kifo cha Kristo cha kidhabihu, ambacho kina uwezo wa “kumfanya kuwa si kitu yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi” na “kuwaweka huru wale wote ambao kwa hofu ya kifo walitiishwa kwenye utumwa maisha zao zote.” (Waebrania 2:14, 15) Hebu wazia hilo—kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo! Je, uhuru wa aina hiyo haukufurahishi?
Lakini, vipi juu ya utumwa ambao tulizungumzia hapo mwanzoni? Je, kuna wakati ambapo watu hawatatumikishwa tena kwa nguvu?
Msingi Hakika wa Kuwa na Tumaini
Bila shaka, twaweza kuwa na uhakika kwamba utumwa huo wenye kuchukiza utakomeshwa. Kwa nini? Hebu fikiria jambo hili: Yehova Mungu alihusika moja kwa moja katika ukombozi mkubwa zaidi wa watumwa katika historia yote. Huenda ikawa unafahamu simulizi hilo.
Waisraeli walitumikishwa na Wamisri, wakalazimishwa kufanya kazi ngumu na kutendewa kwa ukatili. Wakamlilia Mungu awasaidie, naye, akisukumwa na huruma zake nyingi, akawasikia na kutenda. Yehova akawatumia Musa na Aroni kama wasemaji wake ili kumwamuru Farao Mmisri awaachilie huru Waisraeli. Mfalme huyo mwenye kiburi akakataa katakata, hata baada ya Yehova kuleta mapigo ambayo yaliharibu nchi hiyo. Hatimaye, Mungu akamnyenyekeza Farao. Waisraeli wakaachiliwa huru!—Kutoka 12:29-32.
Ni simulizi lenye kusisimua, sivyo? Hata hivyo, huenda ukajiuliza kwa nini Mungu hajafanya tendo kama hilo katika nyakati zetu. Mbona hajaingilia shughuli za wanadamu na kukomesha utumwa? Kumbuka, Shetani ndiye “mtawala wa ulimwengu” wala si Yehova. Kwa sababu ya masuala yaliyozushwa huko Edeni, Yehova amemruhusu Adui huyo mwovu kutawala kwa kipindi kifupi. Utumwa, uonevu, na ukatili ni ishara za utawala wa Shetani. Kwa sababu ya Shetani, utawala wa wanadamu umeshindwa kabisa. Biblia inaeleza vizuri utawala huo inaposema hivi: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989.
Lakini kwa muda gani? Biblia inaeleza kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” wakati ambapo ubinafsi na pupa zingeongezeka sana. (2 Timotheo 3:1, 2) Hiyo inamaanisha kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu, ambao Yesu alitufundisha tusali juu yake, utaanzisha jamii yenye uadilifu na utumwa utapigwa marufuku. (Mathayo 6:9, 10) Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu, atachukua hatua ya kukomesha utumwa wa aina zote hadi adui wa mwisho, kifo, atakapofanywa kuwa si kitu.—1 Wakorintho 15:25, 26.
Siku hiyo itakapofika, wanadamu waaminifu watatambua kwamba ule ukombozi ambao watu wa Mungu walipata kutoka utumwani huko Misri ulikuwa wonyesho mdogo tu wa ukombozi huo mkubwa zaidi. Naam, muda si muda, “viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu.” Hatimaye, kila mtu ataweza kufurahia kikamili “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Waroma 8:21.
-