-
“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”Mnara wa Mlinzi—2008 | Julai 1
-
-
“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”
MARIA alitazama juu akiwa amekodoa macho, mgeni alipoingia nyumbani kwao. Mgeni huyo hakumwuliza kuhusu baba wala mama yake kwani alikuwa amekuja kumwona yeye! Alikuwa na hakika kwamba mgeni huyo hakuwa mkaaji wa Nazareti. Katika mji mdogo kama huo, ilikuwa rahisi kuwatambua wageni. Mgeni huyu angetambuliwa kwa urahisi mahali popote pale. Alimsalimu Maria kwa njia isiyo ya kawaida, alipomwambia hivi: “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.”—Luka 1:28.
-
-
“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”Mnara wa Mlinzi—2008 | Julai 1
-
-
Malaika Anamtembelea
Huenda unajua kwamba mgeni wa Maria hakuwa mwanadamu bali ni malaika Gabrieli. Alipomwita ‘aliyependelewa sana,’ Maria ‘alishtushwa sana’ na maneno hayo na kushangazwa na salamu hizo zisizo za kawaida. (Luka 1:29) Alipendelewa sana na nani? Maria hakutarajia kupendelewa sana miongoni mwa wanadamu. Lakini malaika alikuwa akizungumza kuhusu kupendelewa na Yehova Mungu. Hilo lilikuwa muhimu kwake. Lakini Maria hakukata kauli kwa kiburi kwamba anapendelewa na Mungu. Tukijitahidi kupata kibali cha Mungu, bila kujivuna tukifikiri kwamba tayari tumekipata, tutajifunza somo muhimu ambalo Maria alielewa kabisa. Mungu anawapinga wenye majivuno, lakini anawapenda na kuwategemeza watu wa hali ya chini na wanyenyekevu.—Yakobo 4:6.
Maria angehitaji kuwa mnyenyekevu hivyo, kwa sababu malaika alimtolea pendeleo la ajabu. Alimwambia kwamba angemzaa mtoto ambaye angekuwa mwanadamu muhimu zaidi ya wote. Gabrieli alisema hivi: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Bila shaka Maria alijua ahadi ambayo Mungu alikuwa amempa Daudi miaka zaidi ya elfu moja mapema, kwamba mmoja wa wazao wake angetawala milele. (2 Samweli 7:12, 13) Hivyo, mwana wake angekuwa masihi aliyekuwa akitarajiwa na watu wa Mungu kwa karne nyingi!
Zaidi ya hayo, malaika alimwambia Maria kwamba mwana wake ‘angeitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi.’ Mwanamke wa kibinadamu angeweza jinsi gani kuzaa Mwana wa Mungu? Kwa kweli, Maria angeweza jinsi gani kuzaa mwana? Alikuwa amechumbiwa na Yosefu lakini hawakuwa wameoana. Maria aliuliza swali hilo waziwazi kwa maneno haya: “Hilo litawezekanaje, kwa kuwa silali na mwanamume?” (Luka 1:34) Ona kwamba alizungumza kuhusu ubikira wake bila kuona aibu hata kidogo. Kinyume na hilo, alijivunia kuwa bikira. Leo, vijana wengi wako tayari kutupilia mbali ubikira wao na wanawadhihaki wale ambao bado ni mabikira. Bila shaka ulimwengu umebadilika. Hata hivyo, Yehova hajabadilika. (Malaki 3:6) Kama ilivyokuwa katika siku za Maria, bado Yehova anawathamini wale wanaoshikilia viwango vyake vya maadili.—Waebrania 13:4.
Ingawa alikuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu, Maria alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu. Hivyo basi, angeweza jinsi gani kuzaa mtoto mkamilifu, Mwana wa Mungu? Gabrieli alieleza: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa sababu hiyo pia kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Kitu kitakatifu ni kitu “safi” na “kilichotakata.” Kwa kawaida, watoto wanarithi hali ya kutokamilika kutoka kwa wazazi wao. Lakini katika kisa hiki, Yehova angefanya muujiza wa pekee. Angehamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria, kisha nguvu zake za utendaji, au roho takatifu, ‘ingemfunika’ Maria ili kumzuia kabisa mtoto huyo asipate dhambi. Je, Maria aliamini ahadi ya malaika? Aliitikia namna gani?
Itikio la Maria kwa Gabrieli
Ni jambo ngumu kwa watu wenye mashaka, kutia ndani wanatheolojia wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, kuamini kwamba bikira anaweza kuzaa. Hata ingawa wana elimu nyingi, wameshindwa kuelewa kweli fulani rahisi. Kama alivyosema Gabrieli, “kwa Mungu hakuna tangazo lolote lisilowezekana.” (Luka 1:37) Maria alikubali maneno ya Gabrieli kuwa ya kweli, kwa sababu alikuwa mwanamke mwenye imani kubwa. Hata hivyo, Maria hakuamini tu alichoambiwa bila uthibitisho kamili. Kama mtu yeyote anayefikiri, Maria alihitaji uthibitisho ambao ungetegemeza imani yake na Gabrieli alikuwa tayari kumpa uthibitisho zaidi. Alimwambia kuhusu Elisabeti, mtu wa ukoo wake, aliyezeeka na kwa muda mrefu alijulikana kuwa tasa. Mungu alikuwa amemwezesha achukue mimba kimuujiza!
Sasa Maria angefanya nini? Alikuwa amepewa mgawo na kuthibitishiwa kwamba Mungu angetimiza mambo yote aliyosema Gabrieli. Tusifikiri kwamba pendeleo hilo halikutokeza mahangaiko au matatizo yoyote. Kwanza, alihitaji kufikiria kuhusu uchumba wake na Yosefu. Je, bado Yosefu angekubali kumwoa baada ya kugundua kwamba ana mimba? Pia, huenda mgawo wenyewe ulionekana kuwa mzito sana. Alipaswa kubeba uhai wa kiumbe chenye thamani zaidi kati ya viumbe vyote vya Mungu, yaani, Mwana mpendwa wa Mungu! Angemtunza akiwa kitoto kichanga kisicho na uwezo na kumlinda katika ulimwengu mbovu. Kwa kweli huo ulikuwa mgawo mzito sana!
Biblia inaonyesha kwamba nyakati nyingine hata wanaume waaminifu na wenye nguvu walisita kukubali migawo migumu waliyopewa na Mungu. Musa alisema kwamba hangeweza kuzungumza kwa ufasaha vya kutosha ili kutumiwa akiwa msemaji wa Mungu. (Kutoka 4:10) Yeremia alisema kwamba alikuwa “mvulana tu,” mchanga sana asiweze kukubali mgawo aliopewa na Mungu. (Yeremia 1:6) Naye Yona aliukimbia mgawo wake! (Yona 1:3) Lakini Maria alitenda jinsi gani?
Maneno yake ya unyenyekevu na utii yamekumbukwa kwa miaka mingi. Alimwambia Gabrieli hivi: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” (Luka 1:38) Kijakazi ndiye aliyekuwa mtumishi wa chini zaidi kati ya watumishi wote kwani maisha yake yalikuwa mikononi mwa bwana wake. Hivyo ndivyo alivyohisi Maria kumwelekea Bwana wake, Yehova. Alijua kwamba alikuwa salama mikononi mwake, kwamba ni mshikamanifu kwa wale walio washikamanifu kwake, na Yehova angembariki ikiwa angejitahidi kutimiza mgawo huo mgumu.—Zaburi 18:25.
Nyakati fulani Mungu anatuambia tufanye jambo linaloonekana kuwa gumu, hata lisilowezekana machoni petu. Hata hivyo, katika Neno lake anatupa sababu nzuri za kumtegemea, yaani, kujiweka mikononi mwake kama alivyofanya Maria. (Methali 3:5, 6) Je, tutafanya hivyo? Tukifanya hivyo atatuthawabisha, na kutupa sababu za kuimarisha imani yetu kwake hata zaidi.
-