Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Pigano Letu la Kubaki Wenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Desemba 1
    • Simulizi la Maisha

      Pigano Letu la Kubaki Wenye Nguvu Kiroho

      Limesimuliwa na Rolf Brüggemeier

      Barua ya kwanza niliyopokea nikiwa gerezani ilitoka kwa rafiki fulani. Alinijulisha kwamba mama yangu na ndugu zangu wadogo, Peter, Jochen, na Manfred walikuwa pia wamekamatwa. Hivyo, dada zetu wawili wadogo wakabaki bila wazazi wala ndugu na dada. Kwa nini wenye mamlaka wa Ujerumani Mashariki waliitesa familia yetu? Ni nini kilichotusaidia kubaki wenye nguvu kiroho?

  • Pigano Letu la Kubaki Wenye Nguvu Kiroho
    Mnara wa Mlinzi—2006 | Desemba 1
    • Kutumikia Chini ya Marufuku

      Kwa sababu ya marufuku, tulilazimika kuingiza kisiri vichapo vya Biblia Ujerumani Mashariki. Nilisafirisha vichapo kutoka magharibi mwa Berlin, ambako vichapo vyetu havikuwa vimepigwa marufuku na kuviingiza nchini. Nilihepa polisi mara kadhaa, lakini Novemba (Mwezi wa 11) 1950, nilikamatwa.

      Stasi walinitia katika chumba cha chini ya ardhi ambacho hakikuwa na dirisha. Sikuruhusiwa kulala mchana, na usiku nilihojiwa, na nyakati nyingine nilipigwa. Sikuweza kupashana habari na mtu yeyote wa familia yetu hadi Machi (Mwezi wa 3) 1951, wakati Mama, Peter, na Jochen walipokuja kusikiza kesi yangu. Nilihukumiwa kifungo cha miaka sita.

      Peter, Jochen, na Mama walikamatwa siku sita baada ya kusikizwa kwa kesi yangu. Baadaye, mwamini mwenzetu alimtunza dada yangu Hannelore, aliyekuwa na miaka 11, na shangazi yetu akamchukua Sabine, aliyekuwa na miaka 7. Walinzi wa Stasi waliwatendea Mama na ndugu zangu kama wahalifu hatari, na hata waliwanyang’anya kamba zao za viatu. Walilazimika kusimama muda wote walipokuwa wakihojiwa. Wao pia walihukumiwa kifungo cha miaka sita kila mmoja.

      Mnamo 1953, mimi pamoja na wafungwa wengine Mashahidi tulipewa kazi ya kujenga uwanja mdogo wa ndege za kijeshi. Tulikataa kazi hiyo. Wenye mamlaka walituadhibu kwa kututenga na wengine kwa siku 21, bila kazi, barua, na chakula cha kutosha. Dada fulani Wakristo walibakisha mkate kutokana na posho yao ndogo na kutuletea kisiri. Hilo liliniwezesha kumfahamu Anni, mmoja wa dada hao, na kisha kumuoa baada ya kutoka gerezani mwaka wa 1956, na yeye mwaka wa 1957. Mwaka mmoja baada ya kuoana, binti yetu Ruth, alizaliwa. Peter, Jochen, na pia Hannelore walifunga ndoa karibu wakati huohuo.

      Miaka mitatu hivi baada ya kutoka gerezani, nilikamatwa tena. Ofisa wa Stasi alijaribu kunishawishi niwe mpelelezi. Alisema: “Bwana mpendwa Brüggemeier, tafadhali tumia akili. Unajua jinsi maisha yalivyo gerezani, na hatutaki uteseke tena. Unaweza kubaki ukiwa Shahidi, kuendelea kujifunza, na kuzungumza kuhusu Biblia kama upendavyo. Tunataka tu utujulishe mambo mapya. Fikiria mke wako na binti yako mdogo.” Maneno hayo ya mwisho yaliniumiza sana. Hata hivyo, nilijua kwamba nikiwa gerezani, Yehova angetunza familia yangu vizuri zaidi kuliko jinsi ambavyo ningeitunza, naye alifanya hivyo!

      Wenye mamlaka walijaribu kumlazimisha Anni afanye kazi wakati wote na kuwacha watu wengine wamtunze Ruth katikati ya juma. Anni alikataa, naye alifanya kazi usiku ili amtunze Ruth mchana. Ndugu zetu walitujali sana na walimpa mke wangu vitu vingi hivi kwamba aliweza kuwagawia wengine. Wakati huo, nilikaa gerezani karibu miaka sita zaidi.

      Jinsi Tulivyodumisha Imani Tulipokuwa Gerezani

      Baada tu ya kurudi gerezani, Mashahidi tuliofungwa nao walitaka sana kujua habari mpya ambazo zilikuwa zimechapishwa karibuni. Nilifurahi sana kwamba nilikuwa nimejifunza kwa makini gazeti la Mnara wa Mlinzi na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ili niweze kuwatia moyo kiroho!

      Tulipowaomba walinzi Biblia, walijibu hivi: “Kuwapa Mashahidi wa Yehova Biblia ni hatari kama tu kumpa mhalifu aliye gerezani vifaa vya kuvunja gereza ili atoroke.” Kila siku, ndugu walioongoza walichagua andiko la Biblia ambalo tungezungumzia. Kila siku tuliporuhusiwa kutembea kwa dakika 30 kwenye uwanja wa gereza, tulipendezwa zaidi kuchunguza andiko la Biblia la siku kuliko kufanya mazoezi ya mwili ama kupunga hewa. Ingawa kila mmoja alipaswa kuwa umbali wa meta 5 hivi kutoka kwa mwenzake na ingawa hatukuruhusiwa kuzungumza, bado tulipata njia za kujulisha wengine andiko la siku. Tuliporudi katika vyumba vyetu gerezani, kila mmoja alisema yale ambayo aliweza kusikia, na kisha tukawa na mazungumzo yetu ya kila siku ya Biblia.

      Hatimaye, mpelelezi fulani alitusaliti, nami nikawekwa katika kifungo cha upweke. Ilikuwa baraka kama nini kwamba kufikia wakati huo nilikuwa nimetia akilini mamia kadhaa ya maandiko! Nilitumia siku hizo za upweke kutafakari kuhusu habari mbalimbali za Biblia. Kisha, nilihamishiwa kwenye gereza lingine ambako mlinzi aliniweka katika chumba ambamo mlikuwa na Mashahidi wengine wawili, na jambo lenye kufurahisha zaidi ni kwamba alitupa Biblia. Baada ya kukaa kwa miezi sita katika kifungo cha upweke, nilithamini sana kuweza tena kuzungumzia habari za Biblia pamoja na waamini wenzangu.

      Ndugu yangu Peter anaeleza jambo ambalo lilimsaidia kuvumilia alipokuwa katika gereza lingine: “Nilifikiria maisha katika ulimwengu mpya na kutafakari kuhusu habari za Biblia. Sisi Mashahidi tuliimarishana kwa kuulizana maswali ya Biblia au mitihani mingine ya Kimaandiko. Maisha hayakuwa rahisi. Wakati mwingine tuliwekwa watu 11 katika chumba kidogo chenye ukubwa wa meta 12 za mraba. Tulilazimika kufanya kila kitu humo—kula, kulala, kuoga, hata kwenda choo. Tulikuwa wenye wasiwasi na hasira.”

      Jochen, mmoja wa ndugu zangu, anasema hivi kuhusu hali yake gerezani: “Niliimba nyimbo za kitabu chetu cha nyimbo ambazo niliweza kukumbuka. Kila siku nilitafakari kuhusu moja ya maandiko ambayo nilikumbuka. Baada ya kuachiliwa huru, niliendelea na zoea zuri la kujielimisha kiroho. Kila siku nilisoma andiko la Biblia la siku pamoja na familia yangu. Pia, tulitayarisha mikutano yote.”

      Mama Atoka Gerezani

      Baada ya kukaa gerezani kwa miaka miwili hivi, Mama aliachiliwa huru. Alitumia uhuru wake kujifunza Biblia pamoja na Hannelore na Sabine akiwasaidia kujiwekea msingi mzuri wa imani. Aliwafundisha pia kushughulikia masuala au mambo mbalimbali yaliyotokea shuleni kwa sababu ya imani yao katika Mungu. Hannelore anasema: “Hatukujali sana hali ingekuwaje kwa sababu tulihimizana nyumbani. Uhusiano wa karibu wa familia yetu ulitusaidia kukabiliana na tatizo lolote.”

      Hannelore anaendelea kusema: “Pia, tuliwapelekea chakula cha kiroho ndugu zetu waliokuwa gerezani. Kwa kutumia maandishi madogo, tuliandika kwa mkono nakala ndogo ya gazeti zima la Mnara wa Mlinzi kwenye karatasi yenye nta.” Kisha, tukafunika kurasa hizo kwa karatasi isiyolowa maji na kuificha katika furushi lenye matunda makavu tulilotuma kila mwezi. Tulifurahi kwelikweli walipotuambia kwamba matunda tuliyotuma yalikuwa ‘matamu sana.’ Tulikazia sana fikira kazi yetu hivi kwamba sina budi kusema kuwa huo ulikuwa wakati mzuri ajabu!”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki