-
Je, Utatoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu?Mnara wa Mlinzi—2005 | Agosti 15
-
-
Je, Utatoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu?
‘Tunatoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova.’—2 WAKORINTHO 3:18.
1. Musa aliona nini, na ni nini kilichotukia baadaye?
NI MOJAWAPO ya maono yenye kuogopesha sana ambayo mwanadamu amewahi kuona. Akiwa peke yake juu ya Mlima Sinai, Musa alitoa ombi lisilo la kawaida ambalo lilikubaliwa. Aliruhusiwa kuona jambo ambalo hakuna mwanadamu mwingine yeyote aliwahi kuona, yaani, utukufu wa Yehova. Ni kweli kwamba Musa hakumwona Yehova moja kwa moja. Sura ya Mungu ni yenye utukufu mwingi sana hivi kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumwona na kuendelea kuishi. Lakini Yehova aliweka “mkono” wake juu ya Musa kama kisitiri cha kumlinda mpaka Alipopita, huku akitumia malaika. Kisha Yehova akamruhusu Musa kuona mwangaza uliobaki baada ya wonyesho huo wa utukufu Wake. Pia, Yehova alizungumza na Musa kupitia malaika. Biblia inaeleza kilichotukia baadaye inaposema: “Sasa ikawa kwamba Musa alipoteremka kutoka katika Mlima Sinai, . . . ngozi ya uso wake ilikuwa ikitoa miale kwa sababu alikuwa amesema [na Yehova].”—Kutoka 33:18–34:7, 29.
2. Mtume Paulo aliandika nini kuhusu utukufu ambao Wakristo hutoa mrudisho wake?
2 Hebu wazia ukiwa juu ya mlima huo pamoja na Musa. Inaweza kusisimua kama nini kuona utukufu wenye kustaajabisha wa Mweza-Yote na kusikiliza maneno yake! Linaweza kuwa pendeleo kubwa kama nini kuteremka Mlima Sinai pamoja na Musa, mpatanishi wa agano la Sheria! Lakini, je, ulijua kwamba kwa njia fulani Wakristo wa kweli hutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko Musa? Wazo hilo lenye kuamsha fikira linazungumziwa katika barua fulani iliyoandikwa na mtume Paulo. Aliandika kwamba Wakristo watiwa-mafuta ‘hutoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova.’ (2 Wakorintho 3:7, 8, 18) Kwa njia fulani, Wakristo walio na tumaini la kuishi duniani hutoa pia mrudisho wa utukufu wa Mungu.
Jinsi Wakristo Wanavyotoa Mrudisho wa Utukufu wa Mungu
3. Ni kwa njia gani tumejua mambo fulani kumhusu Yehova ambayo Musa hakuyajua?
3 Tunawezaje kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu? Hatujamwona wala kumsikia Yehova kwa njia ambayo Musa alimwona na kumsikia. Hata hivyo, tumejua mambo fulani kumhusu Yehova ambayo Musa hakuyajua. Yesu alikuja akiwa Masihi miaka 1,500 hivi baada ya Musa kufa. Hivyo, Musa hangeweza kujua jinsi ambavyo Sheria ingetimia kuhusiana na Yesu, ambaye alikufa ili kuwakomboa wanadamu kutokana na utawala mkatili wa dhambi na kifo. (Waroma 5:20, 21; Wagalatia 3:19) Isitoshe, Musa alijua kwa kiasi fulani tu kusudi tukufu la Yehova, ambalo linahusiana sana na Ufalme wa Kimasihi, na Paradiso ya kidunia itakayoletwa na Ufalme huo. Hivyo, tunaona utukufu wa Yehova, si kwa macho yetu halisi, bali kwa macho ya imani inayotegemea mafundisho ya Biblia. Zaidi ya hayo, tumeisikia sauti ya Yehova, si kupitia malaika, bali kupitia Biblia, na hasa kupitia vitabu vya Injili ambavyo vinaeleza kwa njia bora sana mafundisho na huduma ya Yesu.
4. (a) Wakristo watiwa-mafuta hutoaje mrudisho wa utukufu wa Mungu? (b) Ni kwa njia zipi wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu?
4 Ingawa Wakristo hawatoi mrudisho wa utukufu wa Mungu kupitia miale inayong’aa usoni, nyuso zao hung’aa kwa kiasi fulani wanapowaeleza wengine kuhusu utu mtukufu wa Yehova na makusudi yake matukufu. Kuhusu siku zetu, nabii Isaya alitabiri kwamba watu wa Mungu “hakika watatangaza juu ya utukufu [wa Yehova] kati ya mataifa.” (Isaya 66:19) Isitoshe, kwenye 2 Wakorintho 4:1, 2, tunasoma hivi: “Kwa kuwa sisi tuna huduma hii . . . tumeyakataa mambo ya kichinichini ambayo ni ya kuonea aibu, si kutembea kwa ujanja, wala kulichanganya na kitu neno la Mungu, bali kwa kufanya kweli iwe wazi tukijipendekeza kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.” Paulo alikuwa akizungumza hasa kuhusu Wakristo watiwa-mafuta, ambao ni “wahudumu wa agano jipya.” (2 Wakorintho 3:6) Lakini huduma yao imewachochea watu wengi sana ambao wamepata tumaini la kuishi milele duniani. Huduma ya vikundi hivyo viwili inatia ndani kutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova kupitia mafundisho yao na pia kupitia matendo yao. Tuna daraka na pendeleo la kutoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Mungu Aliye Juu Zaidi!
5. Ufanisi wetu wa kiroho unathibitisha nini?
5 Leo, kama vile Yesu alivyotabiri, habari njema tukufu za Ufalme wa Mungu zinahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Watu wa mataifa yote, makabila, vikundi vya watu, na lugha wamekubali kwa uchangamfu habari njema hizo na wamebadili maisha yao ili wafanye mapenzi ya Mungu. (Waroma 12:2; Ufunuo 7:9) Kama vile Wakristo wa karne ya kwanza, hawawezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo wameyaona na kuyasikia. (Matendo 4:20) Leo, watu zaidi ya milioni sita wanatoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, na hiyo ni idadi kubwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Je, wewe ni mmoja wao? Ufanisi wa kiroho wa watu wa Mungu unatoa uthibitisho wenye nguvu kwamba Yehova anawabariki na kuwalinda. Tunatambua waziwazi kwamba tuna roho ya Yehova tunapoona majeshi yenye nguvu yaliyosimama dhidi yetu. Acheni sasa tuone sababu zinazounga mkono jambo hilo.
Watu wa Mungu Hawatanyamazishwa
6. Kwa nini unahitaji imani na ujasiri ili kumuunga mkono Yehova?
6 Tuseme umeombwa ufike mahakamani ili utoe ushahidi dhidi ya mhalifu sugu. Unajua kwamba mhalifu huyo ana genge lenye nguvu na kwamba atajitahidi juu chini ili akuzuie usifichue habari zake. Ili utoe ushahidi dhidi ya mhalifu huyo, itakubidi uwe jasiri na uwe na uhakika wa kwamba wenye mamlaka watakulinda. Sisi pia tunakabili hali kama hiyo. Tunapotoa ushahidi kumhusu Yehova na makusudi yake, tunatoa ushahidi dhidi ya Shetani Ibilisi na kumfichua kuwa muuaji na mwongo anayeipotosha dunia yote inayokaliwa. (Yohana 8:44; Ufunuo 12:9) Unahitaji imani na ujasiri ili kumuunga mkono Yehova na kumpinga Ibilisi.
7. Shetani ana uwezo mwingi kadiri gani, naye hujaribu kufanya nini?
7 Bila shaka, Aliye Mkuu Zaidi ni Yehova. Ana nguvu nyingi sana kuliko Shetani. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaweza na pia yuko tayari kutulinda tunapomtumikia kwa ushikamanifu. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Hata hivyo, Shetani ndiye mtawala wa roho waovu na wa ulimwengu wa wanadamu waliojitenga na Mungu. (Mathayo 12:24, 26; Yohana 14:30) Kwa kuwa ametupwa duniani akiwa na “hasira kali,” Shetani huwapinga vikali watumishi wa Yehova, naye hutumia ulimwengu ulio chini ya uongozi wake kujaribu kuwanyamazisha wale wote wanaohubiri habari njema. (Ufunuo 12:7-9, 12, 17) Anafanyaje hivyo? Anatumia angalau njia tatu.
8, 9. Shetani hutumiaje upendo wa vitu vya kimwili, na kwa nini tunapaswa kuchagua kwa uangalifu watu wa kushirikiana nao?
8 Njia moja ambayo Shetani hutumia ili kutukengeusha ni mahangaiko ya maisha. Watu katika hizi siku za mwisho wanapenda pesa, wanajipenda wenyewe, na wanapenda raha. Hawampendi Mungu. (2 Timotheo 3:1-4) Kwa kuwa wanahangaikia tu shughuli zao za maisha, watu wengi ‘hawajali’ juu ya habari njema tunazowapelekea. Hawataki kujifunza kweli za Biblia. (Mathayo 24:37-39) Mtazamo kama huo unaweza kutuathiri na kutulegeza kiroho. Tukisitawisha upendo kwa ajili ya mali na raha za maisha, upendo wetu kwa Mungu utapoa.—Mathayo 24:12.
9 Hiyo ndiyo sababu Wakristo huchagua kwa uangalifu watu wa kushirikiana nao. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Acheni ‘tutembee’ na wale wanaotoa mrudisho wa utukufu wa Mungu. Inafurahisha sana kufanya hivyo! Tunapokusanyika pamoja na ndugu na dada zetu wa kiroho kwenye mikutano yetu na pindi nyinginezo, tunatiwa moyo na upendo wao, imani yao, shangwe yao, na hekima yao. Ushirika huo unaofaa huimarisha azimio letu la kuendelea kutimiza huduma yetu.
10. Shetani ametumiaje dhihaka juu ya wale wanaotoa mrudisho wa utukufu wa Mungu?
10 Njia ya pili ambayo Shetani hutumia kujaribu kuwazuia Wakristo wote wasitoe mrudisho wa utukufu wa Mungu ni dhihaka. Mbinu hiyo haitushangazi. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu Kristo alidhihakiwa—alichekwa kwa dharau, alitendewa kwa dharau, na hata akatemewa mate. (Marko 5:40; Luka 16:14; 18:32) Wakristo wa mapema walidhihakiwa pia. (Matendo 2:13; 17:32) Watumishi wa Yehova wa leo hukabili hali kama hiyo. Kulingana na mtume Petro, wangeitwa “manabii wa uwongo.” Petro alitabiri hivi: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki na dhihaka zao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, . . . mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.’” (2 Petro 3:3, 4) Watu wa Mungu hudhihakiwa kwamba wamezubaa. Viwango vya maadili vya Biblia huonwa kuwa vimepitwa na wakati. Wengi huona ujumbe tunaohubiri kuwa upumbavu. (1 Wakorintho 1:18, 19) Kwa kuwa sisi ni Wakristo, huenda tukadhihakiwa shuleni, kazini, na nyakati nyingine hata katika familia. Lakini sisi hatuvunjiki moyo, bali tunaendelea kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu kwa kuhubiri, na kama Yesu tunajua kwamba Neno la Mungu ndiyo kweli.—Yohana 17:17.
11. Shetani ametumiaje mateso ili kujaribu kuwanyamazisha Wakristo?
11 Njia ya tatu ambayo Ibilisi hutumia ili kujaribu kutunyamazisha ni upinzani au mateso. Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: ‘Watu watawatia ninyi katika dhiki na kuwaua ninyi, nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.’ (Mathayo 24:9) Naam, sisi Mashahidi wa Yehova tumekabili mateso makali katika maeneo mengi ya dunia. Tunajua kwamba zamani za kale Yehova alitabiri kutakuwa na chuki, au uadui, kati ya wale wanaomtumikia Mungu na wale wanaomtumikia Shetani Ibilisi. (Mwanzo 3:15) Pia tunajua kwamba tukidumisha utimilifu tunapokabili majaribu, tunaunga mkono enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote mzima. Kujua hilo kunaweza kutuimarisha hata katika hali ngumu sana. Tukiendelea kuazimia kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu, hakuna mateso yoyote yatakayotunyamazisha kabisa.
12. Kwa nini tunapaswa kushangilia tunapodumu waaminifu licha ya upinzani wa Shetani?
12 Je, wewe hupinga vishawishi vya ulimwengu na kuwa mwaminifu licha ya dhihaka na upinzani? Ikiwa ndivyo, basi una sababu ya kushangilia. Yesu aliwahakikishia hivi wale ambao wangemfuata: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mathayo 5:11, 12) Uvumilivu wako unaonyesha kwamba una roho takatifu ya Yehova yenye nguvu, na inakuimarisha kutoa mrudisho wa utukufu wake.—2 Wakorintho 12:9.
Yehova Anatusaidia Kuvumilia
13. Ni sababu gani kuu tuliyo nayo ya kuvumilia katika huduma ya Kikristo?
13 Sababu kuu inayotufanya tuvumilie katika huduma ni kwamba tunampenda Yehova na tunafurahia kutoa mrudisho wa utukufu wake. Wanadamu huiga watu ambao wanapenda na kuheshimu, na Yehova Mungu ndiye anayestahili zaidi kuigwa. Kwa sababu ya upendo wake mwingi, alimtuma Mwana wake duniani ili kutoa ushahidi kuhusu kweli na kuwakomboa wanadamu watiifu. (Yohana 3:16; 18:37) Kama Mungu, tunatamani watu wa namna zote wafikie toba na wokovu; na ndiyo sababu tunawahubiria. (2 Petro 3:9) Tamaa hiyo, pamoja na azimio letu la kumwiga Mungu, hutuchochea kuendelea kutoa mrudisho wa utukufu wake kupitia huduma yetu.
14. Yehova hutuimarishaje kuvumilia katika huduma yetu?
14 Hata hivyo, nguvu zetu za kuvumilia katika huduma ya Kikristo hutoka kwa Yehova. Yeye hutusaidia na kutuimarisha kupitia roho yake, tengenezo lake, na Neno lake, Biblia. Yehova ‘huwatolea uvumilivu’ wale wanaotaka kutoa mrudisho wa utukufu wake. Yeye hujibu sala zetu na kutupa hekima ili tukabiliane na majaribu. (Waroma 15:5; Yakobo 1:5) Isitoshe, Yehova haruhusu tupatwe na jaribu lolote ambalo hatuwezi kulihimili. Tukimtegemea Yehova, atafanyiza njia ili tuendelee kutoa mrudisho wa utukufu wake.—1 Wakorintho 10:13.
15. Ni nini kinachotusaidia kuvumilia?
15 Uvumilivu katika huduma yetu huonyesha kwamba tuna roho ya Mungu. Kwa mfano: Tuseme mtu fulani anakuomba uende nyumba kwa nyumba ukiwagawia watu mkate bila malipo. Anakuomba ufanye kazi hiyo kwa wakati wako na ulipie gharama zako. Isitoshe, muda si muda unagundua kwamba ni watu wachache sana wanaotaka mkate wako; wengine hata wanapinga jitihada zako za kuugawa. Je, unaweza kuendelea kufanya kazi hiyo mwezi baada ya mwezi, miaka nenda miaka rudi? Huenda usifanye hivyo. Hata hivyo, huenda umetumia pesa zako na wakati wako ili kuhubiri habari njema kwa bidii kwa miaka mingi, au hata kwa makumi ya miaka. Kwa nini? Hapana shaka ni kwa sababu unampenda Yehova na kupitia roho yake amebariki jitihada zako kwa kukusaidia kuvumilia!
Kazi Itakayokumbukwa
16. Uvumilivu katika huduma utakuwa na matokeo gani kwetu na kwa wale wanaotusikiliza?
16 Huduma ya agano jipya ni zawadi isiyo na kifani. (2 Wakorintho 4:7) Vivyo hivyo, huduma ya Kikristo inayofanywa na kondoo wengine duniani kote ni hazina. Kama vile Paulo alivyomwandikia Timotheo, unapoendelea kuvumilia katika huduma yako, unaweza ‘kujiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.’ (1 Timotheo 4:16) Hebu fikiria maana ya maneno hayo. Habari njema unayohubiri huwapa wengine nafasi ya kuishi milele. Unaweza kuwa na urafiki wa karibu pamoja na wale unaowasaidia kiroho. Hebu wazia jinsi utakavyofurahia kuishi milele katika Paradiso pamoja na wale uliowasaidia kujifunza juu ya Mungu! Bila shaka, hawatasahau jitihada ulizofanya kuwasaidia. Naam, utapata uradhi mwingi sana!
17. Kwa nini kipindi chetu ni cha pekee sana katika historia ya wanadamu?
17 Unaishi katika kipindi cha pekee sana katika historia ya wanadamu. Habari njema haitahubiriwa tena kamwe katika ulimwengu wa wanadamu waliojitenga na Mungu. Noa aliishi katika ulimwengu kama huo, naye aliuona ukipitilia mbali. Hapana shaka alishangilia kujua kwamba amefanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu kwa kujenga safina iliyomwezesha yeye na familia yake kuokolewa! (Waebrania 11:7) Wewe pia unaweza kushangilia kama yeye. Hebu wazia jinsi utakavyohisi katika ulimwengu mpya utakapokumbuka utendaji wako katika hizi siku za mwisho, huku ukijua kwamba ulifanya yote unayoweza kuendeleza mambo ya Ufalme.
18. Yehova anawatiaje moyo watumishi wake, naye anawahakikishia nini?
18 Basi, acheni tuendelee kutoa mrudisho wa utukufu wa Mungu. Tukifanya hivyo, tutakumbuka jambo hilo milele. Yehova pia hukumbuka kazi zetu. Biblia inatutia moyo hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu. Lakini tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho, ili msiwe goigoi, bali muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Waebrania 6:10-12.
-
-
Wakristo Hutoa Mrudisho wa Utukufu wa YehovaMnara wa Mlinzi—2005 | Agosti 15
-
-
Wakristo Hutoa Mrudisho wa Utukufu wa Yehova
“Yenye furaha ni macho yenu kwa sababu hayo yanaona, na masikio yenu kwa sababu hayo yanasikia.”—MATHAYO 13:16.
1. Ni swali gani ambalo linazuka kuhusiana na jinsi Waisraeli walivyotenda walipomwona Musa kwenye Mlima Sinai?
WAISRAELI waliokuwa wamekusanyika kwenye Mlima Sinai walikuwa na sababu nzuri za kumkaribia Yehova. Alikuwa amewakomboa kutoka Misri kwa mkono wenye nguvu. Alihangaikia mahitaji yao kwa kuwaandalia chakula na maji nyikani. Kisha akawapa ushindi juu ya jeshi la Waamaleki lililowashambulia. (Kutoka 14:26-31; 16:2–17:13) Wakiwa wamepiga kambi nyikani mbele ya Mlima Sinai, watu hao waliogopeshwa sana na mingurumo na radi hivi kwamba wakatetemeka. Baadaye, walimwona Musa akishuka kutoka kwenye Mlima Sinai, huku uso wake ukitoa mrudisho wa utukufu wa Yehova. Lakini, badala ya kustaajabu na kuonyesha uthamini, walirudi nyuma. ‘Waliogopa kumkaribia Musa.’ (Kutoka 19:10-19; 34:30) Kwa nini waliogopa kuona mrudisho wa utukufu wa Yehova, yule aliyekuwa amewafanyia mambo mengi sana?
2. Kwa nini huenda Waisraeli waliogopa kuona utukufu wa Mungu ambao Musa alitoa mrudisho wake?
2 Labda woga wa Waisraeli wakati huo ulihusiana sana na mambo yaliyokuwa yametukia awali. Yehova alikuwa amewaadhibu walipomwasi kimakusudi kwa kutengeneza ndama ya dhahabu. (Kutoka 32:4, 35) Je, walijifunza kutokana na nidhamu ya Yehova na kuithamini? La, wengi wao hawakufanya hivyo. Alipokaribia kufa, Musa alizungumzia tena kisa cha ndama ya dhahabu na pindi nyingine ambazo Waisraeli hawakutii. Aliwaambia watu hivi: ‘Mliasi agizo la Yehova Mungu wenu, nanyi hamkumwamini wala hamkuisikiliza sauti yake. Mmejionyesha kuwa wenye tabia ya kumwasi Yehova tangu siku niliyowajua ninyi.’—Kumbukumbu la Torati 9:15-24.
3. Musa alitumiaje utaji?
3 Fikiria jinsi Musa alivyotenda alipoona woga wa Waisraeli. Simulizi hilo linasema: “Musa alipomaliza kusema nao, alikuwa akiweka utaji juu ya uso wake. Lakini Musa alipokuwa akiingia ndani [ya ile maskani] mbele za Yehova kusema naye, alikuwa akiutoa utaji mpaka wakati wa kutoka kwake nje. Naye akatoka nje na kusema na wana wa Israeli mambo aliyokuwa akiamriwa. Nao wana wa Israeli wakauona uso wa Musa, kwamba ngozi ya uso wa Musa ilitoa miale; naye Musa akaurudisha utaji juu ya uso wake mpaka alipoingia ndani kusema [na Yehova].” (Kutoka 34:33-35) Kwa nini nyakati nyingine Musa aliufunika uso wake kwa utaji? Tunajifunza nini kutokana na hilo? Majibu ya maswali hayo yanaweza kutusaidia kuchunguza uhusiano wetu pamoja na Yehova.
Walikosa Kutumia Nafasi Walizopata
4. Mtume Paulo alifunua nini kuhusu sababu ya Musa ya kujifunika utaji?
4 Mtume Paulo alieleza kwamba sababu ya Musa ya kujifunika utaji ilihusiana na hali ya Waisraeli ya akilini na ya moyoni. Paulo aliandika hivi: “Wana wa Israeli hawakuweza kuutazama uso wa Musa kwa sababu ya utukufu wa uso wake . . . Nguvu zao za akili zilitiwa uzito.” (2 Wakorintho 3:7, 14) Inasikitisha sana! Waisraeli walikuwa watu wa Yehova waliochaguliwa, naye aliwataka wamkaribie. (Kutoka 19:4-6) Hata hivyo, hawakutaka kuutazama sana mrudisho wa utukufu wa Mungu. Badala ya kuelekeza mioyo yao na akili zao kwa Yehova kwa kujitoa kwa upendo, ni kana kwamba walikuwa wamempa kisogo.
5, 6. (a) Kulikuwa na ulinganifu gani kati ya Waisraeli wa karne ya kwanza na wale wa wakati wa Musa? (b) Kulikuwa na tofauti gani kati ya wale waliomsikiliza Yesu na wale ambao hawakumsikiliza?
5 Hali kama hiyo ilitokea katika karne ya kwanza W.K. Kufikia wakati ambapo Paulo aligeuka na kuwa Mkristo, agano jipya lilikuwa limechukua mahali pa agano la Sheria. Yesu Kristo, Musa Mkuu Zaidi, ndiye mpatanishi wa agano jipya. Kwa maneno na kwa matendo, Yesu alitoa kwa ukamili mrudisho wa utukufu wa Yehova. Paulo aliandika hivi kumhusu Yesu aliyefufuliwa: “Yeye ndiye mng’ao wa utukufu [wa Mungu] na mwakilisho sawasawa wa utu wake wenyewe.” (Waebrania 1:3) Wayahudi walikuwa na nafasi bora sana! Wangeweza kusikiliza maneno ya uzima wa milele kutoka kwa Mwana wa Mungu mwenyewe! Inasikitisha kwamba watu wengi ambao Yesu aliwahubiria hawakumsikiliza. Yesu alizungumza juu yao aliponukuu unabii huu wa Yehova kupitia Isaya: “Moyo wa watu hawa umekuwa mgumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia, nao wamefunga macho yao; ili wasione kamwe kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kuelewa maana kwa mioyo yao na kugeuka, nami niwaponye.”—Mathayo 13:15; Isaya 6:9, 10.
6 Kulikuwa na tofauti kubwa kati ya Wayahudi na wanafunzi wa Yesu, ambao Yesu alisema hivi juu yao: “Yenye furaha ni macho yenu kwa sababu hayo yanaona, na masikio yenu kwa sababu hayo yanasikia.” (Mathayo 13:16) Wakristo wa kweli wanatamani kumjua na kumtumikia Yehova. Wanafurahia kufanya mapenzi yake ambayo yanafunuliwa katika Biblia. Kwa hiyo, Wakristo watiwa-mafuta hutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova katika huduma yao ya agano jipya, na wale wa kondoo wengine wanafanya hivyo pia.—2 Wakorintho 3:6, 18.
Kwa Nini Habari Njema Imefunikwa Utaji?
7. Kwa nini haishangazi kwamba watu wengi hukataa habari njema?
7 Kama tulivyoona, katika siku za Yesu na katika siku za Musa, Waisraeli wengi walikataa kutumia nafasi bora waliyokuwa nayo. Hali iko hivyo leo. Watu wengi wanakataa habari njema tunayohubiri. Hilo halitushangazi. Paulo aliandika hivi: “Basi, ikiwa kwa kweli habari njema tunayotangaza imefunikwa utaji, imefunikwa utaji katikati ya wale wanaoangamia, ambao katikati yao mungu wa mfumo huu wa mambo amezipofusha akili za wasioamini.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Zaidi ya jitihada za Shetani za kujaribu kuficha habari njema, watu wengi pia hufunika nyuso zao kwa utaji kwa sababu hawataki kuona.
8. Ni kwa njia gani watu wengi wanapofushwa kwa sababu ya kutojua, nasi tunawezaje kuepuka kuathiriwa kwa njia hiyohiyo?
8 Macho ya mfano ya watu wengi yamepofushwa kwa sababu ya kutojua. Biblia inasema kwamba mataifa yako ‘katika giza kiakili, na yametenganishwa mbali na uzima ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutojua ambako kumo ndani yao.’ (Waefeso 4:18) Kabla ya kuwa Mkristo, Paulo, ambaye aliifahamu sana Sheria, alikuwa amepofushwa sana kwa sababu ya kutojua hivi kwamba alilitesa kutaniko la Mungu. (1 Wakorintho 15:9) Hata hivyo, Yehova alimfunulia ile kweli. Paulo anaeleza hivi: “Sababu iliyofanya nionyeshwe rehema ilikuwa kwamba kupitia mimi nikiwa ndiye wa kwanza kabisa Kristo Yesu aonyeshe ustahimilivu wake wote kuwa mfano wa wale watakaokuwa na imani yao kwake kwa ajili ya uzima wa milele.” (1 Timotheo 1:16) Kama vile Paulo, watu wengi ambao zamani waliipinga kweli ya Mungu sasa wanamtumikia Yehova. Hiyo ni sababu nzuri ya kuendelea kuwahubiria hata wale wanaotupinga. Wakati huohuo, tukijifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kulielewa, tutalindwa tusitende kwa kutojua na hivyo kumkasirisha Yehova.
9, 10. (a) Wayahudi wa karne ya kwanza walionyeshaje kwamba walishikilia sana maoni yao na kwamba hawakutaka kufundishwa? (b) Je, hali kama hiyo iko katika dini zinazodai kuwa za Kikristo leo? Eleza.
9 Watu wengi hawaelewi mambo ya kiroho kwa sababu hawataki kufundishwa na wanashikilia sana maoni yao. Wayahudi wengi walimkataa Yesu na mafundisho yake kwa sababu walishikilia kwa ushupavu Sheria ya Musa. Ni kweli kwamba kuna wale waliomkubali. Kwa mfano, baada ya Yesu kufufuliwa, ‘umati mkubwa wa makuhani ulianza kuitii imani.’ (Matendo 6:7) Hata hivyo, Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi wengi: “Mpaka leo wakati wowote maandishi ya Musa yanaposomwa, utaji hukaa juu ya mioyo yao.” (2 Wakorintho 3:15) Yaonekana Paulo alijua kile ambacho Yesu alikuwa amewaambia viongozi wa dini Wayahudi: “Ninyi mnayachunguza Maandiko, kwa sababu mnafikiri kwamba kwa njia yake mtakuwa na uzima wa milele; na hayo yenyewe ndiyo yanayotoa ushahidi juu yangu.” (Yohana 5:39) Maandiko ambayo walikuwa wakiyachunguza kwa makini yalipaswa kuwasaidia kuelewa kwamba Yesu ndiye Masihi. Hata hivyo, Wayahudi walikuwa na maoni yao wenyewe, na hata hawakutaka kusadikishwa na Mwana wa Mungu aliyefanya miujiza.
10 Leo, wengi walio katika dini zinazodai kuwa za Kikristo wako katika hali hiyohiyo. Sawa na Wayahudi wa karne ya kwanza, “wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Ingawa wengine wao hujifunza Biblia, hawataki kuamini yale inayosema. Hawataki kukubali kwamba Yehova huwafundisha watu wake kupitia jamii yake ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara ya Wakristo watiwa-mafuta. (Mathayo 24:45) Hata hivyo, sisi tunaelewa kwamba Yehova anawafundisha watu wake na kwamba sikuzote amefunua kweli yake hatua kwa hatua. (Methali 4:18) Tunapokubali kufundishwa na Yehova tunabarikiwa kujua mapenzi yake na kusudi lake.
11. Ukweli umefichwaje kwa sababu ya watu kuamini tu mambo ambayo wanapenda?
11 Wengine wamepofushwa kwa sababu wanataka tu kuamini mambo wanayopenda. Ilitabiriwa kwamba watu fulani watawadhihaki watu wa Mungu na kuudhihaki ujumbe ambao wanatangaza kuhusu kuwapo kwa Yesu. Mtume Petro aliandika hivi: “Kulingana na kupenda kwao, wao hawalioni jambo hili,” kwamba Mungu alileta gharika juu ya ulimwengu wa siku za Noa. (2 Petro 3:3-6) Vivyo hivyo, watu wengi wanaodai kuwa Wakristo hukubali kwa utayari kwamba Yehova huonyesha rehema, fadhili, na msamaha; lakini wanapuuza au kukataa kwamba yeye huwaadhibu wakosaji. (Kutoka 34:6, 7) Wakristo wa kweli hujitahidi kuelewa yale ambayo Biblia hufundisha hasa.
12. Watu wamepofushwaje na mapokeo?
12 Watu wengi wanaoenda kanisani hupofushwa na mapokeo. Yesu aliwaambia hivi viongozi wa dini wa siku zake: “Mmelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu.” (Mathayo 15:6) Baada ya kurudi kutoka utekwani huko Babiloni, Wayahudi walirudisha ibada safi kwa bidii, lakini makuhani wakawa na kiburi na kujiona kuwa waadilifu. Sherehe za kidini zikawa za kidesturi tu, na hazikufanywa kwa njia iliyoonyesha heshima ya kweli kwa Mungu. (Malaki 1:6-8) Kufikia wakati wa Yesu, waandishi na Mafarisayo walikuwa wameongeza mapokeo mengi sana katika Sheria ya Musa. Yesu alisema wazi kwamba watu hao ni wanafiki kwa sababu hawakufuata tena kanuni adilifu zilizoitegemeza Sheria. (Mathayo 23:23, 24) Ni lazima Wakristo wa kweli wawe waangalifu wasije wakakubali mapokeo ya kidini yaliyotungwa na wanadamu yawakengeushe kutoka katika ibada safi.
‘Kumwona Yeye Asiyeonekana’
13. Musa aliona utukufu wa Mungu kwa kadiri fulani kupitia njia gani mbili?
13 Akiwa mlimani, Musa aliomba aone utukufu wa Mungu, naye akaonyeshwa mwangaza uliobaki wa utukufu wa Yehova. Alipoingia katika ile maskani, hakujifunika utaji. Musa alikuwa na imani yenye nguvu na alitamani kufanya mapenzi ya Mungu. Ingawa alibarikiwa kuona utukufu wa Yehova kwa kadiri fulani katika maono, ni kana kwamba tayari alikuwa amemwona Mungu kwa macho ya imani. Biblia inasema kwamba Musa “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27; Kutoka 34:5-7) Musa alitoa mrudisho wa utukufu wa Mungu si tu kupitia miale iliyotoka usoni pake kwa muda fulani, bali pia kupitia jitihada zake za kuwasaidia Waisraeli kumjua na kumtumikia Yehova.
14. Yesu aliuonaje utukufu wa Mungu, naye alifurahia nini?
14 Akiwa huko mbinguni, Yesu aliuona utukufu wa Mungu moja kwa moja kwa miaka mingi sana, hata kabla ya ulimwengu kuumbwa. (Methali 8:22, 30) Katika kipindi hicho chote, uhusiano wenye upendo mwingi sana ulisitawi. Yehova Mungu alionyesha upendo mwororo zaidi kwa mwana huyo mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote. Yesu pia alionyesha upendo mwingi sana kwa Mungu, ambaye alimpa uhai. (Yohana 14:31; 17:24) Baba na Mwana walionyeshana upendo mkamilifu. Kama vile Musa, Yesu alifurahia kutoa mrudisho wa utukufu wa Yehova kupitia mambo aliyofundisha.
15. Ni katika njia gani Wakristo huukazia uangalifu utukufu wa Mungu?
15 Kama vile Musa na Yesu, Mashahidi wa Mungu waliopo duniani leo wanatamani sana kuukazia uangalifu utukufu wa Yehova. Wao hawajakataa habari njema zilizo tukufu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kunapokuwa na tendo la kugeuka kumwelekea Yehova [ili kufanya mapenzi yake], utaji huondolewa mbali.” (2 Wakorintho 3:16) Tunajifunza Maandiko kwa sababu tunataka kufanya mapenzi ya Mungu. Tunavutiwa na utukufu unaoangazwa na uso wa Mwana wa Yehova, Yesu Kristo, ambaye ni Mfalme mtiwa-mafuta, nasi tunaiga mfano wake. Kama vile Musa na Yesu, tumekabidhiwa huduma ya kuwafundisha wengine kuhusu Mungu mtukufu tunayemwabudu.
16. Kwa nini ni pendeleo kubwa kuijua kweli?
16 Yesu alisali hivi: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, . . . kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa watoto.” (Mathayo 11:25) Yehova huwapa wanyoofu na watu walio wanyenyekevu moyoni uelewaji wa makusudi yake na utu wake. (1 Wakorintho 1:26-28) Anatulinda na kutufundisha jinsi tunavyoweza kufaidika kikamili maishani. Acheni tutumie vizuri kila nafasi tunayopata ya kumkaribia Yehova kwa kuthamini maandalizi yake mengi yanayotusaidia kumjua vizuri zaidi.
17. Tunapataje kujua sifa za Yehova kwa kadiri kubwa zaidi?
17 Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Sisi . . . tunapotoa kama vioo mrudisho wa utukufu wa Yehova tukiwa na nyuso zisizo na utaji, tunageuzwa na kuwa katika mfano uleule kutoka utukufu mpaka utukufu.” (2 Wakorintho 3:18) Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani, kadiri tunavyomjua Yehova, yaani, kujua sifa zake na utu wake uliofunuliwa katika Biblia, ndivyo tunavyozidi kuwa kama yeye. Tukitafakari na kuthamini maisha, huduma, na mafundisho ya Yesu Kristo, tutaiga sifa za Yehova kwa kadiri kubwa zaidi. Tunashangilia kama nini kujua kwamba tunamletea sifa Mungu wetu, ambaye tunajitahidi kutoa mrudisho wa utukufu wake!
-