Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • (1 Tim. 3:4, 12) Akina dada pia wana jukumu la kudumisha usafi, hasa ndani ya nyumba. (Tito 2:4, 5) Watoto waliozoezwa vizuri hutimiza jukumu lao kwa kuwa wasafi na kudumisha mpangilio mzuri na usafi wa vyumba vyao. Hivyo, familia hushirikiana kusitawisha utaratibu wa usafi ambao tutafuata katika ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu.

      11 Watumishi wengi wa Yehova leo hutumia magari kwenda kwenye mikutano. Katika maeneo fulani, inalazimu kuwa na gari katika huduma. Gari hilo linapaswa kuwa safi na kudumishwa vizuri. Nyumba na magari yetu yanapaswa kuonyesha kwamba sisi ni watu wa Yehova walio safi na watakatifu. Kanuni hiyo inahusu pia mikoba na Biblia tunazotumia katika utumishi wa shambani.

      12 Mavazi na mapambo yetu yanapaswa kupatana na kanuni za Mungu. Hatuwezi kwenda mbele ya watu mashuhuri tukiwa tumevaa isivyofaa au ovyoovyo. Je, hatupaswi kuvaa vizuri hata zaidi tunapomwakilisha Yehova katika utumishi wa shambani au jukwaani? Mavazi na mapambo yetu yanaweza kuathiri jinsi wengine wanavyoiona ibada ya Yehova. Bila shaka haingefaa kuvaa kwa njia isiyo na kiasi au bila kuwajali wengine. (Mika 6:8; 1 Kor. 10:31-33; 1 Tim. 2:9, 10) Kwa hiyo, tunapojitayarisha kwenda utumishi wa shambani, mikutanoni au makusanyikoni, tunapaswa kukumbuka yale ambayo Biblia husema kuhusu usafi wa kimwili, mavazi na mwonekano wetu. Sikuzote tunataka kumheshimu na kumtukuza Yehova.

      Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna wajibu wa kusema na kufanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova

      13 Tunapaswa kufuata kanuni hiyo pia tunapotembelea makao makuu au ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Kumbuka kwamba jina Betheli linamaanisha “Nyumba ya Mungu.” Kwa hiyo, tunapaswa kuvaa, kujipamba, na kujiendesha kama tunavyofanya tunapohudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme.

      14 Hata tunapokuwa katika tafrija na burudani, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mavazi na mapambo yetu. Tunaweza kujiuliza, ‘je, mavazi na mapambo yangu yatanifanya nione aibu kutoa ushahidi isivyo rasmi?’

      TAFRIJA NA BURUDANI ZINAZOFAA

      15 Tunahitaji kupumzika na kujiburudisha kwa ajili afya. Wakati fulani Yesu aliwaambia wanafunzi wake waende naye mahali patulivu ili ‘wapumzike kidogo.’ (Marko 6:31) Vipindi vya mapumziko, tafrija au burudani inayofaa zinaweza kustarehesha. Vinaweza kutupa nguvu za kuendelea na shughuli zetu za kawaida.

      16 Kwa sababu kuna aina nyingi za tafrija, Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu na kutumia hekima ya Mungu katika kila jambo wanalofanya. Ingawa tafrija ni muhimu, haipaswi kuwa jambo kuu maishani. Tunaonywa kwamba katika “siku za mwisho,” watu ‘watapenda raha badala ya kumpenda Mungu.’ (2 Tim. 3:1, 4) Tafrija na burudani nyingi leo haziwafai wale wanaotamani kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova.

      17 Wakristo wa mapema walikataa mtazamo usiofaa wa ulimwengu uliofuatia sana raha. Wakati wa michezo ya Waroma, watazamaji walitumbuizwa kwa kuwatazama wengine wakiteseka. Watu wengi waliburudishwa kwa kutazama jeuri, umwagaji wa damu, na upotovu wa maadili kingono, lakini Wakristo wa mapema hawakujihusisha na mambo hayo. Leo, burudani nyingi ulimwenguni zina mambo kama hayo ambayo yamekusudiwa kutosheleza tamaa zisizofaa za wanadamu. Tunahitaji ‘kuendelea kuangalia sana’ jinsi tunavyotembea, tukiepuka burudani zinazopotosha maadili. (Efe. 5:15, 16; Zab. 11:5) Hata ingawa huenda burudani isiwe mbaya, mara nyingi kuwepo kwa watu wa ulimwengu na ushawishi wao unaweza kutuathiri.—1 Pet. 4:1-4.

      18 Kuna tafrija na burudani zinazofaa ambazo Wakristo wanaweza kufurahia. Wengi wamefaidika kwa kufuata ushauri wa Maandiko na mapendekezo mazuri yanayopatikana katika machapisho yetu.

      19 Nyakati nyingine, huenda familia kadhaa zikaalikwa katika nyumba fulani kufurahia ushirika wa Kikristo. Au ndugu na dada wanaweza kualikwa harusini au kwenye matukio mengine kama hayo. (Yoh. 2:2) Wale wanaoalika wageni wanapaswa kutambua kuwa watawajibika kwa mambo yote yatakayotokea. Kwa kweli, ni muhimu kuwa waangalifu ikiwa kutakuwa na watu wengi. Hali ya starehe katika vikusanyiko kama hivyo imewafanya wengine wavuke mipaka ya mwenendo unaowafaa Wakristo, na hivyo kula na kunywa kupita kiasi na hata kutumbukia katika dhambi nyingine nzito. Wakristo wenye utambuzi wanaona ni jambo la hekima kuweka idadi hususa ya watu watakaohudhuria na muda wa vikusanyiko hivyo. Ikiwa kutakuwa na pombe, inapaswa kutumiwa kwa kiasi. (Flp. 4:5) Wakristo wakijitahidi kuhakikisha kwamba tafrija zao zinajenga na kuburudisha kiroho, vyakula na vinywaji havitakuwa jambo kuu katika pindi hizo.

      20 Ni vizuri kuwa wakaribishaji wageni. (1 Pet. 4:9) Tunapowaalika Wakristo wengine nyumbani kwetu kwa ajili ya chakula, viburudisho, starehe, na ushirika, tunapaswa kuwakumbuka wale wenye uhitaji. (Luka 14:12-14) Tunapoalikwa, mwenendo wetu unapaswa kupatana na ushauri unaopatikana kwenye Marko 12:31. Sikuzote ni vizuri kuthamini fadhili tunazotendewa na wengine.

      21 Wakristo hufurahia zawadi nyingi kutoka kwa Mungu na wanajua kwamba wanaweza “kula na kunywa na kufurahia kazi [yao] yote ngumu.” (Mhu. 3:12, 13) Tunapofanya “mambo yote kwa utukufu wa Mungu,” wale walioandaa tafrija na vilevile wageni watakumbuka jinsi walivyoburudishwa kiroho.

      KAZI ZA SHULENI

      22 Watoto wa Mashahidi wa Yehova hunufaishwa na elimu ya msingi. Wanapokuwa shuleni, wanajitahidi kujifunza kusoma na kuandika vizuri. Mambo mengine ambayo vijana husoma shuleni yanaweza kuwasaidia wanapojitahidi kufikia malengo yao ya kiroho. Wanapokuwa shuleni, wanajitahidi sana ‘kumkumbuka Muumba wao’ kwa kutanguliza mambo ya kiroho.—Mhu. 12:1.

      23 Ikiwa wewe ni kijana Mkristo uliye shuleni, uwe mwangalifu sana ili usishirikiane isivyo lazima na vijana wa ulimwengu. (2 Tim. 3:1, 2) Kwa kuwa Yehova hukupa ulinzi unaohitaji, una mengi ya kufanya yanayoweza kukusaidia kuepuka vishawishi vya ulimwengu. (Zab. 23:4; 91:1, 2) Hivyo, ili ujilinde, tumia kikamili maandalizi ya Yehova.—Zab. 23:5.

      24 Ili kujitenga na ulimwengu wakiwa wangali shuleni, vijana wengi Mashahidi huamua kutojihusisha katika shughuli za baada ya masomo. Huenda wanafunzi wenzako na walimu wasielewe msimamo wako. Hata hivyo, jambo muhimu ni kumpendeza Mungu. Ili kufanya hivyo, unahitaji kufuata dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia na kuazimia kabisa kutohusika katika mashindano ya kilimwengu au mambo ya kizalendo. (Gal. 5:19, 26) Mkisikiliza ushauri wa Maandiko kutoka kwa wazazi wenu Wakristo, na kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko, ninyi vijana mtashika viwango vya uadilifu vya Yehova.

      KAZI NA WATU TUNAOSHIRIKIANA NAO

      25 Vichwa vya familia wana wajibu wa Kimaandiko wa kuandalia mahitaji watu wa nyumbani mwao. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, wakiwa wahudumu wanatambua kwamba kuutafuta Ufalme ni muhimu zaidi kuliko kazi ya kimwili. (Mt. 6:33; Rom. 11:13) Wanaepuka mahangaiko na mitego ya kufuatilia vitu vya kimwili kwa kumtumikia Mungu kwa bidii na kuridhika na chakula na mavazi.—1 Tim. 6:6-10.

      26 Wakristo wote waliojiweka wakfu wanapaswa kukumbuka kanuni za Maandiko katika kazi zao za kimwili. Tunapaswa kuwa wanyofu tunapotafuta riziki, na hivyo kuepuka mambo yanayovunja sheria za Mungu au sheria za nchi. (Rom. 13:1, 2; 1 Kor. 6:9, 10) Tukumbuke hatari ya kushirikiana na marafiki wabaya. Tukiwa wanajeshi wa Kristo, tunaepuka kufanya biashara zinazovunja viwango vya Mungu, zinazoweza kulegeza msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa, au zinazohatarisha hali yetu ya kiroho. (Isa. 2:4; 2 Tim. 2:4) Pia, hatushirikiani na “Babiloni Mkubwa,” adui wa kidini wa Mungu.—Ufu. 18:2, 4; 2 Kor. 6:14-17.

      27 Kufuata viwango vya uadilifu vya Mungu, kutatuepusha kutumia vibaya ushirika wetu wa Kikristo ili kuendeleza biashara au faida zetu za kibinafsi. Kusudi la kushirikiana na wenzetu kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo ni kumwabudu Yehova. Tunalishwa katika meza yake ya kiroho na tunafurahia ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12; Ebr. 10:24, 25) Kwenye ushirika huo tunapaswa kuzungumzia mambo ya kiroho.

      KUKAA KATIKA UMOJA WA KIKRISTO

      28 Ili watu wa Yehova wafuate viwango vyake vya uadilifu wanahitaji “kudumisha roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.” (Efe. 4:1-3) Badala ya kujifikiria wenyewe, kila mmoja hujitahidi kufanya mambo yanayowapendeza wengine. (1 The. 5:15) Bila shaka umejionea roho hiyo katika kutaniko lako. Bila kujali kabila, taifa, jamii, hali yetu ya kiuchumi au elimu yetu, sote tunaongozwa na viwango vilevile vya uadilifu. Hata watu wasio Mashahidi wameona sifa hiyo ya pekee ya watu wa Yehova.—1 Pet. 2:12.

      29 Akikazia msingi wa umoja, mtume Paulo aliandika hivi: “Kuna mwili mmoja, na roho moja, kama mlivyoitwa kwenye tumaini moja; Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja; Mungu mmoja ambaye ni Baba wa wote, aliye juu ya wote, na kupitia wote na katika wote.” (Efe. 4:4-6) Maneno hayo yanatuchochea tuwe na ufahamu uleule wa mafundisho ya msingi na pia mafundisho yenye kina ya Biblia ili tuonyeshe kwamba tunatambua mamlaka kuu ya Yehova. Kwa kweli, Yehova amewapa watu wake lugha safi ya kweli inayowawezesha wamtumikie bega kwa bega.—Sef. 3:9.

      30 Umoja na amani ya kutaniko la Kikristo huwaburudisha wote wanaomwabudu Yehova. Tumeshuhudia utimizo wa ahadi hii ya Yehova: “Kwa umoja nitawaweka kama kondoo zizini.” (Mika 2:12) Tunataka kudumisha umoja na amani hiyo kwa kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova.

      31 Wenye furaha ni wale waliokubaliwa katika kutaniko safi la Yehova! Tunapaswa kujidhabihu kwa njia yoyote ile ili tuitwe kwa jina la Yehova. Tunapodumisha uhusiano wetu wenye thamani na Yehova, tutajitahidi sana kufuata viwango vyake vya uadilifu na kuwafundisha wengine kufanya hivyo.—2 Kor. 3:18.

  • Kudumisha Amani na Usafi wa Kutaniko
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • SURA YA 14

      Kudumisha Amani na Usafi wa Kutaniko

      KAMA unabii wa Biblia ulivyotabiri, kila mwaka maelfu ya watu humiminika kwenye nyumba ya Yehova ya ibada safi. (Mika 4:1, 2) Tunafurahia kwelikweli kuwakaribisha katika “kutaniko la Mungu”! (Mdo. 20:28) Wanathamini sana kumtumikia Yehova pamoja nasi na kufurahia mazingira safi na yenye amani ya paradiso yetu ya kiroho. Roho takatifu ya Mungu na hekima ya Neno lake inatusaidia kudumisha amani na usafi wa kutaniko.—Zab. 119:105; Zek. 4:6.

      2 Tunapofuata kanuni za Biblia, tunavaa “utu mpya.” (Kol. 3:10) Hatutilii maanani mabishano madogo-madogo na tofauti za kibinafsi. Tunashinda ushawishi unaosababisha migawanyiko ulimwenguni, na kufanya kazi kwa umoja tukiwa undugu wa kimataifa kwa sababu tuna maoni kama ya Yehova.—Mdo. 10:34, 35.

      3 Hata hivyo, mara kwa mara matatizo hutokea ambayo huathiri amani na umoja wa kutaniko. Yanasababishwa na nini? Katika visa vingi, husababishwa na kutofuata ushauri wa Biblia. Bado tunapambana na mwelekeo wetu mbaya tukiwa wanadamu wasio wakamilifu. Hakuna hata mmoja wetu asiyetenda dhambi. (1 Yoh. 1:10) Huenda mtu fulani akachukua hatua isiyofaa ambayo inaweza kuchafua maadili au usafi wa kiroho wa kutaniko. Tunaweza kumkosea mtu fulani kwa kutenda au kusema bila kufikiri, au huenda tukakwazika kwa sababu ya jambo ambalo mtu fulani amesema au kutenda. (Rom. 3:23) Katika hali kama hizo, tunaweza kufanya nini ili kunyoosha mambo?

      4 Kwa upendo Yehova amefikiria mambo yote hayo. Neno lake linatushauri kuhusu kutatua matatizo yanapotokea. Msaada wa kibinafsi unapatikana kutoka kwa wachungaji wenye upendo, yaani wazee. Kwa kufuata ushauri wao wa Kimaandiko, tunaweza kurejesha uhusiano mzuri na wengine na kudumisha msimamo mzuri na Yehova. Ikiwa tunatiwa nidhamu au kukaripiwa kwa sababu ya kosa fulani tulilofanya, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yetu wa mbinguni anaturekebisha kwa kuwa anatupenda.— Met. 3:11, 12; Ebr. 12:6.

      KUTATUA TOFAUTI NDOGO-NDOGO

      5 Nyakati fulani huenda kukatokea mabishano au kutoelewana kati ya ndugu na dada kutanikoni kwa sababu ya mambo madogo-madogo. Hali hiyo inapaswa kutatuliwa haraka na kwa roho ya upendo wa kindugu. (Efe. 4:26; Flp. 2:2-4; Kol. 3:12-14) Huenda ukatambua kwamba matatizo ya kibinafsi yanayohusu uhusiano wako na Mkristo mwenzako kutanikoni yanaweza kutatuliwa kwa kufuata ushauri huu wa mtume Petro: “Pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.” (1 Pet. 4:8) Biblia inasema: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yak. 3:2) Kwa kufuata ile Kanuni Bora, yaani, kuwatendea wengine kwa njia ambayo tungependa watutendee, mara nyingi tunaweza kusamehe na kusahau makosa madogo ya wengine.—Mt. 6:14, 15; 7:12.

      6 Ukitambua kwamba umemkosea mtu fulani kwa yale uliyosema au kutenda, unapaswa kuchukua hatua ili kufanya amani bila kukawia. Kumbuka kwamba uhusiano wako pamoja na Yehova pia unaathiriwa. Yesu aliwashauri wanafunzi wake hivi: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo unakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, iache zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, uende zako. Kwanza fanya amani na ndugu yako, kisha urudi na kutoa zawadi yako.” (Mt. 5:23, 24) Huenda mmoja wenu ameelewa jambo fulani kimakosa. Ikiwa ndivyo, zungumzieni jambo hilo waziwazi. Mawasiliano mazuri kati ya washiriki wote wa kutaniko husaidia kuzuia kutoelewana na kutatua matatizo yanayotokea kwa sababu ya kutokamilika.

      KUTOA USHAURI WA MAANDIKO

      7 Nyakati nyingine, huenda waangalizi wakaona kwamba wanapaswa kumshauri mtu fulani ili arekebishe maoni yake. Kwa kawaida si rahisi kufanya hivyo. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa Galatia: “Akina ndugu, hata mtu akichukua hatua isiyofaa kabla hajajua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo kwa roho ya upole.”—Gal. 6:1.

      8 Wanapolichunga kundi, waangalizi hulinda kutaniko dhidi ya hatari za kiroho na hivyo kuzuia matatizo makubwa yasitokee. Wazee wanapaswa kujitahidi kulitumikia kutaniko kama Yehova alivyoahidi kupitia Isaya: “Na kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujificha kutokana na upepo, na mahali pa kujisitiri kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha jabali kubwa katika nchi iliyokauka.”—Isa. 32:2.

      KUWATIA ALAMA WATU WASIOFUATA UTARATIBU

      9 Mtume Paulo aliwaonya watu fulani ambao wangeweza kuwa na ushawishi mbaya ndani ya kutaniko. Paulo alisema hivi: “Sasa akina ndugu, tunawaagiza . . . mjiepushe na kila ndugu asiyefuata utaratibu na desturi mlizopokea kutoka kwetu.” Kisha akafafanua taarifa yake kwa kuandika hivi: “Lakini ikiwa yeyote hatii maneno yetu kupitia barua hii, mtieni alama na mwache kushirikiana naye, ili aone aibu. Lakini msimwone mtu huyo kama adui, bali endeleeni kumwonya kama ndugu.”—2 The. 3:6, 14, 15.

      10 Pindi fulani, huenda mtu akapuuza kimakusudi viwango vya Biblia vya Kikristo ingawa hajafanya dhambi nzito inayoweza kumfanya atengwe na kutaniko. Hilo linaweza kutia ndani mambo kama vile kuwa mvivu, mchambuzi, au mchafu kupita kiasi. Huenda ‘anajiingiza katika mambo yasiyomhusu.’ (2 The. 3:11) Au huenda anawatumia wengine kwa hila kujipatia faida za kimwili au anafurahia burudani ambayo kwa wazi haifai. Mwenendo huo usiofaa ni jambo zito linaloharibu sifa ya kutaniko, na pia unaweza kuenea kati ya Wakristo wengine.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki