Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Swali Muhimu Zaidi ya Yote
    Amkeni!—2011 | Novemba
    • Swali Muhimu Zaidi ya Yote

      “JE, KUNA swali muhimu zaidi katika maisha ya mwanadamu kuliko hili: ‘Kuna Mungu?’” ndivyo alivyouliza mtaalamu wa chembe za urithi, Francis S. Collins. Anatoa hoja hii muhimu. Ikiwa hakuna Mungu, basi hatuwezi kupata mwongozo kutoka kwa mamlaka iliyo juu zaidi kuhusu masuala ya maadili.

      Sababu moja inayowafanya watu fulani watilie shaka kuwepo kwa Mungu ni kwamba wanasayansi wengi hawaamini kuna Mungu. Hata hivyo, nyakati nyingine maoni ya watu wengi yanaweza kuwa yenye makosa sana, kama makala inayofuata itakavyoonyesha.

      Kwa kusikitisha, dini nyingi zimefanya jambo hilo liwe lenye kutatanisha hata zaidi kwa kufundisha mambo yanayopingana na mambo hakika ya kisayansi. Mfano mmoja ni fundisho lisilo la Kimaandiko kwamba miaka elfu kadhaa iliyopita, Mungu aliumba ulimwengu katika kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja.

      Nadharia na falsafa hizo zenye kupingana hufanya watu wengi waache kutafuta ukweli kuhusu kuwepo kwa Mungu. Lakini hakuna jambo muhimu zaidi na linaloathiri maisha ya mtu kuliko kupata jibu la swali hilo muhimu. Ni kweli kwamba hatujawahi kumwona Mungu, wala hatukuwepo alipoumba ulimwengu na uhai. Kwa hiyo, iwe tunaamini Mungu yuko au la, maoni yetu yanategemea imani kwa kiasi fulani. Lakini ni imani ya aina gani inayohitajika?

      Imani ya Kweli Inategemea Uthibitisho Imara

      Imani ni sehemu muhimu ya maisha yetu—angalau kwa kiasi fulani. Tunakubali kuajiriwa, tukiwa na imani kwamba tutalipwa mshahara. Tunapanda mbegu tukiwa na uhakika kwamba zitachipuka. Tunawaamini rafiki zetu. Na tuna imani katika sheria zinazoongoza ulimwengu. Hiyo si imani isiyo na msingi bali inategemea uthibitisho. Vivyo hivyo, imani ya kwamba Mungu yuko inategemea uthibitisho.

      Biblia inasema hivi kwenye Waebrania 11:1: “Imani ni . . . uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” Tafsiri nyingine inasema: “Imani . . . hutusadikisha kabisa kuhusu mambo tusiyoyaona.” (The New English Bible) Fikiria mfano huu: Unatembea ufuoni, na ghafula unahisi ardhi ikitetemeka. Kisha unaona maji yakitoweka ghafula baharini. Mara moja unatambua kwamba matukio hayo ni onyo kuwa tsunami inakuja. Katika mfano huo, tetemeko na kutoweka kwa maji ni “uthibitisho ulio wazi” wa jambo ambalo bado halijaonekana, yaani, mawimbi yanayokuja. Imani yako iliyo na msingi, inakuchochea ukimbilie usalama mahali palipoinuka.

      Vivyo hivyo, ili mtu aamini kuwa Mungu yuko anapaswa kuwa na imani iliyo na msingi baada ya kujionea uthibitisho wenye kusadikisha. Hapo tu ndipo Mungu atakuwa ‘halisi kwako ingawa haonekani.’ Je, ni lazima uwe mwanasayansi ili uweze kuchanganua uthibitisho huo? Vladimir Prelog, mshindi wa Tuzo la Nobeli, anasema kwamba hata “washindi wa Tuzo la Nobeli hawajui mengi kuhusu Mungu, dini, na uhai baada ya kifo kuliko watu wengine.”

      Kuwa na moyo mnyoofu na kutaka kujua ukweli kunapaswa kukuchochea uchunguze uthibitisho uliopo bila ubaguzi wowote na uache uthibitisho huo ukuongoze ufikie mkataa unaofaa. Kuna uthibitisho gani?

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Mkulima ana imani ya kwamba mbegu zitaota na kukua

  • Chunguza Uthibitisho
    Amkeni!—2011 | Novemba
    • Chunguza Uthibitisho

      UKO katika kisiwa kilicho mbali sana ambacho hakina watu. Unapotembea ufuoni, unaona maandishi “John 1800” yakiwa yamechongwa kwenye mwamba. Kwa kuwa kisiwa hicho kiko mbali na hakina watu, je, ungekata kauli kwamba maandishi hayo yalitokezwa na mmomonyoko uliosababishwa na upepo au maji? Bila shaka la! Ungekata kauli kwamba mtu fulani alichonga maandishi hayo. Kwa sababu gani? Kwanza, kwa sababu nambari na herufi zinazoonekana waziwazi, hata kama zimeandikwa katika lugha ya kigeni, haziwezi kujitokeza zenyewe. Pili, maandishi hayo yana maana, na hilo linaonyesha kwamba yaliandikwa na mtu mwenye akili.

      Kila siku, tunapata habari zilizoandikwa katika njia mbalimbali—kama vile maandishi ya vipofu (Braille) au herufi za alfabeti, na pia michoro, noti za muziki, maneno, ishara za mkono, mawimbi ya redio, na programu za kompyuta zinazotumia binari, yaani, nambari moja kadhaa na sufuri kadhaa. Habari inaweza kupitishwa kwa njia yoyote ile, iwe ni kwa mawimbi ya mwangaza au ya redio au iwe imeandikwa kwa wino kwenye karatasi. Vyovyote vile, kwa kawaida watu hutambua kwamba habari muhimu iliandikwa na mtu fulani mwenye akili, lakini inashangaza kwamba wengi wanashindwa kutambua hilo habari hiyo inapokuwa imeandikwa ndani ya chembe iliyo hai. Wanamageuzi wanasema kwamba habari iliyo ndani ya chembe ilijitokeza au kujiandika yenyewe. Lakini, je, hilo ni kweli? Hebu chunguza uthibitisho.

      Je, Habari Tata Inaweza Kujiandika Yenyewe?

      Kiini cha kila chembe iliyo hai katika mwili wako kina habari fulani yenye kustaajabisha inayoitwa deoksiribonyukilia asidi, au kwa ufupi DNA. Habari hizo zimehifadhiwa katika molekuli ndefu yenye nyuzi mbili inayofanana na ngazi iliyojipinda. DNA yako ni kama maagizo ya upishi, au programu ambayo inaongoza kutokezwa, kukua, kudumishwa, na kujigawanya kwa matrilioni ya chembe zinazofanyiza mwili wako. Molekuli za DNA zimefanyizwa kwa molekuli ndogo zinazoitwa nukliotidi. Molekuli hizo ndogo zinawakilishwa na herufi A, C, G, na T, ikitegemea kemikali zinazozifanyiza.a Kama herufi za alfabeti, herufi hizo nne zinaweza kuunganishwa katika njia mbalimbali na kufanyiza “sentensi,” yaani maagizo ambayo huongoza kunakiliwa kwa molekuli ya DNA na utendaji mwingine ndani ya chembe.

      Habari yote iliyohifadhiwa katika DNA yako inaitwa genome. Herufi fulani zinapatikana tu katika DNA yako kwa kuwa DNA yako ina habari kukuhusu wewe tu kama vile, rangi ya macho yako, rangi ya ngozi yako, umbo la pua lako, na kadhalika. Kwa ufupi, genome yako inaweza kufananishwa na maktaba kubwa yenye habari kuhusu kila sehemu ya mwili wako, ambayo inakufanyiza wewe.

      “Maktaba” hiyo ni kubwa kadiri gani? Ina urefu wa “herufi,” au nukliotidi, bilioni tatu hivi. Kulingana na Mradi wa Kuchunguza Chembe za Urithi za Mwanadamu, ikiwa herufi hizo zingeandikwa kwenye karatasi, zingejaza mabuku yapatayo 200, kila buku likitoshana na kitabu chenye anwani na nambari za simu chenye kurasa 1,000.

      Hilo linatukumbusha sala moja iliyoandikwa miaka 3,000 hivi iliyopita. Sala hiyo inayopatikana katika kitabu cha Biblia cha Zaburi 139:16 inasema hivi: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa.” Bila shaka, mwandikaji huyo hakuwa akizungumzia mambo kwa njia ya sayansi, lakini kwa maneno rahisi anazungumzia hoja sahihi inayoonyesha hekima na nguvu za ajabu za Mungu. Sala hiyo ni tofauti kabisa na maandishi ya kale ya kidini yaliyojaa hekaya na ushirikina!

      Ni Nani Aliyefanyiza “Maktaba” Hiyo?

      Ikiwa ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba maandishi “John 1800” yaliyochongwa kwenye mwamba yaliandikwa na mtu mwenye akili, je, haipatani na akili hata zaidi kuamini kwamba habari tata sana na iliyo muhimu inayopatikana kwenye DNA iliandikwa na mtu mwenye akili? Isitoshe, habari ni habari haidhuru inapatikana wapi au imepitishwa kwa njia gani. Donald E. Johnson, ambaye ni mtaalamu wa kompyuta na habari alisema kwamba kulingana na sheria za kemia na fizikia, habari au mfumo unaochanganua habari hauwezi kujitokeza wenyewe. Na inapatana na akili kwamba kadiri habari ilivyo tata, ndivyo inavyohitaji mtu mwenye akili zaidi kuiandika. Mtoto anaweza kuandika “John 1800.” Lakini ni mtu mwenye akili inayopita ya mwanadamu anayeweza kuandika maagizo ya uhai. Isitoshe, “kadiri tunavyojifunza kuhusu mwili wa mwanadamu, ndivyo uvumbuzi huo mpya unavyozidi kututatanisha,” linasema jarida Nature.

      Kusema kwamba maktaba tata yenye habari za DNA ilijitokeza yenyewe bila kuelekezwa na mtu yeyote hakupatani na akili na ufahamu wa wanadamu.b Imani hiyo haina msingi.

      Wakijaribu kuonyesha kwamba hakuna Mungu, nyakati nyingine wanamageuzi wamefikia mkataa ambao baadaye ulionekana kuwa wenye makosa. Fikiria kwa mfano maoni ya kwamba asilimia 98 hivi ya habari zilizo katika DNA yetu “hazihitajiki.” Hilo linamaanisha kwamba maktaba hiyo ya maagizo ina mabilioni ya maneno yasiyo na maana.

      Je, Kweli Ni DNA “Zisizohitajika”?

      Kwa miaka mingi, wanabiolojia waliamini kwamba DNA ina maagizo ya kutengeneza protini peke yake. Hata hivyo, baada ya muda, iligunduliwa kwamba ni asilimia 2 tu ya DNA iliyo na maagizo ya kutengeneza protini. Asilimia ile nyingine 98 ya DNA hufanya kazi gani? Watu wengi walikata kauli kwamba DNA hizo zisizojulikana “hazihitajiwi kwa sababu ni habari za ziada zilizosalia baada ya mageuzi kukamilika,” akasema John S. Mattick, profesa wa Biolojia ya Molekuli katika Chuo Kikuu cha Queensland huko Brisbane, Australia.

      Mwanamageuzi Susumu Ohno, ndiye aliyeanzisha usemi “DNA ‘zisizohitajiwa.’” Katika makala yake yenye kichwa “DNA Nyingi Sana ‘Zisizohitajiwa’ Katika Genome Yetu” (“So Much ‘Junk’ DNA in Our Genome”), alisema kwamba mfuatano wa DNA zinazosalia “ni mabaki ya majaribio ya kiasili ambayo hayakufanikiwa. Dunia imejaa mabaki ya wanyama waliotoweka zamani; je, ni ajabu kwamba mwili wetu umejaa mabaki ya chembe za urithi ambazo hazihitajiwi tena?”

      Nadharia ya kwamba kuna DNA “zisizohitajiwa” iliathiri kwa njia gani uchunguzi wa chembe za urithi? Wojciech Makalowski, mwanabiolojia wa molekuli anasema kwamba maoni hayo “yaliwazuia watafiti wengi wasichunguze DNA [zisizohitajiwa] ambazo hazitengenezi protini,” isipokuwa wanasayansi wachache sana ambao, “wakiwa katika hatari ya kudhihakiwa, walichunguza DNA hizo ambazo hazikuwa zimewahi kuchunguzwa. Kwa sababu ya uchunguzi wao, maoni kuhusu DNA zisizohitajiwa . . . yalianza kubadilika mwanzoni mwa miaka ya 1990.” Anaongezea kusema kwamba siku hizi wanabiolojia huziona DNA hizo ambazo zilisemekana hazihitajiwi kuwa “hazina ya chembe za urithi.”

      Mattick anasema kwamba nadharia ya DNA zisizohitajiwa ni mfano bora zaidi unaoonyesha jinsi watu hufuata maoni ya watu wengi “badala ya kuchunguza mambo ya hakika.” “Kukosa kutambua matokeo ya kukata kauli kwa njia hiyo,” anaongezea, “kunaweza kuwa mojawapo ya makosa makubwa zaidi katika biolojia ya molekuli.” Ni wazi kwamba mikataa ya kisayansi inapaswa kufikiwa kwa kutegemea uthibitisho uliopo si kwa kufuata maoni ya watu wengi. Kwa msingi wa hilo, uthibitisho wa hivi karibuni umefunua nini kuhusu kazi ya DNA “zisizohitajiwa”?

      Kazi ya DNA “Zisizohitajiwa”

      Kiwanda cha kutengeneza magari hutumia mashini kutengeneza sehemu za magari. Tunaweza kufananisha sehemu hizo na protini katika chembe. Kiwanda hicho pia kinahitaji vifaa na mifumo ambayo itaunganisha sehemu hizo hatua kwa hatua na mitambo ya kuongoza, au kudhibiti kuunganishwa kwa sehemu hizo. Ndivyo ilivyo na utendaji ndani ya chembe. Watafiti wanasema kwamba hiyo ndiyo kazi ya DNA “zisizohitajiwa.” Nyingi ya DNA hizo zina maagizo ya molekuli tata inayoitwa RNA (ribonucleic acid), ambayo hudhibiti ukuzi na utendaji wa chembe.c Mwanabiolojia na mwanahisabati Joshua Plotkin, anasema hivi katika gazeti Nature: “Kuwepo kwa molekuli hizo zinazodhibiti ukuzi kunaonyesha kwamba uelewaji wetu wa mambo ya msingi . . . ni mdogo sana.”

      Ili kiwanda kifanye kazi vizuri kinahitaji pia mfumo mzuri wa mawasiliano. Ndivyo ilivyo na chembe. Tony Pawson, mtaalamu wa chembe katika Chuo Kikuu cha Toronto huko Ontario, anaeleza: “Badala ya kutumia njia rahisi na ambazo hazijaungana, chembe hutumia mtandao tata sana wa kupitisha habari,” na hivyo kufanya mfumo wote “kuwa tata sana” kuliko ilivyodhaniwa awali. Kwa kweli, kama alivyosema mtaalamu mmoja wa chembe za urithi katika Chuo Kikuu cha Princeton, “utendaji na maagizo yanayoongoza yale yanayotukia ndani ya chembe na kudhibiti jinsi chembe zinavyofanya kazi pamoja bado ni fumbo.”

      Kila uvumbuzi mpya kuhusu chembe unaonyesha utaratibu na ustadi wa hali ya juu. Hivyo basi kwa nini watu wengi bado wanashikilia dhana ya kwamba uhai na mfumo wa habari wa hali ya juu ulitokezwa na mageuzi yasiyo na mpangilio?

      [Maelezo ya Chini]

      a Kila nukliotidi imefanyizwa kwa mojawapo ya kemikali nne za msingi: (A) adenine, (C) cytosine, (G) guanine, na (T) thymine.

      b Inasemekana kwamba mageuzi yanatokana na mabadiliko katika chembe za urithi wa vitu vilivyo hai. Mambo hayo yatazungumziwa kwa ufupi katika makala inayofuata.

      c Utafiti wa hivi karibuni unaonyesha kwamba RNA ndefu ambazo hazitokezi protini ni tata sana na kwamba zinahitajiwa kwa ukuzi wa kawaida. Watafiti wamegundua kwamba kasoro fulani katika RNA hizo zinahusianishwa na magonjwa mengi kama vile aina fulani za kansa, magonjwa ya ngozi, na hata ugonjwa wa Alzheimer. DNA ambazo hapo awali zilionekana kuwa “hazihitajiwi” huenda zikatumiwa katika kugundua na kutibu magonjwa mbalimbali!

      [Sanduku katika ukurasa wa 5]

      DNA YAKO NI NDEFU KADIRI GANI?

      DNA katika chembe moja mwilini mwako inaponyooshwa ina urefu wa mita 2 hivi. Ikiwa ungechukua DNA zote zilizo katika matrilioni ya chembe mwilini mwako na kuzinyoosha na kuziunganisha moja baada ya nyingine, inakadiriwa kwamba zingekuwa na urefu wa kutoka duniani hadi kwenye jua na kurudi karibu mara 670. Kusafiri umbali huo kwa mwendo wa nuru kutachukua saa 185 hivi.

  • Ni Maoni Gani Yanayopatana Zaidi na Akili?
    Amkeni!—2011 | Novemba
    • Ni Maoni Gani Yanayopatana Zaidi na Akili?

      HAKUNA mwanadamu aliyeona uhai ukianza duniani. Wala hakuna mtu ambaye ameona uhai ukigeuka na kuwa aina nyingine ya uhai, yaani, mnyama anayetambaa akigeuka na kuwa mamalia.a Kwa hiyo, ni lazima tutegemee uthibitisho uliopo ili kufikia mkataa kuhusu chanzo cha uhai. Na inafaa tuamini yale ambayo uthibitisho huo unaonyesha badala ya kuulazimisha ukubaliane na maoni yetu.

      Hata hivyo, watu wengi wanaoamini hakuna Mungu wanaamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe bila msaada wowote wa nguvu zisizo za kawaida. “Tulifanya uamuzi mapema . . . kwamba ulimwengu ulijitokeza,” akaandika mwanamageuzi Richard C. Lewontin. “Kwa kuwa wazo la kwamba ulimwengu ulijitokeza ndilo wazo pekee linalopatana na akili, hatupaswi hata kufikiri kuna Muumba.” Hivyo, watu wanaoamini kwamba ulimwengu ulijitokeza wenyewe hawana jambo lingine ila kuamini mageuzi.

      Watu wa kidini pia wanaweza kuwa na maoni yasiyofaa ambayo hupotosha mtazamo wao kuelekea sayansi. Kwa mfano, kama ilivyotajwa awali, wanauumbaji fulani wanashikilia maoni yenye makosa kwamba maelfu ya miaka iliyopita Mungu aliuumba ulimwengu mzima kwa siku sita zenye saa 24. Kwa kuwa tayari waliamua hivyo mapema, wanajaribu kulazimisha uthibitisho uliopo uunge mkono ufafanuzi wao wa Biblia. (Ona sanduku “‘Siku’ Moja Ina Urefu Gani?” kwenye ukurasa wa 9.) Watu walio na maoni ya kishupavu kuielekea Biblia na sayansi hawana majibu yenye kuridhisha wanapotafuta uthibitisho wa imani yao.

      Ni Maoni Gani Yanayohusisha Mambo Yote Hakika?

      Wanamageuzi fulani huamini mambo yafuatayo kuhusu chanzo cha molekuli tata ambazo hufanyiza viumbe hai:

      1. Vitu vya msingi viliungana kwa njia fulani na kufanyiza molekuli za msingi.

      2. Kisha molekuli hizo ziliungana pamoja kwa mfuatano uleule unaohitajiwa kufanyiza DNA, RNA, au protini zenye uwezo wa kuhifadhi habari inayohitajika ili kutekeleza utendaji muhimu kwa ajili ya uhai.

      3. Kwa njia fulani, molekuli hizo zilifanyiza mfuatano hususa unaohitajiwa ili ziweze kujigawanya. Hakuwezi kuwa na mageuzi wala uhai ikiwa molekuli hazitajigawanya.

      Molekuli zinazohitajiwa kwa ajili ya uhai zilifanyizwa namna gani na zilipata wapi uwezo wao wa ajabu pasipo mbuni mwenye akili kuingilia kati? Utafiti wa wanamageuzi haujaeleza vizuri au kutoa majibu yenye kuridhisha kwa maswali kuhusu chanzo cha uhai. Kwa kweli wale wanaopinga kwamba Muumba alihusika kwa njia fulani, wanadai eti nguvu za asili na molekuli zisizo na akili zilikuwa na nguvu kama za Mungu za kutokeza uhai.

      Hata hivyo, mambo hakika yanaonyesha nini? Uthibitisho uliopo unaonyesha kwamba badala ya molekuli kukua na kuwa viumbe hai vilivyo tata, mambo hutendeka kinyume: Sheria za fizikia zinasema kwamba vitu tata—mashini, nyumba, na hata chembe iliyo hai—huharibika baada ya muda.b Hata hivyo, wanamageuzi husema kwamba mambo hutendeka kinyume. Kwa mfano, kitabu Evolution for Dummies kinasema kwamba mageuzi hutukia kwa sababu dunia “inapata nishati nyingi sana kutoka kwa jua, na nishati hiyo ndiyo hufanya vitu viwe tata.”

      Ni kweli kwamba nishati inahitajika ili kutokeza kitu tata—kwa mfano, nishati inahitajika ili kuunganisha matofali, mbao, na misumari ili ziwe nyumba. Hata hivyo, nishati hiyo inapaswa kudhibitiwa kwa uangalifu na kuelekezwa kwa njia sahihi kwa sababu huenda nishati isiyodhibitiwa ikafanya vitu vidhoofike haraka, kama vile tu nishati kutoka kwenye jua na hali ya hewa zinaweza kufanya jengo liharibike haraka.c Watu wanaoamini mageuzi hawawezi kueleza kwa njia inayoridhisha jinsi ambavyo nishati hudhibitiwa ili kufanyiza vitu tata.

      Kwa upande mwingine, tukiwa na maoni ya kwamba uhai na ulimwengu ni kazi ya Muumba mwenye hekima ambaye ana “wingi wa nguvu zenye msukumo,” tunaweza kueleza chanzo cha mfumo tata wa habari na pia kani zilizopimwa kwa usahihi kabisa ambazo huongoza vitu vidogo zaidi kama atomu na vikundi vikubwa vya nyota.d—Isaya 40:26.

      Kuamini kwamba kuna Muumba pia kunapatana na maoni yanayofuatwa na wengi kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Mwanzo 1:1 inasema: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”

      Kila mara kunapokuwa na uvumbuzi mpya, inakuwa vigumu kutetea falsafa ya kwamba ulimwengu na uhai ulijitokeza wenyewe, na jambo hilo limefanya baadhi ya watu wanaoamini kwamba hakuna Mungu wabadili maoni yao.e Watu ambao hapo awali waliamini hakuna Mungu wamefikia mkataa wa kwamba maajabu ya ulimwengu ni uthibitisho ulio wazi wa “sifa zake ambazo hazionekani” na ‘nguvu za milele’ za Muumba wetu, Yehova Mungu. (Waroma 1:20) Je, ungependa kuchunguza jambo hilo kwa undani zaidi? Kufanya hivyo kungekuwa jambo muhimu zaidi maishani mwako.f

      [Maelezo ya Chini]

      a Ingawa aliamini kabisa katika mageuzi, mwanabiolojia Ernst Mayr alikubali kwamba “mabaki ya wanyama yanaonyesha pengo fulani,” yaani, viumbe vipya vilitokea ghafula.

      b Wanasayansi huuita mwelekeo huo wa vitu kuharibika, “athari ya joto.” Kwa ufupi, sheria hiyo husema kwamba utaratibu hudhoofika hatua kwa hatua na kutokeza mvurugo.

      c DNA inaweza kubadilika kwa sababu ya mabadiliko katika chembe za urithi yanayotokezwa na mnururisho na kemikali fulani. Lakini mabadiliko hayo hayatokezi viumbe vipya.—Ona habari yenye kichwa “Je, Mageuzi Ni Jambo Hakika?” katika gazeti Amkeni! la Septemba (Mwezi wa 9) 2006.

      d Ona kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      e Ona habari yenye kichwa “Nililelewa na Wazazi Walioamini Hakuna Mungu,” katika toleo la Amkeni! la Novemba 2010.

      f Kwa habari zaidi kuhusu suala la uumbaji na mageuzi, ona broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, zilizochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      [Sanduku katika ukurasa wa 8]

      JE, WANADAMU WANAGEUKA NA KUWA VIUMBE BORA AU WANAZOROTA?

      Wanasayansi fulani wana wasiwasi kwamba DNA ya wanadamu inadhoofika kwa sababu ya mabadiliko katika chembe za urithi, au kutokamilika. Ikiwa hilo ni kweli, jambo hilo lingepinga wazo la kwamba tunageuka, au hali yetu inazidi kuwa bora. Lakini ikiwa Mungu ndiye aliyeumba DNA ya mwanadamu, kwa nini ina kasoro? Biblia inatueleza mambo ambayo sayansi haiwezi kutueleza—kwamba kutokamilika kwa mwanadamu kulitokana na dhambi, au kutokumtii Mungu. Waroma 5:12 inasema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” Kwa hiyo basi, DNA inayozorota inapinga mageuzi na kuunga mkono Biblia. Je, hilo linamaanisha kwamba DNA itaendelea kuzorota mpaka wakati usiojulikana? La! Mungu ameahidi kuingilia mambo ya wanadamu na kuondoa madhara yote yaliyosababishwa na wazazi wetu wa kwanza. Naam, Muumba wetu, na si mageuzi, ndiye atakayefanya DNA yetu iwe kamilifu.—Ufunuo 21:3, 4.

      [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      “SIKU” MOJA INA UREFU GANI?

      Katika Biblia, neno “siku” linaweza kurejelea vipindi mbalimbali vya wakati. Kwa mfano, kwenye Mwanzo 2:4, kipindi chote cha uumbaji cha “siku” sita kinatajwa kuwa “siku ambayo Yehova Mungu aliifanya dunia na mbingu.” Ni wazi kwamba kila siku ilihusisha kipindi kirefu cha wakati. Jambo la kuzingatiwa ni kwamba ingawa Biblia inataja kihususa mwisho wa “siku” sita za kwanza, haitaji mwisho wa siku ya saba. Kwa nini? Kwa sababu bado siku hiyo inaendelea.—Mwanzo 2:3; Waebrania 4:4-6, 11.

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Vitu huharibika visipotunzwa

      [Picha katika ukurasa wa 8, 9]

      Nguvu na sifa nyingine za Mungu zinaonekana katika ulimwengu

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki